Saturday, December 26, 2009

Vyombo vya habari na matangazo ya biashara ya elimu feki

Biashara ya elimu ‘feki’ ama kwa kiingereza‘diploma/degree mills’ inaendelea kushamiri Duniani.Hili ni tatizo la Ulimwengu, huku wadadidi wa mambo ya biashara ya Elimu wakikadiria kuwa zaidi ya karne sasa Ulimwengu unasumbuliwa na kansa hii.

Nini maana ya ‘Diploma mills’ hii ni taasisi iliyokuwa tayari kukupa hati ya kielimu bila hata ‘kisomo’ au kuingia darasani. Tafsiri hii inatia ndani pia hata kama ukawa unahudhuria na testi umefanya na kufaulu kwa viwango vya taasisi yako lakini ‘doa’ ni kwamba hautambuliki.

Katika zama za mawasilinao ya ‘kompyuta’ ambapo mtu anaweza kufyatua vyeti na kuthibitisha kuwa na taaluma husika kwa ngazi ya shahada ya kwanza, ya uzamili au Uzamivu(PhD) biashara hii imekuwa kwa kasi mno. Watu wengi ama kwa kufahamu au kutofahamu wamejikuta wakiingia katika mkumbo wa kupata shahada feki.

Ulimwengu unahangaika, watu maarufu na viopngozi wa umma na taasisi zake wako bega kwa bega kupiga vita ‘elimu feki’. Mwa mfalme Prince Charles, amewahi kukemea suala hili na kutaka juhudi za wazi zichukuliwe ili kudhibiti hali hii.
Tanzania ya leo inasukwasukwa na wimbi la upatikanaji wa wataalamu wenye vyeti feki.

Pamoja na tahadhari zinazotolewa juu ya hatari ya shahada ‘feki’ lakini la kustaajabisha ni kwamba idadi ya watu wanaopata na kununua elimu hii inaongezeka, FBI na Interpol wanaweka wazi kuwa biashara hii inashamirishwa na wateja wenyewe.

Katika Amerika sheria za majimbo zinajaribu kukaba, na kupambana vilivyo na hali hii, lakini yatupasa kufahamu kuwa kabla hatujasema chuo fulani kuwa kuna vyuo vimenyagwanywa ‘hadhi’ katika ya safari baada ya kubainika kuwa mchezo wao si mwea kitaaluma.

Kutotambulika ni hasa pale unapotaka kujiendeleza, mathalani umefanya elimu kwa ngazi ya cheti kwa elimu ya kompyuta kwenye chuo fulani pale ‘Kariakoo’. Cheti hiki kama hakikupi kinga ya kujiendeleza kielimu kwa ngazi ya Diploma ya elimu ya kompyuta katika vyuo makini, kama vile UDSM, IFM! Ni wazi kuwa chuo ulichosoma ni ‘feki’.

Biashara hii imekuwa ikishamiri na kwa kiasi kikubwa ingawa hakuna takwimu sahihi lakini kuwepo kwa wahitimu hao ni dalili ya wazi, pia kuongezeka kwa vyuo vyenyewe ni mwanga tosha kuwa biashara yao ina wateja. Mafanikio haya yamechangiwa na vyombo vya habari pia sekta binafsi kwa kukubali wahitimu wa vyuo hivi.

Magazeti makubwa kama Forbes, Herald, the Economist yamekuwa yakitoa matangazao ya vyuo hivi ingawa yanaelewa ni njia maoja wapo ya kushamirisha ‘dploma mills’. Mara zote wahariri wanapoulizwa kuhusu, mustakabili wa wao kukubali kutoa matangazo ya vyuo ‘bomu’.Hudai kuwa wasomaji wao ni watu makini na wanajuanini wanachokifanya kwa hivyo ni jukumu la wateja kujikinga.

Safari hii mteja hana msaada na amekuwa daraja la watu kujipatia utajiri. Katika Tanzania magazeti yetu na TV za umma na binafsi vinashindana kutangaza vyuo ambavyo havitambuliki na NACTE, VETA wala TCU kwa taaluma wanazotoa.

‘Intake’ ya Januari inakuja kwa vyuo vingi vya Ulaya, Amerika na Asia Kusini. Ni wazi kuwa usipokuwa makini utajikuta umeingia katika ‘gogoro’ la kusoma chuo feki.

Makala haya itajaribu kutoa mbinu chache ili uweze kujinasua na mtego wa kuingia gharama za kusoma chuo kisichotambulika.

Mosi ni vyema kufuatilia kila wakati ilikujua mwenendo wa Chuo chako ukoje .Je kinaendelea kutambulika au kimeingizwa katika mkumbo wa vyuo feki?Na hasa unapoenda kusoma Vyuo binafsi nje ya Tanzania.

Kwa mfano Chuo cha Pacific Western University (PWU) ni chuo kilichoanzishwa mwaka 1977, kikiwa na wasomi wengi hodari na walioweza kufikia katika ngazi ya U-profesa na wengine Marais wakiwa wanaheshimika na taasisi kubwa kama IFM na Benki ya Dunia.

Profesa Bingu wa Mutharika, PhD yake ya ‘Development Economics’ kaisomea PWU, mwaka 1984 (fuatilia htt://www.un.org/ecosoc/docs/pdfs/Mutharika.bio.pdf.)

Chuo hiki kilikuja kupoteza hadhi yake pale kilipotoa PhD ya miezi 12!Katika 2006 kwa mmoja kati ya wakurugenzi wa Taasisi ya Marie Currie, taasisi yenye kuheshimika sana Duniani.

Hii haimaanishi kuwa PhD ya Mheshimiwa Rais Bingu wa Mutharika ni feki, hapana kwani Chuo kilipoteza hadhi wakati yeye keshamaliza. Tunachosema hapa ni mwamba yakupasa kufuatilia mwenendo wa shule yako mara kwa mara.

Ni wazi kuwa katika mfumo wa soko huria ukaona kuna rafiki yako ambaye amesoma chuo ‘feki’ akiwa ameajiriwa katika taasisi binafsi. Hili lipo sana, vyeti hivi vinakumbana na ‘kigingi’ pale vinapojaribu kupenya katika taasisi za ‘serikali’Fulani kasoma pale haitakusaidia sana. Utawezaje kutambua kuwa shahada hii au chuo changu ni feki?

Tumeshaonesha hapo juu kuwa, biashara ya Ulimwengu ya vyeti feki inashamirishwa na vyombo vya habari hasa TV, magazeti redio tena ni vyombo vinavyoheshimika.

Chukulia mfano Chuo A unakikuta kinatangaza nafasi za masomo katika gazeti la The Economist, hadhi ya hicho chuo utakichukuliaje?Ni wazi kuwa unaweza ukanasa katika mtego huo.Vivyo hivyo magazeti ya nyumbani kunayanayoshamirisha elimu feki.

Ukiona chuo chako kinatoa elimu chini ya muda uliozoeleka, diploma ya miezi ya sita, PhD ya miezi 12, hapa anza kuwa na shaka!

Fuatilia kama chuo kimesajiliwa na kinatambulika kweli.Tahadhari kuwepo kwa utambulisho kutoka kwa wahusika kunaweza kukupumbuza. Mara nyingi wanatumia nembo za ithibati za kitapeli ambazo wala nazo hazitambuliki.
Kwani mara zote vyuo hivi feki vimekuwa vikijinadi kwa kuweka nembo na ithibati zenye kuthibitishika lakini ukweli wa mambo ni ‘waongo’. Yakupasa kutembelea tovuti za nchi husika za elimu. Na kama unaweza tembelea balozi ya nchi husika kwa taarifa za awali.

Kwa Tanzania kuna taasisi zinazojihusisha na mwenendo mzima wa kuratibu elimu, kuna VETA, NACTE na TCU ni vyema ukatembelea tovuti zao, ama kubisha hodi katika ofisi zao kabla hata hujalipa ada.

Ada pia inaweza kuwa kigezo cha kukustua pia. Vyuo bora na vyenye kuheshimika katika Uingereza kwa mfano kwa ‘elimu’ za kijamii vinaanzia na ada ya paundi 8,500 kwa mwaka kwa wanafunzi wa kimataifa. Ukikuta chini ya hapo, weka shaka!

Hatutaki kusema kuwa bei ndiyo kigezo muhimu lakini pia elimu bora siku hizi inahitaji pia gharama hasa kwa elimu za magharibi. Profesa atakaye fundisha mwanafunzi wa cheti, atafundisha pia kwa PhD na amshahara wake uko pale pale hivyo ada itakuwa juu kwa cheti pia.

Kuwa makini na vyuo vya binafsi. Katika Ulaya na Marekani vyuo vingi vya umma vina majina ya miji husika. Sasa unapokwenda katika vyuo ambavyo vinamajina matamu ya watu, jaribu kutia shaka. Ni wazi kuwa yakupasa kutoamini kila kitu, na hasa siku hizi za utapeli wa kielimu.

Chukua tahadhari na vyuo vinavyotofautiana herufi. Hapa namaanisha kwamba kuna vyuo vinajaribu ‘kukopi’ sasa tofauti ni ndogo tu unaweza kuingia katika mtego wa elimu feki. Kwa mfano Greenwich University hiki ni feki, halisi ni University of Greenwich. Wamecheza na maneno. London School of what what, hawa ni jamaa wanaoiga ukongwe wa London School of Economics kuwa makini!

Kama unaenda kusoma Marekani ni vyema ukatembelea tovuti ya www.edu.gov, huku utakuta mwenendo mzima wa vyuo feki na vyenye hadhi na ‘wameposti’ ili ukasome kwa heri katika vyuo vyenye heshima na thamani ya pesa yako.

Epuka mtego wa taasisi za kidini zinazoendesha vyuo vikuu na hasa Marekani.Taasisi hizi zimeruhusiwa kutoa shahada za elimu za dini, lakini inapokuja kuwa wanatoa shahada nyingine kuwa makini na vyuo hivyo. Vingi ya vyuo hivi vinaanzishwa baada ya kanisa kufunguliwa na ndani ya wiki mbili wanaleta PhD sokoni tofauti na elimu ya dini.
Mara nyingi Serikali ya Marekani imeshindwa kuvibana vyuo hivi lakini ukweli wa mambo vingi havina hadhi.
.
Mapambano ya elimu feki, diploma za miezi sita na PhD za miezi 12 ni vita ya jamii nzima. Vyombo vya habari Tanzania vina nafasi ya kusitisha kukua kwa biashara hii, pasi kujali faida kwao tu, bali pia kujali masilahi ya Tanzania.
Vyombo vya habari kwa sasa vinaangali nani ana elimu feki tu, lakini wao kimsingi wanachangia vijana wa kitanzania kuingia katika mkumbo huo kwa kukubali kutoa matangazo haya.
Matangazo ya vyuo vya Ulaya, Marekani na Asia kusini yamejaa kweli kweli katika magazeti ya Tanzania. Hakuna anayejiuliza kama kweli vyuo hivyo vina hadhi na ithibati katika mfumo wa elimu ya Tanzania.
Tupo kimya. Yatupasa kubadilika, na kubadilika ni kukataa matangazo ya vyuo feki pia katika magazeti yetu. Na si kusubiri wasome wakirudi ndiyo tuanze kuwashambulia.

Hili la kukataa matangazo ya vyuo feki tunaweza, ni vyema tukilifanyi

Sunday, December 20, 2009

Haki inapodumaza ukuaji wa biashara, si haki tena

Katika nchi ‘zinazofaa’ kufanya biashara Duniani Tanzania ni ya 115, kwa mujibu wa rekodi za mwaka jana za Benki ya Dunia. Ni wazi kuwa changamoto hii inasababishwa na mambo mengi ikiwemo hili la kisheria. Tanzania imekuwa ikionekana kuwa ni ‘pagumu’ mno kufanya biashara kwa sababu ya taratibu za kisheria tulizo jiwekea.
Ucheleshwaji wa haki za kisheria imekuwa ni kona moja wapo inayodumaza ukuaji wa biashara katika Tanzania. Tangu nchi kuingia katika mfumo wa uchumi unaoongozwa kwa nguvu za soko, mabadiliko makubwa ya kisheria yamefanywa, na yanaendelea kutekelezwa ikiwemo uanzishwaji wa Mahakama ya Biashara.
Mahakama hii iliyoanzishwa 16, Septemba 1999 kwa msaada wa DANIDA imekuwa ni mwanzo mwema kwa mwenendo wa kutafuta haki za kibiashara katika Tanzania. Makala haya haitajikita katika kona ya kisheria kungalia nini kinatokea huko katika sheria, ila itaangalia masilahi ya kibiashara kwa hatima ya wajasiramali ambao nchi inajitahidi kuwaibua na siku zao zijazao za ukuaji wa biashara kwa Tanzania.
Katika ukanda wa Afrika Mashariki Tanzania inaendelea ‘kuchanua’ kwa ukuaji wa uwekezaji wa mitaji toka nje. Ni wazi kuwa kiu ya mwekezaji yoyote awe wa ndani au wa nje ni kuona kuwa lengo kuu la mtaji linafikiwa. Nalo ni faida.
Ili kufikia dhima hii ‘muda’ ni suala la muhimu. Hakuna biashara isiyoendana na muda kwani hiki ni kiungo muhimu katika ya wateja na mzalishaji bila kujali muda ni wazi kuwa ‘utawachefua’ wateja wako.
Mwanamuziki wa kizaki kipya Farid Kubanda, Fid Q, katika mashairi ya wimbo wa ‘Fid Q’ anaweka wazi kuwa….muda si rafiki wa mwandamu’.Ni muhimu kukimbizana na adui muda katika heka heka za kila siku.Na mara zote ukiachwa nyuma na muda ni majuto, ndiyo maana tunasema kuwa si rafiki wa mwanadamu kwa vile matokeo yake ni ‘mabaya’.
Vivyo hivyo mteja wa mahakama anapopeleka shauri lake mahakamani anategemea kupata suluhu ya suala lake kwa haraka ili akimbizane na muda
Tanzania mambo ni kinyume chake. Wakili na Mkuu wa Idara ya Sheria ya Benki ya NBC 1997 Ltd, Felix Kibodya, anakadiria kuwa kuna zaidi ya bilioni 100 za kitanzania zimekwama katika mikono ya kisheria kwa kesi zilizofunguliwa muda ‘mrefu’ mahakamani.
Hasara inayotokana na kucheleshwa kwa haki mahakamni katika Tanzania haijawahi bado kuwekwa katika tarakimu, na inakadiriwa mara nyingi shauri uchukua kati ya wastani wa miaka 3 na zaidi.
Bilioni 100 ni pesa nyingi sana, niwazi kuwa biashara zilizoathiriwa na ucheleshwaji wa kesi mahakamani ‘zinachechemea’ na kama si kufa kabisa. Unapokuwa na ‘fungu’ kubwa kama hili halizunguki katika mfumo uliowazi wa kibiashara ni wazi kuwa tunayo yaona ni wazi kuwa ni matokeo ya ‘uzubavu’ huu.
Hili la uchelewashaji wa haki nalo linaonekana kuwa kikwazo kwa taasisi za kifedha kukopesha wajasiriamali. Asilimia 4 ya wajasiriamali ndiyo wanaofaidi na mikopo.

Ni wazi kuwa kunauhusiano kati ya taasisi iliyo na kesi nyingi na fedha nyingi zimedumaa kwa kusubiria haki kuwa itapunguza utoaji wa mikopo kwa wateja na hata kuweka masharti magumu.

Mahakama ya Biasahra ilipoanzishwa mwaka 1999, kesi 116 zilifunguliwa, huku Taasisi za kifedha zikiwa ndiyo wateja wakubwa. CRDB pekee ilikuwa na kesi 18. Tunachoweza kujionea ni kuwa kesi zipo nyingi zenye muelekeo wa kibiashara na zitaendelea kufunguliwa mahakamani.
Hapa isieleke kuwa Mahakama ya Bishara haikuwa na kasi katika kupatia suluhu ya baadhi ya mashitaka yaliyo mbele yake. La hasha, takwimu zinaonesha mwaka 2001 kesi 301 zilifunguliwa, 227 zilipatiwa ufumbuzi, 2002 kesi 351 ziliripotiwa na suluhu kwa kesi 243.
Mabadilko ya kisheria ya mwaka 2002 iliifanya mahakama hii kupopekea kesi chache mwaka 2003, kesi 153 tu zilifunguliwa na hoja 242 zilipatiwa suluhu ukijumlisha na ‘viporo’.
Upungufu huu wa kesi ulitokana na mabadilko ya sheria ambayo yalihitaji mashitaka yawe na thamani ya milioni 100 na kuendelea ili uweze kufungua kesi katika kanda hii ya Mahakama.
Kutokana na mabadiliko haya ni wazi kuwa zile zote zilizo chini ya milioni 100 zimelundikana katika makahama za mwanzo na wilaya.
Jitihada za wazi za muhimili huu wa dola wa kuongeza ajira za mahakimu ni za kupongezwa.
Lakini tunahitaji kwenda mbele zaidi na hasa katika kesi za biashara. Kwani muda hausubiri na ni wazi kuwa wajasiriamali wataathirika kwa kukosa haki kwa wakati.
Bilioni 100 ‘kukukaa’ bila kuzunguka ni hatari kwa ukuaji wa biashara katika Tanzania.
Hakuna ajuaye athari za muuza mahindi aliye na kesi mahakamani kwa kukosa mahindi zaidi ya yeye na familia yake. Kidhibiti kinakaa hadi kinaoza wakati kimeshaonekana!Kwa nini kisiuzwe, pesa ikapunguza maumivu kwa mshindi baadaye.

