Friday, October 30, 2009

Stakabadhi ghalani inahitaji ubunifu zaidi na si kusambaza 'woga'(SEHEMU YA KWANZA)

Siku chache zilizopita vyombo vya habari nchini viliripoti hoja ya kupinga kwa stakabadhi ghalani (warehouse receipt) toka kwa wabunge. Miongoni mwa wapinzani wa ‘stakabadhi ghalani’ ni Mheshimiwa Zito Zuberi Kabwe(Kigoma), Mohamed Sinani (Mtwara Mjini), Dustan Mkapa (Nanyumbu),Juma Abdalah Njwayo(Tandahimba) na Rainald Mrope (Masasi), Abdalah Mtutura (Tunduru) na Ibrahim Sanya (Mji Mkongwe).
Hoja yao ni kwamba stakabadhi ghalani ni mfumo wa ‘kinyonyaji’ kwa vile unamkopa mkulima, na kuna wanaodai kuwa mfumo huu ni wa kumtenga mkulima mdogo. Tunakiri kwamba mfumo huu ulipata upinzani mkubwa tangu kuasisiwa mkoani Mtwara.
Lakini upinzani wa safari hii umekuwa ni ‘mkali’ mno.Na linalotia shaka ni kuona kupungua kwa ‘ubunifu’ miongoni mwa viongozi katika kuboresha hali ya biashara ya mazao nchini.
Ubunifu (Innovation) ndiyo msingi mkuu wa mafanikio katika biashara ya ulimwengu wa leo. Biashara haihitaji tena woga,ila inahitaji kujitoa mhanga na kugeuza ‘woga’ kuwa changamoto huku ukifanikiwa kupitiwa changamoto.
Daima changamoto hazikosekani, na kwa mbunifu hizo ndizo chachu za kusonga mbele na si kurudi nyuma wala kukiri ‘kufeli’. Tanzania ya leo inahitaji viongozi wajasiriamali na si waoga ingawa kitu ni kizuri.
Kwa mfano Mheshimiwa Mrope anasema kuwa mkulima anakopwa na hapati malipo kwa wakati, hili linawezekana kutatuliwa tukijapanga na tukiongeza ‘ubunifu’. Hili haliwezi kutufanya kufuta mfumo huu.
Lingine linalotufanye tuone ni ‘uwoga’ wa kisiasa na kupungua kwa ubunifu ni hili la Mheshimiwa Njwayo.Mbunge Juma Abdalah Njwayo alichomewa nyumba yake mwaka juzi kisa alikuwa anatetea mfumo huu,leo hii ‘amebadilika’ hautaki kabisa!Nini kinamfanya mbunge huyu kubadilika ghafla namna hii? Ni kweli kuwa stakabadhi ghalani haifai na ni mfumo wa kinyonyaji kama anavyodai Mheshimiwa Dastan Mkapa?
Hatumaanishi kuwa Mheshimiwa Mbunge Juma Njwayo hakupaswa kubadilika, la hasha, ‘flexibility’ inakubalika katika nadharia za ‘kioungozi’ hasa baada ya kuona mapungufu ya kile ulichokuwa unaamni. Ila nadharia hii ya ‘kubadilika’ kimtizamo imejikita katika kutafuta ‘ukweli’ kabla ya kubadilka.
Hapa hatuzungumzii ukweli wa ‘kisiasa’ eti kwa vile 2010 yaja basi yapasa kusaka imani za wapiga kura. La hasha ni ukweli wa mwenendo wa kibiashara duniani na hasa biashara za mazao na hali ya wakulima wa nchi masikini.
Upinzani kwa mfumo huu wa ununuzi wa korosho haupo bungeni tu. Oktoba mosi mwaka 2007 wakulima wa Tandahimba waliandamana kupinga stakabadhi ghalani. Adnani Mbwana mwenyekiti wa Chama Cha Wakulima wa Korosho Tandahimba alipata hasara ya 1.8 milioni baada ya mikorosho yake kufyekwa.Kisa anaungama katika stakabadhi ghalani!
Naye mwenyekiti wa TANECU, Mbaraka Mjagama ni mhanga wa stakabadhi ghalani kwani nyumba yake ilibomolewa, (soma gazeti la habari leo 22,Oktoba.2007). Wapinga mfumo huu hawakuishia hapo kwani waliongeza kufuri katika maghala ili kudumaza jitihada za kuanza ununuzi wa korosho kupitia mfumo huu.
Mifano inaweza kuwa mingi kwani wanasiasa kama vile katibu Mkuu wa CUF Maalim Seif Sharif Hamad naye alijitokeza kupinga mfumo huu soma gazeti la Tanzania Daima, 22.Oktoba. 2007.
Lenye kustaajabisha ni kwamba wakati Tandahimba wanakebehi na kupinga stakabadhi ‘ghalani’ wakulima wa pamba wanauomba kwa udi na uvumba. Wakulima katika wilaya za Getia na Kahama wanapigia chapuo mfumo huu uende katika pamba!
Mtu makini lazima atajiuliza mara mbili kwa nini korosho waupinge, pamba waulilie! Hawa wapamaba nini kinawafanya waulilie? Jibu rahisi ni kwamba wakulima wa pamba wamechoshwa na ‘kuhujumiwa’.
Tunaweka wazi msimamo wetu kwamba upinzani wa sasa wa stakabadhi ghalani ni kupungua kwa ‘ubunifu’ miongoni mwa viongozi wetu na ni dalili za kueneza hofu bila hata kupitia mwenendo mzima wa biashara ya mazao ya kilimo katika Tanzania.
Hivyo basi makala haya itatupia jicho mfumo huu, umuhimu wake kwa wakulima wa nchi hii, chagamoto zake na kushauri nini kifanyike katika siku za baadae ili kuboresha biashara ya mazao katika Tanzania.
Stakabadhi ghalani (warehouse receipt) ni nini?Si mfumo mpya duniani, wataalamu wa historia ya biashara wanabainisha kuwa ulianza katika Mesopotamia, na ulikua na kushamiri katika Marekani katika karne ya kumi na nane. Sheria ya kwanza imara na madhubuti kuhusu stakabadhi ghalani ilipitishwa katika Marekani mwaka 1916.
Asili ya stakabadhi ghalani ni nini?stakabadhi ghalani hutumika hasa katika kilimo, ni mfumo ambao umeibuliwa ili kuweza kupunguza kuyumba kwa bei ya mazao ya kilimo (price volatility) hasa wakati wa mavuno, na kumsababishia mkulima hasara kubwa na umasikini ambao huwa unamzunguka daima dumu.
Kutokana na kukosa bei ya uhakika wa mazao mara zote kilimo kimekuwa hakikopesheki, na hatari ‘risk’ kwa mikopo ya kilimo imekuwa ni kubwa na mara zote benki zimekuwa zikionesha kisogo sekta hii.
Hili likafanya nadharia ya stakabadhi ghalani kuchipuka Duniani nia ikiwa kumpatia mkulima bei yenye kuridhisha.Mara baada ya kusambaratika kwa jumuiya ya Ki-Soviet nchi za Ulaya Mashariki nazo zilijikuta haziwezi tena kulinda wakulima wake. Nchi kama Bulgaria, Kazakhstani, Hangari, Slovakia na Lithuania ni miongoni mwa vinara wa stakabadhi ghalani na wanaitumia huku wakulima wakineemeka.
Pia wakati wa kudorora kwa bei ya mazao ndiyo ulikuwa wakati wa ‘bush buyers’ walanguzi kujipenyeza na kununua kwa ‘lumbesa’ au ‘kangomba’. Nalo hili stakabadhi ghalani imelidhibiti. Taarifa za karibuni zinaonesha kuhimarika kwa ubora wa korosho.
Kimsingi mkulima hupewa hati mara baada ya kuuza mazao yake kwa ushirika, na malipo ya kati ya asilimia 65-70 hufanyika. Na mara zote sehemu iliyobaki hutegemea mauzo yake kwa wafanya biashara wanaonunua; safari hii hawakutani na mkulima bali ushirika, na si tena gunia moja bali ni tani zilizokusanywa pamoja.
Uwezo kwa kujadili bei umeongezeka kutegemeana na ushirika imara. Ila kubwa zaidi ni kwamba hati ya mauzo yaliyo ghalani ni ‘pesa’. Ina nguvu kama ‘negotiable instruments’ kutegemeana na sheria za nchi husika. Katika nchi zilizoendelea stakabadhi inayotolewa na ghala la serikali ndiyo huwa yenyekuaminika zaidi. Benki ya Dunia inasema hadi miaka kumi wakulima wa nchi za Ulaya Mashariki huweka mazao yao ghalani, huku wakiwinda bei nzuri!
Tafiti fulani iliyofanywa katika Tanzania na Zambia inataja wanunuzi wa mazao( bush buyers) hujipatia faida ya 70 asilimia na huku wakitumia gharama za kuhifadhi kwa 25 asimilia ya bei ya kununulia baada ya muda wa miezi miwili tu toka msimu wa mavuno.
Katika Tanzania stakabadhi ghalani imeingia baada ya upembuzi ya kinifu uliofanywa na Taasisi ya Maliasili( Natural Resource Institute) ya Chuo Kikuu cha Greenwich nchini Uingereza. Tafiti hii ilifanyika katika Zambia na Uganda pia katika miaka ya 1990 na kukamilika mwaka 1997.Na mazao ya kujaribia nadharia hii yalianza kama Kahawa na Korosho. Ndipo fuko la Common Fund for Commodities lilipotoa chagizo la kuundwa kwa stakabadhi ghalani na sheria ya kwanza ilikuwa June 2005 ilifikishwa Bungeni (unaweza kutembelea www.nri.org/project)
Msimu wa ununzi wa korosho wa 2007 ulishuhudia kuanza kwa mfumo huu, ikiwa ni kivuli cha kugoma kwa kampuni za kununua korosho zilizokuwa zinanunua chini ya bei ya makubaliano.
Kampuni hizi zilipinga agizo la Rais Jakaya Kikwete, kampuni sita zilinyang’anywa leseni. Hili la kupinga agizo la Rais ni fedheha kwa nchi, na utatuzi wake lazima uwe wa kisayansi na hapo ndipo ‘stakabadhi ghalani’ inachipuka.
Serikali haikuleta mfumo huu kama ubabaishaji tu, la hasha, kwani ni kilio cha wakulima wenyewe dhidi ya uonevu wa kampuni za ununuzi wa korosho, leo hii inatushangaza kusikia kuwa wawakilishi wa wananchi( wabunge) wanataka kuundoa mfumo huu.
Wanataka kuturudisha wapi? Kule tulikotoka, kwa wafanya biashara wahuni na wevi. Hata kidogo.
Lakini lililowazi ni kwamba tumeona kuwa mfumo huu hauna muda mrefu nchini na unalengo la kumlinda mkulima wa Tanzania. Basi yatupasa kutupia jicho hizo changamoto zinazoletwa na wapinzani wa stakabadhi ghalani pia tutatoa maoni yetu jinsi ya kuzikabili na kuona mifano halisi ya mafanikio ya stakabadhi ghalani si Tanzania tu pia katika nchi za Ulaya Mashariki ambako mfumo huu unatumika pia.

