Sunday, November 29, 2009

Kampuni za Tanzania zinahitaji kurudisha sehemu ya faida kwa miradi endelevu

Biashara ulimwenguni kote imekuwa ikipitia katika vipindi tofauti vya kinadharia juu ya masilahi ya wateja. Katika nchi za Magharibi kuna changamoto ya ulinganisho wa faida na manufaa wanayopata jamii husika toka kwa kampuni zinazofanya biashara katika eneo husika.
Wateja hawataki tena kampuni ambazo ni ‘mumiani’ kampuni zinazovuna faida tu bila kujali masilahi ya jamii husika. Tanzania wateja hawana nguvu kama nchi za Ulaya na Marekani ambako kuna vyama imara vya kutetea masilahi ya walaji. Na hili ndilo linafanya kampuni zetu kubweteka.
Hili linafanya kampuni za kitanzania zione ‘wadau’ na hasa walaji ni watu wa kukamuliwa tu, na wala wasiohitaji marejesho ya faida ya kampuni. Ingawa suala la marejesho ya faida kwa jamii ni lenye kuhitjai zaidi muongozo wa bodi ya kurugenzi ya kamapuni husika.Lakini kwa Tanzania kuna matukio yanatufanya tujiulize hivi hizi kampuni zetu zinaamini kweli katika kile inachokisema au ni masihara?
Kuna kampuni ambazo zinajigamba kuwa zinarejesha faida iliyopata kwa wateja na hasa kupita maofisa matukio wao. Na hili limekuwa likitokea hasa wakati wa kutoa zawadi kwa washindi wa ‘kamali’. Sasa hivi katika Tanzania kila kampuni kubwa imejikita katika kuchezesha ‘kamali’ kwa kivuli cha ‘promotion’ za kujishindia zawadi.
Na ndiko huko wanakojificha wakijidai wanarudisha faida kwa jamii! Si kweli kwani kimsingi wachezaji wamechangia wao wenyewe na kampuni nyingi zinakuwa zimejinyakulia faida nono kabla ya ‘draw’ na kama haijavutia wachezaji tumeshuhudia zikisogezwa mbele.Kama kweli ‘promotion’ kwa nini wasogeze mbele draw?
Kuna kampuni moja ya simu ambayo ilichezesha ‘kamali’ yake baada ya kujikusanyia milioni 100 ya faida! Huku wateja wakiambuali vijizawadi vya muda wa maongezi wa kwa mtindo wa kuchangiana wao wenyewe.
Hii si ‘promotion’ kama vile wao wanavyotaka tuamini, kwani sales promotion ni faida kwa mteja kwa kupata huduma au bidhaa kwa bure au chini ya bei ya soko kwa kipindi maalumu.
Isieleweke kuwa hakuna kampuni ambazo hazifanyi na wala hazina juhudi lakini kwa faida zinazochuma mara zote imekuwa hailingani na kile wanachotoa na zimekuwa zile zile kila mara kuna kampuni zingine zinastaajabisha kabisa. Ukizialika katika michango ya ujenzi wa shule utawaona wanatoa mifuko ya sementi tani moja. Huku taarifa za TRA zinasema kampuni imepata faida ya zaidi ya bilioni 20 tena baada ya kulipa kodi!
Ila mara nyingi kampuni zetu zimejikita katika miradi ambayo si yakudumu, na wala haina faida ya muda mrefu kwa jamii husika. Mara nyingi imejikita kufuturisha watanzania wakati wa ramadhani, huku kampuni hizo zikijipatia faida kubwa na wakatia mwingine kutoa zawadi wakati wa Krismasi katika vituo vya kulelea yatima kwa magunia ya mchele na mafuta ya kupikia.
iliandaa harambeee hii miaka miwieli
Kimsingi kamapuni zetu zinahitaji kwenda zaidi ya hapo.Tanzania ya leo inamatatizo mengi na tukiunganisha nguvu zetu tunaweza kufika mbali na si kufanya mambo kwa staili ya ‘kiini’ macho.