Biashara inahitaji haki kupatikana kwa haraka, ni vyema tukaimarisha mhimili huu wa dola kwa maendeleo ya sekta ya biashara ya Tanzania.
Kucheleweshwa kwa haki kibiashara hakuna mwisho mwema kwa taasisi za kifedha wala ‘mjasiriamali’. Ni vema tukajipanga kuondoa kero ya kuchelewa kwa haki mahakami kwa nia njema.
Jaji Mkuu, Augustino Ramadhani ameliweka wazi hili kuwa ufinyu wa bajeti ni kikwazo kwa sekta hii kuhakikisha haki inapatikan kwa watanzania. Ni wazi kuwa hili linaathiri ukuaji wa mitaji na biashara kwa wajasiriamali katika Tanzania.
Ni vema hili tukalikabili kama nchi na kwa maajaliwa ya uchumi wa nchi yetu.

Saturday, December 12, 2009

SEKTA BINAFSI NA MAJAALIWA YA TANZANIA

Kwa zaidi ya miongo miwili sasa serikali ya Tanzania inajitahidi kila iwezalo kuhimarisha sekta binafasi. Mageuzi ya kiuchumi na mifumo ya kisheria na kiutendaji inafanyika katika kuhakikisha kuwa sekta hii ambayo ni mwajiri mkubwa kwa sasa inkuwa. Kwa hakika sekta binafsi ndiyo muajiri, ndiyo muongozaji wa uchumi wa Tanzania.
Kukua kwa biashara yoyote kinadharia inahitaji kuwepo kwa kuaminiana (trust) kati ya mteja na mtoa huduma bila kusahau kuwa masilahi ya jamii husika yanalindwa. Na hili linatokea hata muuzaji akakupa mzigo wa mamilioni ya shilingi bila hata kusainishana, akiwa na tumaini kuwa utarejesha stahiki yake.
Kuaminiana ndiyo biashara ya leo ya ulimwengu, jaribu kufikira mtu anayenunua gari toka Japan akiwa Nakapanya Masasi kwa kutumia ‘internet’ ameona tu picha na maelezo ya kampuni husika akaamini na kutuma fedha bila ‘woga’ Japan bila hata kusani mkataba akanunua gari akiamini kuwa litatumwa.
Ujenzi wa imani si kazi ya siku moja katika biashara, ni mfululizo wa matukio na utendaji ndiyo yanayoimarisha mawazo ya mteja na kuhisi kuwa analindwa na kuthaminiwa na kampuni husika. Kimsingi zinatia ndani hata kampuni zenyewe zinajiendashaje, kampuni yenye madeni na kesi nyungi mahakamani za kushitakiwa ni wazi kuwa inapoteza imani za wateja.
Wateja wa sekta binafsi katika Tanzania ni watanzania, ambao wamegawanyika katika makundi mawili wateja wa nje(walaji) na wandani (wafanyakazi).Katika Tanzania sekta binafsi pia inaendesha shughuli ambazo zamani zilikuwa zinafanywa na serikali, kama kukusanya kodi, kusanya taka, kuendesha harambee, kutuo elimu mifano inaweza kuwa mingi. Lakini lililowazi ni kwamba sekta hii imechukua nafasi kubwa ya serikali katika maeneo mengi ya kiuchumi katika Tanzania.
Muunganiko huu unatufanya tuone kuwa suala la maendeleo si tena kitu cha ‘kuhodhiwa’ na serikali. Lengo kuu ni kufanikisha maendeleo kwa mtanzania. Swali ni, je mandeleo haya yatapatikana au ni ndoto tu?
Ni muunganiko unaoonesha kuwa bila kudhibitiwa hautakuwa na mwisho mwema. Matokeo mengi yanayotokea sasa katika uchumi wa Tanzania yanatufanya tujiulize hivi kweli sekta binafsi ni mkombozi au kitanzi?
Serikali kwa nia njema inashamirisha sekta hii, kuanzia miaka ya 1990. Uhusiano huu kati ya serikali na sekta binafsi (Public-Private Sector Partinership) kuna maeneo yanatupa wasi wasi!
Hivi karibuni kuliripotiwa kufutwa kwa mkataba wa kukusanya kodi katika ‘stand’ ya ubungo kwa kampuni ya Smart Holdings. Kampuni hii ilikuwa inadai inakusanya milioni moja kwa siku, lakini serikali kupitia Jiji la Dar-es-Salaam leo hii inakusanya milioni 4 kwa siku!
Smart Holdings ‘imeonekana’ tena katika jengo jipya la Machinga Complex kama msimamizi wa makusanyo, wa Jengo hilo. Na taarifa za awali zinaonesha wafanya biashara kupitia umoja wao wameikataa ‘SMART’. Hii ni fedheha.Lakini linalotia uchungu ni taarifa za kukataliwa kwa kampuni iliyoonesha kuwa inaweza kuleta pato la bilioni 1.2!
Lengo ni kupata fedha kwa ajili ya maendeleo vip tena tunakataa dau kubwa tunakubali dogo?Inawezekana ikawa aliyeleta dau kubwa ametia ‘chumvi’ hesabu zake, lakini hili halina nguvu sana katika biashara.
Sekta binafsi inaonekana wazi kuwa ni kichaka cha watu wachache kuja kufaidi jasho la walio wengi bila hata tija kwa pato wanalochuma. Kimsingi huu ni mwanguko wa maadili ya biashara.
Ni wazi kuwa hakuna maadili ya biashara kama hakuna maadili ya umma au ya kijamii. Mwenyekiti wa Jengo la Machinga Complex Iddi Azzan ‘Zungu’ mbunge wa Ilala amekaririwa akiweka wazi kuwa hata kabla jengo halijakamilika kampuni hii imepewa kazi hiyo ya kukusanya ushuru, na lenye kuumiza zaidi bila hata vikao halali vya ‘tenda’ kuketi.Sasa walijuaje kuwa kuna mshindani aliyeleta ‘dau’ bilioni 1.2 amekataliwa!Lisemwalo lipo waswahili wanasema.
Hii ndiyo Tanzania ya leo. Mwenendo kama huu wa kampuni kupewa kazi bila hata vikao halali katika Tanzania umeonekana maeno mengi na hasa katika wilaya. Kuna watu wanakampuni nyingi za mifukoni wakijipa ‘tenda’ za kuendesha kazi za serikali kwa manufaa ya umma lakini hata uwajibikaji hawana.
Hapa ndipo tunapojiuliza majaaliwa ya Tanzania katika nyakati zama za sekta binafsi, wapi sekta hii inatupekela?Isielweke kuwa hatuitaki sekta binafsi ila tunahitaji ‘mbinyo’ (regulations) zaidi katika kuongoza sekta hii kwa manufaa ya watanzania wote.
Sekta binafsi imekuwa ni watu wenye kulia sana kuomba misamaha ya kodi na uwanja huru wa biashara. Lakini lenye kutia hofu ni juu ya mwenendo mzima wa sekta hii hasa katika kulinda na kujali masilahi ya watanzaia.
Matukio ya rushwa na kuongezeka kwa vitendo visivyo vya maadili vimekuwa ni vitu vya kawaida katika mazingira ya biashara ya Tanzania.Hupati akzi kama huna ‘ten percent’ Wakati umefika wa watu walio katika sekta binafsi kujiangalia mara mbili, wanahitaji kuendesha sekta hii kwa manufaa ya Taifa au ni kwa uroho wa kujilimbikizia mali na kuwaacha watanzania wakiwa watumwa daima dumu.
Mpaka leo sekta binafsi inakaata kuongeza mishahara mipya kwa uajanja wa ujanja wa vikao visivyo kwisha. Kuendesha uchumi si kwa ‘maumivu’ ya wafanyakazi. Ni kwa masilahi ya wadau wote. Kampuni inapata faida ya bilioni 26 baada ya kulipa kodi, ‘bonus’ ya mwaka ikitoka kuna wafanyakazi wanapata 2000/= kampuni yenye wafanyakazi 600 tu.
Waziri Mkuu Mizengo Kayanza Pinda hivi karibuni amekaririwa na gazeti moja la kila wiki akiikemea kampuni moja ya Kichina inayojenga barabara ya Arusha hadi Namanga kuwa ulipaji wao wa mishahara midogo ndiyo chanzo cha kukosa wafanya kazi wenye sifa. Kwa hakika hii ndiyo sifa ya sekta binafsi, ni mishahara midogo na malipo ya ‘kujuana’ wanasema huna ‘address utaishia hapo hapo’.
Yanayotendeka huko yanatia uchungu, rafiki yangu yupo katika kampuni moja ananiambia kuwa alikuwa anaongozwa na meneja wa kidato cha nne, naye alikuwa analipwa mshahara mkubwa kuliko yeye ‘graduate’ .
Kampuni zingine zinaheshimika katika Tanzania lakini utakuta watu wake ni ‘vihiyo’ na wanalipwa pesa nyingi ili kuwavunja moyo wahitimu wenye sifa. Mwenendo huu hauna mwisho mwema kwa biashara ya Tanzania na sekta yenyewe kwa ujuma. Kwani mfanyakazi asiyepata motisha hawezi kuwa ‘mbunifu’
Sekta hii kiuchumi ni muhimu lakini tunahitaji kuiangalia mara mbili na kutunga sheria na taratibu zinazoendesha sekta hii kwa uwazi kutoka katika ajira zake, mishahara, marupurupu na stahiki zingine na si kuacha kila kitu kiendeshwe na wao kama wanavyopenda.
Kama wanahitaji misamaha ya kodi ni lazima nao pia waoneshe jinsi wanavyojali wafanyakazi wao na si kupata misamaha huku wakilipa mishahara inayodhalilisha wazawa huku wageni wakilipwa mishahara minono bila tena hata sifa za kielemu kwa nafasi wanaozishikilia.
Hakuna nchi duniani iliyojengwa na wageni wala na watu watoa rushwa na wasiopend maadili. Ni wazi kuwa kiu yetu na matumaini yetu ya kuona sekta binafsi inatupeleka katika nchi ya ‘asali na maziwa’ haitakuwa na maana kama sekta hii itakuwa inaendesha mambo yake kwa stahili ya sasa.
Tujenge mwenendo wa kuaminiana kukosa imani kwa wateja na kukataa kampuni ni wazi kuwa hili ni doa kwa sekta binafsi. Basi yatupasa kujenga imani za wateja kwa vitendo na si ubabaishaji wala rushwa havina mwisho mwema.