Sunday, October 25, 2009

Mwangwi wa jina batili 'mafua ya nguruwe' na biashara ya minofu ya nguruwe

‘Makosa yamekwishafanyika , na hakuna anayeweza kurudisha imani ya wateja kwa haraka minofu ya nguruwe na hasa ya dola 20 kwa nguruwe….sijui ni nani alileta uzushi huu wa ‘mafua ya nguruwe’, wanalalamika wakulima wa jimbo la Minesota,Marekani jimbo linaloshika nafasi ya tatu katika biashara ya nyama ya nguruwe na bidhaa zake.
Tangu kuibuka kwa ugonjwa huu, vyombo vya habari na wataalamu wa afya duniani wamejikuta wakiuita kwa jina ambalo wakulima na wataalamu wa magonjwa ya wanyama hawakubaliani nalo, nalo ni ‘mafua ya nguruwe’ (Swine Flu).
Lililowazi ni kwamba imani ya walaji hasa wa Ulaya imepungua tangu kutokea kwa kosa la kuuita ugonjwa huu ‘mafua ya nguruwe’.
Watu wengi wamepoteza maisha katika zaidi ya nchi 24 duniani. Ikiwa inakadiriwa watu 1000 wamefariki katika Marekani pekee, na kumfanya Rais Barack Obama kutangaza hali ya hatari, nia ikiwa kupunguza urasimu wa kisheria katika kutoa tiba kwa wagonjwa.
Mexico ni nchi ya kwanza kukumbwa na ugonjwa huu, ikiwa siku tatu kabla ya ujio wa Rais Barack Obama aliyetembelea nchi hiyo kwa nusu siku 16,April,2009, mtu ambaye alishikana naye mikono na kumuongoza katika maeneo ya makumbusho, mkurugenzi wa mambo ya kale na makumbusho (National Anthropology Museum) Felipe Solis, alifariki wiki moja baada ya tukio hilo, linaandika gazeti la Daily Mail la Uingereza.
Ingawa White House iliwahi kubainisha kuwa afya ya Rais i salama na hilo walilizangatia kabla hajafanya ziara hiyo, nayo serikali ya Mexico kukanusha kuwa Felipe Solis hajafariki kwa mafua ya nguruwe, lakini vyombo vya habari na jamii ya Mexico inaamini dalili zote zilikuwa wazi hadi kifo chake kuwa ni AH1N1.
Pamoja na vifo vingi vinavyotokana na ugonjwa huu duniani malalamiko ya wakulima wa nguruwe ni dhidi ya jina hili na hasa kuhusianisha moja moja kwa na nguruwe.
Shirika la Afya Duniani (WHO) limesema litaacha kuuita ugonjwa huu ‘mafua ya nguruwe’ ili kukwepa madhila ya makosa ya jina kwa biashara ya nguruwe duniani.
Nchini Tanzania taarifa ya karibuni ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya iliyosambazwa kwa vyombo vya habari na Mheshimwa Blandina Nyoni, iliendeleza kutumia jina ‘mafua ya nguruwe’.
Ingwa katika taarifa ile iliyopatatikana kulikuwa na maneno yenye kutia moyo kuwa ugonjwa huu hautokani na ‘kula nyama’ ya nguruwe. Lakini maneno haya hayakupewa uzito na vyombo vya habari.
Waatalamu wa biashara wanasema ‘mpe mbwa jina baya’ (Give a dog bad name) wakimaanisha katika ‘branding’ kosa likifanyika na jamii ikaamini katika hilo, lazima kazi ya ziada ifanyike ili kurudisha imani ya walaji.Hivyo umakini unahitajika sana katika kutoa jina.Nyama ya nguruwe sasa imepewa jina baya, tena ambalo hata haliusiki nalo kisayansi.
Watanzania ni mashahidi na bado tunakumbuka jinsi Mzee Yusuph Makamba alivyokauka koo kujaribu kurudisha imani ya wavaaji wa ndala zilizopewa jina masihala la ‘yebo yebo’ wakati akiwa Mkuu wa Mkoa wa Daresalaam. Kuna waliopigana na kujeruhiwa na wengine kuripotiwa kupoteza uhai kisa jina baya la ‘yebo yebo’
Hakuna anayejua madhala ya ndala zile za kwa kiwanda husika, lakini zile ndala ni zinazopendwa katika Ulaya na Uchina na hasa kwa maeneo ya baharini. Lakini katika Tanzania si mali kitu, na ni fedheha kwa mavaaji. Hii yote inaonesha uhusiano wa jina baya na imani ya mlaji.
Nguruwe ni nyama nyeupe ambayo katika soko la Ulaya na Marekani ni nyama pendwa kwa sababu za kiafaya ukilinganisha na nyama nyekundu.Ni wazi kuwa imani ya walaji nyama nyeupe katika soko la Ulaya, Amerika ambako walaji nyama wameonesha kuacha kula nyama nyekundu (ng’ombe na kondoo) sasa wataanza kula nyama nyeupe nyingine tofauti na nguruwe, yaaani kuku ambayo ilipigwa mweleka na ‘mafua ya ndege’!
Hili si sana kwa walaji wa Afrika, kwani walaji wa nyama wa ulaya hawataki kula nyama nyekundu kwa sababu za kiafya, na ni wazi kuwa mauzo ya mboaga za asilia (organic vegetable) zitapata nafasi kubwa kutokana na makosa haya ya ‘jina baya’ kwa nguruwe.
Profesa Marie Grammer wa Chuo Kikuu cha Minnesota, nchini Marekani ambaye pia mtaalamu wa magonjwa ya nguruwe anasema kitaalamu hakuna uhusiano wa wazi kati ya minofu ya nguruwe na bidhaa zake na H1N1. Isipokuwa ugonjwa unaotokana na muingiliano kati ya binadamu na wanyama.
Na wala ugonjwa hauwezi kuambukizwa kwa kula nyama ‘iliyoandaliwa vizuri’ au mazao mengine ya nguruwe.
Maneno vizuri yanabainisha hali ya usalama, hivyo pasi na usafi kuzingatiwa ni wazi kuwa nyama ya nguruwe inaweza kuwa hatari!
Kituo cha kupambana na magonjwa ya kuambukiza cha Marekani kinasema virusi vinavyoleta magonjwa kwa nguruwe ni ,A influenza, na wala hakuna uhusiano na H1N1 na nguruwe hivyo kutaka makosa ya jina yasahihishwe.
Tangu rai ya kuomba kubadilishwa makosa haya mara tu ugonjwa huu ulipojitokeza mwezi Aprili nchini Mexico, bado jina hili limeendelea kutumika na vyobmo vya habari nchini Tanzania na Dunia kwa ujumla.
Ingawa takwimu hazipo wazi ni kwa kiasi gani biashara ya nyama ya nguruwe ilivyo na manufaa lakini ukweli ni kwamba, kuna jamii nyingi katika mikoa ya Mbeya, Morogoro,Arusha,Iringa,Sumbawanga,Kilimanjaro, Morogoro na Daresalaam wameathirika na wanaendelea kuathirka kutokana na hofu hii kwa walaji.
Daresalaam ni soko kuu la nyama ya nguruwe maarufu kama ‘kitimoto’ambayo sasa katika miji na vitongoji vingi vya kibiashara nchini ni rahisi kukuta mabanda ya kuchoma nyama ya nguruwe. Basi yatupasa kurekebisha kuita ‘jina sahihi’ maana hofu tunayoijenga haina mwisho mwema kwa jamii ya wafugaji wa nguruwe.

Friday, October 23, 2009

Kuelekea usawa tunahitaji tahadhari

Siku za karibuni katika mikutano,makongamano,semina na warsha mbalimbali watu mashuhuri wamesikika wakiweka wazi ya kuwa nafasi za ushiriki wa wanawake katika bunge zinahitajika kuongezeka hadi kufikia asilimia 50.