Wakati fulani iliwahi kuripotiwa na vyombo vya habari kuwa Waziri Mkuu aliyejiuzuru Mheshimiwa Edward Lowasa aliwahi kukataa michango ya kampuni fulani katika harambee ya kuchangia bweni la wasichana wa Chuo Kikuu Mzumbe. Mzumbe inahitaji kufikia lengo la asilimia hamsini kwa hamsini ya udahili wa wanawake na wanaume.
Hivyo iliandaa harambee hii miaka miwili iliyopita Jijini Dar-Es-Salaaam ,kichekesho ni kwamba kampuni inapata faida ya bilioni 26 baada ya kulipa kodi inatoa machango wa milioni tano kwa mradi wa kuwezesha wanawake wengi kupata elimu ya juu!
Hii ndio hali ya kampuni za Tanzania ni kupenda kutumia nguvu kazi pasi hata kurejesha wala kutolea jasho. Nyingi ya hizi kampuni ndizo waajiri wakubwa lakini hawaweki nguvu hata kidogo katika kuboresha hali ya elimu nchini.
Hii haimaanishi hakuna kampuni ambazo hazijielekezi katika kuboresha hali za watanzania katika miradi ‘endelevu’ zipo kama vile Zain ambayo hutoa ufadhili kwa wanafunzi wa shahada ya kwanza katika fani mbalimbali nchini. Lakini juhudi hizi ni kwa kampuni chache huku zingine wakiwa kama watazamaji au hawajui matatizo ya watanzania. Ila katika kudhamini ‘matamasha’ huko utawaona!
Rais Mstaafu wa Awamu ya Tatu Mzee Benjamin William Mkapa akiwa Uganda katika mahafali ya Chuo Kikuu Makerere ambako alitunukiwa PhD ya heshima ya Sheria amenukuriwa na na vyombo vya habari akiweka bayana kuwa nchi za Ulaya haziweki nguvu katika kufadhili elimu ya juu badala yake zipo katika elimu ya msingi, na hakuna taifa linatakalo ondokana na umasikini kwa kuwa na watu wenye elimu ya msingi bila wa na wataalamu wa elimu ya juu.
Hii ni wazi, upungufu wa udhamini wa elimu ya juu nchini unaweza kupunguzwa na udhamini wa kampuni za ndani kama tukijipanga.
Yatupasa kuweka nguvu katika miradi endelevu kama elimu ya juu kwa kutoa ‘udhamini ‘ kwa wahadhiri pia. Hili linawezekana hebu tuangalie kwa Uchache tuone namana kampuni zetu zinavyotumia pesa katika matangazo.
Mwaka 1997 kampuni za Tanzania zilikuwa zinatumia 1.1 asilimia ya pato la Taifa kwa ajili ya matangazo. Kampuni kumi bora za Tanzania katika matumizi kwa ajili ya matangazo zilitumia bilioni 14.2(2005), 18.9 (2006) na 25.2(2007) ( Advertising Age, Desemba 8, 2007).
Matumizi kwa matangazo ni kwa kampuni zile tu ambazo zimeruhusiwa kufanya matangazo katika Televisheni na Radio acha kampuni kubwa kama TCC watengenezaji wa sigara ambao sheria inawabana kutumia rediao na TV wao wanatumia mabango na udhamini wa matamasha.
Matumizi haya kwa ajili ya matangazo kwa makampuni kumi ni wazi kuwa kampuni zetu zinapata faida kubwa, lakini hazirejeshi hata chembe ndogo kwa jamii ya kitanzania kwa uwiano unaolingana na hasa miradi endelevu.
Ulinganisho haupo katika kurudisha faida kwa miradi ya jamii, na badala yake wakitoa mchele utaona jinsi wanavyojitangaza katika redio na televisheni! Si sawa kwani matangazo hayafanani na faida wanayopata au kurusha kipindi maalum.
Kama nchi tumekosa cha kuzifanya kampuni hizi na ndiyo maana zinapata faida kubwa bila hata kujali sehemu ya jamii. Tuangalie mfano mdogo tu ambao unaonesha jinsi kampuni zetu zilivyolala katika kupeleka faida kwa jamii husika.