Saturday, December 5, 2009

kuhamasisha mitaji toka nje ni 'mbio' za ubora si uwingi

Katika ukanda wa Afrika Mashariki na Afrika kwa ujumla Tanzania inafanya vyema katika kuvutia mitaji toka nje. Ripoti ya UNCTAD ya mwaka 2008 inataja eneo la Afrika Mashariki kuvutia asilimia 4 ya fedha zote zilizoingia Afrika, huku Uganda na Tanzania zikijizolea chumo kubwa. Ila changamoto kubwa ni kupunguza migogoro inayochangiwa na kuvutia mitaji ‘isiyo na ubora’ bali ni kujali ‘uwingi’.
Tanzania sasa ‘inazizima’ na vyombo vya habari kila kukicha vinapambwa na hekaheka za TRL ni vilio na maneno ya kukata tamaa toka kwa wateja(abiria) na wafanyakazi. Ni wazi kuwa hali si shwari, hali ya sintofahamu imetawala lakini lililokubwa ni majaaliwa ya sera zetu katika kuvutia mitaji toka nje(Foreign Direct Investment).
Changamoto hii ya migogoro katika kila ujio wa mwekezaji imekuwa ni ya kawaida sasa nchini, ila wakati wote imekuwa hatujifunzi somo. Ni kwanini migogoro hii kwa kiasi kikubwa inakuwepo katika mitaji(FDI) inayowekezwa na watu kutoka nchi zinazoendelea?
Mbio za kutafuta mitaji tangu zilipoanza katika Tanzania na hasa hizi za pili akiacha zile za miaka ya 1960, imekuwa ni kuangalia wingi tu na si ‘ubora’ wa mitaji. Wakati wote taarifa tunazopewa nikuwa tumeajiri watu wangapi na wala si kama kinachotumika na kampuni husika kina kiachangiaji katika kuinua hali za watanzania ya Tanzania. Manufaa yake ni chanya au hasi.
Mwanazuoni maarufu Profesa Issa Shivji anawaita wawekezaji ‘uchwara’ ni wazi kuwa jamii nzima toka wasomi hadi watu wa kawaida siku hadi siku wanaona FDI na namna tulivyoikumbatia nadharia hii kama mkombozi wetu wa kiuchumi haina mwisho mwema.
Mgogoro wa NBC ambao bado unafukuta ndani kwa ndani ni mwekezaji toka Afrika Kusini, kiwanda cha Sukari Mtibwa ni ‘mgogoroo’ kati ya Mwekezaji toka ‘Mauritius’, Kilombero Sukari ni hao hao toka ‘Afrika Kusini’. Wajasiriamali wanalia hawapati hata nafasi ya kuuza ‘embe’ kila kitu kinatoka ‘Afrika Kusini’ ndiyo mwekezaji aliyechukua hoteli tulizojenga wakati wa Ujamaa anatoka Afrika Kusini!NetGroup Solution walitoka Afrika Kusini na ATCL iliwahi kuwa na ndoa yenye utata na Shirika la Ndege la Afrika Kusini. Hili la sasa la TRL ni mwekezaji toka India.
Hatuna nia ya kusema kuwa wakati umefika kwa kuangalia miradi ambayo inakuja nchini inatoka wapi (origin) lakini kila dalili inaonesha hawa wenzetu wanaokuja katika nchi zetu hawana nia ya kutuona tunaneemeka, wala hawana nia ya kuiona nchi inajikongoja ila ni kuhakikisha wanatafuta ,malighafi’ na ‘masoko’ kwa ajili ya viwanda vyao.
Lazima tutambue kuwa hawa wawekezaji toka nchi zinazoendelea wanamashaka kama yetu na yatupasa kujipanga vizuri kisera na kimaamuzi.Ni wazi kuwa mitaji hii kutoka nchi zinazoendelea ni sawa na kucheza na mtu hatari(Dancing with devil), huku ukiamini labda amebadilika, lakini tunayoyaona nchini ni wazi kuwa uwekezaji huu hauna mwisho mwema.
Tumefika mahali tumegeuzwa soko la bidhaa zao huku sisi tukizalisha malighafi na kuwauzia kwa bei ya ‘kutupa’ kwa faida ya ajira ya watu 500 hadi 1000 tena vibarua wasio na bima wala kitambulisho wakifanya kazi kwa zaidi ya miaka 5!
Mwekezaji atafungua hoteli utapewa takwimu za kuwa anaweza kuajiri watanzania zaidi ya 100 ajira ya moja ya moja kwa moja na 300 ajira ya isiyo moja kwa moja! Mbio hizi hazina mwisho mwema na ndiyo hizo zimetukisha hapa tulipo.Yote haya ni mbio za ‘wingi’(quantity) huku tukikipa kisogo ‘ubora’(quality).
Ni vigumu kutafrisi ubora wa ‘mtaji’ ukawa na tafiri inayoichukua kila nchi,lakini lililokubwa ni kuangalia hali ya maendeleo ya nchi na nini inataka kupata kutokana na huo mtaji (FDI Spillover effects). Kwa mfano Tanzania haihitaji muwekezaji anayekuja kuuza ‘pipi au vyombo’ vya plastiki kama wale Wachina wa Kariakoo, au wale Wahindi wanaozunguka na biskuti duka hadi duka kutafuta mnunuzi wa jumla!
Hizi biashara ni za wazawa, lazima tuweke maeneo ya wageni kuja kuwekeza na wakiwekeza basi kuwe na tija kwa wazawa si kuwekeza katika kiwanda kisha unaleta mahitaji yote kutoka katika nchi ‘mama’.
Tunakumbuka jinsi TBL walivyoanza kuagiza chupa za bia kutoka Afrika Kusini mara tu walipochukua kiwanda huku tunakiwanda cha KIOO hali ambayo ilisababisha watanzania kukosa kazi, hadi leo hii mambo yamebadilika lakini baada ya vuta ni kuvute.Hali pia inatia matumaini kwa wakulima wa shayiri mkoani Arusha ambao wamepata nafasi ya kuuza malighafi yao kwa TBL huku wakihimarishwa katika kulima shayiri bora, hii ndiyo mitaji yenye ubora kwa nchi (positive spillover of FDI).Lakini hali si kwa viwanda vyote nchini.
Sasa tunalia na kiwanda cha betri cha Yuasa kilichopo vingunguti, kimefungwa kisa kuna mwekezaji anaagiza betri kutoka Uchina na Thailand. Tumegeuzwa soko huku kiwanda tunacho. Sasa wale vijana tunaowasomesha uhandisi na ufundi michundo huku tukiimiza wapende sayansi na tukiwalipia ada kwa asilimia mia watapata kazi wapi kama viwanda vinakufa ‘kibudu’ namna hii! Atalipaje deni lake la mkopo wa elimu kama hana kazi kwa vile kiwanda kimefungwa kwa kujali tu mwekezaji aliyefungua ‘store’ ya kuuza betri za magari toka nje.
Kilio kipo kwa KIBO Match group dhidi ya mwekezaji mjanja mjanja anayejidai anazalisha viberiti kumbe ameweka ghala na anavileta kutoka Pakstani. Huu si ushindani hata kidogo!Vile vile kwa wazalishaji wa makaa ya mawe Mbeya, ambao wakipeleka katika kiwanda cha sementi pale Wazo Hill wanaambiwa hayana ubora hivyo wanaagiza ‘makaa’ ya mawe kutoka Afrika Kusini. Ila tumekosa soko ndani Ujerumani wanasema haya ndiyo bora tena yenyewe. Hii ni ajabu, lakini ndiyo hali halisi.
Hili la kuongeza mbio katika ‘wingi’ tukiacha kuweka mkazo katika ‘ubora’ limepelekea kuibuka tatizo la uwekezaji ambao haufanani na kile walichokisema wakati wa kutia saini kwa mbwembwe za miali ya kamera na ‘champagne’. Hili la kukosa ‘ubora’ ni kero hasa kwa mitaji toka nchi zinazoendelea.
Kwa mfano Brookside wasindikaji wa maziwa ambao wapo Kenya wakiendesha kiwanda cha usindikaji wa maziwa na bidhaa zake. Mwaka 2007 walikuja Tanzania wakanunua kiwanda cha maziwa Arusha kwa ahadi ya kuwekeza zaidi ya dola milioni 20 kwa kiwanda cha UHT chenye uwezo wa kusindika lita 60,000 kwa siku. Baada ya miaka miwili ikabainika kuwa wamegeuza Tanzania kuwa eneo la kukusanya malighafi huku wakipeleka maligahfi hiyo Kenya! Sasa kampuni hii imezuiwa kufanya Tanzania kama ‘shamba la bibi’ na badala yake itimize yale yaliyokuwa yamewaleta.
Huu ni mfano mmoja lakini kampuni nyingi zimekuja nchini kwa ahadi na maneno kede kede ya kuwekeza katika mitaji ambayo ina manufaa kwa nchi badala yake wakaanza kuleta mitumba na kujenga gesti.
Changamoto nyingine ya mitaji hii kutoka nje ambayo inaikabii Tanzania ni hili la kufukuzia mitaji toka katika nchi ambazo zinaongoza kwa rushwa. Kenya, Nigeria zinawekeza katika Tanzania lakini hizi nchi zinatajwa kuwa zinaongoza kwa rushwa. Sasa unapokuwa na mwekezaji ambaye asili yake ametokea katika rushwa ndiyo yale yale kila ‘skendo’ mbili moja ni mwekezaji anatoka katika nchi zinazoendelea. Hii inadumaza ubora wa mitaji katika kufikia lengo.
Rushwa ni adui wa haki hivyo yule aliyekuwa makini na mwenye sifa hakupewa kapewa mtoa rushwa, kila siku ni vurugu na hatutaki kila kona badla ya kuchapa kazi kwani hana mtaji ana maneno. Haya ndiyo majaaliwa ya rushwa.
Katika siku za mwanzo za uhuru wake Kenya alichagua kuwabana wawekezaji toka nje na kuwaonesha maeno ya kuwekeza na si kila eneo walipewa nafasi. Wawekezaji hawakuruhusiwa kuwekeza katika maeneo ambayo wazawa waliweza na hili lilifanyika bila kificho. Leo hii Tanzania inaugulia namna ya kuwabana wawekezaji wanauza matufaa na vyombo vya plastiki mitaa ya kariakoo.
Nchi zisizokuwa na rushwa yenye kukera ndizo zinazopendwa sasa sisi kwa nini tusiamue kuwakataa hawa watu wanokuja kuwekeza kwetu kutoka maeneo ambayo rushwa ni tatizo. Matatizo yake ndiyo hayo Waziri Mustapha Mkulo amekiri wazi kuwa rushwa ni ngumu kuisha katika Tanzania na serikali haiiwezi, sasa kama jibu ndilo hilo haki za wafanyakazi na ubora wa mwekezaji utaupata wapi?
Katika siku za mwanzo za uongozi wake Mkuu wa Mkoa wa Dar-Es-Salaam William Lukuvi aliweka bayana kuwa atapambana na wamachina ambao ni ‘wamachinga’ katika mitaa ya kariakoo, lakini hadi leo hali ya mambo ni ngumu.
Mitaji yenye ‘ubora’ ni suala la kisera pia si suala la maneno ‘matamu’ yasiyoongozwa na kanuni wala ‘miongozo’.
Tangu ukoloni ilikuwa inajulikana wazi kuwa benki na vyanzo vya fedha vilivyoanzishwa vilikuwa kwa ajili ya matabaka, na ni wazi kuwa waafrika tulikosa kufaidi utamu wa uchumi katika ardhi yetu wenyewe kwa kukosa vyanzo vya kifedha. Hali hii iliendelea katika siku za mwanzo za Uhuru hadi pale tulipotaifisha taasisi hizi kuwa za taifa. Lakini leo hii hali ile ile imejirudia mtanzania hakopesheki, ila mgeni anakuja na dola moja anarudi na mtaji kwao.
Kilio cha kuwa hatukopesheki ni dhidi ya benki nyingi zenye asili ya India, Kenya na Afrika Kusini. Ni wazi kuwa mitaji hii imewekwa ili kuwanufaisha binamu zao wanaofanya biashara nchini! Kati ya watu waliokuwa katika jopo la kushauri juu ya kuuzwa kwa NBC kwa ABSA, Wakili Nimrod Mkono amekiri kupitia vyombo vya habari kuwa walifanya kosa kuiuza NBC kwa dola milioni 15!
Hili linawezekana kwa vile wao ndiyo wanamiliki mitaji na maduka ya kuuza mitaji yaani benki,hivyo mitaji kama hii haina maana wala tija kwa Tanzania hata kama ikawa benki zipo na zinachipua kila siku lakini ni za wageni maana yake wanakuja kurahisisha ndugu zao kujipatia mitaji na kuongoza uchumi wetu.
Haya ndiyo makaosa ya FDI bila kujali itakuja kumtumikia nani?Umepokea bila kujali ulikuwa umeweka mawazo katika uwingi.Na ndiyo manaa ukimuuliza mtanzania wa kawaida atakwambia pato la taifa linakuwa lakini haoni manufaa yake, kwa vile hawa waliokuja na mitaji yao wakipata tano yote inaenda kwao kununua matufaa(apple) kuku, nyama ya ngombe. Wakati matufaa yapo Iringa yanaoza. Zaidi ya asimilia 60 ya matunda Tanzania yanaaribikia shambani huku tunaagiza mananasi toka Afrika Kusini mukiyashabikia katika maduka ya Shoprite na Games.Hapa kuna tatizo nalo ni kwamba hatukuangalia ubora.
Shirika la Umoja wa mataifa la UNCTAD linabaisha wazi kuwa senti 75 za kila dola inayoenda Singapore kama mtaji toka nje katika kiwanda cha kufyatua Compact Disc (CD) inabaki humo humo, Afrika ni senti 37 tu. Tena hizi ni Takwimu za Nchi zenye mafuta na zenye uchumi imara miongoni mwa bara hili.
Hali inawezekana ikawa ngumu kwa Tanzania ambayo inaruhusu muwekezaji kukodi ndege kuagiza nyama ya kuku huku kuku wapo wanafugwa Kibaha, ukiuliza wananuka ‘dagaa’! Ohh mara hawana zaidi ya kilo mbili. Mbona ukienda katika supermarket zao utaona wapo wa kuanzia gramu 700 hadi 2500 katika majokofu na wanauzwa bei tofauti tofauti sasa siwachuukuliwe na hawa wawekwe katika mtindo huo huo!Muwekezaji anatupangia sisi nini cha kufanya katika nchi yetu kwa manufaa yake!
Hali inaonesha tunahitaji zaidi mabadiliko ya kisera Tanzania ni yetu leo na vizazi vyetu kesho. Makosa yetu leo kwa hongo zisizo na maana nikikwazo kwa vizazi vijavyo. Sera zetu lazima zioneshe kuwa tunahitaji ‘ubora’ katika FDI na si kuhesabu miradi mwaka huu ni mia kadhaa, haina mwisho mwema.
Shime wenye mamlaka, sasa wakati umefika wa kufikiria zaidi Tanzania kwanza si mpaka mukitoka ofisini ndiyo mnajifanya kujuta kupitia magazeti.
Mungu Ibariki Afrika
Mungu Ibariki Tanzania.

Sunday, November 29, 2009

Kampuni za Tanzania zinahitaji kurudisha sehemu ya faida kwa miradi endelevu

Biashara ulimwenguni kote imekuwa ikipitia katika vipindi tofauti vya kinadharia juu ya masilahi ya wateja. Katika nchi za Magharibi kuna changamoto ya ulinganisho wa faida na manufaa wanayopata jamii husika toka kwa kampuni zinazofanya biashara katika eneo husika.
Wateja hawataki tena kampuni ambazo ni ‘mumiani’ kampuni zinazovuna faida tu bila kujali masilahi ya jamii husika. Tanzania wateja hawana nguvu kama nchi za Ulaya na Marekani ambako kuna vyama imara vya kutetea masilahi ya walaji. Na hili ndilo linafanya kampuni zetu kubweteka.
Hili linafanya kampuni za kitanzania zione ‘wadau’ na hasa walaji ni watu wa kukamuliwa tu, na wala wasiohitaji marejesho ya faida ya kampuni. Ingawa suala la marejesho ya faida kwa jamii ni lenye kuhitjai zaidi muongozo wa bodi ya kurugenzi ya kamapuni husika.Lakini kwa Tanzania kuna matukio yanatufanya tujiulize hivi hizi kampuni zetu zinaamini kweli katika kile inachokisema au ni masihara?
Kuna kampuni ambazo zinajigamba kuwa zinarejesha faida iliyopata kwa wateja na hasa kupita maofisa matukio wao. Na hili limekuwa likitokea hasa wakati wa kutoa zawadi kwa washindi wa ‘kamali’. Sasa hivi katika Tanzania kila kampuni kubwa imejikita katika kuchezesha ‘kamali’ kwa kivuli cha ‘promotion’ za kujishindia zawadi.
Na ndiko huko wanakojificha wakijidai wanarudisha faida kwa jamii! Si kweli kwani kimsingi wachezaji wamechangia wao wenyewe na kampuni nyingi zinakuwa zimejinyakulia faida nono kabla ya ‘draw’ na kama haijavutia wachezaji tumeshuhudia zikisogezwa mbele.Kama kweli ‘promotion’ kwa nini wasogeze mbele draw?
Kuna kampuni moja ya simu ambayo ilichezesha ‘kamali’ yake baada ya kujikusanyia milioni 100 ya faida! Huku wateja wakiambuali vijizawadi vya muda wa maongezi wa kwa mtindo wa kuchangiana wao wenyewe.
Hii si ‘promotion’ kama vile wao wanavyotaka tuamini, kwani sales promotion ni faida kwa mteja kwa kupata huduma au bidhaa kwa bure au chini ya bei ya soko kwa kipindi maalumu.
Isieleweke kuwa hakuna kampuni ambazo hazifanyi na wala hazina juhudi lakini kwa faida zinazochuma mara zote imekuwa hailingani na kile wanachotoa na zimekuwa zile zile kila mara kuna kampuni zingine zinastaajabisha kabisa. Ukizialika katika michango ya ujenzi wa shule utawaona wanatoa mifuko ya sementi tani moja. Huku taarifa za TRA zinasema kampuni imepata faida ya zaidi ya bilioni 20 tena baada ya kulipa kodi!
Ila mara nyingi kampuni zetu zimejikita katika miradi ambayo si yakudumu, na wala haina faida ya muda mrefu kwa jamii husika. Mara nyingi imejikita kufuturisha watanzania wakati wa ramadhani, huku kampuni hizo zikijipatia faida kubwa na wakatia mwingine kutoa zawadi wakati wa Krismasi katika vituo vya kulelea yatima kwa magunia ya mchele na mafuta ya kupikia.
iliandaa harambeee hii miaka miwieli
Kimsingi kamapuni zetu zinahitaji kwenda zaidi ya hapo.Tanzania ya leo inamatatizo mengi na tukiunganisha nguvu zetu tunaweza kufika mbali na si kufanya mambo kwa staili ya ‘kiini’ macho.
Wakati fulani iliwahi kuripotiwa na vyombo vya habari kuwa Waziri Mkuu aliyejiuzuru Mheshimiwa Edward Lowasa aliwahi kukataa michango ya kampuni fulani katika harambee ya kuchangia bweni la wasichana wa Chuo Kikuu Mzumbe. Mzumbe inahitaji kufikia lengo la asilimia hamsini kwa hamsini ya udahili wa wanawake na wanaume.
Hivyo iliandaa harambee hii miaka miwili iliyopita Jijini Dar-Es-Salaaam ,kichekesho ni kwamba kampuni inapata faida ya bilioni 26 baada ya kulipa kodi inatoa machango wa milioni tano kwa mradi wa kuwezesha wanawake wengi kupata elimu ya juu!
Hii ndio hali ya kampuni za Tanzania ni kupenda kutumia nguvu kazi pasi hata kurejesha wala kutolea jasho. Nyingi ya hizi kampuni ndizo waajiri wakubwa lakini hawaweki nguvu hata kidogo katika kuboresha hali ya elimu nchini.
Hii haimaanishi hakuna kampuni ambazo hazijielekezi katika kuboresha hali za watanzania katika miradi ‘endelevu’ zipo kama vile Zain ambayo hutoa ufadhili kwa wanafunzi wa shahada ya kwanza katika fani mbalimbali nchini. Lakini juhudi hizi ni kwa kampuni chache huku zingine wakiwa kama watazamaji au hawajui matatizo ya watanzania. Ila katika kudhamini ‘matamasha’ huko utawaona!
Rais Mstaafu wa Awamu ya Tatu Mzee Benjamin William Mkapa akiwa Uganda katika mahafali ya Chuo Kikuu Makerere ambako alitunukiwa PhD ya heshima ya Sheria amenukuriwa na na vyombo vya habari akiweka bayana kuwa nchi za Ulaya haziweki nguvu katika kufadhili elimu ya juu badala yake zipo katika elimu ya msingi, na hakuna taifa linatakalo ondokana na umasikini kwa kuwa na watu wenye elimu ya msingi bila wa na wataalamu wa elimu ya juu.
Hii ni wazi, upungufu wa udhamini wa elimu ya juu nchini unaweza kupunguzwa na udhamini wa kampuni za ndani kama tukijipanga.
Yatupasa kuweka nguvu katika miradi endelevu kama elimu ya juu kwa kutoa ‘udhamini ‘ kwa wahadhiri pia. Hili linawezekana hebu tuangalie kwa Uchache tuone namana kampuni zetu zinavyotumia pesa katika matangazo.
Mwaka 1997 kampuni za Tanzania zilikuwa zinatumia 1.1 asilimia ya pato la Taifa kwa ajili ya matangazo. Kampuni kumi bora za Tanzania katika matumizi kwa ajili ya matangazo zilitumia bilioni 14.2(2005), 18.9 (2006) na 25.2(2007) ( Advertising Age, Desemba 8, 2007).
Matumizi kwa matangazo ni kwa kampuni zile tu ambazo zimeruhusiwa kufanya matangazo katika Televisheni na Radio acha kampuni kubwa kama TCC watengenezaji wa sigara ambao sheria inawabana kutumia rediao na TV wao wanatumia mabango na udhamini wa matamasha.
Matumizi haya kwa ajili ya matangazo kwa makampuni kumi ni wazi kuwa kampuni zetu zinapata faida kubwa, lakini hazirejeshi hata chembe ndogo kwa jamii ya kitanzania kwa uwiano unaolingana na hasa miradi endelevu.
Ulinganisho haupo katika kurudisha faida kwa miradi ya jamii, na badala yake wakitoa mchele utaona jinsi wanavyojitangaza katika redio na televisheni! Si sawa kwani matangazo hayafanani na faida wanayopata au kurusha kipindi maalum.
Kama nchi tumekosa cha kuzifanya kampuni hizi na ndiyo maana zinapata faida kubwa bila hata kujali sehemu ya jamii. Tuangalie mfano mdogo tu ambao unaonesha jinsi kampuni zetu zilivyolala katika kupeleka faida kwa jamii husika.
Ukipita katika barabara ya Alli Hassan Mwinyi utaona abiria wapo juani pembeni kuna Ofisi za kampuni kubwa na zenye kuheshimika kwa jamii ya kitanzania. Hiki ni kituoa cha daladala kampuni zimeshindwa walau kuweka kibanda cha abiria kujisitiri kwa jua na mvua.
Sasa hivi Krismas inakuja utaoana kampuni zetu ndogo na kubwa zinavyoshindana kutoa zawadi za mbuzi na mchele kwa mafuta ya kupikia. Kimsingi hatupingi zawadi hizi, lakini matatizo ya watoto hawa si kula ya siku moja au pilau, wengi wao wanahitaji elimu jitokezeni mulipie karo za watoto hawa na si kuvizia ‘picha’ Mifano ipo mingi kampuni kubwa na zenye kuheshimika mbele ya ofisi zao abiria wanakaa juani na wananyeshewa mvua wakati wa masika bila hata kujali sehemu hii ya jamii na wakati mwingine hawa na wateja wao.
Hii ni mifano midogo lakini inaonesha jinsi kampuni zetu zinavyoona kurudisha chumo lake kwa jamii ni ngumu.
Tanzania ina kabiliwa na changamoto ya kukosa fedha kwa ajili ya tafiti za kitaalamu kwa maendeleo ya nchi. Serikali ndiyo inasema labda itajaribu kuweka fedha zake kwa walau asilimia 0.1 ya bajaeti kwa ajili ya tafiti kwa miaka ijayo ni suala la kusubiri na kuona .
Ila hili ni eneo lingine kampuni zetu zimekaa kimya wala haziinui mkono wala ‘mdomo’ ili kuonesha njia lakini ‘show’ za urembo wanamwaga fedha huku wakishindana kutoa zawadi. Matamasha ya ‘bongo fleva’ wanapigana vikumbo ili waonekane kuwa ndiyo vinara.
Wanashindana kuleta wanamuziki wa magharibi, ni wazi kuwa burudani ni muhimu kwa jamii lakini tutanachekesha kwani mbio zetu kwa mambo ya kupita ni za kasi mno kuliko mambo ya msingi ambayo tumeyapa kisogo.Kampuni inatumia bilioni 5.1 kwa matangazo kwa mwaka ni wazi kuwa inaweza hata kuchangia kwa kiasi kikubwa katika kutoa fedha kwa ajili ya tafiti za kitaalamu zitakazoweza kuinua taifa na kampauni husika pia.
Hakuna taifa lilillopiga hatua duniani bila tafiti na kikubwa ni kwamba hzio tafiti chanzo chake ufadhili kikiwa ni cha ‘ndani’. Na tafiti hizi zikifanywa kwa mazingira ya Tanzania ni wazi kuwa zitapelekea mafanikio kwa kampuni zetu za ndani katika kutumia tafiti hizi kwa urahisi. Lakini hakuna kitu kama hicho badala yake ni miradi ya muda mfupi ndiyo inayopendwa na kushabikiwa na kampuni zetu.
Tafiti zinazofanywa na vyuo vya Magharibi nyingi zinagharimiwa na kampuni zao kwa kuweka pesa katika vyuo na wao wananufaika na matokeo ya tafiti. Huku ndiyo kurudisha ‘chumo’ kwa jamii na si kuchezesha ‘kamali’ alafu munajigamba kuwa munarudisha chumo kwa jamii.
Kampuni zetu zinapata faida ‘nono’ lakini mgao kwa jamii bado ni mdogo yatupasa kubadilika, kwani biashara ni kujali jamii husika kwa miradi endelevu na ‘ujanja ujanja’ na maneno mengi yasiyo na tija na kuhimiza ‘press coverage’ ili muonekane munatoa.
Yatupasa kama nchi kufahamu kuwa tunahitaji kwenda hatua za mbele zaidi ili kutatua matatizo yetu na faida inayochumwa na kamapuni zetu ikitumika vizuri inaweza kuleta mabadilko kwa maisha wa watanzania walio wengi, na si kufadhili ‘burudani’ tu.

