Monday, June 14, 2010

RFID ni suluhu moja wapo kwa bidhaa feki kwa nchi zinazoendelea

Radio Frequency Indentification (RFID) si teknolojia mpya duniani, ila inaelezewa kuchipua sana katika miaka ya 2000. Teknolojia hii ilianza kutumika kwa mara ya kwanza wakati wa vita ya pili ya Dunia na waingereza katika rada za kijeshi kuweza kutambua ndege za maadui na washirika wake.
Tokea wakati huo RFID imekuwa ikitumika sana katika mambo ya kijeshi, ila miaka ya karibuni kuna mabadiliko makubwa hasa katika nyanja ya biashara kuanza kutumia technolojia hii katika kuongeza uongozi wa usambazaji bidhaa (supply chain management) na kupunguza hasara kampuni imekuwa zikipata.
Kampuni kubwa General Motor, imeanza kutumia tangu miaka ya 1984 kwa utambuzi wa bidhaa zenye thamani kubwa hasa injini za magari, pia Toyota kwa kiwanda chake kilichopo Afika Kusini. RFID ni nini?
RFID ni miali ambayo inasafiri katika mawimbi ya redio ikiweza kufanya utambuzi wa kitu bila hata kuweza kuangaliwa moja kwa moja na muhusika. Kwa sasa ulimwengu unatumia ‘bar code’ ili kuweza kutambua kama mzigo husika ni sahihi kwa kusoma namba na kutafsiri, lakini kwa RFDI unaweza kupata taarifa toka mbali bila hata kuona mzigo kama tulivyokwisha kusema.
Katika bidhaa husika badala ya kubandikwa ‘bar code’ RFID tag itabandikwa na msomaji akisaidiwa na mtambo ambao unafahamika kama RFID reader ataweza kung’amua nini kinaendelea kwa mzigo husika. Kuna aina tatu za RFID tag lakini tofauti kubwa ambayo wataalamu wa TEKNOHAMA wanaikubali ipo,ni ile inayotumia betri na isiyotumia betri.
Bidhaa ambazo hazina thamani kubwa hutumia ‘RFID tag’ zisizo na betri, ili kuweza kung’amua mpangilio wa bidhaa ndani ya ghala au hata bidhaa iliyo katika hatari ya kuharibika kwa uzembe wa mpokeaji. Kwa mfano maziwa yanaweza kusahaulika kuwekwa katika hali ya ubaridi RFID tag ina uwezo wa kupeleka taarifa kwa msomaji na kutambua kuwa kuna mabadiliko ya joto kwa bidhaa husika, hivyo kuharakisha uhifadhi sahihi wa bidhaa kama hizi zenye kuhitaji umakini wa hali ya juu.
Katika siku za karibuni ongezeko la bidhaa 'feki' limekuwa ni tatizo kwa nchi nyingi zilizoendelea na zinazoendelea Tanzania ikiwemo. Wakati wote huu Uchina imekuwa ikibeba lawama kuwa ndiyo mhusika na ni muendelezaji wa uuzaji wa bidhaa feki, kwa Afrika.
Hivi karibuni kuna sakata la kondomu feki, likiwa tu linafuatia baada ya sanya sanya ya taulo za usafi za kina mama, ‘always fake’ kukamatwa katika maduka mkoani Arusha. Hangaiko la bidhaa feki ni la uliwengu mzima, lakini jithihada za kupambana zinatofautiana toka nchi moja hadi nyingine.
Tanzania bidhaa zenye ubora mdogo zinatusumbua. Makala haya itajaribu kutupia jicho hali ya bidhaa feki na uwezekano wa teknolojia ya RFID katika kukabili changamoto hii.
Kamisheni ya Ushindani (FCC) inataja kuwa kiwi za milioni 20 na ‘tubelight’ za aina ya Phillips na Britimax zenye thamani ya dola 18000 zimeteketezwa mwaka 2007, kwa mujibu wa gazeti la Daily News la tarehe 1 Mei 2009.
Pia inakadiriwa kwa mwezi Machi pekee 2008, bidhaa zenye thamani ya dola za kimarekani 224,000, ziliteketezwa na FCC. Ni wazi kuwa FCC kwa uchanga wake inafanya kazi kadiri inavyoweza ili kudhibiti bidhaa ‘feki’.
Ni wazi kuwa vita hii inahitaji kuongezewa nguvu na sheria inayowapa walaji nafasi ya kuwa na chama imara chenye kuwalinda tena chenye nguvu ya kulinda masilahi ya walaji.Katika nchi nyingi vyama hivi vipo na vimekuwa mwiba na vimefanikiwa kulinda nchi zao kuwa majalala ya bidhaa ‘bomu’ si toka nje tu hata wazalishaji wa ndani.
Wataalamu wa TEKNOHAMA wanaelezea RFID kama teknolojia moja wapo yenye nguvu yakuweza kumpa mtu uwezo wa kutambua bidhaa tangu pale inapotengezwa kusafirishwa hadi kufika kwa mteja. Kimsingi inaongeza usalama na uwezo wa kufuatilia bidhaa wapi imetoka na imekumbana na hitilafu gani njiani.
