Saturday, December 26, 2009

Vyombo vya habari na matangazo ya biashara ya elimu feki

Biashara ya elimu ‘feki’ ama kwa kiingereza‘diploma/degree mills’ inaendelea kushamiri Duniani.Hili ni tatizo la Ulimwengu, huku wadadidi wa mambo ya biashara ya Elimu wakikadiria kuwa zaidi ya karne sasa Ulimwengu unasumbuliwa na kansa hii.

Nini maana ya ‘Diploma mills’ hii ni taasisi iliyokuwa tayari kukupa hati ya kielimu bila hata ‘kisomo’ au kuingia darasani. Tafsiri hii inatia ndani pia hata kama ukawa unahudhuria na testi umefanya na kufaulu kwa viwango vya taasisi yako lakini ‘doa’ ni kwamba hautambuliki.

Katika zama za mawasilinao ya ‘kompyuta’ ambapo mtu anaweza kufyatua vyeti na kuthibitisha kuwa na taaluma husika kwa ngazi ya shahada ya kwanza, ya uzamili au Uzamivu(PhD) biashara hii imekuwa kwa kasi mno. Watu wengi ama kwa kufahamu au kutofahamu wamejikuta wakiingia katika mkumbo wa kupata shahada feki.

Ulimwengu unahangaika, watu maarufu na viopngozi wa umma na taasisi zake wako bega kwa bega kupiga vita ‘elimu feki’. Mwa mfalme Prince Charles, amewahi kukemea suala hili na kutaka juhudi za wazi zichukuliwe ili kudhibiti hali hii.
Tanzania ya leo inasukwasukwa na wimbi la upatikanaji wa wataalamu wenye vyeti feki.

Pamoja na tahadhari zinazotolewa juu ya hatari ya shahada ‘feki’ lakini la kustaajabisha ni kwamba idadi ya watu wanaopata na kununua elimu hii inaongezeka, FBI na Interpol wanaweka wazi kuwa biashara hii inashamirishwa na wateja wenyewe.

Katika Amerika sheria za majimbo zinajaribu kukaba, na kupambana vilivyo na hali hii, lakini yatupasa kufahamu kuwa kabla hatujasema chuo fulani kuwa kuna vyuo vimenyagwanywa ‘hadhi’ katika ya safari baada ya kubainika kuwa mchezo wao si mwea kitaaluma.

Kutotambulika ni hasa pale unapotaka kujiendeleza, mathalani umefanya elimu kwa ngazi ya cheti kwa elimu ya kompyuta kwenye chuo fulani pale ‘Kariakoo’. Cheti hiki kama hakikupi kinga ya kujiendeleza kielimu kwa ngazi ya Diploma ya elimu ya kompyuta katika vyuo makini, kama vile UDSM, IFM! Ni wazi kuwa chuo ulichosoma ni ‘feki’.

Biashara hii imekuwa ikishamiri na kwa kiasi kikubwa ingawa hakuna takwimu sahihi lakini kuwepo kwa wahitimu hao ni dalili ya wazi, pia kuongezeka kwa vyuo vyenyewe ni mwanga tosha kuwa biashara yao ina wateja. Mafanikio haya yamechangiwa na vyombo vya habari pia sekta binafsi kwa kukubali wahitimu wa vyuo hivi.

Magazeti makubwa kama Forbes, Herald, the Economist yamekuwa yakitoa matangazao ya vyuo hivi ingawa yanaelewa ni njia maoja wapo ya kushamirisha ‘dploma mills’. Mara zote wahariri wanapoulizwa kuhusu, mustakabili wa wao kukubali kutoa matangazo ya vyuo ‘bomu’.Hudai kuwa wasomaji wao ni watu makini na wanajuanini wanachokifanya kwa hivyo ni jukumu la wateja kujikinga.

Safari hii mteja hana msaada na amekuwa daraja la watu kujipatia utajiri. Katika Tanzania magazeti yetu na TV za umma na binafsi vinashindana kutangaza vyuo ambavyo havitambuliki na NACTE, VETA wala TCU kwa taaluma wanazotoa.

‘Intake’ ya Januari inakuja kwa vyuo vingi vya Ulaya, Amerika na Asia Kusini. Ni wazi kuwa usipokuwa makini utajikuta umeingia katika ‘gogoro’ la kusoma chuo feki.

Makala haya itajaribu kutoa mbinu chache ili uweze kujinasua na mtego wa kuingia gharama za kusoma chuo kisichotambulika.

Mosi ni vyema kufuatilia kila wakati ilikujua mwenendo wa Chuo chako ukoje .Je kinaendelea kutambulika au kimeingizwa katika mkumbo wa vyuo feki?Na hasa unapoenda kusoma Vyuo binafsi nje ya Tanzania.

Kwa mfano Chuo cha Pacific Western University (PWU) ni chuo kilichoanzishwa mwaka 1977, kikiwa na wasomi wengi hodari na walioweza kufikia katika ngazi ya U-profesa na wengine Marais wakiwa wanaheshimika na taasisi kubwa kama IFM na Benki ya Dunia.

Profesa Bingu wa Mutharika, PhD yake ya ‘Development Economics’ kaisomea PWU, mwaka 1984 (fuatilia htt://www.un.org/ecosoc/docs/pdfs/Mutharika.bio.pdf.)

Chuo hiki kilikuja kupoteza hadhi yake pale kilipotoa PhD ya miezi 12!Katika 2006 kwa mmoja kati ya wakurugenzi wa Taasisi ya Marie Currie, taasisi yenye kuheshimika sana Duniani.