Saturday, November 21, 2009

Biashara bila ushirikiano ni bure

Biashara ni mzunguko wa Vita na Amani( War and Peace) lakini yenye kuhitaji kushirikiana na adui yako, Waingereza wanaiita nadharia hii kama (Coopetition), ni muunganiko wa maneno mawili ya Kiingereza Cooperation and Competition. Sina neno zuri la Kiswahili kwa tafrisi ya Coopetition, lakini nitalitumia kama lilivyo.

Coopetition kama nadharia iliibuliwa na Ray Nadal Mkurugenzi wa Novel na kuletwa katika Ulimwengu wa elimu ya biashara na kwa tafiti za Adam M. Brandenburger na Barry J Nalebuff ambao waliandika kitabu kilichoitwa ‘Co-opetition’ na kufanikiwa kuwa miongoni mwa vitabu vilivyouzwa sana duniani katika miaka ya 1997.

Coopetition ni muungano ambao mara nyingi si wa kudumu kati ya kampuni ambazo zipo katika ushindani . Mfano mzuri ni jinsi kampuni za mifumo ya kompyuta zilivyoweza kupeleka sokoni ubunifu wa JAVA uliofanywa na Sun Microsystems, kampuni za IBM, Apple na Netscape ziliungana kwa pamoja.Wapinzani wa nadharia hii huiita 'cartel' lakini katika elimu ya mbinu biashara(Business Strategy) hii ni mbinu bora kwa kueneza ubunifu wenye kukuza ushindani.

Duniani kote nadharia hii inashamiri, katika Tanzania kuna maeneo yanayotia moyo lakini kwa ujumla hali si shwari miongoni mwa wajasiriamali. Kinachonifanya niandike makala haya ni habari za hivi karibuni zinazoonesha wafanyabiashara wa Tanzania kukosa kuuza zabuni katika ‘kampuni’ kubwa ya Barrick Gold Mining ya Shinyanga.

Barrick ni kampuni kubwa inayohitaji kila aina ya bidhaaa huku ikitumia zaidi ya dola milioni 200 za kimarekani kwa mwaka, na hii ni nafasi ya wajasiriamali wetu kuweza kunufaika na uwekezaji wandani. Lakini taarifa za kampuni hii zinasema kuwa hata wale walio karibu na Barick hawanufaiki, na kampuni hii kibiashara.

Hili linachangiwa na wao kutoweza kutumia mawasiliano ya mtandao wa kompyuta wa kampuni hii kuweza kuuza bidhaa na kupata zabuni mbalimbali zinazotangazwa.Hali hii haipo kwa Barick au wafanyabishara wa Shinyanga tu, ni Tanzania nzima.

Wakati fulani iliwahi kuripotiwa kuwa kuna mjasiriamali aliyeshindwa kutimiza masharti ya mteja wake aliyekuwa anahitaji tani 'mia moja' za korosho zilizobanguliwa, hivyo akakosa kutimiza mahitaji ya mteja wake kwa vile alishindwa kushirikiana na wajasiriamali wenzake katika kuishambulia 'tenda'.Ni wazi kuwa mteja aliyevunjwa moyo hawezi kurudi tena!

Hili halikutokea kwa sababu nyingine isipokuwa ni kukosa ufahanmu wa namna ya kuweza 'kushirikiana na kushindana'.
Biashara ni ushindani na ndiyo maana tunasema ni 'vita', lakini hili halifanyi kuwa mfanyabiashara mwenzako awe adui la hasha. Maana yake ni kwamba utabuni na utajaribu kujifunza nini mwenzako anafanya huku mukishirikiana kuleta hali nzuri kwa wateja.

Ni muhimu wafanyabiashara wetu waungane ili kuhakikisha wanawafikia wadau wao kwa ukaribu zaidi na kwa ufanisi. Kuna mifano kama vile muungano wa Vodacom na Zantel, kampuni ya Zantel inatumia minara ya Vodacom, hii haimaanishi kuwa Voda watakosa wateja hapana isipokuwa itaongeza kavereji ya zantel kwa gharama nafuu kwa kampuni zote mbili katika kuhudumia minara yao.
Pia mfano mwingine ni UMOJA ATM za banki DCB, ACCESS BANK, BOA BANK, AKIBA COMMERCIAL na AZANIA BANK.Kwa ktumia msine hizi wameweza kufikisha huduma kwa wateja wao huku 'wakishindana'.
Kuna watanzania wengi waliokuwa wakiipigia chapuo nadharia hii kuingia katika biashara ya Tanzania, kama Vile Mzee Reginald Mengi alipokuwa akihimiza kampuni za simu kutumia minara ya pamoja au warusha matangazo ya Redio na Televisheni. Hili halikufanikiwa sana, kwa sababu ya 'umimi' miongoni mwa wafanyabiashara wa Tanzania.

Wajasiriamali wanashindwa kujitangaza au kufikika kwa vile hawana namna bora za kisasa ambazo mteja au msambazaji anaweza kuwafikia na kufahamu wapi kunahitajika nini?. Hili linaweza kutatuliwa kama wajasiriamali wakiwa na tovuti ya pamoja.

Tovuti ni kitu ambacho kinaweza kutumika na wajasiriamali wadogo, wakati na wakubwa kwa pamoja kwa kuweka bidhaa zao katika tovuti hiyo moja huku wakitumia gharama nafuu kuiendesha pia mteja akifahamu wapi walipo kwa kutembelea tovuti husika.

Mfano mzuri ni Google na eBay ambazo kimsingi zote wakati zinaanza zilikuwa na lengo moja tu kuwa ‘search engine’ huku kampuni zinazofanya biashara zikijiweka mbele kuwa zinakuwa zakwazwa kuonekana mara baada ya 'mtumia mtandao' kutafuta taarifa fulani kama vile ya bidhaa.

Kampuni hizi zilipoungana, sasa hivi miongoni mwa wateja inajulikana kama unataka ‘kuuza’ basi uza na eBay na kama unataka kuongeza wateja’traffic’ katika tovuti yako jiweke na Google. Lakini lililowazi ni kwamba eBay anatumia Google kuongeza traffic, huku 12 asilimia ya wateja wanapitia Google kwanza ili kufika eBay.

Si kama hawana biashara zinazofanana la hasha, eBay ana Skype,Google,ana Gmail/Talk hizi ni kampuni za mawasiliano ya simu kwa kutumia ‘Internet’. eBay ana Paypal, Google ana Forhtcomming.

Taarifa za karibuni zinaonesha wote kunufaika na mapato yao yakiimarika mara baada ya 'kushirikiana' huku 'wakishindana'.
Ukweli ni kwamba ubunifu wa ‘Google’ ni faraja ya eBay, pia ubunifu wa eBay katika biashara yake ni faraja ya Google.

Ndipo tunasema biashara ni Vita na Amani, ….Vita tena Amani ….. ni mzunguko.Coopetition ni kukubali ubunifu wa mwenzako huku nawe ukiboresha kazi yake kwa faida ya wadau. Tupia jicho pia wanamuziki wa ‘Kikongo’ ikiwa Ndombolo, kila mwanamuziki ataitumia hiyo 'staili', bila kujali nani aliianzisha,huku akiweka ‘nakshi’(ubunifu) tofauti na wakwanza, 'Kiwazenza' wote 'kiwazenza'.

Tanzania hali ni tofauti kabisa, Kapteni John Komba amekuja na ‘Achimenengule’ ngoma ya wayao wa Masasi ni mwanamuziki mmoja tu amejaribu kuitumia!

Ni muhimu wafanyabiashara wetu wakajitahidi kufikiria kuungana na kushindana kuliko kukalia ushindani bila ‘kushirikiana’. Ni wazi kuwa ushirikiano ni nyumba ya ubunifu.

Hakuna 'adui' wa 'kudumu' wala 'rafiki' wa kudumu katika biashara, ila cha msingi ni kuimarisha ushirikiano kwa faida ya wadau wote. Na si kuikalia 'tenda' ambayo unajua hauwezi kuitekeleza bila ushirikiano. Wajasiriamali yawapasa kushirikiana ili kusonga mbele, ushindani si vita tu, bali amani pia kwa maana ya kwamba utaweza kunufaika na ubunifu wa adui yako pia.

Friday, November 6, 2009

Stakabadhi ghalani inahitaji ubunifu zaidi na si kusambaza 'woga'(SEHEMU YA PILI)

Soko la mazao la Tanzania tangu kuingia kwa kwa dhana ya soko huria vilio vya wakulima vimesikika kila kona. Hili halina nafasi katika makala haya kwani tunaamini mengi yamezungumzwa. Ila lililowazi ni kwamba tumeonesha jinsi wanunuzi wa korosho walivyokaidi agizo la Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika sehemu ya kwanza ya makala haya.
Tulishaonesha msimamo wetu katika makala yetu kuwa hatukubaliani na mawazo ya waheshimiwa wabunge kufuta stakabadhi ghalani pamoja na changamoto za sasa zilizopo katika zao la korosho.
Hebu tutupie jicho kidogo katika hoja zao mbili ambazo, mosi ni kuwa stakabadhi ghalani ni mfumo wakinyoyaji na pili unawatenaa wakulima wadogo.
Tuanze kwa kubainisha wazi kuwa si kweli kuwa mfumo wa stakabadhi ghalani ni kuwa wakinyonyaji. Isipokuwa ni mfumo ambao kinadharia unaleta uhuru wa kweli kwa wakulima wa nchi hii. Wakulima wa korosho wameshuhudia kulipwa katika mikupuo miwili na maeneo mengine mikupuo mitatu zaidi ya bei ya soko.
Wale waliouza korosho katika msimu wa mwaka jana kuna waliouza kwa kilo 650/= walichukua malipo yao na baadaye walilipwa mafao yao ya nyongeza ambayo baada ya kuuza korosho ilifikia kilo shilingi 800. Hivyo kufanya nyongeza ya zaidi ya shilingi mia kwa kilo.
Katika hali kama hii mkulima amenyonywa nini! Na liliwalowazi wale waliouza katika mtindo wa stakabadi ghalani walipata nafasi ya kujiwekea akiba kwa ajili ya pembejeo, lazima ieleweke watanzania walio wengi na hasa walio vijijini hawafaidi huduma za kibenki, hivyo kupitia stakabadhi ghalani wakulima wanaanza kuhifadhi kipato chao, kama vile mwenye akaunti, kwani hii ni ‘negotiable instrument’ inaweza kuthaminishwa. Hapa tunahitaji ubunifu katika sheria madhubuti katika kuhakikisha benki inapokea stakabadhi kama ‘inventory credit’.
Mfumo huu umeleta neema si katika korsho tu, hata katika kahawa , katika tafiti ya Gideon E. Onumah na Fedelis Temu ya mwaka 2005 katika kahawa na pamba iliyoitwa ‘Reducing Marketing Constraints and Enhancing Producer Income Through Warehouse System’ ilibaini kunufaika kwa wakulima wa Tarakea, Moshi kwa kipato kizuri kwa wanachama wa ushirika wa Tarakea ambao waliuza kahawa kwa kilo 1800/= tofauti na wenzao waliouza kwa mfumo wa soko huria wa kwa kilo 1250/=.
Ushirika hauchagui hivyo hoja ya kuwa mfumo huu unamtenga mkulima mdogo si sahihi. Ila ili mfumo huu usonge mbele unahitaji ushirika imara ambao umeundwa na wakulima wenyewe kwa ridhaa yao.
Mifano inaewza kuwa mingi kama vile IFAD inavyoshuhudia wakulima wa mahindi katika Karatu wanavyonufaika na mpango huu, huku wakiimarisha maisha yao. Mahindi yanauzwa 13,000/= kwa gunia wakati wa mavuno, lakini sasa wakulima wanaweka ghalani, wanuza hadi gunia la kilo mia 26,000/=.
Na lililowazi ni kwamba wengi wa kulima hawa ni wadogo walioungana kupitia ushirika wao kwa hiyari. Na wala hakuna tishio la kumnyonya mkulima mdogo. Sasa hili la kuwa stakabadhi ghalani ni tishio linatoka wapi?
Wataalmu wa biashara ya mazao wanabainisha kuwa mara zote adui mkubwa wa stakabadhi ghalani ni kilimo cha mikataba (Contract farming). Tanzania ina kampuni chache zinazofanya kilimo cha mikataba, kama vile Starbuck tena wapo katika kahawa wilayani Mbinga.
Inawezekana katika nchi yetu kilimo hiki kisiwe tishio kwa sasa ila yatupasa kuangalia namna yakufanya vyote viende kwa pamoja kwani vinamanufaa kwa wakulima wan nchi hii.
Pili upinzani wa stakabadhi ghalani unasababishwa na ‘bush buyers’ na kampuni za kinyonyaji zisizotaka kumuona mkulima anainuka. Hili ndilo lipo sana Tanzania.
Walanguzi wa korosho wapo wengi sana, wanakaa mjini msimu( Mwezi wa Kumi) ukifika kila mmoja na gunia la dagaa wa Mwanza au wa kigoma, chumvi na nguo za kichina au mitumba hujifanya wanauza kwa kubadirisha kwa korosho.
Hawa wananunua kwa kubadilishana ‘barter trade’. Ubaya wa biashara hii hutumia ‘kangomba’ (Ni kopo lenye kuingia kilo mbili na nusu) kubadilisha na mtumba au dagaa wa Mwanza wengi wame neemeka kupitia njia hii siyo rasimi.
Sasa hawa kwa vile ni watu waliokatiwa utamu bila jasho wanaona mwishowao unahatarishwa kwani sasa wakulima wamekombolewa, ndiyo wanaleta vitisho vya kuhamasiha kunyima kura wabunge na vurugu zote zile tulizo ziona katika makala haya sehemu ya kwanza chanzo ni hawa wanununzi wa ‘kangomba’.
Pia kampuni hizi za kihindi za ‘mfukoni’ zinamkono katika kuhimiza kuonekana kwa stakabadhi ghalani si mali kitu. Hizi kampuni zinafanya kazi kwa ‘ujanja ujanja’ Wengi wao kiukweli hawana mtaji, ila kinachotokea ni kwamba wao wanakubali kwenda vijijini na kujifanya wananunuzi kwa walau tofauti ya shilingi 20-100, ambayo wao huchukua kama cha juu. Hii biashara ya udalali imewanufaisha wengi hasa Mtwara Mjini.
Merehemu Profesa Seith Chachage anawaita makuadi wa soko huria. Na hawa nao hufanya kazi kupita mtindo huu wa soko huria kwa kusambaza vitisho.
Makuwadi hawa wanavyofanya ni unyonyaji ambao hauuvumiliki kama unaipenda nchi yako, kuna rafiki zangu walifanya kazi katika kampuni za korosho simulizi zao ni kwamba mkulima anapofika kuna madalali ambao wao wanijifanya ‘kumjua’ tajiri na bila wao ‘hauuzi’, sasa kwa vile mkulima ametoka Kitangari au Nambali hamjui tajiri wa kihindi anamkabidhi huyo ‘dalali’ kazi ya kufuatilia mauzo ya korosho zake.
Anazunguka anakuja na vijana ambao’ wanapiga’ bambo kutathimini ubora wa korosho kisha hudai kuwa ubora uko chini, hivyo hawawezi kununua.Hiki ni kitisho cha wazi. Mkulima amekodi gari na mjini siyo kwao, ataanza ‘kuweweseka’ tayari amekiwsha!
Wanauza korosho kwa bei kubwa na watachukua wao cha juu, kisha mkulima ataambulia maumivu, hawana huruma hata kidogo. Stakabadhi ghalani imewaondoa ndiyo hao ‘wanaugulia’ maumivu kwa kuleta hoja chakavu na hawa nao wananguvu ya kisiasa kwani wengi wao ni wapigaji wa ‘mdomo’ hasa vijiweni, basi wabunge wanajifanya kuleta hoja kuwa mfumo mbovu kumbe kutaka masilahi ‘uchwara’ yasiyo na tija, kwa walio wengi.
Changamoto ya kutolipa kwa wakati tumeshaona jitihada za serikali ilivyofuta madeni ya vyama vya ushirika ili viweze kukopesheka.Hili lilifanyika kwa baadhi ya vyama vya ushirika katika mkoa wa Mtwara na viliweza kupata mikopo kutoka benki ya CRDB. Ni wazi kuwa huu ni uamuzi mgumu na wa hali ya juu, ila yatupasa kwenda zaidi ya hapa.
Yatupasa kuhakikisha vyama vinakuwa na wataalmu wa kutosha, kwani katika ripoti ya mwaka 1967 ya Ushirika (Presidential Inquiry on Cooperative) mkoa wa Mtwara ulioneka kukosa wataalamu wa ushirika na masuala ya fedha. Ingawa muda ni mrefu lakini inawezekana kuwa tatizo hili mpaka leo lipo.
Lakini hili haliwezi kutufanya turudi nyuma. Wabunge lazima wabuni mbinu bora za kuhahakisha viongozi wanapata elimu ya kuweza kuendeleza ushirika katika maeneo yao
Pamoja na faida zake zote stakabadhi ghalani na hasa kwa Tanzania ina changamoto ambazo kimsingi tunapaswa kuzitafutia dawa na kitu kikubwa ni ubunifu.
Changamoto kubwa ni uhifadhi wa mazao, hapa tunazungumzia maghala yetu?Je yana bima? Ikitokea ghala limeshika moto, hatima ya mkulima wetu ikoje?
Kuhifadhi (Storage) ni taaluma, je tunawataalamu na mbinu za kutosha katika uhifadhi wa kisasa?
Nguvu ya stakabadhi tunayo mpatia mkulima wetu inakubalika katika taasisi zetu za kifedha kama ‘negotiable instruments’? Kama hapana tunaboreshaje?Kama ndiyo je uhalali wake ukoje kifedha?Sheria zetu zinasemaje kuhusu inventory credit?
Hatari nyingine ni kughushi (fraud) mara zote stakabadhi ghalani inaambatana na tatizo hili.
Ripoti moja ya Shirika la Umoja la Mataifa linaloshughulika na Chakula (FAO) inasema kama kilimo kinahitaji kuinua maisha na maendeleo kwa walio wengi basi mfumo imara wa mikopo unahitajika, na stakabadhi ghalani ni suluhu ya kudumu kwa wakulima kupata mikopo.
Tukijipanga na kuongeza ubunifu tunaweza.