Taasisi moja ya wanaharakati wanaojihusisha na mabadiliko katika jamii ya kitanzania wakati wa maandamano yaliyokuwa yameaandaliwa kwa kumpongeza Dk. Asha Rose Migiro ambaye kwa sasa ni Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa iliweka wazi juu ya kuhimiza kuongezwa kwa nafasi za wanawake hadi kufikia 50% katika nyumba za maamuzi.

Gazeti la Mtanzania la siku ya ijumaa tarehe 9 machi mwaka 2008 likimnukuu Waziri wa Maendeleo ya Jamii,Jinsia na Watoto; Mheshimiwa Sophia Simba liliandika kuwa nyongeza ya nafasi za wanawake bungeni ni lazima kufikia hamsini asilimia.

Hili la nyongeza ya wanawake katika bunge ni suala ambalo halina ubishi na ni la kupigiwa chapuo katika jamii ya watanzania katika kuona wanawake walioachwa nyuma kwa muda mrefu katika mchakato wa kupigania maendeleo ya nchi hii wanashiriki vilivyo katika kila harakati.

Jamii ya watanzania wanaona na kusikia ndugu zetu wa kike wakionewa,wakinyanyaswa na kudharauliwa kwa vile tu ni wanawake. Kwa ujumla wanawake ni wa watu wanaataabika katika kila jambo linaloihusu jamii yetu hii.

Hivyo kufanya nia yoyote itakayo pelekea mabadiliko yatakayo lipa nafasi kundi hili kubwa la watu katika idadi ya watanzania ambao wanakisiwa kuwa zaidi ya nusu ya watanzania wote kuwa ni jambo la lazima. Hili ni kwa mantiki ya ujenzi wa Tanzania yenye neema.

Hakuna anayeweza kulipa gharama za mateso na manyanyaso wanayokutana nayo wanawake katika juhudi zao za kila siku kwa leo hii katika Tanzania.Ingawa ni wazi kuwa hali hii ya kuwaweka nyuma wanawake katika kila jambo ni suala lililo na asili toka enzi za ukoloni. Kutokana na ukweli huoa 'affirmative action' kuelekea usawa katika jamii yetu kuwa ni jambo la maana na kuhimizwa kwa nguvu zote.

Ila katika kitimiza nia hii itakayosaidia katika kupunguza makosa yaliyotokea muda mrefu katika jamii yetu nilaizma tahadhari kuchukuliwa hasa kwa kufahamu ukweli kuwa kundi lililonyuma katika Tanzania ya leo si wanawake tu.

Kuna walemavu,vijana na masikini,Hivyo basi katika kutimiza lengo hili la nafasi za upendeleo ni lazima tujiridhishe kwa kuangalia pia hao wanawake wanaoingia katika nafasi hizo za upendeleo wasiwe tu toka katika kundi lilelile la jamii iliyokwisha 'nufaika'.

Ukweli lazima uwekwe wazi katika hii asilimia 50% wanawake vijana watakuwa asilimia ngapi? Uwakilishi wa wanawake walemavu utakuwa wa asilimia ngapi?

Pia hili nalo ni la kujiuliza pia katika wanawake hao,wanawake wa 'KIISLAMU' watakuwa wangapi? Hili ni jambo la wazi na wala si kwa ushabiki tu. Uwakilishi huu lazima uwe unaochukua watu wa kutoka makundi yote katika jamii.

Basi nia hii lazima iweke wazi juu ya ushiriki wa makundi yaliyo achwa nyuma kwa kipindi kirefu miongoni mwa wanawake. Na wala isije ikawa mwisho wa safari tunaona sura zile zile katika,uongozi huo. Huu hautakuwa 'usawa' kwa maana pana ya usawa ni lazima tuweke wazi hili mapema. kwani leo pia tunapigia chapuo lakini wakati ukifika utaona majina yale yale yanapita.

Kwani tusipokuwa wakweli unaweza kuona nafasi hizi zikiongezeka wakipata wake wa wakubwa na watoto wao.Tena walio nz umri mkubwa huku ushiriki wa vijana ukiachwa kando.

Pia tahadhzri inahitajika kwani 'affirmative action' katika kuelekea usawa si kufikia 'idadi' fulani la hasha; bali kujiridhisha kuwa watu hao walio nje ya mfumo kwa muda mrefu wana sifa na kweli wameandaliwa kuchukua majukumu hayo.

Kwa mfano hauwezi kupigia kelele kwamba itungwe sheria inayohitaji ofisi ziwe za serikali au binafsi ziwe zinaajiri wanawake kwa asilimia fulani bila kwanza kuhakikisha kuwa wanawake wenyewewe wana ujuzi huo.Au kusema tu kila ofisi inakuwa inaajiri walemavu kwa idadi fulani bila kwanzn kuwa na maandalizi ya kuwapa ujuzi hao wanaotakiwa kuchukua nafasi hizo hivyo basi kufanya kila linalo amriwa kuwa halina maana.

Mchungaji Jesse Jackson katika waraka wake kwa vyombo vya habari wa mwaka 1995; alioupa jina 'Affirming Affrimative Action', anasema hatua za upendeleo katika jamii siyo 'quotas'- Kwa kuzingatia ukweli; utakuwa uvunjaji wa sheria kumpendelea asiye na sifa dhidi ya aliye na sifa. Kile 'affirmative action' inatupatia ni kutumia kwa malengo na dira ili kushirikisha nguvu kubwa zaidi ya jeshi katika kufanya kazi ( Tafsiri ni yangu)

Nchini kwa sasa juhudi zozote za kuelekea usawa hasa katika kupata kazi na nafasi za uwakilishi katika mabaraza mbalimbali ya kutoa maamuzi hayaweki wazi ni asilimia ngapi ya watu wanao wakilisha makundi ya kijamii ambayo yalinyanyasika na wanaendelea na mataabilko wanahitajika.

Yatupasa kuwa wakeli kuwa nasafi za upendeleo ziwe kwa wale waliokosa nafasi na si waliokwwisha 'neemeka' kutumia njia hii kuendeleza, unyonyaji wao usio na tija. Basi tahadhari inahitajika katika kuwaandaa wale walio nyuma kama wanawake kielimu, Chuo Kikuu Mzumbe kimeonesha njia kwa kudahili 50 kwa 5o ya wasichana na wavulana, huu ni mwanzo mwema kuelekea usawa kwa vitendo, na wengine waige!

Je ninaweza kuishi na mtu asiye wa dini yangu?

UTAFITI FULANI UNAONESHA KUNA DINI NA MADHEHEBU YAPATAYO 10000,DUNIANI.AFRIKA PEKEE IKIWA NA DINI 6000.INAKADIRIWA PIA KWA WATU WAZIMA WAPATAO 16% KATIKA KILA NCHI WAMEWAHI KUBADILI DINI,HIVYO KATIKA MAISHA YA KILA SIKU NI KAWAIDA KWA BINADAMU KUKUTANA NA MTU AMBAYE SI DINI YAKE.
LAKINI DINI NI NINI?
DINI INAWEZA KUTAFSIRIWA KAMA MUONGOZO WA MAISHA YA BINADAMU KATIKA NGUVU ZISIZO WEZA KUFIKIKA AU KUONEKANA,YAANI NGUVU ZA ASILI.
KAMA TUKIKUBALIANA NGUVU NI MFUMO UNAOONGOZA MATENDO YALIYO MEMA YA KIBINADAMU BASI UKOMUNISTI NAO PIA WAWEZA KUWA NI DINI!
VIPI KAMA WATU WANAKATA MITI,WANAHARIBU MAZALIA YA SAMAKI KWA UVUVI HARAMU HAWAJALI MAZINGIRA KWA UJUMLA.HAPA MABUDHA WAO WANAONA HIYO SI DINI,WANASEMA "IWEJE DINI IONE KUFANYA MAPENZI NI DHAMBI LAKINI KUHARIBU MAZINGIRA SI DHAMBI"
KWA NAMNA YOYOTE ITAKAVYOKUWA DINI TAFSIRI YAKE LAZIMA ITIE NDANI MUONGOZO UNAOELEKEZA MATAKWA YA WATU KATIKA KUTENDA MATENDO MEMA.
HIVYO BASI NI KAWAIDA KUONA KATIKA UKOO KUWA NA WATU WA DINI TOFAUTI.
HALI YA ULIMWENGU
UGAIDI,VITA VYA KIDINI NA MACHAFUKO YA AINA MBALIMBALI YANAKUFANYA UCHUKIE WATU WA DINI NYINGINE?
MKRISTO UNATAKIWA UISHI VIP?NINI MAONI YA BIBLIA KUHUSU KUISHI NA WATU WA DINI NYINGINE?
HUENDA KATI YA WATU AMBAO SI WA DINI YAKO AKAWA NI BABA YAKO AU MAMA YAKO.BIBLIA INASEMA HIVI ....MHESHIMU BABA NA MAMA YAKO;KUTOKA.20:12.HAPA BIBLIA HAITAJI HUYO MZAZI WAKO NI WADINI GANI HIVYO BASI,NENO LA MUNGU LILITAMBUA KUWA ULIMWENGU UTAKUWA NA DINI NYINGI KUTOKANA NA MAMLAKA YA YULE MUOVU.FUNDISHO HAPA NI KWAMBA TUWE TAYARI KUISHI NA HESHIMA KWA WATU WA DINI NYINGINE, TUWATENDEA KWA STAHA NA FADHILI.