Hii haimaanishi kuwa PhD ya Mheshimiwa Rais Bingu wa Mutharika ni feki, hapana kwani Chuo kilipoteza hadhi wakati yeye keshamaliza. Tunachosema hapa ni mwamba yakupasa kufuatilia mwenendo wa shule yako mara kwa mara.

Ni wazi kuwa katika mfumo wa soko huria ukaona kuna rafiki yako ambaye amesoma chuo ‘feki’ akiwa ameajiriwa katika taasisi binafsi. Hili lipo sana, vyeti hivi vinakumbana na ‘kigingi’ pale vinapojaribu kupenya katika taasisi za ‘serikali’Fulani kasoma pale haitakusaidia sana. Utawezaje kutambua kuwa shahada hii au chuo changu ni feki?

Tumeshaonesha hapo juu kuwa, biashara ya Ulimwengu ya vyeti feki inashamirishwa na vyombo vya habari hasa TV, magazeti redio tena ni vyombo vinavyoheshimika.

Chukulia mfano Chuo A unakikuta kinatangaza nafasi za masomo katika gazeti la The Economist, hadhi ya hicho chuo utakichukuliaje?Ni wazi kuwa unaweza ukanasa katika mtego huo.Vivyo hivyo magazeti ya nyumbani kunayanayoshamirisha elimu feki.

Ukiona chuo chako kinatoa elimu chini ya muda uliozoeleka, diploma ya miezi ya sita, PhD ya miezi 12, hapa anza kuwa na shaka!

Fuatilia kama chuo kimesajiliwa na kinatambulika kweli.Tahadhari kuwepo kwa utambulisho kutoka kwa wahusika kunaweza kukupumbuza. Mara nyingi wanatumia nembo za ithibati za kitapeli ambazo wala nazo hazitambuliki.
Kwani mara zote vyuo hivi feki vimekuwa vikijinadi kwa kuweka nembo na ithibati zenye kuthibitishika lakini ukweli wa mambo ni ‘waongo’. Yakupasa kutembelea tovuti za nchi husika za elimu. Na kama unaweza tembelea balozi ya nchi husika kwa taarifa za awali.

Kwa Tanzania kuna taasisi zinazojihusisha na mwenendo mzima wa kuratibu elimu, kuna VETA, NACTE na TCU ni vyema ukatembelea tovuti zao, ama kubisha hodi katika ofisi zao kabla hata hujalipa ada.

Ada pia inaweza kuwa kigezo cha kukustua pia. Vyuo bora na vyenye kuheshimika katika Uingereza kwa mfano kwa ‘elimu’ za kijamii vinaanzia na ada ya paundi 8,500 kwa mwaka kwa wanafunzi wa kimataifa. Ukikuta chini ya hapo, weka shaka!

Hatutaki kusema kuwa bei ndiyo kigezo muhimu lakini pia elimu bora siku hizi inahitaji pia gharama hasa kwa elimu za magharibi. Profesa atakaye fundisha mwanafunzi wa cheti, atafundisha pia kwa PhD na amshahara wake uko pale pale hivyo ada itakuwa juu kwa cheti pia.

Kuwa makini na vyuo vya binafsi. Katika Ulaya na Marekani vyuo vingi vya umma vina majina ya miji husika. Sasa unapokwenda katika vyuo ambavyo vinamajina matamu ya watu, jaribu kutia shaka. Ni wazi kuwa yakupasa kutoamini kila kitu, na hasa siku hizi za utapeli wa kielimu.

Chukua tahadhari na vyuo vinavyotofautiana herufi. Hapa namaanisha kwamba kuna vyuo vinajaribu ‘kukopi’ sasa tofauti ni ndogo tu unaweza kuingia katika mtego wa elimu feki. Kwa mfano Greenwich University hiki ni feki, halisi ni University of Greenwich. Wamecheza na maneno. London School of what what, hawa ni jamaa wanaoiga ukongwe wa London School of Economics kuwa makini!

Kama unaenda kusoma Marekani ni vyema ukatembelea tovuti ya www.edu.gov, huku utakuta mwenendo mzima wa vyuo feki na vyenye hadhi na ‘wameposti’ ili ukasome kwa heri katika vyuo vyenye heshima na thamani ya pesa yako.

Epuka mtego wa taasisi za kidini zinazoendesha vyuo vikuu na hasa Marekani.Taasisi hizi zimeruhusiwa kutoa shahada za elimu za dini, lakini inapokuja kuwa wanatoa shahada nyingine kuwa makini na vyuo hivyo. Vingi ya vyuo hivi vinaanzishwa baada ya kanisa kufunguliwa na ndani ya wiki mbili wanaleta PhD sokoni tofauti na elimu ya dini.
Mara nyingi Serikali ya Marekani imeshindwa kuvibana vyuo hivi lakini ukweli wa mambo vingi havina hadhi.
.
Mapambano ya elimu feki, diploma za miezi sita na PhD za miezi 12 ni vita ya jamii nzima. Vyombo vya habari Tanzania vina nafasi ya kusitisha kukua kwa biashara hii, pasi kujali faida kwao tu, bali pia kujali masilahi ya Tanzania.
Vyombo vya habari kwa sasa vinaangali nani ana elimu feki tu, lakini wao kimsingi wanachangia vijana wa kitanzania kuingia katika mkumbo huo kwa kukubali kutoa matangazo haya.
Matangazo ya vyuo vya Ulaya, Marekani na Asia kusini yamejaa kweli kweli katika magazeti ya Tanzania. Hakuna anayejiuliza kama kweli vyuo hivyo vina hadhi na ithibati katika mfumo wa elimu ya Tanzania.
Tupo kimya. Yatupasa kubadilika, na kubadilika ni kukataa matangazo ya vyuo feki pia katika magazeti yetu. Na si kusubiri wasome wakirudi ndiyo tuanze kuwashambulia.