Friday, October 30, 2009

Stakabadhi ghalani inahitaji ubunifu zaidi na si kusambaza 'woga'(SEHEMU YA KWANZA)

Siku chache zilizopita vyombo vya habari nchini viliripoti hoja ya kupinga kwa stakabadhi ghalani (warehouse receipt) toka kwa wabunge. Miongoni mwa wapinzani wa ‘stakabadhi ghalani’ ni Mheshimiwa Zito Zuberi Kabwe(Kigoma), Mohamed Sinani (Mtwara Mjini), Dustan Mkapa (Nanyumbu),Juma Abdalah Njwayo(Tandahimba) na Rainald Mrope (Masasi), Abdalah Mtutura (Tunduru) na Ibrahim Sanya (Mji Mkongwe).
Hoja yao ni kwamba stakabadhi ghalani ni mfumo wa ‘kinyonyaji’ kwa vile unamkopa mkulima, na kuna wanaodai kuwa mfumo huu ni wa kumtenga mkulima mdogo. Tunakiri kwamba mfumo huu ulipata upinzani mkubwa tangu kuasisiwa mkoani Mtwara.
Lakini upinzani wa safari hii umekuwa ni ‘mkali’ mno.Na linalotia shaka ni kuona kupungua kwa ‘ubunifu’ miongoni mwa viongozi katika kuboresha hali ya biashara ya mazao nchini.
Ubunifu (Innovation) ndiyo msingi mkuu wa mafanikio katika biashara ya ulimwengu wa leo. Biashara haihitaji tena woga,ila inahitaji kujitoa mhanga na kugeuza ‘woga’ kuwa changamoto huku ukifanikiwa kupitiwa changamoto.
Daima changamoto hazikosekani, na kwa mbunifu hizo ndizo chachu za kusonga mbele na si kurudi nyuma wala kukiri ‘kufeli’. Tanzania ya leo inahitaji viongozi wajasiriamali na si waoga ingawa kitu ni kizuri.
Kwa mfano Mheshimiwa Mrope anasema kuwa mkulima anakopwa na hapati malipo kwa wakati, hili linawezekana kutatuliwa tukijapanga na tukiongeza ‘ubunifu’. Hili haliwezi kutufanya kufuta mfumo huu.
Lingine linalotufanye tuone ni ‘uwoga’ wa kisiasa na kupungua kwa ubunifu ni hili la Mheshimiwa Njwayo.Mbunge Juma Abdalah Njwayo alichomewa nyumba yake mwaka juzi kisa alikuwa anatetea mfumo huu,leo hii ‘amebadilika’ hautaki kabisa!Nini kinamfanya mbunge huyu kubadilika ghafla namna hii? Ni kweli kuwa stakabadhi ghalani haifai na ni mfumo wa kinyonyaji kama anavyodai Mheshimiwa Dastan Mkapa?
Hatumaanishi kuwa Mheshimiwa Mbunge Juma Njwayo hakupaswa kubadilika, la hasha, ‘flexibility’ inakubalika katika nadharia za ‘kioungozi’ hasa baada ya kuona mapungufu ya kile ulichokuwa unaamni. Ila nadharia hii ya ‘kubadilika’ kimtizamo imejikita katika kutafuta ‘ukweli’ kabla ya kubadilka.
Hapa hatuzungumzii ukweli wa ‘kisiasa’ eti kwa vile 2010 yaja basi yapasa kusaka imani za wapiga kura. La hasha ni ukweli wa mwenendo wa kibiashara duniani na hasa biashara za mazao na hali ya wakulima wa nchi masikini.
Upinzani kwa mfumo huu wa ununuzi wa korosho haupo bungeni tu. Oktoba mosi mwaka 2007 wakulima wa Tandahimba waliandamana kupinga stakabadhi ghalani. Adnani Mbwana mwenyekiti wa Chama Cha Wakulima wa Korosho Tandahimba alipata hasara ya 1.8 milioni baada ya mikorosho yake kufyekwa.Kisa anaungama katika stakabadhi ghalani!
Naye mwenyekiti wa TANECU, Mbaraka Mjagama ni mhanga wa stakabadhi ghalani kwani nyumba yake ilibomolewa, (soma gazeti la habari leo 22,Oktoba.2007). Wapinga mfumo huu hawakuishia hapo kwani waliongeza kufuri katika maghala ili kudumaza jitihada za kuanza ununuzi wa korosho kupitia mfumo huu.
Mifano inaweza kuwa mingi kwani wanasiasa kama vile katibu Mkuu wa CUF Maalim Seif Sharif Hamad naye alijitokeza kupinga mfumo huu soma gazeti la Tanzania Daima, 22.Oktoba. 2007.
Lenye kustaajabisha ni kwamba wakati Tandahimba wanakebehi na kupinga stakabadhi ‘ghalani’ wakulima wa pamba wanauomba kwa udi na uvumba. Wakulima katika wilaya za Getia na Kahama wanapigia chapuo mfumo huu uende katika pamba!
Mtu makini lazima atajiuliza mara mbili kwa nini korosho waupinge, pamba waulilie! Hawa wapamaba nini kinawafanya waulilie? Jibu rahisi ni kwamba wakulima wa pamba wamechoshwa na ‘kuhujumiwa’.
Tunaweka wazi msimamo wetu kwamba upinzani wa sasa wa stakabadhi ghalani ni kupungua kwa ‘ubunifu’ miongoni mwa viongozi wetu na ni dalili za kueneza hofu bila hata kupitia mwenendo mzima wa biashara ya mazao ya kilimo katika Tanzania.
Hivyo basi makala haya itatupia jicho mfumo huu, umuhimu wake kwa wakulima wa nchi hii, chagamoto zake na kushauri nini kifanyike katika siku za baadae ili kuboresha biashara ya mazao katika Tanzania.
Stakabadhi ghalani (warehouse receipt) ni nini?Si mfumo mpya duniani, wataalamu wa historia ya biashara wanabainisha kuwa ulianza katika Mesopotamia, na ulikua na kushamiri katika Marekani katika karne ya kumi na nane. Sheria ya kwanza imara na madhubuti kuhusu stakabadhi ghalani ilipitishwa katika Marekani mwaka 1916.
Asili ya stakabadhi ghalani ni nini?stakabadhi ghalani hutumika hasa katika kilimo, ni mfumo ambao umeibuliwa ili kuweza kupunguza kuyumba kwa bei ya mazao ya kilimo (price volatility) hasa wakati wa mavuno, na kumsababishia mkulima hasara kubwa na umasikini ambao huwa unamzunguka daima dumu.
Kutokana na kukosa bei ya uhakika wa mazao mara zote kilimo kimekuwa hakikopesheki, na hatari ‘risk’ kwa mikopo ya kilimo imekuwa ni kubwa na mara zote benki zimekuwa zikionesha kisogo sekta hii.
Hili likafanya nadharia ya stakabadhi ghalani kuchipuka Duniani nia ikiwa kumpatia mkulima bei yenye kuridhisha.Mara baada ya kusambaratika kwa jumuiya ya Ki-Soviet nchi za Ulaya Mashariki nazo zilijikuta haziwezi tena kulinda wakulima wake. Nchi kama Bulgaria, Kazakhstani, Hangari, Slovakia na Lithuania ni miongoni mwa vinara wa stakabadhi ghalani na wanaitumia huku wakulima wakineemeka.
Pia wakati wa kudorora kwa bei ya mazao ndiyo ulikuwa wakati wa ‘bush buyers’ walanguzi kujipenyeza na kununua kwa ‘lumbesa’ au ‘kangomba’. Nalo hili stakabadhi ghalani imelidhibiti. Taarifa za karibuni zinaonesha kuhimarika kwa ubora wa korosho.
Kimsingi mkulima hupewa hati mara baada ya kuuza mazao yake kwa ushirika, na malipo ya kati ya asilimia 65-70 hufanyika. Na mara zote sehemu iliyobaki hutegemea mauzo yake kwa wafanya biashara wanaonunua; safari hii hawakutani na mkulima bali ushirika, na si tena gunia moja bali ni tani zilizokusanywa pamoja.
Uwezo kwa kujadili bei umeongezeka kutegemeana na ushirika imara. Ila kubwa zaidi ni kwamba hati ya mauzo yaliyo ghalani ni ‘pesa’. Ina nguvu kama ‘negotiable instruments’ kutegemeana na sheria za nchi husika. Katika nchi zilizoendelea stakabadhi inayotolewa na ghala la serikali ndiyo huwa yenyekuaminika zaidi. Benki ya Dunia inasema hadi miaka kumi wakulima wa nchi za Ulaya Mashariki huweka mazao yao ghalani, huku wakiwinda bei nzuri!
Tafiti fulani iliyofanywa katika Tanzania na Zambia inataja wanunuzi wa mazao( bush buyers) hujipatia faida ya 70 asilimia na huku wakitumia gharama za kuhifadhi kwa 25 asimilia ya bei ya kununulia baada ya muda wa miezi miwili tu toka msimu wa mavuno.
Katika Tanzania stakabadhi ghalani imeingia baada ya upembuzi ya kinifu uliofanywa na Taasisi ya Maliasili( Natural Resource Institute) ya Chuo Kikuu cha Greenwich nchini Uingereza. Tafiti hii ilifanyika katika Zambia na Uganda pia katika miaka ya 1990 na kukamilika mwaka 1997.Na mazao ya kujaribia nadharia hii yalianza kama Kahawa na Korosho. Ndipo fuko la Common Fund for Commodities lilipotoa chagizo la kuundwa kwa stakabadhi ghalani na sheria ya kwanza ilikuwa June 2005 ilifikishwa Bungeni (unaweza kutembelea www.nri.org/project)
Msimu wa ununzi wa korosho wa 2007 ulishuhudia kuanza kwa mfumo huu, ikiwa ni kivuli cha kugoma kwa kampuni za kununua korosho zilizokuwa zinanunua chini ya bei ya makubaliano.
Kampuni hizi zilipinga agizo la Rais Jakaya Kikwete, kampuni sita zilinyang’anywa leseni. Hili la kupinga agizo la Rais ni fedheha kwa nchi, na utatuzi wake lazima uwe wa kisayansi na hapo ndipo ‘stakabadhi ghalani’ inachipuka.
Serikali haikuleta mfumo huu kama ubabaishaji tu, la hasha, kwani ni kilio cha wakulima wenyewe dhidi ya uonevu wa kampuni za ununuzi wa korosho, leo hii inatushangaza kusikia kuwa wawakilishi wa wananchi( wabunge) wanataka kuundoa mfumo huu.
Wanataka kuturudisha wapi? Kule tulikotoka, kwa wafanya biashara wahuni na wevi. Hata kidogo.
Lakini lililowazi ni kwamba tumeona kuwa mfumo huu hauna muda mrefu nchini na unalengo la kumlinda mkulima wa Tanzania. Basi yatupasa kutupia jicho hizo changamoto zinazoletwa na wapinzani wa stakabadhi ghalani pia tutatoa maoni yetu jinsi ya kuzikabili na kuona mifano halisi ya mafanikio ya stakabadhi ghalani si Tanzania tu pia katika nchi za Ulaya Mashariki ambako mfumo huu unatumika pia.