Ukosefu wa soko la uhakika ni kitanzi kwa ukuaji wa sanaa ya uchongaji

"Tumelalamika katika vikao mbalimbali vya kimkoa kuhusu ukosefu wa soko la vinyago nakuiomba serikali ya mkoa itusaidie;lakini kilio chetu kimekuwa hakisikiki"hayo ni maneno ya Mzee Joseph Rashid Adrea wa kikundi cha Jikwamue;kilichopo katika manispaa ya Mtwara eneo la Magomeni karibu na Kanisa Katoliki la Kristu Mfalme.

Mzee Rashid yupo katika sanaa ya uchongaji wavinyago kwa miaka 40 sasa.Anabainisha kuwa sanaa hii aliyoirithi toka kwa baba yake kwa sasa haina nafasi yakuvutia vijana katika mkoa wa Mtwara;kwa vile watu wengi wanaona hakuna sababu ya kuwapeleka watoto wao kujifunza kitu ambacho hakitaweza kumpatia riziki.

Vinyago vyao vipo katika mitindo tofauti kama 'ujamaa' ambacho ni muunganiko wa watu wengi walio pamoja wakiwawameshikana kwa urefu,'mawingu' huu hauna sura isipokuwa ni maumbo tu ya kitu husika,'nandenga' kwa kiswahili ni shetani,kitashwira inafanana hasa na michoro ya Tinga Tinga,pia huwa wanachonga vinyago vya dini kama misalaba,Yesu na Maria na mingine mingi kutegemeana na matakwa ya mteja.

Mtwara ni miongoni mwa mikoa ambayo inakabiriwa na tatizo la ajira hasa kwa kufahamu kwamba sanaa hii ya uchongaji ingeweza kuondoa kundi kubwa la vijana ambao wapo 'vijiweni' kwa kuwapa ajira lakini ukweli wa mambo haupo hivyo.Mtwara haina viwanda,kilimo ni cha msimu basi soko la uhakika kwa vinyago lingeweza kukomboa wanamtwara toka katika umasikini.

Hali ya kukosekana kwa soko la uhakika haikuwepo katika siku za nyuma kwa wachongaji wa vinyago katika Mtwara. Mzee Rashid aliyeanza sanaa hii mwaka 1966,anasema historia ya ununuzi wa vinyago Mkoani Mtwara ilianzishwa na kasisi wa kikatoliki wa Kijerumani anayemtaja kwa jina moja kuwa aliitwa 'Keki'.

Mjerumani huyu ndiye aliyewafumbua macho kuwa vinyago ni mali katika mkoa wa Mtwara kwenye miaka ya 1968. Keki alipofariki wahindi walichukua nafasi,lakini walilegalega na hatimaye walishindwa. Katika miaka ya 1976 walianzisha chama chao;Makonde Carving; kilichokuwa kikinunua vinyago katika maeneo mbalimbali ya mkoa huu.Nacho kikafa kibudu!

Hali ilibadilika katika miaka ya 1990 pale kasisi wa kanisa la katoliki la mtakatifu Paulo;Padri Edelfonse (Marehemu) alipojitokeza kununua vinyago kwa kila siku ya alhamisi.Vinyago hivi vilikuwa vikisafirishwa Ulaya na hasa Ujerumani.Lakini Tangu kifo cha kasisi huyu mambo yamekuwa magumu kwao na hali yao ya kipato tangu kifo cha kasisi huyu hali imekuwa ikizorota siku hadi siku.

Ukiacha wanunuzi wa nje wateja wandani wanakuja kununua vinyago lakini si kwa kasi kubwa na wala si wakutegemea. Viongozi mbalimbali hununua vinyago kwao wakitembelea Mtwara.Mzee Rashid anamtaja Jaji Mkuu Mstaafu Banabars Samatta aliwahi kununua vinyagovyake mwaka 2004,pia aliwahi kuweka nakshi katika sebule nyumba ya Waziri wa Usamala wa Raia wa zamani Mzee Bakari Harith Mwapachu.

Mzee Yustin James wa kikundi cha sabasaba katika manispaa ya Mtwara naye anatoa kilio kile kile cha kukosekana kwa soko la vinyago ndiko kunakozidi kuwadidimiza kimaisha. Ujuzi huu wa Mzee Yustin 'amerithi' kwa baba yake mwaka 1968,hali ambayo anasema sasa hivi ni ngumu kumrithisha kijana wake kwani fani hii sasa hivi ni majuto matupu.

Kijana anaona wazi kuwa hakuna unafuu wowote wa maisha atakaoupata kutokana na yeye kuwana ujuzi wa uchongaji hasa akiangalia Mzee wake anavyoteseka kwa kukosa soko la vinyago la uhakika.

Hili la kukosekana kwasoko linaoonekana kufanya kuwa ndiyo mwanzo wa mwisho wa sanaa ya uchongaji wa vinyago vya mpingo mkoani Mtwara na hasa kwa kufahamu wazi kuwa hakuna damu changa inayojifunza sanaa hii kwa sasa tofauti na zamani.

Mzee Rashid anasema umaarufu wa vinyago wa Mtwara haupo Mwenge Dar-Es-Salaam,ila hii ni sanaa ya 'makonde' na utambulisho wa kabila hili nje na ndani ya nchi,basi serkali inapaswa kubuni mbinu bora katika kuhakikisha inaendelezwa.

Msanii Danieli Mkalunde wa kikundi cha saba saba anasema hali ya soko si nzuri kwa sasa huku akitolea mfano wa kuwa walinunua mti wa mpingo mwaka 2004,lakini hadi leo hawajamaliza kuchonga kwa vile hakuna wateja wa sanaa zao.Hili linaonesha wazi kuwa soko la vinyago linazidi kuporomoka kila siku katika Mtwara.

Kilio kingine cha wasanii hawa wa vinyago ni bei ya mti wa mpingo kuwa ni ghali na wao hawaimudu bei ya shilingi 75,000.Nikiwauliza kuwa serikali imeongeza bei ya mpingo,wanasema hawana taarifa lakini lililowazi ni kuwa bei ya zamani ilikuwa inawashinda basi hata hiyo mpya wataweza wageni na kampuni kubwa na si wachongaji wadogo kama wao.

Akiliongelea suala hilo kwa uchungu Mzee Rashid anasema maofisa wa maliasili siku hizi wala hawajali katika kiwanda chake cha Jinasue,kwani walikuwa wanachukua kodi ya shilingi 100,000 kwa mwaka.Anadai aliwahi kuwauliza maofisa hao kuwa wanafanya juhudi za kumkamua ng'ombe ambaye hawafanyi juhudi zozote za kumlisha kwa kumtafutia soko la sanaa zake.

Kwa ujumla wao hawana kipingamiza na kupanda kwa kodi ya mpingo lakini serikali ilipaswa kwanza kuwatafutia soko la uhakika kwa bidhaa zao.Na si kupandisha kodi,kwani kama wao wasanii watashindwa kununua mti wa mpingo huku soko la kazi zao halipo.

Mapendekezo yao ni kuwepo kwa kijiji cha sanaa ya vinyago katika Manispaa ya Mtwara;pia kjiji hicho kiwe na wasanii wengine kama wachoraji;ili kupunguza adha kwa wateja wanaotembelea Mtwara kuweza kununua sanaa zao kwa urahisi kama vile ilivyo kijiji cha makonde Mwenge.

Kwa sasa wasanii hawapo pamoja katika manispaa ya Mtwara hivyo kuwa kero kwa wateja wao kwani hulazimaka kutembea bila uhakika wa kuwakuta wachongaji.

Pia wanatoa changamoto kwa serikali kupitia wizara ya maliasili na utalii kukuza na kuhifadhi sanaa hii ya uchongaji wa vinyago kwa kuwatafutia masoko ya uhakika wachongaji hawa wa mkoa wa Mtwara. Hili lisipopatiwa suluhu sanaa hii iliyolipatia taifa sifa na umaarufu mkubwa Duniani itapotea na wala wasindanganyike na wachongaji wachache wa Mwenge kwani wale wanaowaona Mwenge walifunzwa Mtwara ndipo wakaja huko.

Sasa kama hakuna 'kuni' katika jiko la wasanii hawa litazimika.Na 'kuni' ni kupatikana kwa soko la uhakika kwa wachongaji waliopo Mtwara.Vinyago ni utambulisho wa Mtanzania na kila mgeni mkubwa wa kitaifa nayeingia au kuondoka zawadi ya sanaa ya vinyago imekuwa ikitolewa na Rais, Makamu wa Rais au Waziri Mkuu. Hii ni ishara ya wazi kuwa inaheshima, basi yatupasa kuheshimu pia kazi hii kwa kuwatafutia soko la uhakika wasanii hawa wa Mtwara.