Hili la kukataa matangazo ya vyuo feki tunaweza, ni vyema tukilifanyi

Sunday, December 20, 2009

Haki inapodumaza ukuaji wa biashara, si haki tena

Katika nchi ‘zinazofaa’ kufanya biashara Duniani Tanzania ni ya 115, kwa mujibu wa rekodi za mwaka jana za Benki ya Dunia. Ni wazi kuwa changamoto hii inasababishwa na mambo mengi ikiwemo hili la kisheria. Tanzania imekuwa ikionekana kuwa ni ‘pagumu’ mno kufanya biashara kwa sababu ya taratibu za kisheria tulizo jiwekea.
Ucheleshwaji wa haki za kisheria imekuwa ni kona moja wapo inayodumaza ukuaji wa biashara katika Tanzania. Tangu nchi kuingia katika mfumo wa uchumi unaoongozwa kwa nguvu za soko, mabadiliko makubwa ya kisheria yamefanywa, na yanaendelea kutekelezwa ikiwemo uanzishwaji wa Mahakama ya Biashara.
Mahakama hii iliyoanzishwa 16, Septemba 1999 kwa msaada wa DANIDA imekuwa ni mwanzo mwema kwa mwenendo wa kutafuta haki za kibiashara katika Tanzania. Makala haya haitajikita katika kona ya kisheria kungalia nini kinatokea huko katika sheria, ila itaangalia masilahi ya kibiashara kwa hatima ya wajasiramali ambao nchi inajitahidi kuwaibua na siku zao zijazao za ukuaji wa biashara kwa Tanzania.
Katika ukanda wa Afrika Mashariki Tanzania inaendelea ‘kuchanua’ kwa ukuaji wa uwekezaji wa mitaji toka nje. Ni wazi kuwa kiu ya mwekezaji yoyote awe wa ndani au wa nje ni kuona kuwa lengo kuu la mtaji linafikiwa. Nalo ni faida.
Ili kufikia dhima hii ‘muda’ ni suala la muhimu. Hakuna biashara isiyoendana na muda kwani hiki ni kiungo muhimu katika ya wateja na mzalishaji bila kujali muda ni wazi kuwa ‘utawachefua’ wateja wako.
Mwanamuziki wa kizaki kipya Farid Kubanda, Fid Q, katika mashairi ya wimbo wa ‘Fid Q’ anaweka wazi kuwa….muda si rafiki wa mwandamu’.Ni muhimu kukimbizana na adui muda katika heka heka za kila siku.Na mara zote ukiachwa nyuma na muda ni majuto, ndiyo maana tunasema kuwa si rafiki wa mwanadamu kwa vile matokeo yake ni ‘mabaya’.
Vivyo hivyo mteja wa mahakama anapopeleka shauri lake mahakamani anategemea kupata suluhu ya suala lake kwa haraka ili akimbizane na muda
Tanzania mambo ni kinyume chake. Wakili na Mkuu wa Idara ya Sheria ya Benki ya NBC 1997 Ltd, Felix Kibodya, anakadiria kuwa kuna zaidi ya bilioni 100 za kitanzania zimekwama katika mikono ya kisheria kwa kesi zilizofunguliwa muda ‘mrefu’ mahakamani.
Hasara inayotokana na kucheleshwa kwa haki mahakamni katika Tanzania haijawahi bado kuwekwa katika tarakimu, na inakadiriwa mara nyingi shauri uchukua kati ya wastani wa miaka 3 na zaidi.
Bilioni 100 ni pesa nyingi sana, niwazi kuwa biashara zilizoathiriwa na ucheleshwaji wa kesi mahakamani ‘zinachechemea’ na kama si kufa kabisa. Unapokuwa na ‘fungu’ kubwa kama hili halizunguki katika mfumo uliowazi wa kibiashara ni wazi kuwa tunayo yaona ni wazi kuwa ni matokeo ya ‘uzubavu’ huu.
Hili la uchelewashaji wa haki nalo linaonekana kuwa kikwazo kwa taasisi za kifedha kukopesha wajasiriamali. Asilimia 4 ya wajasiriamali ndiyo wanaofaidi na mikopo.

Ni wazi kuwa kunauhusiano kati ya taasisi iliyo na kesi nyingi na fedha nyingi zimedumaa kwa kusubiria haki kuwa itapunguza utoaji wa mikopo kwa wateja na hata kuweka masharti magumu.