Sunday, October 25, 2009

Mwangwi wa jina batili 'mafua ya nguruwe' na biashara ya minofu ya nguruwe

‘Makosa yamekwishafanyika , na hakuna anayeweza kurudisha imani ya wateja kwa haraka minofu ya nguruwe na hasa ya dola 20 kwa nguruwe….sijui ni nani alileta uzushi huu wa ‘mafua ya nguruwe’, wanalalamika wakulima wa jimbo la Minesota,Marekani jimbo linaloshika nafasi ya tatu katika biashara ya nyama ya nguruwe na bidhaa zake.
Tangu kuibuka kwa ugonjwa huu, vyombo vya habari na wataalamu wa afya duniani wamejikuta wakiuita kwa jina ambalo wakulima na wataalamu wa magonjwa ya wanyama hawakubaliani nalo, nalo ni ‘mafua ya nguruwe’ (Swine Flu).
Lililowazi ni kwamba imani ya walaji hasa wa Ulaya imepungua tangu kutokea kwa kosa la kuuita ugonjwa huu ‘mafua ya nguruwe’.
Watu wengi wamepoteza maisha katika zaidi ya nchi 24 duniani. Ikiwa inakadiriwa watu 1000 wamefariki katika Marekani pekee, na kumfanya Rais Barack Obama kutangaza hali ya hatari, nia ikiwa kupunguza urasimu wa kisheria katika kutoa tiba kwa wagonjwa.
Mexico ni nchi ya kwanza kukumbwa na ugonjwa huu, ikiwa siku tatu kabla ya ujio wa Rais Barack Obama aliyetembelea nchi hiyo kwa nusu siku 16,April,2009, mtu ambaye alishikana naye mikono na kumuongoza katika maeneo ya makumbusho, mkurugenzi wa mambo ya kale na makumbusho (National Anthropology Museum) Felipe Solis, alifariki wiki moja baada ya tukio hilo, linaandika gazeti la Daily Mail la Uingereza.
Ingawa White House iliwahi kubainisha kuwa afya ya Rais i salama na hilo walilizangatia kabla hajafanya ziara hiyo, nayo serikali ya Mexico kukanusha kuwa Felipe Solis hajafariki kwa mafua ya nguruwe, lakini vyombo vya habari na jamii ya Mexico inaamini dalili zote zilikuwa wazi hadi kifo chake kuwa ni AH1N1.
Pamoja na vifo vingi vinavyotokana na ugonjwa huu duniani malalamiko ya wakulima wa nguruwe ni dhidi ya jina hili na hasa kuhusianisha moja moja kwa na nguruwe.
Shirika la Afya Duniani (WHO) limesema litaacha kuuita ugonjwa huu ‘mafua ya nguruwe’ ili kukwepa madhila ya makosa ya jina kwa biashara ya nguruwe duniani.
Nchini Tanzania taarifa ya karibuni ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya iliyosambazwa kwa vyombo vya habari na Mheshimwa Blandina Nyoni, iliendeleza kutumia jina ‘mafua ya nguruwe’.
Ingwa katika taarifa ile iliyopatatikana kulikuwa na maneno yenye kutia moyo kuwa ugonjwa huu hautokani na ‘kula nyama’ ya nguruwe. Lakini maneno haya hayakupewa uzito na vyombo vya habari.
Waatalamu wa biashara wanasema ‘mpe mbwa jina baya’ (Give a dog bad name) wakimaanisha katika ‘branding’ kosa likifanyika na jamii ikaamini katika hilo, lazima kazi ya ziada ifanyike ili kurudisha imani ya walaji.Hivyo umakini unahitajika sana katika kutoa jina.Nyama ya nguruwe sasa imepewa jina baya, tena ambalo hata haliusiki nalo kisayansi.
Watanzania ni mashahidi na bado tunakumbuka jinsi Mzee Yusuph Makamba alivyokauka koo kujaribu kurudisha imani ya wavaaji wa ndala zilizopewa jina masihala la ‘yebo yebo’ wakati akiwa Mkuu wa Mkoa wa Daresalaam. Kuna waliopigana na kujeruhiwa na wengine kuripotiwa kupoteza uhai kisa jina baya la ‘yebo yebo’
Hakuna anayejua madhala ya ndala zile za kwa kiwanda husika, lakini zile ndala ni zinazopendwa katika Ulaya na Uchina na hasa kwa maeneo ya baharini. Lakini katika Tanzania si mali kitu, na ni fedheha kwa mavaaji. Hii yote inaonesha uhusiano wa jina baya na imani ya mlaji.
Nguruwe ni nyama nyeupe ambayo katika soko la Ulaya na Marekani ni nyama pendwa kwa sababu za kiafaya ukilinganisha na nyama nyekundu.Ni wazi kuwa imani ya walaji nyama nyeupe katika soko la Ulaya, Amerika ambako walaji nyama wameonesha kuacha kula nyama nyekundu (ng’ombe na kondoo) sasa wataanza kula nyama nyeupe nyingine tofauti na nguruwe, yaaani kuku ambayo ilipigwa mweleka na ‘mafua ya ndege’!
Hili si sana kwa walaji wa Afrika, kwani walaji wa nyama wa ulaya hawataki kula nyama nyekundu kwa sababu za kiafya, na ni wazi kuwa mauzo ya mboaga za asilia (organic vegetable) zitapata nafasi kubwa kutokana na makosa haya ya ‘jina baya’ kwa nguruwe.
Profesa Marie Grammer wa Chuo Kikuu cha Minnesota, nchini Marekani ambaye pia mtaalamu wa magonjwa ya nguruwe anasema kitaalamu hakuna uhusiano wa wazi kati ya minofu ya nguruwe na bidhaa zake na H1N1. Isipokuwa ugonjwa unaotokana na muingiliano kati ya binadamu na wanyama.
Na wala ugonjwa hauwezi kuambukizwa kwa kula nyama ‘iliyoandaliwa vizuri’ au mazao mengine ya nguruwe.
Maneno vizuri yanabainisha hali ya usalama, hivyo pasi na usafi kuzingatiwa ni wazi kuwa nyama ya nguruwe inaweza kuwa hatari!
Kituo cha kupambana na magonjwa ya kuambukiza cha Marekani kinasema virusi vinavyoleta magonjwa kwa nguruwe ni ,A influenza, na wala hakuna uhusiano na H1N1 na nguruwe hivyo kutaka makosa ya jina yasahihishwe.
Tangu rai ya kuomba kubadilishwa makosa haya mara tu ugonjwa huu ulipojitokeza mwezi Aprili nchini Mexico, bado jina hili limeendelea kutumika na vyobmo vya habari nchini Tanzania na Dunia kwa ujumla.
Ingawa takwimu hazipo wazi ni kwa kiasi gani biashara ya nyama ya nguruwe ilivyo na manufaa lakini ukweli ni kwamba, kuna jamii nyingi katika mikoa ya Mbeya, Morogoro,Arusha,Iringa,Sumbawanga,Kilimanjaro, Morogoro na Daresalaam wameathirika na wanaendelea kuathirka kutokana na hofu hii kwa walaji.
Daresalaam ni soko kuu la nyama ya nguruwe maarufu kama ‘kitimoto’ambayo sasa katika miji na vitongoji vingi vya kibiashara nchini ni rahisi kukuta mabanda ya kuchoma nyama ya nguruwe. Basi yatupasa kurekebisha kuita ‘jina sahihi’ maana hofu tunayoijenga haina mwisho mwema kwa jamii ya wafugaji wa nguruwe.

Friday, October 23, 2009

Kuelekea usawa tunahitaji tahadhari

Siku za karibuni katika mikutano,makongamano,semina na warsha mbalimbali watu mashuhuri wamesikika wakiweka wazi ya kuwa nafasi za ushiriki wa wanawake katika bunge zinahitajika kuongezeka hadi kufikia asilimia 50.

Taasisi moja ya wanaharakati wanaojihusisha na mabadiliko katika jamii ya kitanzania wakati wa maandamano yaliyokuwa yameaandaliwa kwa kumpongeza Dk. Asha Rose Migiro ambaye kwa sasa ni Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa iliweka wazi juu ya kuhimiza kuongezwa kwa nafasi za wanawake hadi kufikia 50% katika nyumba za maamuzi.

Gazeti la Mtanzania la siku ya ijumaa tarehe 9 machi mwaka 2008 likimnukuu Waziri wa Maendeleo ya Jamii,Jinsia na Watoto; Mheshimiwa Sophia Simba liliandika kuwa nyongeza ya nafasi za wanawake bungeni ni lazima kufikia hamsini asilimia.

Hili la nyongeza ya wanawake katika bunge ni suala ambalo halina ubishi na ni la kupigiwa chapuo katika jamii ya watanzania katika kuona wanawake walioachwa nyuma kwa muda mrefu katika mchakato wa kupigania maendeleo ya nchi hii wanashiriki vilivyo katika kila harakati.

Jamii ya watanzania wanaona na kusikia ndugu zetu wa kike wakionewa,wakinyanyaswa na kudharauliwa kwa vile tu ni wanawake. Kwa ujumla wanawake ni wa watu wanaataabika katika kila jambo linaloihusu jamii yetu hii.

Hivyo kufanya nia yoyote itakayo pelekea mabadiliko yatakayo lipa nafasi kundi hili kubwa la watu katika idadi ya watanzania ambao wanakisiwa kuwa zaidi ya nusu ya watanzania wote kuwa ni jambo la lazima. Hili ni kwa mantiki ya ujenzi wa Tanzania yenye neema.

Hakuna anayeweza kulipa gharama za mateso na manyanyaso wanayokutana nayo wanawake katika juhudi zao za kila siku kwa leo hii katika Tanzania.Ingawa ni wazi kuwa hali hii ya kuwaweka nyuma wanawake katika kila jambo ni suala lililo na asili toka enzi za ukoloni. Kutokana na ukweli huoa 'affirmative action' kuelekea usawa katika jamii yetu kuwa ni jambo la maana na kuhimizwa kwa nguvu zote.

Ila katika kitimiza nia hii itakayosaidia katika kupunguza makosa yaliyotokea muda mrefu katika jamii yetu nilaizma tahadhari kuchukuliwa hasa kwa kufahamu ukweli kuwa kundi lililonyuma katika Tanzania ya leo si wanawake tu.

Kuna walemavu,vijana na masikini,Hivyo basi katika kutimiza lengo hili la nafasi za upendeleo ni lazima tujiridhishe kwa kuangalia pia hao wanawake wanaoingia katika nafasi hizo za upendeleo wasiwe tu toka katika kundi lilelile la jamii iliyokwisha 'nufaika'.

Ukweli lazima uwekwe wazi katika hii asilimia 50% wanawake vijana watakuwa asilimia ngapi? Uwakilishi wa wanawake walemavu utakuwa wa asilimia ngapi?

Pia hili nalo ni la kujiuliza pia katika wanawake hao,wanawake wa 'KIISLAMU' watakuwa wangapi? Hili ni jambo la wazi na wala si kwa ushabiki tu. Uwakilishi huu lazima uwe unaochukua watu wa kutoka makundi yote katika jamii.

Basi nia hii lazima iweke wazi juu ya ushiriki wa makundi yaliyo achwa nyuma kwa kipindi kirefu miongoni mwa wanawake. Na wala isije ikawa mwisho wa safari tunaona sura zile zile katika,uongozi huo. Huu hautakuwa 'usawa' kwa maana pana ya usawa ni lazima tuweke wazi hili mapema. kwani leo pia tunapigia chapuo lakini wakati ukifika utaona majina yale yale yanapita.

Kwani tusipokuwa wakweli unaweza kuona nafasi hizi zikiongezeka wakipata wake wa wakubwa na watoto wao.Tena walio nz umri mkubwa huku ushiriki wa vijana ukiachwa kando.

Pia tahadhzri inahitajika kwani 'affirmative action' katika kuelekea usawa si kufikia 'idadi' fulani la hasha; bali kujiridhisha kuwa watu hao walio nje ya mfumo kwa muda mrefu wana sifa na kweli wameandaliwa kuchukua majukumu hayo.

Kwa mfano hauwezi kupigia kelele kwamba itungwe sheria inayohitaji ofisi ziwe za serikali au binafsi ziwe zinaajiri wanawake kwa asilimia fulani bila kwanza kuhakikisha kuwa wanawake wenyewewe wana ujuzi huo.Au kusema tu kila ofisi inakuwa inaajiri walemavu kwa idadi fulani bila kwanzn kuwa na maandalizi ya kuwapa ujuzi hao wanaotakiwa kuchukua nafasi hizo hivyo basi kufanya kila linalo amriwa kuwa halina maana.

Mchungaji Jesse Jackson katika waraka wake kwa vyombo vya habari wa mwaka 1995; alioupa jina 'Affirming Affrimative Action', anasema hatua za upendeleo katika jamii siyo 'quotas'- Kwa kuzingatia ukweli; utakuwa uvunjaji wa sheria kumpendelea asiye na sifa dhidi ya aliye na sifa. Kile 'affirmative action' inatupatia ni kutumia kwa malengo na dira ili kushirikisha nguvu kubwa zaidi ya jeshi katika kufanya kazi ( Tafsiri ni yangu)

Nchini kwa sasa juhudi zozote za kuelekea usawa hasa katika kupata kazi na nafasi za uwakilishi katika mabaraza mbalimbali ya kutoa maamuzi hayaweki wazi ni asilimia ngapi ya watu wanao wakilisha makundi ya kijamii ambayo yalinyanyasika na wanaendelea na mataabilko wanahitajika.

Yatupasa kuwa wakeli kuwa nasafi za upendeleo ziwe kwa wale waliokosa nafasi na si waliokwwisha 'neemeka' kutumia njia hii kuendeleza, unyonyaji wao usio na tija. Basi tahadhari inahitajika katika kuwaandaa wale walio nyuma kama wanawake kielimu, Chuo Kikuu Mzumbe kimeonesha njia kwa kudahili 50 kwa 5o ya wasichana na wavulana, huu ni mwanzo mwema kuelekea usawa kwa vitendo, na wengine waige!

Je ninaweza kuishi na mtu asiye wa dini yangu?

UTAFITI FULANI UNAONESHA KUNA DINI NA MADHEHEBU YAPATAYO 10000,DUNIANI.AFRIKA PEKEE IKIWA NA DINI 6000.INAKADIRIWA PIA KWA WATU WAZIMA WAPATAO 16% KATIKA KILA NCHI WAMEWAHI KUBADILI DINI,HIVYO KATIKA MAISHA YA KILA SIKU NI KAWAIDA KWA BINADAMU KUKUTANA NA MTU AMBAYE SI DINI YAKE.
LAKINI DINI NI NINI?
DINI INAWEZA KUTAFSIRIWA KAMA MUONGOZO WA MAISHA YA BINADAMU KATIKA NGUVU ZISIZO WEZA KUFIKIKA AU KUONEKANA,YAANI NGUVU ZA ASILI.
KAMA TUKIKUBALIANA NGUVU NI MFUMO UNAOONGOZA MATENDO YALIYO MEMA YA KIBINADAMU BASI UKOMUNISTI NAO PIA WAWEZA KUWA NI DINI!
VIPI KAMA WATU WANAKATA MITI,WANAHARIBU MAZALIA YA SAMAKI KWA UVUVI HARAMU HAWAJALI MAZINGIRA KWA UJUMLA.HAPA MABUDHA WAO WANAONA HIYO SI DINI,WANASEMA "IWEJE DINI IONE KUFANYA MAPENZI NI DHAMBI LAKINI KUHARIBU MAZINGIRA SI DHAMBI"
KWA NAMNA YOYOTE ITAKAVYOKUWA DINI TAFSIRI YAKE LAZIMA ITIE NDANI MUONGOZO UNAOELEKEZA MATAKWA YA WATU KATIKA KUTENDA MATENDO MEMA.
HIVYO BASI NI KAWAIDA KUONA KATIKA UKOO KUWA NA WATU WA DINI TOFAUTI.
HALI YA ULIMWENGU
UGAIDI,VITA VYA KIDINI NA MACHAFUKO YA AINA MBALIMBALI YANAKUFANYA UCHUKIE WATU WA DINI NYINGINE?
MKRISTO UNATAKIWA UISHI VIP?NINI MAONI YA BIBLIA KUHUSU KUISHI NA WATU WA DINI NYINGINE?
HUENDA KATI YA WATU AMBAO SI WA DINI YAKO AKAWA NI BABA YAKO AU MAMA YAKO.BIBLIA INASEMA HIVI ....MHESHIMU BABA NA MAMA YAKO;KUTOKA.20:12.HAPA BIBLIA HAITAJI HUYO MZAZI WAKO NI WADINI GANI HIVYO BASI,NENO LA MUNGU LILITAMBUA KUWA ULIMWENGU UTAKUWA NA DINI NYINGI KUTOKANA NA MAMLAKA YA YULE MUOVU.FUNDISHO HAPA NI KWAMBA TUWE TAYARI KUISHI NA HESHIMA KWA WATU WA DINI NYINGINE, TUWATENDEA KWA STAHA NA FADHILI.

Ukosefu wa soko la uhakika ni kitanzi kwa ukuaji wa sanaa ya uchongaji

"Tumelalamika katika vikao mbalimbali vya kimkoa kuhusu ukosefu wa soko la vinyago nakuiomba serikali ya mkoa itusaidie;lakini kilio chetu kimekuwa hakisikiki"hayo ni maneno ya Mzee Joseph Rashid Adrea wa kikundi cha Jikwamue;kilichopo katika manispaa ya Mtwara eneo la Magomeni karibu na Kanisa Katoliki la Kristu Mfalme.

Mzee Rashid yupo katika sanaa ya uchongaji wavinyago kwa miaka 40 sasa.Anabainisha kuwa sanaa hii aliyoirithi toka kwa baba yake kwa sasa haina nafasi yakuvutia vijana katika mkoa wa Mtwara;kwa vile watu wengi wanaona hakuna sababu ya kuwapeleka watoto wao kujifunza kitu ambacho hakitaweza kumpatia riziki.

Vinyago vyao vipo katika mitindo tofauti kama 'ujamaa' ambacho ni muunganiko wa watu wengi walio pamoja wakiwawameshikana kwa urefu,'mawingu' huu hauna sura isipokuwa ni maumbo tu ya kitu husika,'nandenga' kwa kiswahili ni shetani,kitashwira inafanana hasa na michoro ya Tinga Tinga,pia huwa wanachonga vinyago vya dini kama misalaba,Yesu na Maria na mingine mingi kutegemeana na matakwa ya mteja.

Mtwara ni miongoni mwa mikoa ambayo inakabiriwa na tatizo la ajira hasa kwa kufahamu kwamba sanaa hii ya uchongaji ingeweza kuondoa kundi kubwa la vijana ambao wapo 'vijiweni' kwa kuwapa ajira lakini ukweli wa mambo haupo hivyo.Mtwara haina viwanda,kilimo ni cha msimu basi soko la uhakika kwa vinyago lingeweza kukomboa wanamtwara toka katika umasikini.

Hali ya kukosekana kwa soko la uhakika haikuwepo katika siku za nyuma kwa wachongaji wa vinyago katika Mtwara. Mzee Rashid aliyeanza sanaa hii mwaka 1966,anasema historia ya ununuzi wa vinyago Mkoani Mtwara ilianzishwa na kasisi wa kikatoliki wa Kijerumani anayemtaja kwa jina moja kuwa aliitwa 'Keki'.

Mjerumani huyu ndiye aliyewafumbua macho kuwa vinyago ni mali katika mkoa wa Mtwara kwenye miaka ya 1968. Keki alipofariki wahindi walichukua nafasi,lakini walilegalega na hatimaye walishindwa. Katika miaka ya 1976 walianzisha chama chao;Makonde Carving; kilichokuwa kikinunua vinyago katika maeneo mbalimbali ya mkoa huu.Nacho kikafa kibudu!