Ukipita katika barabara ya Alli Hassan Mwinyi utaona abiria wapo juani pembeni kuna Ofisi za kampuni kubwa na zenye kuheshimika kwa jamii ya kitanzania. Hiki ni kituoa cha daladala kampuni zimeshindwa walau kuweka kibanda cha abiria kujisitiri kwa jua na mvua.
Sasa hivi Krismas inakuja utaoana kampuni zetu ndogo na kubwa zinavyoshindana kutoa zawadi za mbuzi na mchele kwa mafuta ya kupikia. Kimsingi hatupingi zawadi hizi, lakini matatizo ya watoto hawa si kula ya siku moja au pilau, wengi wao wanahitaji elimu jitokezeni mulipie karo za watoto hawa na si kuvizia ‘picha’ Mifano ipo mingi kampuni kubwa na zenye kuheshimika mbele ya ofisi zao abiria wanakaa juani na wananyeshewa mvua wakati wa masika bila hata kujali sehemu hii ya jamii na wakati mwingine hawa na wateja wao.
Hii ni mifano midogo lakini inaonesha jinsi kampuni zetu zinavyoona kurudisha chumo lake kwa jamii ni ngumu.
Tanzania ina kabiliwa na changamoto ya kukosa fedha kwa ajili ya tafiti za kitaalamu kwa maendeleo ya nchi. Serikali ndiyo inasema labda itajaribu kuweka fedha zake kwa walau asilimia 0.1 ya bajaeti kwa ajili ya tafiti kwa miaka ijayo ni suala la kusubiri na kuona .
Ila hili ni eneo lingine kampuni zetu zimekaa kimya wala haziinui mkono wala ‘mdomo’ ili kuonesha njia lakini ‘show’ za urembo wanamwaga fedha huku wakishindana kutoa zawadi. Matamasha ya ‘bongo fleva’ wanapigana vikumbo ili waonekane kuwa ndiyo vinara.
Wanashindana kuleta wanamuziki wa magharibi, ni wazi kuwa burudani ni muhimu kwa jamii lakini tutanachekesha kwani mbio zetu kwa mambo ya kupita ni za kasi mno kuliko mambo ya msingi ambayo tumeyapa kisogo.Kampuni inatumia bilioni 5.1 kwa matangazo kwa mwaka ni wazi kuwa inaweza hata kuchangia kwa kiasi kikubwa katika kutoa fedha kwa ajili ya tafiti za kitaalamu zitakazoweza kuinua taifa na kampauni husika pia.
Hakuna taifa lilillopiga hatua duniani bila tafiti na kikubwa ni kwamba hzio tafiti chanzo chake ufadhili kikiwa ni cha ‘ndani’. Na tafiti hizi zikifanywa kwa mazingira ya Tanzania ni wazi kuwa zitapelekea mafanikio kwa kampuni zetu za ndani katika kutumia tafiti hizi kwa urahisi. Lakini hakuna kitu kama hicho badala yake ni miradi ya muda mfupi ndiyo inayopendwa na kushabikiwa na kampuni zetu.
Tafiti zinazofanywa na vyuo vya Magharibi nyingi zinagharimiwa na kampuni zao kwa kuweka pesa katika vyuo na wao wananufaika na matokeo ya tafiti. Huku ndiyo kurudisha ‘chumo’ kwa jamii na si kuchezesha ‘kamali’ alafu munajigamba kuwa munarudisha chumo kwa jamii.
Kampuni zetu zinapata faida ‘nono’ lakini mgao kwa jamii bado ni mdogo yatupasa kubadilika, kwani biashara ni kujali jamii husika kwa miradi endelevu na ‘ujanja ujanja’ na maneno mengi yasiyo na tija na kuhimiza ‘press coverage’ ili muonekane munatoa.
Yatupasa kama nchi kufahamu kuwa tunahitaji kwenda hatua za mbele zaidi ili kutatua matatizo yetu na faida inayochumwa na kamapuni zetu ikitumika vizuri inaweza kuleta mabadilko kwa maisha wa watanzania walio wengi, na si kufadhili ‘burudani’ tu.