Mahakama ya Biasahra ilipoanzishwa mwaka 1999, kesi 116 zilifunguliwa, huku Taasisi za kifedha zikiwa ndiyo wateja wakubwa. CRDB pekee ilikuwa na kesi 18. Tunachoweza kujionea ni kuwa kesi zipo nyingi zenye muelekeo wa kibiashara na zitaendelea kufunguliwa mahakamani.
Hapa isieleke kuwa Mahakama ya Bishara haikuwa na kasi katika kupatia suluhu ya baadhi ya mashitaka yaliyo mbele yake. La hasha, takwimu zinaonesha mwaka 2001 kesi 301 zilifunguliwa, 227 zilipatiwa ufumbuzi, 2002 kesi 351 ziliripotiwa na suluhu kwa kesi 243.
Mabadilko ya kisheria ya mwaka 2002 iliifanya mahakama hii kupopekea kesi chache mwaka 2003, kesi 153 tu zilifunguliwa na hoja 242 zilipatiwa suluhu ukijumlisha na ‘viporo’.
Upungufu huu wa kesi ulitokana na mabadilko ya sheria ambayo yalihitaji mashitaka yawe na thamani ya milioni 100 na kuendelea ili uweze kufungua kesi katika kanda hii ya Mahakama.
Kutokana na mabadiliko haya ni wazi kuwa zile zote zilizo chini ya milioni 100 zimelundikana katika makahama za mwanzo na wilaya.
Jitihada za wazi za muhimili huu wa dola wa kuongeza ajira za mahakimu ni za kupongezwa.
Lakini tunahitaji kwenda mbele zaidi na hasa katika kesi za biashara. Kwani muda hausubiri na ni wazi kuwa wajasiriamali wataathirika kwa kukosa haki kwa wakati.
Bilioni 100 ‘kukukaa’ bila kuzunguka ni hatari kwa ukuaji wa biashara katika Tanzania.
Hakuna ajuaye athari za muuza mahindi aliye na kesi mahakamani kwa kukosa mahindi zaidi ya yeye na familia yake. Kidhibiti kinakaa hadi kinaoza wakati kimeshaonekana!Kwa nini kisiuzwe, pesa ikapunguza maumivu kwa mshindi baadaye.

Biashara inahitaji haki kupatikana kwa haraka, ni vyema tukaimarisha mhimili huu wa dola kwa maendeleo ya sekta ya biashara ya Tanzania.
Kucheleweshwa kwa haki kibiashara hakuna mwisho mwema kwa taasisi za kifedha wala ‘mjasiriamali’. Ni vema tukajipanga kuondoa kero ya kuchelewa kwa haki mahakami kwa nia njema.
Jaji Mkuu, Augustino Ramadhani ameliweka wazi hili kuwa ufinyu wa bajeti ni kikwazo kwa sekta hii kuhakikisha haki inapatikan kwa watanzania. Ni wazi kuwa hili linaathiri ukuaji wa mitaji na biashara kwa wajasiriamali katika Tanzania.
Ni vema hili tukalikabili kama nchi na kwa maajaliwa ya uchumi wa nchi yetu.