Wednesday, October 21, 2009

Kilimo kwanza na changamoto ya nishati katika chai

Tatizo la nishati katika ‘chai’ changamoto ya KILIMO KWANZA

Takwimu zilizowahi kutolewa na Shirika Kongwe la Umeme Tanzania (TANESCO) baada ya kuibuka mjadala wa ‘tozo’ kubwa kwa ‘unit’ kwa watumiaji, ilikuwa ni ya kujigamba kuwa wateja wa Tanzannia ndiyo wanaokula umeme kwa bei ya chini katika Afrika Mashariki, 0.08 US huku Kenya na Uganda walaji wakitozwa 0.16.
Tanesco walitoa taarifa hizi kupitia Ofisa Uhusiano wa wakatia huo zilizojaa uhakika wa kutatua tatizo la nishati na mara zote zilikuwa ni za kutia matumaini. Pamoja na matumaini hayo yote na bei kuwa ndogo katika ukanda huu bado Tanzania ni nchi yenye watumiaji wachache wa Umeme kwa asilimia 10 ya wananchi wake ndiyo wana umeme.
Katika nchi yenye watu zaidi ya milioni 40 kwa takwimu za 2008 za Benki Kuu ya Dunia, ni wazi kuwa, ukuaji wa sekta nyingine zinazoendana na nishati utabaki kuwa nyuma. Sekta ya viwanda ni moja wapo ambayo inaonekana kuchangia kiasi kidogo katika pato la taifa, na hili ndilo hasa linachangia katika kutufanya tuwe watu wakuuza nje mazao ‘ghafi’.
Ukiwa na mashaka ya upatikanaji wa nishati, niwazi kuwa utakuwa na uwezo mdogo wa kuvutia wawekazaji katika viwanda, hali inayochangia kabisa kudorora kwa kilimo. Nishati ni Viwanda, Viwanda ni Kilimo, basi Kilimo nacho ni Nishati! Uhusiano huu wa wazi unaweza kufanya mnyororo usikamilike endapo mahali popote panalegalega hufanya kukatika kabisa.
Sekta ya Kilimo bado haijaweza kuvutia mitaji toka nje na jitihada nyingi zinafanywa katika kuboresha hali ya wawekezaji katika kilimo ikiwa kubadilisha sheria ya ardhi ili kutoa umiliki wa muda mrefu wa hadi miaka 99. Mageuzi pia yanatokea katika sekta za fedha ili kuchochea mikopo katika kilimo.
Kitaasisi kuna maeneo ya uwekazaji kama EPZ ( Economics Processing Zone) ambayo yanampatia ‘motisha’ mwekezaji ya kufanya biashara kwa miaka kumi bila kutozwa baadhi ya kodi, ikiwa pia anatakiwa kuuza asilimia 80% katika soko la nje. Jitihada zipo nyingi lakini bado tunaendelea kushuhudia asilimia 5 tu ya FDI katika kilimo, na ushiriki wa Tanzania katika AGOA ndiyo unatoa mwanga kamili jinsi ya ugumu wa kukitoa kilimo chetu kilipo bila nishati.
Jitihada za ubinafsishaji bado hazijazaa matunda kwani wengi waliouziwa viwanda wamegeuza ‘maghala’ ya kukusanyia mazao na kuuza nje ya kiwa ghafi, mazao kama korosho bado asilimia 90 inasafirishwa ‘ghafi’ katika masoko ya ASIA na kubanguliwa kisah kuuzwa katika Ulaya, kwa faida nono!
Rais Mstaafu wa awamu ya tatu Mzee Benjamini William Mkapa aliwahi kuwapa changamoto wadau wa korosho wakatika fulani katika kongamano la Kibaha Pwani pale alipokuja na korosho toka Uingereza ambayo haifiki hata robo kilo lakini ikiuzwa kwa zaidi ya dola 4 za Marekani. Hata kama ukisema kwamba katika kila kilo moja ya korosho kuna asilimia 70 ya ‘makapi’ na asilimia 30 ndiyo inayobaki safi kwa kuliwa, niwazi kuwa bei ya kilo 350/= wanayolipwa wakulima wa Newala Tanzania ni ndogo mno!
Hakuna njia nyingine ya kuwakomboa wakulima wetu zaidi ya kuhimiza uwekezaji katika viwanda, vidogo, vya kati na vikubwa, lakini mashaka yakuja na hasa suala la uhaba wa nishati tulio nao!
Hata maoni yako yawe nini, hakuna haja ya kulaumiana tunahitaji mawazo ya pamoja katika kutatua uhaba wa nishati nchini! Gazeti la Mtanzania Daima la tarehe 20.10.2009 linahabari juu ya ‘kukosekan kwa soko la chai’ kwa wakulima wa Milima ya Usambara baada ya kuibuka mgogoro wa ‘msitu’ ambao unatoa kuni kwa ajili ya nishati.
Wakulima ambao wanategemea kiwanda cha Mponde wanapata 6,000, hivyo kufungwa kwa kiwanda hiki ni mashaka kwa familia hizi. Niwazi kuwa ‘steam’ ndiyo teknolojia inayotumika kwa viwanda vingi vya chai vilivyopo mbali na miundo mbinu ya gridi ya Taifa, na si Tanzania tu , Malaysia pia wanatumia kuni, lakini wapo mbioni kubadili na kutumia umeme wa maji.
Chai siyo sawa na ‘tikiti maji’ ambalo linaweza kukaa zaidi ya masaa 24. Chai inahitaji kuvunwa na kufikishwa kiwandani katika kipindi kifupi ndani ya masaa 24 yakizidi tunaongea lugha nyingine.
Tatizo la nishati limeanza tangu 1983 katika Tanzania kwa upande wa viwanda vya Chai, na tangu wakati huo tumeshuhudia viwanda vingi vikigeuka ‘mahame’
Familia ya MULA ndiyo wamiliki wa kiwanda hiki cha Mponde Tanga, lakini pia wanamilki kiwanda cha chai cha Lumbele, kilichopo Iringa ambacho nacho pia kipo katika mgogoro wa kugombea msitu wa nishati ya kuni kwa ajili ya kuendesha mitambo ya chai. Tanga wanagombea na wanakijiji msitu wa ‘SAKARE’ na Iringa ni msitu wa ‘Lyembela’ kwa mujibu wa gazeti la Mtanzania Daima, la 23. Mei, 2008.
Ingawa katika mgogoro wa Iringa kiwanda kilishinda mahakamani katika kesi iliyoendeshwa mahakama ya biashara na kuwa wamiliki halali, mgogoro wa Tanga bado unafukuta na Waziri Mkuu Mizengo Kayanza Pinda, mtoto wa mkulima anaufahamu!
Huu ni mgogoro wa nishati kati ya wakazi na viwanda na safari hii ni kugombea ‘kuni’. Kuni ni mgogoro katika viwanda vingi , hata MeTL kupitia kiwanda chao cha nguo cha Morogoro kilishaingia katika mgogoro huu wa nishati ya kuni, na kutishia uzalishai wake.
Tanzania inazalisha 1% ya chai ya ulimwengu na ni ya nne barani Afrika kwa kuzalisha chai.Nchi kwa sasa ina mkakati wa kuongeza uzalishaji hadi kufikia tani 55,000 kufikia 2013. Chai kwa sasa inaonekana kupanda katika kuingiiza fedha za kigeni Taifa, katika msimu wa 2006-07, dola milioni 39.4 zilikusanywa zikipanda kutoka dola milioni 27 kwa msimu wa 2005-06.
Hili la nishati linaonekana kuwa ‘mwiba’ mkali kwa sekta ndogo ya chai, lazima tujipange kutafuta suluhu kwa wakulima wadogo wapatao 32,000 wanaolima chai nchini na hasa wale walioonesha njia na nia ya kuenda mbele kupitia ushirika.
Basi yatupasa kufahamu kuwa nishati ni changamoto kubwa kwa ‘KILIMO KWANZA’ yatupasa kujipanga kutatua tatizo hili la nishati si kwa chai tu bali viwanda vingine pia. Tuache ‘malumbano’ katika nishati tujipange kama nchi, nani alifanya kosa wapi haina maana kwa sasa, tufikirie kupata nishati kwanza.
Tusipokuwa waangalifu tunaweza kujikuta tumetumia muda mrefu katika kujadili watu na kusahahu kuwa bado tuna tatizo nalo ni nishati.

Monday, October 19, 2009

Uchawi na mafanikio ya biashara katika Tanzania

JE UNAAMINI KAMA UCHAWI UPO?
Gazeti la Mwananchi la tarehe 17 Oktoba, 2009 lina habari ya 'tafrani' katika kiwanda cha JUISI NA MAJI cha MOHAMMED ENTERPRISES kuhusu madai ya 'UCHAWI' dhidi ya Meneja wa kiwanda hicho. Ingawa gazeti halikutaja jina la Meneja, lakini yatupasa kufahamu kuwa kuna jambo kama hilo.
Polisi iliwalazimu kutumia silaha za moto kutawanya wafanyakazi, ni wazi kuwa walichoshwa na hali hii. Madai yao ni kwamba mara zote wamekuwa wakitolewa 'kafara' wafayakazi na wamekuwa wakikumbwa na ugonjwa wa 'kuanguka'.
Kiwanda cha 'OLAM', Mtwara kinacho bangua Korosho matatizo kama haya ya kuanguka kwa wafanyakazi yaliwahi kuripotiwa na kuna wakati 'makumi' waliumia baada ya kukanyagana wakihisi kuna 'dubwana', linawafuata KUWAMALIZA.
Ndiyo hizi ni siku za kafara, na kuabudu katika 'MIUNGU' inayohitaji 'DAMU' kama kafara ili kujiongezea kipato.Katika Biblia neno 'UCHAWI' limetajwa toka enzi za MUSA, YESU na MITUME walikuwa wakikemea kuhusu kushiriki katika UCHAWI.Kitabu kitakatifu cha Biblia kinasema wazi kwamba 'Usimuache mwanamke MCHAWI aishi, je wanawake ndiyo wachawi tu?
Inawezekana kwa namna moja au nyingine kuna wakati ulishindwa kuelewa kama kweli uchawi upo! Na kuna wakati ulikutana na watu wakisema kuwa hawaamini kama uchawi upo. Hata maoni yako yawe nini, suala moja unalopaswa kufahamu ni kwamba UCHAWI upo.
Lililowazi ni kwamba UCHAWI ni nguvu za yule muovu 'SHETANI'. Biblia inasema 'DUNIA' yetu i uwanja wa huyo muovu. La kumbe, tupo katika mji wa muovu, basi ni wazi kuwa UCHAWI unatuzunguka na wao wanataka kutushinda ili tuamini katika 'kushiriki' nao.
Basi kama binadamu yakupasa kuishi maisha yenye neema na kumtumikia 'MUNGU' wako, lakini unaweza kujiuliza kama MUNGU, anakupenda iweje akulete katika Uwanja wa 'SHETANI'?