Saturday, November 21, 2009

Biashara bila ushirikiano ni bure

Biashara ni mzunguko wa Vita na Amani( War and Peace) lakini yenye kuhitaji kushirikiana na adui yako, Waingereza wanaiita nadharia hii kama (Coopetition), ni muunganiko wa maneno mawili ya Kiingereza Cooperation and Competition. Sina neno zuri la Kiswahili kwa tafrisi ya Coopetition, lakini nitalitumia kama lilivyo.

Coopetition kama nadharia iliibuliwa na Ray Nadal Mkurugenzi wa Novel na kuletwa katika Ulimwengu wa elimu ya biashara na kwa tafiti za Adam M. Brandenburger na Barry J Nalebuff ambao waliandika kitabu kilichoitwa ‘Co-opetition’ na kufanikiwa kuwa miongoni mwa vitabu vilivyouzwa sana duniani katika miaka ya 1997.

Coopetition ni muungano ambao mara nyingi si wa kudumu kati ya kampuni ambazo zipo katika ushindani . Mfano mzuri ni jinsi kampuni za mifumo ya kompyuta zilivyoweza kupeleka sokoni ubunifu wa JAVA uliofanywa na Sun Microsystems, kampuni za IBM, Apple na Netscape ziliungana kwa pamoja.Wapinzani wa nadharia hii huiita 'cartel' lakini katika elimu ya mbinu biashara(Business Strategy) hii ni mbinu bora kwa kueneza ubunifu wenye kukuza ushindani.

Duniani kote nadharia hii inashamiri, katika Tanzania kuna maeneo yanayotia moyo lakini kwa ujumla hali si shwari miongoni mwa wajasiriamali. Kinachonifanya niandike makala haya ni habari za hivi karibuni zinazoonesha wafanyabiashara wa Tanzania kukosa kuuza zabuni katika ‘kampuni’ kubwa ya Barrick Gold Mining ya Shinyanga.

Barrick ni kampuni kubwa inayohitaji kila aina ya bidhaaa huku ikitumia zaidi ya dola milioni 200 za kimarekani kwa mwaka, na hii ni nafasi ya wajasiriamali wetu kuweza kunufaika na uwekezaji wandani. Lakini taarifa za kampuni hii zinasema kuwa hata wale walio karibu na Barick hawanufaiki, na kampuni hii kibiashara.

Hili linachangiwa na wao kutoweza kutumia mawasiliano ya mtandao wa kompyuta wa kampuni hii kuweza kuuza bidhaa na kupata zabuni mbalimbali zinazotangazwa.Hali hii haipo kwa Barick au wafanyabishara wa Shinyanga tu, ni Tanzania nzima.

Wakati fulani iliwahi kuripotiwa kuwa kuna mjasiriamali aliyeshindwa kutimiza masharti ya mteja wake aliyekuwa anahitaji tani 'mia moja' za korosho zilizobanguliwa, hivyo akakosa kutimiza mahitaji ya mteja wake kwa vile alishindwa kushirikiana na wajasiriamali wenzake katika kuishambulia 'tenda'.Ni wazi kuwa mteja aliyevunjwa moyo hawezi kurudi tena!