Hali ilibadilika katika miaka ya 1990 pale kasisi wa kanisa la katoliki la mtakatifu Paulo;Padri Edelfonse (Marehemu) alipojitokeza kununua vinyago kwa kila siku ya alhamisi.Vinyago hivi vilikuwa vikisafirishwa Ulaya na hasa Ujerumani.Lakini Tangu kifo cha kasisi huyu mambo yamekuwa magumu kwao na hali yao ya kipato tangu kifo cha kasisi huyu hali imekuwa ikizorota siku hadi siku.

Ukiacha wanunuzi wa nje wateja wandani wanakuja kununua vinyago lakini si kwa kasi kubwa na wala si wakutegemea. Viongozi mbalimbali hununua vinyago kwao wakitembelea Mtwara.Mzee Rashid anamtaja Jaji Mkuu Mstaafu Banabars Samatta aliwahi kununua vinyagovyake mwaka 2004,pia aliwahi kuweka nakshi katika sebule nyumba ya Waziri wa Usamala wa Raia wa zamani Mzee Bakari Harith Mwapachu.

Mzee Yustin James wa kikundi cha sabasaba katika manispaa ya Mtwara naye anatoa kilio kile kile cha kukosekana kwa soko la vinyago ndiko kunakozidi kuwadidimiza kimaisha. Ujuzi huu wa Mzee Yustin 'amerithi' kwa baba yake mwaka 1968,hali ambayo anasema sasa hivi ni ngumu kumrithisha kijana wake kwani fani hii sasa hivi ni majuto matupu.

Kijana anaona wazi kuwa hakuna unafuu wowote wa maisha atakaoupata kutokana na yeye kuwana ujuzi wa uchongaji hasa akiangalia Mzee wake anavyoteseka kwa kukosa soko la vinyago la uhakika.

Hili la kukosekana kwasoko linaoonekana kufanya kuwa ndiyo mwanzo wa mwisho wa sanaa ya uchongaji wa vinyago vya mpingo mkoani Mtwara na hasa kwa kufahamu wazi kuwa hakuna damu changa inayojifunza sanaa hii kwa sasa tofauti na zamani.

Mzee Rashid anasema umaarufu wa vinyago wa Mtwara haupo Mwenge Dar-Es-Salaam,ila hii ni sanaa ya 'makonde' na utambulisho wa kabila hili nje na ndani ya nchi,basi serkali inapaswa kubuni mbinu bora katika kuhakikisha inaendelezwa.

Msanii Danieli Mkalunde wa kikundi cha saba saba anasema hali ya soko si nzuri kwa sasa huku akitolea mfano wa kuwa walinunua mti wa mpingo mwaka 2004,lakini hadi leo hawajamaliza kuchonga kwa vile hakuna wateja wa sanaa zao.Hili linaonesha wazi kuwa soko la vinyago linazidi kuporomoka kila siku katika Mtwara.

Kilio kingine cha wasanii hawa wa vinyago ni bei ya mti wa mpingo kuwa ni ghali na wao hawaimudu bei ya shilingi 75,000.Nikiwauliza kuwa serikali imeongeza bei ya mpingo,wanasema hawana taarifa lakini lililowazi ni kuwa bei ya zamani ilikuwa inawashinda basi hata hiyo mpya wataweza wageni na kampuni kubwa na si wachongaji wadogo kama wao.

Akiliongelea suala hilo kwa uchungu Mzee Rashid anasema maofisa wa maliasili siku hizi wala hawajali katika kiwanda chake cha Jinasue,kwani walikuwa wanachukua kodi ya shilingi 100,000 kwa mwaka.Anadai aliwahi kuwauliza maofisa hao kuwa wanafanya juhudi za kumkamua ng'ombe ambaye hawafanyi juhudi zozote za kumlisha kwa kumtafutia soko la sanaa zake.

Kwa ujumla wao hawana kipingamiza na kupanda kwa kodi ya mpingo lakini serikali ilipaswa kwanza kuwatafutia soko la uhakika kwa bidhaa zao.Na si kupandisha kodi,kwani kama wao wasanii watashindwa kununua mti wa mpingo huku soko la kazi zao halipo.

Mapendekezo yao ni kuwepo kwa kijiji cha sanaa ya vinyago katika Manispaa ya Mtwara;pia kjiji hicho kiwe na wasanii wengine kama wachoraji;ili kupunguza adha kwa wateja wanaotembelea Mtwara kuweza kununua sanaa zao kwa urahisi kama vile ilivyo kijiji cha makonde Mwenge.

Kwa sasa wasanii hawapo pamoja katika manispaa ya Mtwara hivyo kuwa kero kwa wateja wao kwani hulazimaka kutembea bila uhakika wa kuwakuta wachongaji.

Pia wanatoa changamoto kwa serikali kupitia wizara ya maliasili na utalii kukuza na kuhifadhi sanaa hii ya uchongaji wa vinyago kwa kuwatafutia masoko ya uhakika wachongaji hawa wa mkoa wa Mtwara. Hili lisipopatiwa suluhu sanaa hii iliyolipatia taifa sifa na umaarufu mkubwa Duniani itapotea na wala wasindanganyike na wachongaji wachache wa Mwenge kwani wale wanaowaona Mwenge walifunzwa Mtwara ndipo wakaja huko.

Sasa kama hakuna 'kuni' katika jiko la wasanii hawa litazimika.Na 'kuni' ni kupatikana kwa soko la uhakika kwa wachongaji waliopo Mtwara.Vinyago ni utambulisho wa Mtanzania na kila mgeni mkubwa wa kitaifa nayeingia au kuondoka zawadi ya sanaa ya vinyago imekuwa ikitolewa na Rais, Makamu wa Rais au Waziri Mkuu. Hii ni ishara ya wazi kuwa inaheshima, basi yatupasa kuheshimu pia kazi hii kwa kuwatafutia soko la uhakika wasanii hawa wa Mtwara.

Wednesday, October 21, 2009

Kilimo kwanza na changamoto ya nishati katika chai

Tatizo la nishati katika ‘chai’ changamoto ya KILIMO KWANZA

Takwimu zilizowahi kutolewa na Shirika Kongwe la Umeme Tanzania (TANESCO) baada ya kuibuka mjadala wa ‘tozo’ kubwa kwa ‘unit’ kwa watumiaji, ilikuwa ni ya kujigamba kuwa wateja wa Tanzannia ndiyo wanaokula umeme kwa bei ya chini katika Afrika Mashariki, 0.08 US huku Kenya na Uganda walaji wakitozwa 0.16.
Tanesco walitoa taarifa hizi kupitia Ofisa Uhusiano wa wakatia huo zilizojaa uhakika wa kutatua tatizo la nishati na mara zote zilikuwa ni za kutia matumaini. Pamoja na matumaini hayo yote na bei kuwa ndogo katika ukanda huu bado Tanzania ni nchi yenye watumiaji wachache wa Umeme kwa asilimia 10 ya wananchi wake ndiyo wana umeme.
Katika nchi yenye watu zaidi ya milioni 40 kwa takwimu za 2008 za Benki Kuu ya Dunia, ni wazi kuwa, ukuaji wa sekta nyingine zinazoendana na nishati utabaki kuwa nyuma. Sekta ya viwanda ni moja wapo ambayo inaonekana kuchangia kiasi kidogo katika pato la taifa, na hili ndilo hasa linachangia katika kutufanya tuwe watu wakuuza nje mazao ‘ghafi’.
Ukiwa na mashaka ya upatikanaji wa nishati, niwazi kuwa utakuwa na uwezo mdogo wa kuvutia wawekazaji katika viwanda, hali inayochangia kabisa kudorora kwa kilimo. Nishati ni Viwanda, Viwanda ni Kilimo, basi Kilimo nacho ni Nishati! Uhusiano huu wa wazi unaweza kufanya mnyororo usikamilike endapo mahali popote panalegalega hufanya kukatika kabisa.
Sekta ya Kilimo bado haijaweza kuvutia mitaji toka nje na jitihada nyingi zinafanywa katika kuboresha hali ya wawekezaji katika kilimo ikiwa kubadilisha sheria ya ardhi ili kutoa umiliki wa muda mrefu wa hadi miaka 99. Mageuzi pia yanatokea katika sekta za fedha ili kuchochea mikopo katika kilimo.
Kitaasisi kuna maeneo ya uwekazaji kama EPZ ( Economics Processing Zone) ambayo yanampatia ‘motisha’ mwekezaji ya kufanya biashara kwa miaka kumi bila kutozwa baadhi ya kodi, ikiwa pia anatakiwa kuuza asilimia 80% katika soko la nje. Jitihada zipo nyingi lakini bado tunaendelea kushuhudia asilimia 5 tu ya FDI katika kilimo, na ushiriki wa Tanzania katika AGOA ndiyo unatoa mwanga kamili jinsi ya ugumu wa kukitoa kilimo chetu kilipo bila nishati.
Jitihada za ubinafsishaji bado hazijazaa matunda kwani wengi waliouziwa viwanda wamegeuza ‘maghala’ ya kukusanyia mazao na kuuza nje ya kiwa ghafi, mazao kama korosho bado asilimia 90 inasafirishwa ‘ghafi’ katika masoko ya ASIA na kubanguliwa kisah kuuzwa katika Ulaya, kwa faida nono!
Rais Mstaafu wa awamu ya tatu Mzee Benjamini William Mkapa aliwahi kuwapa changamoto wadau wa korosho wakatika fulani katika kongamano la Kibaha Pwani pale alipokuja na korosho toka Uingereza ambayo haifiki hata robo kilo lakini ikiuzwa kwa zaidi ya dola 4 za Marekani. Hata kama ukisema kwamba katika kila kilo moja ya korosho kuna asilimia 70 ya ‘makapi’ na asilimia 30 ndiyo inayobaki safi kwa kuliwa, niwazi kuwa bei ya kilo 350/= wanayolipwa wakulima wa Newala Tanzania ni ndogo mno!
Hakuna njia nyingine ya kuwakomboa wakulima wetu zaidi ya kuhimiza uwekezaji katika viwanda, vidogo, vya kati na vikubwa, lakini mashaka yakuja na hasa suala la uhaba wa nishati tulio nao!
Hata maoni yako yawe nini, hakuna haja ya kulaumiana tunahitaji mawazo ya pamoja katika kutatua uhaba wa nishati nchini! Gazeti la Mtanzania Daima la tarehe 20.10.2009 linahabari juu ya ‘kukosekan kwa soko la chai’ kwa wakulima wa Milima ya Usambara baada ya kuibuka mgogoro wa ‘msitu’ ambao unatoa kuni kwa ajili ya nishati.
Wakulima ambao wanategemea kiwanda cha Mponde wanapata 6,000, hivyo kufungwa kwa kiwanda hiki ni mashaka kwa familia hizi. Niwazi kuwa ‘steam’ ndiyo teknolojia inayotumika kwa viwanda vingi vya chai vilivyopo mbali na miundo mbinu ya gridi ya Taifa, na si Tanzania tu , Malaysia pia wanatumia kuni, lakini wapo mbioni kubadili na kutumia umeme wa maji.
Chai siyo sawa na ‘tikiti maji’ ambalo linaweza kukaa zaidi ya masaa 24. Chai inahitaji kuvunwa na kufikishwa kiwandani katika kipindi kifupi ndani ya masaa 24 yakizidi tunaongea lugha nyingine.
Tatizo la nishati limeanza tangu 1983 katika Tanzania kwa upande wa viwanda vya Chai, na tangu wakati huo tumeshuhudia viwanda vingi vikigeuka ‘mahame’
Familia ya MULA ndiyo wamiliki wa kiwanda hiki cha Mponde Tanga, lakini pia wanamilki kiwanda cha chai cha Lumbele, kilichopo Iringa ambacho nacho pia kipo katika mgogoro wa kugombea msitu wa nishati ya kuni kwa ajili ya kuendesha mitambo ya chai. Tanga wanagombea na wanakijiji msitu wa ‘SAKARE’ na Iringa ni msitu wa ‘Lyembela’ kwa mujibu wa gazeti la Mtanzania Daima, la 23. Mei, 2008.
Ingawa katika mgogoro wa Iringa kiwanda kilishinda mahakamani katika kesi iliyoendeshwa mahakama ya biashara na kuwa wamiliki halali, mgogoro wa Tanga bado unafukuta na Waziri Mkuu Mizengo Kayanza Pinda, mtoto wa mkulima anaufahamu!
Huu ni mgogoro wa nishati kati ya wakazi na viwanda na safari hii ni kugombea ‘kuni’. Kuni ni mgogoro katika viwanda vingi , hata MeTL kupitia kiwanda chao cha nguo cha Morogoro kilishaingia katika mgogoro huu wa nishati ya kuni, na kutishia uzalishai wake.
Tanzania inazalisha 1% ya chai ya ulimwengu na ni ya nne barani Afrika kwa kuzalisha chai.Nchi kwa sasa ina mkakati wa kuongeza uzalishaji hadi kufikia tani 55,000 kufikia 2013. Chai kwa sasa inaonekana kupanda katika kuingiiza fedha za kigeni Taifa, katika msimu wa 2006-07, dola milioni 39.4 zilikusanywa zikipanda kutoka dola milioni 27 kwa msimu wa 2005-06.
Hili la nishati linaonekana kuwa ‘mwiba’ mkali kwa sekta ndogo ya chai, lazima tujipange kutafuta suluhu kwa wakulima wadogo wapatao 32,000 wanaolima chai nchini na hasa wale walioonesha njia na nia ya kuenda mbele kupitia ushirika.
Basi yatupasa kufahamu kuwa nishati ni changamoto kubwa kwa ‘KILIMO KWANZA’ yatupasa kujipanga kutatua tatizo hili la nishati si kwa chai tu bali viwanda vingine pia. Tuache ‘malumbano’ katika nishati tujipange kama nchi, nani alifanya kosa wapi haina maana kwa sasa, tufikirie kupata nishati kwanza.
Tusipokuwa waangalifu tunaweza kujikuta tumetumia muda mrefu katika kujadili watu na kusahahu kuwa bado tuna tatizo nalo ni nishati.

Monday, October 19, 2009

Uchawi na mafanikio ya biashara katika Tanzania

JE UNAAMINI KAMA UCHAWI UPO?
Gazeti la Mwananchi la tarehe 17 Oktoba, 2009 lina habari ya 'tafrani' katika kiwanda cha JUISI NA MAJI cha MOHAMMED ENTERPRISES kuhusu madai ya 'UCHAWI' dhidi ya Meneja wa kiwanda hicho. Ingawa gazeti halikutaja jina la Meneja, lakini yatupasa kufahamu kuwa kuna jambo kama hilo.
Polisi iliwalazimu kutumia silaha za moto kutawanya wafanyakazi, ni wazi kuwa walichoshwa na hali hii. Madai yao ni kwamba mara zote wamekuwa wakitolewa 'kafara' wafayakazi na wamekuwa wakikumbwa na ugonjwa wa 'kuanguka'.
Kiwanda cha 'OLAM', Mtwara kinacho bangua Korosho matatizo kama haya ya kuanguka kwa wafanyakazi yaliwahi kuripotiwa na kuna wakati 'makumi' waliumia baada ya kukanyagana wakihisi kuna 'dubwana', linawafuata KUWAMALIZA.
Ndiyo hizi ni siku za kafara, na kuabudu katika 'MIUNGU' inayohitaji 'DAMU' kama kafara ili kujiongezea kipato.Katika Biblia neno 'UCHAWI' limetajwa toka enzi za MUSA, YESU na MITUME walikuwa wakikemea kuhusu kushiriki katika UCHAWI.Kitabu kitakatifu cha Biblia kinasema wazi kwamba 'Usimuache mwanamke MCHAWI aishi, je wanawake ndiyo wachawi tu?
Inawezekana kwa namna moja au nyingine kuna wakati ulishindwa kuelewa kama kweli uchawi upo! Na kuna wakati ulikutana na watu wakisema kuwa hawaamini kama uchawi upo. Hata maoni yako yawe nini, suala moja unalopaswa kufahamu ni kwamba UCHAWI upo.
Lililowazi ni kwamba UCHAWI ni nguvu za yule muovu 'SHETANI'. Biblia inasema 'DUNIA' yetu i uwanja wa huyo muovu. La kumbe, tupo katika mji wa muovu, basi ni wazi kuwa UCHAWI unatuzunguka na wao wanataka kutushinda ili tuamini katika 'kushiriki' nao.
Basi kama binadamu yakupasa kuishi maisha yenye neema na kumtumikia 'MUNGU' wako, lakini unaweza kujiuliza kama MUNGU, anakupenda iweje akulete katika Uwanja wa 'SHETANI'?

Fuatilia makala haya itakayotoka hivi karibuni.

Friday, October 16, 2009

Kuuza rasilimali watu nje yahitaji tahadhari

Siku chache zilizopita Waziri wa Afrika Mashariki Didorus Kamala alinukuliwa na vyombo vya habari kuwa Tanzania iko mbioni kuwa na mkakati wa kuuza wataalamu nje ya nchi. Hili ni wazo zuri, kwani wakati wote kuna imani kwamba wale walio nje wataleta walu sehemu ya 'mafao' yao nyumbani ambayo kwa namna moja au nyingine yatainua hali za tulio nyumbani ambako umasikini wa kipato unatumaliza. Pili uzoefu wao katika shughuli za maendeleo tunaweza kuamishia nyumbani(Back Home Era) nasi tukabadili hali zetu pia kwa kuongeza ajira kama vile wakianzisha kampuni.