Fuatilia makala haya itakayotoka hivi karibuni.

Friday, October 16, 2009

Kuuza rasilimali watu nje yahitaji tahadhari

Siku chache zilizopita Waziri wa Afrika Mashariki Didorus Kamala alinukuliwa na vyombo vya habari kuwa Tanzania iko mbioni kuwa na mkakati wa kuuza wataalamu nje ya nchi. Hili ni wazo zuri, kwani wakati wote kuna imani kwamba wale walio nje wataleta walu sehemu ya 'mafao' yao nyumbani ambayo kwa namna moja au nyingine yatainua hali za tulio nyumbani ambako umasikini wa kipato unatumaliza. Pili uzoefu wao katika shughuli za maendeleo tunaweza kuamishia nyumbani(Back Home Era) nasi tukabadili hali zetu pia kwa kuongeza ajira kama vile wakianzisha kampuni.

Ulimwengu unashuhudia mapinduzi ya kisayansi yanayotokea India kwa sasa katika teknolojia ya kompyuta na mawasilinao kwa ujumla, haya yote ni kwa ajili ya vijana waliokuwa uhamishoni na hasa nchi za magharibi kuamua kurudi nyumbani(Back Home Era). Sina hakika kama hili linawezekana kwa watanzania!! Ni suala la kusubiri muda.

Kwa sasa watanzania waliopo nje wanaleta kama dola milioni 14,mafao haya ambayo yakiwekwa katika takwimu za kipesa ni madogo ukilinganisha na jirani zetu kama Uganda dola wanaorudisha milioni 896 takwimu hizi ni za mwaka 2007.Pia yatupasa kushukuru. Yatupasa kufahamu pia kurudisha riziki nyumbani ni hali ya ‘moyo wa mtu’ na fadhila aliyonayo na wala tusiiwekee asilimia mia moja katika hili kuwa hali itabadilika endapo watanzania wengi watakuwa nje ya nchi.
Makala haya inatoa tahadhari ya wazi kuwa haikubaliani na Mheshimiwa Waziri na wazo lake kuwa na mkakati wenye tija na kupigiwa ‘chapuo’ kwa nguvu kwa hali ya sasa ya nchi yetu ilipo. Si kila jambo linalotokea kuwa na faida kwa wenzetu nasi yatupasa kulikimbilia. Hapana, na hasa chapuo katika kuuza madaktari wa tiba.
Nadharia rahisi ya mtu anayeweza 'kuuza'(Seeling) ni yule aliye na ‘ziada’ ( You cannot sell if you don’t have surplus). Swali la kujiuliza Tanzania yetu ya leo ina ziada ya wasomi kiasi nasi kujinasibu kuwa tunataka kuingia katika soko la kuuza rasilimaliwatu nje?

Tukijilinganisha na Uganda tunaweza kutafuta sababu za juu tu bila kupata kiini cha kwa nini hatuna wataalamu wengi nje ya Tanzania. Jibu ni kwamba hatuna watu walio na ujuzi stahili. Uganda leo hii wana tawi la chuo kikuu cha KIU (Kampala International University-Dar Campus). UDSM wakongwe kuliko KIU hawana tawi,Mzumbe wameweka tawi Mbeya. Lakini matawi haya ni ya shahada za kijamii si ya sayansi na hasa Udaktari.

Vyuo vya tiba bado haviajwa na udahili wa wanfunzi wengi nchini ingawa idadi yake kwa sasa ni vitano na hili ni kwa sababu ya gharama, na miundo mbinu hafifu kukizi mahitaji ya vyuo hivyo kuanzishwa nchini.
Tena maeneo ambayo Mheshimiwa anayapigia chapuo ni udaktari wa binadamu na uhandisi!Haya ni maeneo nyeti sana na uhaba wake unatisha. Hatumaanishi kuwa watanzania wasiende nje kutafuta kazi na kujiongezea uzoefu, la hasha ila yatupasa kuwa makini katika kuhakikisha tunaweka nguvu katika maeneo kweli ambayo ‘tunafaida ya kiushindani’.
Gazeti la serikali la Habari Leo la tarehe 16 Oktoba lina habari ya uhaba wa madaktari na wauguzi katika hospitali ya Mirembe iliyopo Dodoma, pia hospitali hiyo inahitaji wauguzi 150! Hospitali hii inapokea watanzania zaidi 6000 ikiwa na uwezo mdogo mno wa kutoa huduma. Napata kigugumizi hivi kweli linalozungumzwa na Mheshimiwa ni hoja iliyo katika wakati muafaka kwa Tanzania ya leo.
Kuna maeneo Tanzania inahitaji kwa hakika kuuza wataalamu wake nje,lakini unauza wakatika unadahili asilimia 2 tu ya watu wenye sifa ya kuingia chuo kikuuu. Natumaini hoja ilipaswa kuwa tunahitaji kuongeza nguvu katika elimu ya juu ili tuweze kuuza wataalamu nje.
Kuna maeneo watanzania yatupasa kuyaangalia kwa ‘jicho la tai’ kwani huko tunauwezo wa kufanya vizuri na si vibaya tukajaribu, kwa mfano walimu wa lugha ya Kiswahili. Tusipoongeza udahili na kujipanga sawasawa tutakuwa wachekeshaji, kwani wale tuliowafunza lugha hii adhimu, sasa ndiyo watang’ara kama wakufunzi. Simaanishi hakuna waswahili wanaowafunza waingereza ‘kiingereza’ ila lazima uwiano uwepo kati ya mwenye ‘chake’ na mdandiaji.
Hali ilivyo sasa wakenya wengi wanasoma Kiswahili na wanahitimu wengi chuo kikuu kuliko watanzania tunavyosoma katika ngazi ya shahada Kiswahili chetu! Hapa kuna tatizo nyumbani lazima tulitatue.
Libya imeweka wazi kuwa lugha ya Kiswahili ni kati ya lugha zinazopaswa kutumika nchini humo lakini hakuna walimu, sasa haya ndiyo maeneo tunayopaswa kuweka nguvu kwani tunafaida mlinganisho nayo na hayatatuathiri kimsingi.
Lakini hili la kuuza madaktari wa binadamu nje ni hatari hasa katika nchi kama yetu ambayo watu bado tunakufa kwa magonjwa yanayotibika kama malaria, tumbo, kifua kikuu.Bado wakina mama wanakufa kwa kukosa huduma nzuri wakati wa kujifungua,MIMBA sasa imekuwa ni kuchungulia kaburi!Mimba si ugonjwa lakini kwa vile hakuna wataalamu ndiyo haya yote, ya 108 katika ya akina mama 10000 Iringa wanakufa kila mwaka. Kila dakika kuna mtoto mchanga wa kitanzania anafariki, kisa yuko mbali na kituo cha afya.
Lindi bado inaongoza kwa vifo vya akina mama wajawazito, bado tushabikie kuuza wataalamu wetu nje si sawa . Sina nia ya kupinga wazo hili yatupasa kuweka nguvu katika maeneo yenye tija kwanza, pili yatupasa kuweka nguvu katika kudahili pia na si kama hali ilivyo sasa kisa dola milioni 14 zinapswa kuongezeka!
Bodi ya mikopo ilikuwa na nia ya kutoa mikopo kwa wanafunzi zaidi ya 60,000, sasa idadi imeshuka hadi 24,000! Ni wazi kuwa mambo si mazuri kwani maelfu wamekosa udhamini si kama hawana sifa la hasha ni uhaba wa fedha. Katika hali kama hii kuna maeneo yatakosa wataalamu, Hivyo kupigia chapuo kuuza wataalamu nje tena wa afya au wahandisi ni hatari.Tena katika nchi ambayo vijana hawapendi tena kusoma masomo ya sayansi licha ya kuwepo udhamini wa asilimia mia moja.
Tusiwe kama wamalawi ambao wataalamu wake wa tiba ilio wasomesha kwa shida na gharama kubwa wapo wengi katika Uingereza kuliko walivyo katika MALAWI nzima, kisa pesa kurudisha nyumbani.
Kimsingi kurudisha hela nyumbani ni moyo wa mtu si kwa vile amewaacha watu nyumbani ndiyo atawapatia chochote kitu.
Mifano mizuri tunayo hapa hapa Tanzania,kuna watu wengi tumesahau wapi tulikotoka mara tu baada ya kuingia katika ofisi zenye kiyoyozi na kuendesha magari ya mikopo ya mitumba kutoka Japan, hatuna fadhila na watu waliotulea na hasa wazazi tunawaacha wakihenyeka katika siku za uzeeni!
Msimamo wetu ni kwamba yatupasa kupima mara mbili zaidi faida ya kipato na madhara ya kushabikia mchakato huu na kuweka nguvu ya kuuza wataalamu wetu nje. Yatupasa kuongeza kwanza nguvu katika udahili kwa elimu ya juu, kisha tuanze na walimu wa kishwahili na si kila sekta ni hatari.