Hili halikutokea kwa sababu nyingine isipokuwa ni kukosa ufahanmu wa namna ya kuweza 'kushirikiana na kushindana'.
Biashara ni ushindani na ndiyo maana tunasema ni 'vita', lakini hili halifanyi kuwa mfanyabiashara mwenzako awe adui la hasha. Maana yake ni kwamba utabuni na utajaribu kujifunza nini mwenzako anafanya huku mukishirikiana kuleta hali nzuri kwa wateja.

Ni muhimu wafanyabiashara wetu waungane ili kuhakikisha wanawafikia wadau wao kwa ukaribu zaidi na kwa ufanisi. Kuna mifano kama vile muungano wa Vodacom na Zantel, kampuni ya Zantel inatumia minara ya Vodacom, hii haimaanishi kuwa Voda watakosa wateja hapana isipokuwa itaongeza kavereji ya zantel kwa gharama nafuu kwa kampuni zote mbili katika kuhudumia minara yao.
Pia mfano mwingine ni UMOJA ATM za banki DCB, ACCESS BANK, BOA BANK, AKIBA COMMERCIAL na AZANIA BANK.Kwa ktumia msine hizi wameweza kufikisha huduma kwa wateja wao huku 'wakishindana'.
Kuna watanzania wengi waliokuwa wakiipigia chapuo nadharia hii kuingia katika biashara ya Tanzania, kama Vile Mzee Reginald Mengi alipokuwa akihimiza kampuni za simu kutumia minara ya pamoja au warusha matangazo ya Redio na Televisheni. Hili halikufanikiwa sana, kwa sababu ya 'umimi' miongoni mwa wafanyabiashara wa Tanzania.

Wajasiriamali wanashindwa kujitangaza au kufikika kwa vile hawana namna bora za kisasa ambazo mteja au msambazaji anaweza kuwafikia na kufahamu wapi kunahitajika nini?. Hili linaweza kutatuliwa kama wajasiriamali wakiwa na tovuti ya pamoja.

Tovuti ni kitu ambacho kinaweza kutumika na wajasiriamali wadogo, wakati na wakubwa kwa pamoja kwa kuweka bidhaa zao katika tovuti hiyo moja huku wakitumia gharama nafuu kuiendesha pia mteja akifahamu wapi walipo kwa kutembelea tovuti husika.

Mfano mzuri ni Google na eBay ambazo kimsingi zote wakati zinaanza zilikuwa na lengo moja tu kuwa ‘search engine’ huku kampuni zinazofanya biashara zikijiweka mbele kuwa zinakuwa zakwazwa kuonekana mara baada ya 'mtumia mtandao' kutafuta taarifa fulani kama vile ya bidhaa.

Kampuni hizi zilipoungana, sasa hivi miongoni mwa wateja inajulikana kama unataka ‘kuuza’ basi uza na eBay na kama unataka kuongeza wateja’traffic’ katika tovuti yako jiweke na Google. Lakini lililowazi ni kwamba eBay anatumia Google kuongeza traffic, huku 12 asilimia ya wateja wanapitia Google kwanza ili kufika eBay.

Si kama hawana biashara zinazofanana la hasha, eBay ana Skype,Google,ana Gmail/Talk hizi ni kampuni za mawasiliano ya simu kwa kutumia ‘Internet’. eBay ana Paypal, Google ana Forhtcomming.

Taarifa za karibuni zinaonesha wote kunufaika na mapato yao yakiimarika mara baada ya 'kushirikiana' huku 'wakishindana'.
Ukweli ni kwamba ubunifu wa ‘Google’ ni faraja ya eBay, pia ubunifu wa eBay katika biashara yake ni faraja ya Google.

Ndipo tunasema biashara ni Vita na Amani, ….Vita tena Amani ….. ni mzunguko.Coopetition ni kukubali ubunifu wa mwenzako huku nawe ukiboresha kazi yake kwa faida ya wadau. Tupia jicho pia wanamuziki wa ‘Kikongo’ ikiwa Ndombolo, kila mwanamuziki ataitumia hiyo 'staili', bila kujali nani aliianzisha,huku akiweka ‘nakshi’(ubunifu) tofauti na wakwanza, 'Kiwazenza' wote 'kiwazenza'.