Saturday, December 12, 2009

SEKTA BINAFSI NA MAJAALIWA YA TANZANIA

Kwa zaidi ya miongo miwili sasa serikali ya Tanzania inajitahidi kila iwezalo kuhimarisha sekta binafasi. Mageuzi ya kiuchumi na mifumo ya kisheria na kiutendaji inafanyika katika kuhakikisha kuwa sekta hii ambayo ni mwajiri mkubwa kwa sasa inkuwa. Kwa hakika sekta binafsi ndiyo muajiri, ndiyo muongozaji wa uchumi wa Tanzania.
Kukua kwa biashara yoyote kinadharia inahitaji kuwepo kwa kuaminiana (trust) kati ya mteja na mtoa huduma bila kusahau kuwa masilahi ya jamii husika yanalindwa. Na hili linatokea hata muuzaji akakupa mzigo wa mamilioni ya shilingi bila hata kusainishana, akiwa na tumaini kuwa utarejesha stahiki yake.
Kuaminiana ndiyo biashara ya leo ya ulimwengu, jaribu kufikira mtu anayenunua gari toka Japan akiwa Nakapanya Masasi kwa kutumia ‘internet’ ameona tu picha na maelezo ya kampuni husika akaamini na kutuma fedha bila ‘woga’ Japan bila hata kusani mkataba akanunua gari akiamini kuwa litatumwa.
Ujenzi wa imani si kazi ya siku moja katika biashara, ni mfululizo wa matukio na utendaji ndiyo yanayoimarisha mawazo ya mteja na kuhisi kuwa analindwa na kuthaminiwa na kampuni husika. Kimsingi zinatia ndani hata kampuni zenyewe zinajiendashaje, kampuni yenye madeni na kesi nyungi mahakamani za kushitakiwa ni wazi kuwa inapoteza imani za wateja.
Wateja wa sekta binafsi katika Tanzania ni watanzania, ambao wamegawanyika katika makundi mawili wateja wa nje(walaji) na wandani (wafanyakazi).Katika Tanzania sekta binafsi pia inaendesha shughuli ambazo zamani zilikuwa zinafanywa na serikali, kama kukusanya kodi, kusanya taka, kuendesha harambee, kutuo elimu mifano inaweza kuwa mingi. Lakini lililowazi ni kwamba sekta hii imechukua nafasi kubwa ya serikali katika maeneo mengi ya kiuchumi katika Tanzania.
Muunganiko huu unatufanya tuone kuwa suala la maendeleo si tena kitu cha ‘kuhodhiwa’ na serikali. Lengo kuu ni kufanikisha maendeleo kwa mtanzania. Swali ni, je mandeleo haya yatapatikana au ni ndoto tu?
Ni muunganiko unaoonesha kuwa bila kudhibitiwa hautakuwa na mwisho mwema. Matokeo mengi yanayotokea sasa katika uchumi wa Tanzania yanatufanya tujiulize hivi kweli sekta binafsi ni mkombozi au kitanzi?
Serikali kwa nia njema inashamirisha sekta hii, kuanzia miaka ya 1990. Uhusiano huu kati ya serikali na sekta binafsi (Public-Private Sector Partinership) kuna maeneo yanatupa wasi wasi!
Hivi karibuni kuliripotiwa kufutwa kwa mkataba wa kukusanya kodi katika ‘stand’ ya ubungo kwa kampuni ya Smart Holdings. Kampuni hii ilikuwa inadai inakusanya milioni moja kwa siku, lakini serikali kupitia Jiji la Dar-es-Salaam leo hii inakusanya milioni 4 kwa siku!
Smart Holdings ‘imeonekana’ tena katika jengo jipya la Machinga Complex kama msimamizi wa makusanyo, wa Jengo hilo. Na taarifa za awali zinaonesha wafanya biashara kupitia umoja wao wameikataa ‘SMART’. Hii ni fedheha.Lakini linalotia uchungu ni taarifa za kukataliwa kwa kampuni iliyoonesha kuwa inaweza kuleta pato la bilioni 1.2!
Lengo ni kupata fedha kwa ajili ya maendeleo vip tena tunakataa dau kubwa tunakubali dogo?Inawezekana ikawa aliyeleta dau kubwa ametia ‘chumvi’ hesabu zake, lakini hili halina nguvu sana katika biashara.
Sekta binafsi inaonekana wazi kuwa ni kichaka cha watu wachache kuja kufaidi jasho la walio wengi bila hata tija kwa pato wanalochuma. Kimsingi huu ni mwanguko wa maadili ya biashara.
Ni wazi kuwa hakuna maadili ya biashara kama hakuna maadili ya umma au ya kijamii. Mwenyekiti wa Jengo la Machinga Complex Iddi Azzan ‘Zungu’ mbunge wa Ilala amekaririwa akiweka wazi kuwa hata kabla jengo halijakamilika kampuni hii imepewa kazi hiyo ya kukusanya ushuru, na lenye kuumiza zaidi bila hata vikao halali vya ‘tenda’ kuketi.Sasa walijuaje kuwa kuna mshindani aliyeleta ‘dau’ bilioni 1.2 amekataliwa!Lisemwalo lipo waswahili wanasema.
Hii ndiyo Tanzania ya leo. Mwenendo kama huu wa kampuni kupewa kazi bila hata vikao halali katika Tanzania umeonekana maeno mengi na hasa katika wilaya. Kuna watu wanakampuni nyingi za mifukoni wakijipa ‘tenda’ za kuendesha kazi za serikali kwa manufaa ya umma lakini hata uwajibikaji hawana.
Hapa ndipo tunapojiuliza majaaliwa ya Tanzania katika nyakati zama za sekta binafsi, wapi sekta hii inatupekela?Isielweke kuwa hatuitaki sekta binafsi ila tunahitaji ‘mbinyo’ (regulations) zaidi katika kuongoza sekta hii kwa manufaa ya watanzania wote.
Sekta binafsi imekuwa ni watu wenye kulia sana kuomba misamaha ya kodi na uwanja huru wa biashara. Lakini lenye kutia hofu ni juu ya mwenendo mzima wa sekta hii hasa katika kulinda na kujali masilahi ya watanzaia.
Matukio ya rushwa na kuongezeka kwa vitendo visivyo vya maadili vimekuwa ni vitu vya kawaida katika mazingira ya biashara ya Tanzania.Hupati akzi kama huna ‘ten percent’ Wakati umefika wa watu walio katika sekta binafsi kujiangalia mara mbili, wanahitaji kuendesha sekta hii kwa manufaa ya Taifa au ni kwa uroho wa kujilimbikizia mali na kuwaacha watanzania wakiwa watumwa daima dumu.
Mpaka leo sekta binafsi inakaata kuongeza mishahara mipya kwa uajanja wa ujanja wa vikao visivyo kwisha. Kuendesha uchumi si kwa ‘maumivu’ ya wafanyakazi. Ni kwa masilahi ya wadau wote. Kampuni inapata faida ya bilioni 26 baada ya kulipa kodi, ‘bonus’ ya mwaka ikitoka kuna wafanyakazi wanapata 2000/= kampuni yenye wafanyakazi 600 tu.
Waziri Mkuu Mizengo Kayanza Pinda hivi karibuni amekaririwa na gazeti moja la kila wiki akiikemea kampuni moja ya Kichina inayojenga barabara ya Arusha hadi Namanga kuwa ulipaji wao wa mishahara midogo ndiyo chanzo cha kukosa wafanya kazi wenye sifa. Kwa hakika hii ndiyo sifa ya sekta binafsi, ni mishahara midogo na malipo ya ‘kujuana’ wanasema huna ‘address utaishia hapo hapo’.
Yanayotendeka huko yanatia uchungu, rafiki yangu yupo katika kampuni moja ananiambia kuwa alikuwa anaongozwa na meneja wa kidato cha nne, naye alikuwa analipwa mshahara mkubwa kuliko yeye ‘graduate’ .
Kampuni zingine zinaheshimika katika Tanzania lakini utakuta watu wake ni ‘vihiyo’ na wanalipwa pesa nyingi ili kuwavunja moyo wahitimu wenye sifa. Mwenendo huu hauna mwisho mwema kwa biashara ya Tanzania na sekta yenyewe kwa ujuma. Kwani mfanyakazi asiyepata motisha hawezi kuwa ‘mbunifu’
Sekta hii kiuchumi ni muhimu lakini tunahitaji kuiangalia mara mbili na kutunga sheria na taratibu zinazoendesha sekta hii kwa uwazi kutoka katika ajira zake, mishahara, marupurupu na stahiki zingine na si kuacha kila kitu kiendeshwe na wao kama wanavyopenda.
Kama wanahitaji misamaha ya kodi ni lazima nao pia waoneshe jinsi wanavyojali wafanyakazi wao na si kupata misamaha huku wakilipa mishahara inayodhalilisha wazawa huku wageni wakilipwa mishahara minono bila tena hata sifa za kielemu kwa nafasi wanaozishikilia.
Hakuna nchi duniani iliyojengwa na wageni wala na watu watoa rushwa na wasiopend maadili. Ni wazi kuwa kiu yetu na matumaini yetu ya kuona sekta binafsi inatupeleka katika nchi ya ‘asali na maziwa’ haitakuwa na maana kama sekta hii itakuwa inaendesha mambo yake kwa stahili ya sasa.
Tujenge mwenendo wa kuaminiana kukosa imani kwa wateja na kukataa kampuni ni wazi kuwa hili ni doa kwa sekta binafsi. Basi yatupasa kujenga imani za wateja kwa vitendo na si ubabaishaji wala rushwa havina mwisho mwema.