Wednesday, October 14, 2009

Mifumo yetu ya elimu na heka heka za ufadhili wa kimasomo

Waatalamu wa maendeleo na wachumi kwa pamoja wanaungama kwamba kukosekana kwa 'nafasi sawa'(Lack of Opportunities) mara zote ni sababu kubwa inayopelekea kuongezeka kwa umasikini barani Afrika na hasa Kusini mwa jangwa la Sahara.
Mara zote nafasi inapotokea ama iwe inachelewa kuwafikia walengwa, au hata walengwa kukosa taarifa sahihi wapi waanze na wapi waishie ili kufaidi nafasi husika. Kudoda kwa mapesa ya mabilioni kwa mabilioni katika taasisi za kifenda kwa ajili ya mikopo ya wajasiriamali, kushindwa kujitokeza kwa watu wenye sifa katika nafasi mbalimbali za fadhili za kimasomo nakadhalika nimaeneo machache tu yanayoweza kuorodheshwa.
Changamoto kubwa ipo katika mifumo yetu hasa inapokuwa 'hasi' katika kuhakikisha tunafaidi nafasi hizi za ufadhili zinapotokea. Makala haya itatupia jicho mifumo yetu ya elimu nchini Tanzania na jinsi inavyoviza fadhili mbalimbali kwa watanzania nje au ndani ya nchi kwa ajili ya masomo.
Madai ya kuwa watanzania tumeshindwa kutumia nafasi tena wakati mwingine zinakuja kwa anwani ya kwamba mwanafunzi awe wa Tanzania yamesikika mara nyingi. Na lililowazi ni kwamba nafasi hizi ni adimu na zinatokea katika nchi ambayo si kwamba watu wake wanakipato cha kutosha bado tupo katika dola 270 kwa mwaka. Kwa kuzingatia hili nafasi za ufadhili wa kimasomo ni muhimu kwetu, kwani bado idadi ya walio na sifa kushindwa kuendelea na masomo ni kubwa na lenye kuhuzunisha ni kwamba wakati wote pesa imekuwa ndiyo kikwazo.
Swali ni kwani nini tunashindwa kutumia nafasi hizi?Taasisi za elimu ya juu nchini Tanzania mara zote zimekuwa vigingi katika kuelekea kufaidi nafasi hizi za ufadhili. Hili limetokana na jinsi tunavyofanya kazi ama la kuwa 'kizamani' au 'kuamini' kuwa lazima vikao vikaliwe ndiyo jambo fulani liweze kupitishwa.
Mathalani suala la vyeti na taarifa ya maendeleo ya mwanafunzi (transcript) imekuwa kero hasa kwa wahitimu. Maeneo mengine hati hii inahitaji kusaniwa na DVC! Mifumo hii mara zote inaleta 'uzubavu' katika kutumia nafasi. Hatuna tatizo kwa DVC kusaini, lakini kimtizamo naona DVC wakati wote amekuwa na kazi nyingi, na kimsingi yeye hawezi kuwa anamfahamu mwanafunzi zaidi ya watu wa Idara au Mkuu wa fakati husika ya mwanafunzi.
Kuna vyuo hii nikazi ya Mlezi wa fakati na si kazi ya DVC, katika hili utaona ambavyo mambo hayalegi, matokeo yakitoka idarani mwanafunzi anayathitisha yanaenda kwa Dean hati ya matokeo inasainiwa, kijana anapata 'transcript' anaendelea kusubiri cheti huku heka heka za maisha baada ya chuo zikiendelea.Chuo kinachotumia utaratibu huu ni Mzumbe na mara zote wanafunzi wamekuwa wakijiuliza kwa nini vyuo vingine hati zinachelewa pamoja na vyeti lakini si kwa Mzumbe!
Katika ulimwengu wa leo elimu ni 'biashara' chuo kinacho kuwa makini katika kutoa matokeo na kufanikisha kudahili kwa wakati kinapata wanafunzi wengi tena kwa wakati na wale wanaoweza kujilipia pia wanakuwa wanafanya hivyo.
Tanzania ni nchi ambayo kama niliyotangulia kusema mifumo ya elimu inadumaza kutumia nafasi za ufadhili. Nafasi kede kede zinaendelea bila kupata mtu wa kuzitumia, kisa taarifa ya udahili, oooh kikakao cha seneti bado. Elimu ni biashara narudia tena, lazima iendane na matakwa ya wateja.
Hebu tuangalie mifano michahe kuonesha jinsi tulivyokuwa na mifumo mibovu inayotunyima kutumia nafasi za ufadhili katika nchi yetu za kimasomo. BTC (Belgium Techniocal Cooperation)huwa inatangaza nafasi za ufadhili kwa wanafunzi waliopata udahili kwa vyuo vya ndani na ndani ya Afrika Mashariki. Ufadhili huu unakuwa katika ngazi ya shahada ya Uzamili(Masters) na Uzamivu(PhD).
Matangazo haya mara nyingi huwa yanatoka kati ya mwezi wa nne hadi wa tano kwa mwaka husika. Kipindi hiki vyuo vyetu bado havijatangaza kupokea maombi ya udahili kwa mwaka husika. Bado hata vikao vya udahili havijulikani vitakaa lini na tangazo litatoka katika gazeti gani. Mara zote kuanzia mwezi wa sita hadi nane na mwezi wa tisa heka heka za matangazo na udahili zinakuwazimeanza.
Matokeo kutoka ili kufahamu umepata au umekosa ni mwezi wa tiasa hasa.Na ule udhamini unaotolewa na BTC unakuwa unamwisho wa kutuma maombi mara nyingi tarehe zao zinakuwa ni chini ya kuanza kwa kutuma maombi chuoni. Hii inaonesha wazi mifumo 'iliyozeeka' isivyoweza kuwapa nafasi watanzania kutumia neema ya ufadhili katika kujiendeleza kimasomo katika nchi yao wenyewe!
Shirika jingine la Osienala (Friends of Lake Victoria) lenye makao yake Kenya hutoa udhamini kwa wanafunzi wa Afrika Mashariki kusoma katika vyuo vya nchi hizo kwa shahada ya uzamili katika fani za mazingira, maendeleo, biashara nakadhalika, hutoa nafasi hadi mwezi wa tano tarehe 30. Bado kilio kile kile nafasi hii kwa wasomi wa Tanzania hawawezi kuitumia kwani muda wa udahili na vikao vya seneti bado nchini!
Njia hii ya ukale wa kutuma maombi kwa vyuo vyetu ni wazi kuwa inatutoa katika soko la ushindani wa kielimu. Hivi karibuni nimepata fununu kuwa The Open University of Tanzania watakuwa wanapokea maombi kwa mwaka mzima hii ni hatua ya kupongezwa. Na lililowazi sasa yatupasa kutambua kuwa mfumo wa vikao vya seneti umepitwa na wakati katika kuuza elimu.
Njia sahihi ni kuacha idara iangalie wanafunzi inaowahitaji kwani ndiyo walimu na wao wapeleke majina kwa Idara ya Elimu ya Juu (Directorate of Postigraduate Studies) kwa taarifa na kuandikwa kwa barua kwa mwanafunzi husika.Hili haliitaji seneti kwani 'member' wa seneti siyo wote watakao mfundisha mwanafunzi na wala hawana hata utalaamu wa shahada husika, sasa kwanini wao ndiyo wawe na nguvu katika hili?
Katika nchi za Ulaya na Marekani utumaji wa maombi huwa mwaka mzima na mwanafunzi anapaswa ataje anaingia majira gani ya mwaka, na hili linafanya wanafunzi wawe katika nafasi nzuri ya kutafuta wafadhili.Pia maombi hutumwa kwanza katika idara yako. Tanzania inakuwa kinyume chake,nacho hudumaza heka heka za kutafuta ufadhili.
Vyuo vya elimu ya juu lamiza vibadilike, ili kuhakikisha vinauza elimu na si kuendelea kuwa kigingi katika kuwezesha watanzania kufaidi nafasi za ufadhili. Katika zama za mawasiliano ya kompyuta hili linawezekana.
Yatupasa kutumia nafasi hizi kwa kubadili mifumo yetu, simaanishi kuwa hawapo ambao hawajanufaika na BTC lakini wengi wao waliomba na mara zote ni wale wanaojuana na wahusika ndiyo walipata barua za Partial Admission wakisubiri vikao vya seneti , barua hizi ziliwasaidia kupata ufadhili. Sasa hili ndilo linaloleta umasikini kwani nafasi sasa inakuwa si 'sawa kwa wote' ila wale wanaojua kutupa karata tu.
Vikwazo vya kusubiri hati ya maendeleo ya kitaaluma hadi isainiwe na DVC imepitwa na wakati hii ni kazi ya Dean wa Idara husika. Na hasa katika kipindi hiki cha kuuza elimu ambacho mteja anapaswa kukimbizana na muda kwani muda ni pesa na kuchelewa kwake ndiyo hatari yake ya kupata ufadhili na kukosa kwake ni kukosa kwako (CHUO) kuuza elimu.
Huu ni mzunguko hauja mkomoa mwanafunzi hata chuo nacho kipo katika kukosa mapato pia, na hasa inapokuwa huyo mwanafunzi ana sifa stahili za kupata ufadhili. Shime wasomi wakati umefika wa kuondoa vikwazo katika kuuza elimu na hasa katika kuhakikisha tunakwenda sambamba na matakwa ya wateja hasa wafadhili wa kimasomo, na hili ni kuendana na muda wao tu. Tuanze kudahili kwa wakati na jukumu hili liwe la idara husika, pia tuwe na udahili wa mwaka mzima kupitia mtandao.Ili tuweze kuongeza kipato na kupambana na ukata unaosababishwa na bajeti finyu ya serikali.