Tanzania hali ni tofauti kabisa, Kapteni John Komba amekuja na ‘Achimenengule’ ngoma ya wayao wa Masasi ni mwanamuziki mmoja tu amejaribu kuitumia!

Ni muhimu wafanyabiashara wetu wakajitahidi kufikiria kuungana na kushindana kuliko kukalia ushindani bila ‘kushirikiana’. Ni wazi kuwa ushirikiano ni nyumba ya ubunifu.

Hakuna 'adui' wa 'kudumu' wala 'rafiki' wa kudumu katika biashara, ila cha msingi ni kuimarisha ushirikiano kwa faida ya wadau wote. Na si kuikalia 'tenda' ambayo unajua hauwezi kuitekeleza bila ushirikiano. Wajasiriamali yawapasa kushirikiana ili kusonga mbele, ushindani si vita tu, bali amani pia kwa maana ya kwamba utaweza kunufaika na ubunifu wa adui yako pia.

Friday, November 6, 2009

Stakabadhi ghalani inahitaji ubunifu zaidi na si kusambaza 'woga'(SEHEMU YA PILI)

Soko la mazao la Tanzania tangu kuingia kwa kwa dhana ya soko huria vilio vya wakulima vimesikika kila kona. Hili halina nafasi katika makala haya kwani tunaamini mengi yamezungumzwa. Ila lililowazi ni kwamba tumeonesha jinsi wanunuzi wa korosho walivyokaidi agizo la Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika sehemu ya kwanza ya makala haya.
Tulishaonesha msimamo wetu katika makala yetu kuwa hatukubaliani na mawazo ya waheshimiwa wabunge kufuta stakabadhi ghalani pamoja na changamoto za sasa zilizopo katika zao la korosho.
Hebu tutupie jicho kidogo katika hoja zao mbili ambazo, mosi ni kuwa stakabadhi ghalani ni mfumo wakinyoyaji na pili unawatenaa wakulima wadogo.
Tuanze kwa kubainisha wazi kuwa si kweli kuwa mfumo wa stakabadhi ghalani ni kuwa wakinyonyaji. Isipokuwa ni mfumo ambao kinadharia unaleta uhuru wa kweli kwa wakulima wa nchi hii. Wakulima wa korosho wameshuhudia kulipwa katika mikupuo miwili na maeneo mengine mikupuo mitatu zaidi ya bei ya soko.
Wale waliouza korosho katika msimu wa mwaka jana kuna waliouza kwa kilo 650/= walichukua malipo yao na baadaye walilipwa mafao yao ya nyongeza ambayo baada ya kuuza korosho ilifikia kilo shilingi 800. Hivyo kufanya nyongeza ya zaidi ya shilingi mia kwa kilo.
Katika hali kama hii mkulima amenyonywa nini! Na liliwalowazi wale waliouza katika mtindo wa stakabadi ghalani walipata nafasi ya kujiwekea akiba kwa ajili ya pembejeo, lazima ieleweke watanzania walio wengi na hasa walio vijijini hawafaidi huduma za kibenki, hivyo kupitia stakabadhi ghalani wakulima wanaanza kuhifadhi kipato chao, kama vile mwenye akaunti, kwani hii ni ‘negotiable instrument’ inaweza kuthaminishwa. Hapa tunahitaji ubunifu katika sheria madhubuti katika kuhakikisha benki inapokea stakabadhi kama ‘inventory credit’.
Mfumo huu umeleta neema si katika korsho tu, hata katika kahawa , katika tafiti ya Gideon E. Onumah na Fedelis Temu ya mwaka 2005 katika kahawa na pamba iliyoitwa ‘Reducing Marketing Constraints and Enhancing Producer Income Through Warehouse System’ ilibaini kunufaika kwa wakulima wa Tarakea, Moshi kwa kipato kizuri kwa wanachama wa ushirika wa Tarakea ambao waliuza kahawa kwa kilo 1800/= tofauti na wenzao waliouza kwa mfumo wa soko huria wa kwa kilo 1250/=.