Saturday, December 5, 2009

kuhamasisha mitaji toka nje ni 'mbio' za ubora si uwingi

Katika ukanda wa Afrika Mashariki na Afrika kwa ujumla Tanzania inafanya vyema katika kuvutia mitaji toka nje. Ripoti ya UNCTAD ya mwaka 2008 inataja eneo la Afrika Mashariki kuvutia asilimia 4 ya fedha zote zilizoingia Afrika, huku Uganda na Tanzania zikijizolea chumo kubwa. Ila changamoto kubwa ni kupunguza migogoro inayochangiwa na kuvutia mitaji ‘isiyo na ubora’ bali ni kujali ‘uwingi’.
Tanzania sasa ‘inazizima’ na vyombo vya habari kila kukicha vinapambwa na hekaheka za TRL ni vilio na maneno ya kukata tamaa toka kwa wateja(abiria) na wafanyakazi. Ni wazi kuwa hali si shwari, hali ya sintofahamu imetawala lakini lililokubwa ni majaaliwa ya sera zetu katika kuvutia mitaji toka nje(Foreign Direct Investment).
Changamoto hii ya migogoro katika kila ujio wa mwekezaji imekuwa ni ya kawaida sasa nchini, ila wakati wote imekuwa hatujifunzi somo. Ni kwanini migogoro hii kwa kiasi kikubwa inakuwepo katika mitaji(FDI) inayowekezwa na watu kutoka nchi zinazoendelea?
Mbio za kutafuta mitaji tangu zilipoanza katika Tanzania na hasa hizi za pili akiacha zile za miaka ya 1960, imekuwa ni kuangalia wingi tu na si ‘ubora’ wa mitaji. Wakati wote taarifa tunazopewa nikuwa tumeajiri watu wangapi na wala si kama kinachotumika na kampuni husika kina kiachangiaji katika kuinua hali za watanzania ya Tanzania. Manufaa yake ni chanya au hasi.
Mwanazuoni maarufu Profesa Issa Shivji anawaita wawekezaji ‘uchwara’ ni wazi kuwa jamii nzima toka wasomi hadi watu wa kawaida siku hadi siku wanaona FDI na namna tulivyoikumbatia nadharia hii kama mkombozi wetu wa kiuchumi haina mwisho mwema.
Mgogoro wa NBC ambao bado unafukuta ndani kwa ndani ni mwekezaji toka Afrika Kusini, kiwanda cha Sukari Mtibwa ni ‘mgogoroo’ kati ya Mwekezaji toka ‘Mauritius’, Kilombero Sukari ni hao hao toka ‘Afrika Kusini’. Wajasiriamali wanalia hawapati hata nafasi ya kuuza ‘embe’ kila kitu kinatoka ‘Afrika Kusini’ ndiyo mwekezaji aliyechukua hoteli tulizojenga wakati wa Ujamaa anatoka Afrika Kusini!NetGroup Solution walitoka Afrika Kusini na ATCL iliwahi kuwa na ndoa yenye utata na Shirika la Ndege la Afrika Kusini. Hili la sasa la TRL ni mwekezaji toka India.
Hatuna nia ya kusema kuwa wakati umefika kwa kuangalia miradi ambayo inakuja nchini inatoka wapi (origin) lakini kila dalili inaonesha hawa wenzetu wanaokuja katika nchi zetu hawana nia ya kutuona tunaneemeka, wala hawana nia ya kuiona nchi inajikongoja ila ni kuhakikisha wanatafuta ,malighafi’ na ‘masoko’ kwa ajili ya viwanda vyao.
Lazima tutambue kuwa hawa wawekezaji toka nchi zinazoendelea wanamashaka kama yetu na yatupasa kujipanga vizuri kisera na kimaamuzi.Ni wazi kuwa mitaji hii kutoka nchi zinazoendelea ni sawa na kucheza na mtu hatari(Dancing with devil), huku ukiamini labda amebadilika, lakini tunayoyaona nchini ni wazi kuwa uwekezaji huu hauna mwisho mwema.
Tumefika mahali tumegeuzwa soko la bidhaa zao huku sisi tukizalisha malighafi na kuwauzia kwa bei ya ‘kutupa’ kwa faida ya ajira ya watu 500 hadi 1000 tena vibarua wasio na bima wala kitambulisho wakifanya kazi kwa zaidi ya miaka 5!
Mwekezaji atafungua hoteli utapewa takwimu za kuwa anaweza kuajiri watanzania zaidi ya 100 ajira ya moja ya moja kwa moja na 300 ajira ya isiyo moja kwa moja! Mbio hizi hazina mwisho mwema na ndiyo hizo zimetukisha hapa tulipo.Yote haya ni mbio za ‘wingi’(quantity) huku tukikipa kisogo ‘ubora’(quality).
Ni vigumu kutafrisi ubora wa ‘mtaji’ ukawa na tafiri inayoichukua kila nchi,lakini lililokubwa ni kuangalia hali ya maendeleo ya nchi na nini inataka kupata kutokana na huo mtaji (FDI Spillover effects). Kwa mfano Tanzania haihitaji muwekezaji anayekuja kuuza ‘pipi au vyombo’ vya plastiki kama wale Wachina wa Kariakoo, au wale Wahindi wanaozunguka na biskuti duka hadi duka kutafuta mnunuzi wa jumla!