Thursday, October 8, 2009

Mwangwi wa ushindi wa zabuni kwa Jeetu Patel na hatima ya 'maadili ya biashara' nchini

Vyombo vya habari tena vimekuja na taarifa inayostua masikio na kutia 'simanzi' ukifikiria kwa undani. Lakini ni wazi kuwa hilo linalozunguzwa na kuandikwa ndilo hasa lililotokea. Nalo ni kwamba Jeetu Patel kupitia kampuni yake ya Escort Tanzania ikiwa kampuni mama ipo India, kashinda zabuni ya kusambaza matrekta ya KILIMO KWANZA kwa JKT,zabuni yenye thamani ya bilioni 50 fedha za kitanzania.
Waziri mwenye dhamana amekiri kuwa hakuna shaka yoyote kuhusu kuwepo kwa harufu ya rushwa na zabuni imetolewa katika misingi ya uwazi na uwajibikaji kwa kampuni husika.
Habari hii katika gazeti la Mtanzania Daima iliibuliwa kama vile mfanyabiashara maarufu nchini Yusuffali Mehbub 'Manji' kuwa hakuridhika na 'mchakato' wa ushindi wa Patel. Gazeti hili lilidai kuwa Manji anaona kuna harufu ya 'Takrima' hadi kufanya Jeetu awa mzabuni bora.
Gazeti la serikali la kiswahili 'Habari Leo'lilikuja na kanusho la taarifa za Mtanzania Daima, likinadi wazi kuwa Manji moyo wake mweupe na hana kinyongo na maneno ya Mtanzania Daima hayana hata chembe ya 'ukweli'.Lililowazi ni kwamba Patel kaibuka kidedea katika zabuni ya serikali inayomshitaki!Nasema ukistaajabu ya Musa utayaona ya Firauni.
Makala haya haijadili ushindi wa Jeetu Patel kupitia kampuni yake ulikuwa wa halali au la, hiyo ni kazi ya kipolisi,IGP wakili Said Mwema na vijana wake na upande mwingine Kamanda Dr. Edward Hosea na vijana wake wa TAKUKURU, ndiyo wanaweza kutoa majibu sahihi ya nini kilitokea hadi Manji kakosa Patel akaonekana lulu.
Bali siye tutajaribu kutupia macho ushindi huu wa 'mtuhumiwa' wa kesi ya Uhujumu Uchumi,wa fedha za EPA J Patel una maana gani katika elimu ya maadili ya biashara(Business Ehtics).
Nikisoma maoni ya mtanzania fulani katika mtandao wa gazeti la serikali 'Habari Leo' chini ya habari 'Manji akiri kukosa 'dili' la kilimo kwanza' alionesha wazi kuwa ushindi huu wa zabuni kwa Jeetu Patel umeleta 'ukakasi', kwa kuzingatia kuwa J.Patel ni mtuhumiwa wa EPA!
Hapa kuna mambo mawili tunaweza kuyaangalia mosi sheria zetu na pili ni hili la elimu ya maadili kwa wasomi wa vyuo vikuu. Ambao ninaamini ndiyo waliunda jopo la kupitisha zabuni kwa Jeetu na kampuni yake ya Escort ya India.
Katika sheria inaonekana wazi kuwa hatuna sheria inayodhibiti mtu aliyefikishwa mahakamani kwa kosa kama la 'UHUJUMU UCHUMI' kuendelea kushiriki zabuni tena za serikali nayo ndiyo inayomshitaki!
Katika hili lazima tuangalia sheria zetu kwani zinaonekana wazi kuwa zimezeeka. Kwani kama tumeweza kushikilia pasi yake ya kusafiria, iweje tunashindwa kuweka kipengele kama hiki ili kulinda nidhamu ya mahakama!
Lazima ieleweke kuwa msingi mkuu wa sheria ni kuwatumikia jamii ya watu husika, sasa kama nilivyoonesha hapo juu kuwa watanzania wamepatwa na 'ukakasi' juu ya ushindi wa mfanyabiashara huyu mkubwa nchini, ambaye watu fulani waliweka wazi kuwa yupo katika kila 'utafunaji' mkubwa wa pesa nchini usiao halali.Ni wazi kuwa tunahitaji sheria katika hili, ili kulinda siyo tu heshima ya mahakama, la bali pia kuweka urari uliosawa kwamba mfanyakazi akishitakiwa na kuwepo mahakamani kwa zaidi ya miezi sita basi kuna haki zake zinasimama pia mshahara unaanza kutoka nusu,mfanyabiashara naye hapaswi kufaidi tu huku yu katika kizimba.Hii ni nchi ya wafanyakazi na wakulima,SIYO!
Pili lazima sasa tuanze kufundisha somo la maadili ya bishara(Business Ethics) vyuoni kwa wasomi wetu ama la itakuwa kichekesho kila siku. Maadili ya bishara si sheria, isipokuwa ni uwezo wa kutafsiri nakuamua lipi jema na lipi baya kulingana na hali ya watu wa jamii husika, kwa faida ya jamii hiyo katika tendo husika.
Tanzania vyuo vingi vinafundisha 'Business Ethics and Law', si sawa hata kidogo.Ni IFM(Institute of Finance and Management) pekee ndiyo wana kozi ya Business Ethics kwa wanafunzi wa MBA International Business wanayoendesha na Taasisi ya Biashara ya Nje ya India.Kwani katika kozi ya Business and Law ambayo vyuo vingi vya elimu ya juu wanaendesha wameweka nguvu nyingi katika kufahamu 'vifungu' vya sheria na si maadili ya biashara mara zote hiki kinasahaulika!Kiukweli maadili ndiyo biashara ya Ulimwengu wa leo na hasa ushindi katika soko la Ulaya upo katika kampuni zenye maadili.
Na hili ndiyo hayo matunda ya kumpa zabuni Jeetu, kwani kama sheria haipo wale wahusika katika huu mchakato wangejiuliza tafsiri ya kumpa Jeetu zabuni kwa wakati huu ni nini?Hapa wangeweza kumuondoa mapema katika mchakato. Linawezekana hata kama fedha zenyewe asili yake ni India.
Hebu tuone mifano michache ya maadili ya biashara ili tuone sheria na watawala wanavyoweza kuepukwa na badala yake maadili kufuatwa kwa faida ya jamii na ukuaji wa biashara kwa ujumla.Charles Cadbury wakati majeshi ya Uingereza yanakwenda kupigana Afrika Kusini katika 'Anglo Boer War' alitakiwa kuwauzia biskuti,lakini kwa vile yeye hakuunga mkono ile vita 'kimtizamo' aliuza bila faida! Na hili alilifanya kama uoga kwa utawala wa kifalme lakini alikuwa tayari wafanye wengine ila alilazimishwa.
Vivyo hivyo wakati fulani kampuni zile zote zilizokuwa zikifanya maandalizi ya tamasha la mwanamuzi Robert Kelly maaruku kama R.Kelly na Shawn Carter maarufu kama 'JAY-Z' kwa ajili ya uzinduzi wa albam ya 'Greatest of the both world' zilijitoa pale Kelly alipofikishwa mahakamani kwa madai yakujihusisha na mshichana aliye chini ya miaka 81 kimapenzi.
Si kama walimtenga Kelly wakati wa shida la hasha walimamisha uzinduzi kwa vile ingekuwa ni kama 'kuunga' mkono kitendo alichokuwa 'akituhumiwa' kukifanya kuwa ni cha heri. Na wala siyo kuwa nao pia waliungana 'kumsulubu' Kelly hapana isipokuwa ni kuheshimu maadili ya biashara na kulinda heshima ya mhimili mmoja wapo wa utawala MAHAKAMA.
Ingawa Kelly alishinda tuhuma zile na mahakama huru kumuona hana hatia, lakini lililowazi ni kwamba huwazi kufanya jambo na mtu ambaye yu kizimbani tena ambalo linaleta faida ya kibiashara, hata kama mtu huyo ushahidi unaonesha kuwa yu hana hatia. Na huu ndiyo msingi mkuu wa maadili ya biashara kulinda 'masilahi' ya wengine, vivyo hivyo zabuni ile hakupaswa kupewa Patel ili kulinda masilahi ya Jamhuri ambayo inamshitaki.
Kwa hili hatupaswi kumlaumu Patel, ila kama nilivyosema, huu ni wakati sasa wa kungalia elimu yetu ya biashara na kuingiza somo hili la maadili biashara(Business Ethics) pia kuangalia sheria zetu katika kuhakikisha hatui wachekeshaji katika nchi yetu wenyewe.
Katika nchi za Ulaya na Marekani kampuni zinazozingatia maadili ya biashara ndizo zinazofanya vizuri sokoni na walaji wana muamko katika kuhakikisha bidhaa wanazotumia si za kiyonyaji, hazitumikishi watoto katika kuzalisha bidhaa zake, zinalinda mazingira, hazitoi hongo ndani na nje ya nchi, zinatoa bei nzuri kwa wakulima wa nchi masikini ( Fair Trade na Body Shop). Haya ni maeneo machche tu.