Ushirika hauchagui hivyo hoja ya kuwa mfumo huu unamtenga mkulima mdogo si sahihi. Ila ili mfumo huu usonge mbele unahitaji ushirika imara ambao umeundwa na wakulima wenyewe kwa ridhaa yao.
Mifano inaewza kuwa mingi kama vile IFAD inavyoshuhudia wakulima wa mahindi katika Karatu wanavyonufaika na mpango huu, huku wakiimarisha maisha yao. Mahindi yanauzwa 13,000/= kwa gunia wakati wa mavuno, lakini sasa wakulima wanaweka ghalani, wanuza hadi gunia la kilo mia 26,000/=.
Na lililowazi ni kwamba wengi wa kulima hawa ni wadogo walioungana kupitia ushirika wao kwa hiyari. Na wala hakuna tishio la kumnyonya mkulima mdogo. Sasa hili la kuwa stakabadhi ghalani ni tishio linatoka wapi?
Wataalmu wa biashara ya mazao wanabainisha kuwa mara zote adui mkubwa wa stakabadhi ghalani ni kilimo cha mikataba (Contract farming). Tanzania ina kampuni chache zinazofanya kilimo cha mikataba, kama vile Starbuck tena wapo katika kahawa wilayani Mbinga.
Inawezekana katika nchi yetu kilimo hiki kisiwe tishio kwa sasa ila yatupasa kuangalia namna yakufanya vyote viende kwa pamoja kwani vinamanufaa kwa wakulima wan nchi hii.
Pili upinzani wa stakabadhi ghalani unasababishwa na ‘bush buyers’ na kampuni za kinyonyaji zisizotaka kumuona mkulima anainuka. Hili ndilo lipo sana Tanzania.
Walanguzi wa korosho wapo wengi sana, wanakaa mjini msimu( Mwezi wa Kumi) ukifika kila mmoja na gunia la dagaa wa Mwanza au wa kigoma, chumvi na nguo za kichina au mitumba hujifanya wanauza kwa kubadirisha kwa korosho.
Hawa wananunua kwa kubadilishana ‘barter trade’. Ubaya wa biashara hii hutumia ‘kangomba’ (Ni kopo lenye kuingia kilo mbili na nusu) kubadilisha na mtumba au dagaa wa Mwanza wengi wame neemeka kupitia njia hii siyo rasimi.
Sasa hawa kwa vile ni watu waliokatiwa utamu bila jasho wanaona mwishowao unahatarishwa kwani sasa wakulima wamekombolewa, ndiyo wanaleta vitisho vya kuhamasiha kunyima kura wabunge na vurugu zote zile tulizo ziona katika makala haya sehemu ya kwanza chanzo ni hawa wanununzi wa ‘kangomba’.
Pia kampuni hizi za kihindi za ‘mfukoni’ zinamkono katika kuhimiza kuonekana kwa stakabadhi ghalani si mali kitu. Hizi kampuni zinafanya kazi kwa ‘ujanja ujanja’ Wengi wao kiukweli hawana mtaji, ila kinachotokea ni kwamba wao wanakubali kwenda vijijini na kujifanya wananunuzi kwa walau tofauti ya shilingi 20-100, ambayo wao huchukua kama cha juu. Hii biashara ya udalali imewanufaisha wengi hasa Mtwara Mjini.
Merehemu Profesa Seith Chachage anawaita makuadi wa soko huria. Na hawa nao hufanya kazi kupita mtindo huu wa soko huria kwa kusambaza vitisho.