Hizi biashara ni za wazawa, lazima tuweke maeneo ya wageni kuja kuwekeza na wakiwekeza basi kuwe na tija kwa wazawa si kuwekeza katika kiwanda kisha unaleta mahitaji yote kutoka katika nchi ‘mama’.
Tunakumbuka jinsi TBL walivyoanza kuagiza chupa za bia kutoka Afrika Kusini mara tu walipochukua kiwanda huku tunakiwanda cha KIOO hali ambayo ilisababisha watanzania kukosa kazi, hadi leo hii mambo yamebadilika lakini baada ya vuta ni kuvute.Hali pia inatia matumaini kwa wakulima wa shayiri mkoani Arusha ambao wamepata nafasi ya kuuza malighafi yao kwa TBL huku wakihimarishwa katika kulima shayiri bora, hii ndiyo mitaji yenye ubora kwa nchi (positive spillover of FDI).Lakini hali si kwa viwanda vyote nchini.
Sasa tunalia na kiwanda cha betri cha Yuasa kilichopo vingunguti, kimefungwa kisa kuna mwekezaji anaagiza betri kutoka Uchina na Thailand. Tumegeuzwa soko huku kiwanda tunacho. Sasa wale vijana tunaowasomesha uhandisi na ufundi michundo huku tukiimiza wapende sayansi na tukiwalipia ada kwa asilimia mia watapata kazi wapi kama viwanda vinakufa ‘kibudu’ namna hii! Atalipaje deni lake la mkopo wa elimu kama hana kazi kwa vile kiwanda kimefungwa kwa kujali tu mwekezaji aliyefungua ‘store’ ya kuuza betri za magari toka nje.
Kilio kipo kwa KIBO Match group dhidi ya mwekezaji mjanja mjanja anayejidai anazalisha viberiti kumbe ameweka ghala na anavileta kutoka Pakstani. Huu si ushindani hata kidogo!Vile vile kwa wazalishaji wa makaa ya mawe Mbeya, ambao wakipeleka katika kiwanda cha sementi pale Wazo Hill wanaambiwa hayana ubora hivyo wanaagiza ‘makaa’ ya mawe kutoka Afrika Kusini. Ila tumekosa soko ndani Ujerumani wanasema haya ndiyo bora tena yenyewe. Hii ni ajabu, lakini ndiyo hali halisi.
Hili la kuongeza mbio katika ‘wingi’ tukiacha kuweka mkazo katika ‘ubora’ limepelekea kuibuka tatizo la uwekezaji ambao haufanani na kile walichokisema wakati wa kutia saini kwa mbwembwe za miali ya kamera na ‘champagne’. Hili la kukosa ‘ubora’ ni kero hasa kwa mitaji toka nchi zinazoendelea.
Kwa mfano Brookside wasindikaji wa maziwa ambao wapo Kenya wakiendesha kiwanda cha usindikaji wa maziwa na bidhaa zake. Mwaka 2007 walikuja Tanzania wakanunua kiwanda cha maziwa Arusha kwa ahadi ya kuwekeza zaidi ya dola milioni 20 kwa kiwanda cha UHT chenye uwezo wa kusindika lita 60,000 kwa siku. Baada ya miaka miwili ikabainika kuwa wamegeuza Tanzania kuwa eneo la kukusanya malighafi huku wakipeleka maligahfi hiyo Kenya! Sasa kampuni hii imezuiwa kufanya Tanzania kama ‘shamba la bibi’ na badala yake itimize yale yaliyokuwa yamewaleta.
Huu ni mfano mmoja lakini kampuni nyingi zimekuja nchini kwa ahadi na maneno kede kede ya kuwekeza katika mitaji ambayo ina manufaa kwa nchi badala yake wakaanza kuleta mitumba na kujenga gesti.
Changamoto nyingine ya mitaji hii kutoka nje ambayo inaikabii Tanzania ni hili la kufukuzia mitaji toka katika nchi ambazo zinaongoza kwa rushwa. Kenya, Nigeria zinawekeza katika Tanzania lakini hizi nchi zinatajwa kuwa zinaongoza kwa rushwa. Sasa unapokuwa na mwekezaji ambaye asili yake ametokea katika rushwa ndiyo yale yale kila ‘skendo’ mbili moja ni mwekezaji anatoka katika nchi zinazoendelea. Hii inadumaza ubora wa mitaji katika kufikia lengo.
Rushwa ni adui wa haki hivyo yule aliyekuwa makini na mwenye sifa hakupewa kapewa mtoa rushwa, kila siku ni vurugu na hatutaki kila kona badla ya kuchapa kazi kwani hana mtaji ana maneno. Haya ndiyo majaaliwa ya rushwa.
Katika siku za mwanzo za uhuru wake Kenya alichagua kuwabana wawekezaji toka nje na kuwaonesha maeno ya kuwekeza na si kila eneo walipewa nafasi. Wawekezaji hawakuruhusiwa kuwekeza katika maeneo ambayo wazawa waliweza na hili lilifanyika bila kificho. Leo hii Tanzania inaugulia namna ya kuwabana wawekezaji wanauza matufaa na vyombo vya plastiki mitaa ya kariakoo.