Ulimwengu unashuhudia mapinduzi ya kisayansi yanayotokea India kwa sasa katika teknolojia ya kompyuta na mawasilinao kwa ujumla, haya yote ni kwa ajili ya vijana waliokuwa uhamishoni na hasa nchi za magharibi kuamua kurudi nyumbani(Back Home Era). Sina hakika kama hili linawezekana kwa watanzania!! Ni suala la kusubiri muda.

Kwa sasa watanzania waliopo nje wanaleta kama dola milioni 14,mafao haya ambayo yakiwekwa katika takwimu za kipesa ni madogo ukilinganisha na jirani zetu kama Uganda dola wanaorudisha milioni 896 takwimu hizi ni za mwaka 2007.Pia yatupasa kushukuru. Yatupasa kufahamu pia kurudisha riziki nyumbani ni hali ya ‘moyo wa mtu’ na fadhila aliyonayo na wala tusiiwekee asilimia mia moja katika hili kuwa hali itabadilika endapo watanzania wengi watakuwa nje ya nchi.
Makala haya inatoa tahadhari ya wazi kuwa haikubaliani na Mheshimiwa Waziri na wazo lake kuwa na mkakati wenye tija na kupigiwa ‘chapuo’ kwa nguvu kwa hali ya sasa ya nchi yetu ilipo. Si kila jambo linalotokea kuwa na faida kwa wenzetu nasi yatupasa kulikimbilia. Hapana, na hasa chapuo katika kuuza madaktari wa tiba.
Nadharia rahisi ya mtu anayeweza 'kuuza'(Seeling) ni yule aliye na ‘ziada’ ( You cannot sell if you don’t have surplus). Swali la kujiuliza Tanzania yetu ya leo ina ziada ya wasomi kiasi nasi kujinasibu kuwa tunataka kuingia katika soko la kuuza rasilimaliwatu nje?

Tukijilinganisha na Uganda tunaweza kutafuta sababu za juu tu bila kupata kiini cha kwa nini hatuna wataalamu wengi nje ya Tanzania. Jibu ni kwamba hatuna watu walio na ujuzi stahili. Uganda leo hii wana tawi la chuo kikuu cha KIU (Kampala International University-Dar Campus). UDSM wakongwe kuliko KIU hawana tawi,Mzumbe wameweka tawi Mbeya. Lakini matawi haya ni ya shahada za kijamii si ya sayansi na hasa Udaktari.

Vyuo vya tiba bado haviajwa na udahili wa wanfunzi wengi nchini ingawa idadi yake kwa sasa ni vitano na hili ni kwa sababu ya gharama, na miundo mbinu hafifu kukizi mahitaji ya vyuo hivyo kuanzishwa nchini.
Tena maeneo ambayo Mheshimiwa anayapigia chapuo ni udaktari wa binadamu na uhandisi!Haya ni maeneo nyeti sana na uhaba wake unatisha. Hatumaanishi kuwa watanzania wasiende nje kutafuta kazi na kujiongezea uzoefu, la hasha ila yatupasa kuwa makini katika kuhakikisha tunaweka nguvu katika maeneo kweli ambayo ‘tunafaida ya kiushindani’.
Gazeti la serikali la Habari Leo la tarehe 16 Oktoba lina habari ya uhaba wa madaktari na wauguzi katika hospitali ya Mirembe iliyopo Dodoma, pia hospitali hiyo inahitaji wauguzi 150! Hospitali hii inapokea watanzania zaidi 6000 ikiwa na uwezo mdogo mno wa kutoa huduma. Napata kigugumizi hivi kweli linalozungumzwa na Mheshimiwa ni hoja iliyo katika wakati muafaka kwa Tanzania ya leo.
Kuna maeneo Tanzania inahitaji kwa hakika kuuza wataalamu wake nje,lakini unauza wakatika unadahili asilimia 2 tu ya watu wenye sifa ya kuingia chuo kikuuu. Natumaini hoja ilipaswa kuwa tunahitaji kuongeza nguvu katika elimu ya juu ili tuweze kuuza wataalamu nje.
Kuna maeneo watanzania yatupasa kuyaangalia kwa ‘jicho la tai’ kwani huko tunauwezo wa kufanya vizuri na si vibaya tukajaribu, kwa mfano walimu wa lugha ya Kiswahili. Tusipoongeza udahili na kujipanga sawasawa tutakuwa wachekeshaji, kwani wale tuliowafunza lugha hii adhimu, sasa ndiyo watang’ara kama wakufunzi. Simaanishi hakuna waswahili wanaowafunza waingereza ‘kiingereza’ ila lazima uwiano uwepo kati ya mwenye ‘chake’ na mdandiaji.
Hali ilivyo sasa wakenya wengi wanasoma Kiswahili na wanahitimu wengi chuo kikuu kuliko watanzania tunavyosoma katika ngazi ya shahada Kiswahili chetu! Hapa kuna tatizo nyumbani lazima tulitatue.
Libya imeweka wazi kuwa lugha ya Kiswahili ni kati ya lugha zinazopaswa kutumika nchini humo lakini hakuna walimu, sasa haya ndiyo maeneo tunayopaswa kuweka nguvu kwani tunafaida mlinganisho nayo na hayatatuathiri kimsingi.
Lakini hili la kuuza madaktari wa binadamu nje ni hatari hasa katika nchi kama yetu ambayo watu bado tunakufa kwa magonjwa yanayotibika kama malaria, tumbo, kifua kikuu.Bado wakina mama wanakufa kwa kukosa huduma nzuri wakati wa kujifungua,MIMBA sasa imekuwa ni kuchungulia kaburi!Mimba si ugonjwa lakini kwa vile hakuna wataalamu ndiyo haya yote, ya 108 katika ya akina mama 10000 Iringa wanakufa kila mwaka. Kila dakika kuna mtoto mchanga wa kitanzania anafariki, kisa yuko mbali na kituo cha afya.
Lindi bado inaongoza kwa vifo vya akina mama wajawazito, bado tushabikie kuuza wataalamu wetu nje si sawa . Sina nia ya kupinga wazo hili yatupasa kuweka nguvu katika maeneo yenye tija kwanza, pili yatupasa kuweka nguvu katika kudahili pia na si kama hali ilivyo sasa kisa dola milioni 14 zinapswa kuongezeka!
Bodi ya mikopo ilikuwa na nia ya kutoa mikopo kwa wanafunzi zaidi ya 60,000, sasa idadi imeshuka hadi 24,000! Ni wazi kuwa mambo si mazuri kwani maelfu wamekosa udhamini si kama hawana sifa la hasha ni uhaba wa fedha. Katika hali kama hii kuna maeneo yatakosa wataalamu, Hivyo kupigia chapuo kuuza wataalamu nje tena wa afya au wahandisi ni hatari.Tena katika nchi ambayo vijana hawapendi tena kusoma masomo ya sayansi licha ya kuwepo udhamini wa asilimia mia moja.
Tusiwe kama wamalawi ambao wataalamu wake wa tiba ilio wasomesha kwa shida na gharama kubwa wapo wengi katika Uingereza kuliko walivyo katika MALAWI nzima, kisa pesa kurudisha nyumbani.
Kimsingi kurudisha hela nyumbani ni moyo wa mtu si kwa vile amewaacha watu nyumbani ndiyo atawapatia chochote kitu.
Mifano mizuri tunayo hapa hapa Tanzania,kuna watu wengi tumesahau wapi tulikotoka mara tu baada ya kuingia katika ofisi zenye kiyoyozi na kuendesha magari ya mikopo ya mitumba kutoka Japan, hatuna fadhila na watu waliotulea na hasa wazazi tunawaacha wakihenyeka katika siku za uzeeni!
Msimamo wetu ni kwamba yatupasa kupima mara mbili zaidi faida ya kipato na madhara ya kushabikia mchakato huu na kuweka nguvu ya kuuza wataalamu wetu nje. Yatupasa kuongeza kwanza nguvu katika udahili kwa elimu ya juu, kisha tuanze na walimu wa kishwahili na si kila sekta ni hatari.

Wednesday, October 14, 2009

Mifumo yetu ya elimu na heka heka za ufadhili wa kimasomo

Waatalamu wa maendeleo na wachumi kwa pamoja wanaungama kwamba kukosekana kwa 'nafasi sawa'(Lack of Opportunities) mara zote ni sababu kubwa inayopelekea kuongezeka kwa umasikini barani Afrika na hasa Kusini mwa jangwa la Sahara.
Mara zote nafasi inapotokea ama iwe inachelewa kuwafikia walengwa, au hata walengwa kukosa taarifa sahihi wapi waanze na wapi waishie ili kufaidi nafasi husika. Kudoda kwa mapesa ya mabilioni kwa mabilioni katika taasisi za kifenda kwa ajili ya mikopo ya wajasiriamali, kushindwa kujitokeza kwa watu wenye sifa katika nafasi mbalimbali za fadhili za kimasomo nakadhalika nimaeneo machache tu yanayoweza kuorodheshwa.
Changamoto kubwa ipo katika mifumo yetu hasa inapokuwa 'hasi' katika kuhakikisha tunafaidi nafasi hizi za ufadhili zinapotokea. Makala haya itatupia jicho mifumo yetu ya elimu nchini Tanzania na jinsi inavyoviza fadhili mbalimbali kwa watanzania nje au ndani ya nchi kwa ajili ya masomo.
Madai ya kuwa watanzania tumeshindwa kutumia nafasi tena wakati mwingine zinakuja kwa anwani ya kwamba mwanafunzi awe wa Tanzania yamesikika mara nyingi. Na lililowazi ni kwamba nafasi hizi ni adimu na zinatokea katika nchi ambayo si kwamba watu wake wanakipato cha kutosha bado tupo katika dola 270 kwa mwaka. Kwa kuzingatia hili nafasi za ufadhili wa kimasomo ni muhimu kwetu, kwani bado idadi ya walio na sifa kushindwa kuendelea na masomo ni kubwa na lenye kuhuzunisha ni kwamba wakati wote pesa imekuwa ndiyo kikwazo.
Swali ni kwani nini tunashindwa kutumia nafasi hizi?Taasisi za elimu ya juu nchini Tanzania mara zote zimekuwa vigingi katika kuelekea kufaidi nafasi hizi za ufadhili. Hili limetokana na jinsi tunavyofanya kazi ama la kuwa 'kizamani' au 'kuamini' kuwa lazima vikao vikaliwe ndiyo jambo fulani liweze kupitishwa.
Mathalani suala la vyeti na taarifa ya maendeleo ya mwanafunzi (transcript) imekuwa kero hasa kwa wahitimu. Maeneo mengine hati hii inahitaji kusaniwa na DVC! Mifumo hii mara zote inaleta 'uzubavu' katika kutumia nafasi. Hatuna tatizo kwa DVC kusaini, lakini kimtizamo naona DVC wakati wote amekuwa na kazi nyingi, na kimsingi yeye hawezi kuwa anamfahamu mwanafunzi zaidi ya watu wa Idara au Mkuu wa fakati husika ya mwanafunzi.
Kuna vyuo hii nikazi ya Mlezi wa fakati na si kazi ya DVC, katika hili utaona ambavyo mambo hayalegi, matokeo yakitoka idarani mwanafunzi anayathitisha yanaenda kwa Dean hati ya matokeo inasainiwa, kijana anapata 'transcript' anaendelea kusubiri cheti huku heka heka za maisha baada ya chuo zikiendelea.Chuo kinachotumia utaratibu huu ni Mzumbe na mara zote wanafunzi wamekuwa wakijiuliza kwa nini vyuo vingine hati zinachelewa pamoja na vyeti lakini si kwa Mzumbe!
Katika ulimwengu wa leo elimu ni 'biashara' chuo kinacho kuwa makini katika kutoa matokeo na kufanikisha kudahili kwa wakati kinapata wanafunzi wengi tena kwa wakati na wale wanaoweza kujilipia pia wanakuwa wanafanya hivyo.
Tanzania ni nchi ambayo kama niliyotangulia kusema mifumo ya elimu inadumaza kutumia nafasi za ufadhili. Nafasi kede kede zinaendelea bila kupata mtu wa kuzitumia, kisa taarifa ya udahili, oooh kikakao cha seneti bado. Elimu ni biashara narudia tena, lazima iendane na matakwa ya wateja.
Hebu tuangalie mifano michahe kuonesha jinsi tulivyokuwa na mifumo mibovu inayotunyima kutumia nafasi za ufadhili katika nchi yetu za kimasomo. BTC (Belgium Techniocal Cooperation)huwa inatangaza nafasi za ufadhili kwa wanafunzi waliopata udahili kwa vyuo vya ndani na ndani ya Afrika Mashariki. Ufadhili huu unakuwa katika ngazi ya shahada ya Uzamili(Masters) na Uzamivu(PhD).
Matangazo haya mara nyingi huwa yanatoka kati ya mwezi wa nne hadi wa tano kwa mwaka husika. Kipindi hiki vyuo vyetu bado havijatangaza kupokea maombi ya udahili kwa mwaka husika. Bado hata vikao vya udahili havijulikani vitakaa lini na tangazo litatoka katika gazeti gani. Mara zote kuanzia mwezi wa sita hadi nane na mwezi wa tisa heka heka za matangazo na udahili zinakuwazimeanza.
Matokeo kutoka ili kufahamu umepata au umekosa ni mwezi wa tiasa hasa.Na ule udhamini unaotolewa na BTC unakuwa unamwisho wa kutuma maombi mara nyingi tarehe zao zinakuwa ni chini ya kuanza kwa kutuma maombi chuoni. Hii inaonesha wazi mifumo 'iliyozeeka' isivyoweza kuwapa nafasi watanzania kutumia neema ya ufadhili katika kujiendeleza kimasomo katika nchi yao wenyewe!
Shirika jingine la Osienala (Friends of Lake Victoria) lenye makao yake Kenya hutoa udhamini kwa wanafunzi wa Afrika Mashariki kusoma katika vyuo vya nchi hizo kwa shahada ya uzamili katika fani za mazingira, maendeleo, biashara nakadhalika, hutoa nafasi hadi mwezi wa tano tarehe 30. Bado kilio kile kile nafasi hii kwa wasomi wa Tanzania hawawezi kuitumia kwani muda wa udahili na vikao vya seneti bado nchini!
Njia hii ya ukale wa kutuma maombi kwa vyuo vyetu ni wazi kuwa inatutoa katika soko la ushindani wa kielimu. Hivi karibuni nimepata fununu kuwa The Open University of Tanzania watakuwa wanapokea maombi kwa mwaka mzima hii ni hatua ya kupongezwa. Na lililowazi sasa yatupasa kutambua kuwa mfumo wa vikao vya seneti umepitwa na wakati katika kuuza elimu.
Njia sahihi ni kuacha idara iangalie wanafunzi inaowahitaji kwani ndiyo walimu na wao wapeleke majina kwa Idara ya Elimu ya Juu (Directorate of Postigraduate Studies) kwa taarifa na kuandikwa kwa barua kwa mwanafunzi husika.Hili haliitaji seneti kwani 'member' wa seneti siyo wote watakao mfundisha mwanafunzi na wala hawana hata utalaamu wa shahada husika, sasa kwanini wao ndiyo wawe na nguvu katika hili?
Katika nchi za Ulaya na Marekani utumaji wa maombi huwa mwaka mzima na mwanafunzi anapaswa ataje anaingia majira gani ya mwaka, na hili linafanya wanafunzi wawe katika nafasi nzuri ya kutafuta wafadhili.Pia maombi hutumwa kwanza katika idara yako. Tanzania inakuwa kinyume chake,nacho hudumaza heka heka za kutafuta ufadhili.
Vyuo vya elimu ya juu lamiza vibadilike, ili kuhakikisha vinauza elimu na si kuendelea kuwa kigingi katika kuwezesha watanzania kufaidi nafasi za ufadhili. Katika zama za mawasiliano ya kompyuta hili linawezekana.
Yatupasa kutumia nafasi hizi kwa kubadili mifumo yetu, simaanishi kuwa hawapo ambao hawajanufaika na BTC lakini wengi wao waliomba na mara zote ni wale wanaojuana na wahusika ndiyo walipata barua za Partial Admission wakisubiri vikao vya seneti , barua hizi ziliwasaidia kupata ufadhili. Sasa hili ndilo linaloleta umasikini kwani nafasi sasa inakuwa si 'sawa kwa wote' ila wale wanaojua kutupa karata tu.
Vikwazo vya kusubiri hati ya maendeleo ya kitaaluma hadi isainiwe na DVC imepitwa na wakati hii ni kazi ya Dean wa Idara husika. Na hasa katika kipindi hiki cha kuuza elimu ambacho mteja anapaswa kukimbizana na muda kwani muda ni pesa na kuchelewa kwake ndiyo hatari yake ya kupata ufadhili na kukosa kwake ni kukosa kwako (CHUO) kuuza elimu.
Huu ni mzunguko hauja mkomoa mwanafunzi hata chuo nacho kipo katika kukosa mapato pia, na hasa inapokuwa huyo mwanafunzi ana sifa stahili za kupata ufadhili. Shime wasomi wakati umefika wa kuondoa vikwazo katika kuuza elimu na hasa katika kuhakikisha tunakwenda sambamba na matakwa ya wateja hasa wafadhili wa kimasomo, na hili ni kuendana na muda wao tu. Tuanze kudahili kwa wakati na jukumu hili liwe la idara husika, pia tuwe na udahili wa mwaka mzima kupitia mtandao.Ili tuweze kuongeza kipato na kupambana na ukata unaosababishwa na bajeti finyu ya serikali.