Makuwadi hawa wanavyofanya ni unyonyaji ambao hauuvumiliki kama unaipenda nchi yako, kuna rafiki zangu walifanya kazi katika kampuni za korosho simulizi zao ni kwamba mkulima anapofika kuna madalali ambao wao wanijifanya ‘kumjua’ tajiri na bila wao ‘hauuzi’, sasa kwa vile mkulima ametoka Kitangari au Nambali hamjui tajiri wa kihindi anamkabidhi huyo ‘dalali’ kazi ya kufuatilia mauzo ya korosho zake.
Anazunguka anakuja na vijana ambao’ wanapiga’ bambo kutathimini ubora wa korosho kisha hudai kuwa ubora uko chini, hivyo hawawezi kununua.Hiki ni kitisho cha wazi. Mkulima amekodi gari na mjini siyo kwao, ataanza ‘kuweweseka’ tayari amekiwsha!
Wanauza korosho kwa bei kubwa na watachukua wao cha juu, kisha mkulima ataambulia maumivu, hawana huruma hata kidogo. Stakabadhi ghalani imewaondoa ndiyo hao ‘wanaugulia’ maumivu kwa kuleta hoja chakavu na hawa nao wananguvu ya kisiasa kwani wengi wao ni wapigaji wa ‘mdomo’ hasa vijiweni, basi wabunge wanajifanya kuleta hoja kuwa mfumo mbovu kumbe kutaka masilahi ‘uchwara’ yasiyo na tija, kwa walio wengi.
Changamoto ya kutolipa kwa wakati tumeshaona jitihada za serikali ilivyofuta madeni ya vyama vya ushirika ili viweze kukopesheka.Hili lilifanyika kwa baadhi ya vyama vya ushirika katika mkoa wa Mtwara na viliweza kupata mikopo kutoka benki ya CRDB. Ni wazi kuwa huu ni uamuzi mgumu na wa hali ya juu, ila yatupasa kwenda zaidi ya hapa.
Yatupasa kuhakikisha vyama vinakuwa na wataalmu wa kutosha, kwani katika ripoti ya mwaka 1967 ya Ushirika (Presidential Inquiry on Cooperative) mkoa wa Mtwara ulioneka kukosa wataalamu wa ushirika na masuala ya fedha. Ingawa muda ni mrefu lakini inawezekana kuwa tatizo hili mpaka leo lipo.
Lakini hili haliwezi kutufanya turudi nyuma. Wabunge lazima wabuni mbinu bora za kuhahakisha viongozi wanapata elimu ya kuweza kuendeleza ushirika katika maeneo yao
Pamoja na faida zake zote stakabadhi ghalani na hasa kwa Tanzania ina changamoto ambazo kimsingi tunapaswa kuzitafutia dawa na kitu kikubwa ni ubunifu.
Changamoto kubwa ni uhifadhi wa mazao, hapa tunazungumzia maghala yetu?Je yana bima? Ikitokea ghala limeshika moto, hatima ya mkulima wetu ikoje?
Kuhifadhi (Storage) ni taaluma, je tunawataalamu na mbinu za kutosha katika uhifadhi wa kisasa?
Nguvu ya stakabadhi tunayo mpatia mkulima wetu inakubalika katika taasisi zetu za kifedha kama ‘negotiable instruments’? Kama hapana tunaboreshaje?Kama ndiyo je uhalali wake ukoje kifedha?Sheria zetu zinasemaje kuhusu inventory credit?
Hatari nyingine ni kughushi (fraud) mara zote stakabadhi ghalani inaambatana na tatizo hili.
Ripoti moja ya Shirika la Umoja la Mataifa linaloshughulika na Chakula (FAO) inasema kama kilimo kinahitaji kuinua maisha na maendeleo kwa walio wengi basi mfumo imara wa mikopo unahitajika, na stakabadhi ghalani ni suluhu ya kudumu kwa wakulima kupata mikopo.
Tukijipanga na kuongeza ubunifu tunaweza.