Nchi zisizokuwa na rushwa yenye kukera ndizo zinazopendwa sasa sisi kwa nini tusiamue kuwakataa hawa watu wanokuja kuwekeza kwetu kutoka maeneo ambayo rushwa ni tatizo. Matatizo yake ndiyo hayo Waziri Mustapha Mkulo amekiri wazi kuwa rushwa ni ngumu kuisha katika Tanzania na serikali haiiwezi, sasa kama jibu ndilo hilo haki za wafanyakazi na ubora wa mwekezaji utaupata wapi?
Katika siku za mwanzo za uongozi wake Mkuu wa Mkoa wa Dar-Es-Salaam William Lukuvi aliweka bayana kuwa atapambana na wamachina ambao ni ‘wamachinga’ katika mitaa ya kariakoo, lakini hadi leo hali ya mambo ni ngumu.
Mitaji yenye ‘ubora’ ni suala la kisera pia si suala la maneno ‘matamu’ yasiyoongozwa na kanuni wala ‘miongozo’.
Tangu ukoloni ilikuwa inajulikana wazi kuwa benki na vyanzo vya fedha vilivyoanzishwa vilikuwa kwa ajili ya matabaka, na ni wazi kuwa waafrika tulikosa kufaidi utamu wa uchumi katika ardhi yetu wenyewe kwa kukosa vyanzo vya kifedha. Hali hii iliendelea katika siku za mwanzo za Uhuru hadi pale tulipotaifisha taasisi hizi kuwa za taifa. Lakini leo hii hali ile ile imejirudia mtanzania hakopesheki, ila mgeni anakuja na dola moja anarudi na mtaji kwao.
Kilio cha kuwa hatukopesheki ni dhidi ya benki nyingi zenye asili ya India, Kenya na Afrika Kusini. Ni wazi kuwa mitaji hii imewekwa ili kuwanufaisha binamu zao wanaofanya biashara nchini! Kati ya watu waliokuwa katika jopo la kushauri juu ya kuuzwa kwa NBC kwa ABSA, Wakili Nimrod Mkono amekiri kupitia vyombo vya habari kuwa walifanya kosa kuiuza NBC kwa dola milioni 15!
Hili linawezekana kwa vile wao ndiyo wanamiliki mitaji na maduka ya kuuza mitaji yaani benki,hivyo mitaji kama hii haina maana wala tija kwa Tanzania hata kama ikawa benki zipo na zinachipua kila siku lakini ni za wageni maana yake wanakuja kurahisisha ndugu zao kujipatia mitaji na kuongoza uchumi wetu.
Haya ndiyo makaosa ya FDI bila kujali itakuja kumtumikia nani?Umepokea bila kujali ulikuwa umeweka mawazo katika uwingi.Na ndiyo manaa ukimuuliza mtanzania wa kawaida atakwambia pato la taifa linakuwa lakini haoni manufaa yake, kwa vile hawa waliokuja na mitaji yao wakipata tano yote inaenda kwao kununua matufaa(apple) kuku, nyama ya ngombe. Wakati matufaa yapo Iringa yanaoza. Zaidi ya asimilia 60 ya matunda Tanzania yanaaribikia shambani huku tunaagiza mananasi toka Afrika Kusini mukiyashabikia katika maduka ya Shoprite na Games.Hapa kuna tatizo nalo ni kwamba hatukuangalia ubora.
Shirika la Umoja wa mataifa la UNCTAD linabaisha wazi kuwa senti 75 za kila dola inayoenda Singapore kama mtaji toka nje katika kiwanda cha kufyatua Compact Disc (CD) inabaki humo humo, Afrika ni senti 37 tu. Tena hizi ni Takwimu za Nchi zenye mafuta na zenye uchumi imara miongoni mwa bara hili.
Hali inawezekana ikawa ngumu kwa Tanzania ambayo inaruhusu muwekezaji kukodi ndege kuagiza nyama ya kuku huku kuku wapo wanafugwa Kibaha, ukiuliza wananuka ‘dagaa’! Ohh mara hawana zaidi ya kilo mbili. Mbona ukienda katika supermarket zao utaona wapo wa kuanzia gramu 700 hadi 2500 katika majokofu na wanauzwa bei tofauti tofauti sasa siwachuukuliwe na hawa wawekwe katika mtindo huo huo!Muwekezaji anatupangia sisi nini cha kufanya katika nchi yetu kwa manufaa yake!
Hali inaonesha tunahitaji zaidi mabadiliko ya kisera Tanzania ni yetu leo na vizazi vyetu kesho. Makosa yetu leo kwa hongo zisizo na maana nikikwazo kwa vizazi vijavyo. Sera zetu lazima zioneshe kuwa tunahitaji ‘ubora’ katika FDI na si kuhesabu miradi mwaka huu ni mia kadhaa, haina mwisho mwema.
Shime wenye mamlaka, sasa wakati umefika wa kufikiria zaidi Tanzania kwanza si mpaka mukitoka ofisini ndiyo mnajifanya kujuta kupitia magazeti.
Mungu Ibariki Afrika
Mungu Ibariki Tanzania.