Kwa sasa teknolojia hii ingawa iko katika majaribio makampuni mengi kama wauzaji wa bidhaa za reja reja (supermarkets) kama Wal-Mart, Tesco, ASDA , Zara na IKEA, lakini inaonekana kuvutia mno kampuni hizi kubwa, huku IKEA kampuni kubwa ya samani ikitaja kuweza kudhiti upotevu wa kontena zaidi ya arobaini kwa mwaka.Pia imeonekana ina manufaa kwa sekta ya afya katika kupambana na dawa feki na wagonjwa wasio meza dawa kwa wakati.
Marekani pekee inakadiriwa kupata hasara ya karibia dola bilioni 30 kwa mwaka katika dawa pekee kwa kuingizwa sokoni dawa feki na kughushiwa kwa nembo za kampuni husika (counterfeit). Taasisi ya chakula na dawa ya Marekani kwa kuzingatia hilo imepitisha azimio tangu mwaka 2007 kuhitaji wasambazaji wa dawa kutumia RFID ili kuongeza utambuzi wa dawa.
Wanazuoni Castro Linda na Fosso Wamba katika jarida la kisomi,Journal of Technology Management and Innovation, juzuu ya pili toleo la kwanza la mwaka 2007, wanabainisha wazi kuwa RFID ni teknolojia ya kipekee itakayo ongeza ufanishi na uwazi katika sekta ya afya kwani dawa zitaweza kuonekana tangu malighadi hadi kufika kwa mtumiaji wa mwisho.
Huu ni ushindi dhidi ya mapambano ya bidhaa bandia kwani kampuni nyingi kubwa sasa zinataka wasambazaji wake watumie RFID katika kufikisha bidhaa ili kukabili hali ya bidha feki.Hii ndiyo hali iliyoifanya serikali ya Marekani kuhitaji wasambazaji wa dawa na bidhaa za kitabibu kutumia teknolojia hii ili kuweza kuhakiki kwa uwazi.
Changamoto kubwa iliyopo katika kutumia teknolojia hii ni ukosefu wa wataalamu, bei ya RFID tag bado ni kubwa na nchi nyinyi bado hazijakubali matumimzi ya mawimbi ya redio kwa ajili ya usambazaji wa bidhaa. Na kubwa kuliko yote ni changamoto ya haki ya kuwa na siri (right of privacy), kwani kama RFID tag ikibandikwa katika kiatu ni wazi muuzaji ataweza kutambua wapi kiatu chake kipo, tangu akiuze kimepita, ingawa hili linategemea sana na aina ya RFID tag ambayo kwa hali ya kawaida hakuna kampuni itaweza kuweka tag ya namna hii kutokan na gharama yake.
Changamoto ya kukosa siri imefanya RFID kupingwa na watu wengi katika Marekani, hasa watetezi wa haki za binadamu wakidai kuwa teknolojia hii inaweza kufanya mtu kuweza kufuatiliwa na watu wa usalama na kumnyima uhuru wake.
Pia gharama ya tag ya RFID bado ni ghali, huku ikadiriwa kufikia senti 30 za Marekani kwa tag moja isiyo kuwa na betri, ambayo inakisiwa kupandisha gharama za uzalishaji kwa asilimia 26-60 ya zile za usafirishaji kwa masoko ya Ulaya na Marekani.
Pamoja naukweli kwamba RFID tag bei yake kuwa kubwa sokoni lakini kuna dalili kuwa bei yake imeanza kupungua na hasa baada ya kigingi cha haki miliki kupata suluhu na kampuni nyingi za Asia kuanza kuzalisha. Ila lililowazi ni kwamba Afya haiwekwi rehani ili kukabili dawa feki taratibu Tanzania inaweza kujongea katika matumizi ya teknolojia hii.

Wednesday, June 2, 2010

kigezo ni umri au utashi?

Uchaguzi mkuu wa rais na wabunge unakaribia katika Tanzania,kila kona kunatoka hoja na vioja. Kwa hakika kila mmoja anafaidi uhuru wake wa kuongea. Ndiyo demokrasia.
Katika maongezi hayo kuna kioja cha vijana wengi kujinadi kwa hoja ya umri na 'kuomba' wazeee wa wawapishe.
Hakika hiki ni kihoja, na wala si hoja kwani............................. fuatilia makala hii itakayotoka hivi karibuni.

wazalishaji wa ndani nao wajichunguze

Si kampeni mpya duniani na hasa kwa wale walio na nia ya kulinda ajira na uchumi wa nchi yao. Tanzania kupitia Confederation of Tanzania Industry inahimiza utumia wa bidhaa za nyumbani kwa sababu kadha wa kadha lakini lililokubwa ni kunusuru uchumi wa Tanzania. Katika Amerika kuna nembo kama ‘made in NY state’, ‘A taste of Iowa’ nakadhalika zote zikihimiza kupenda bidhaa za eneo lako.
Pia katika Amerika kuna wanaharakati wanavalia fulana za ‘Toyota made in Japan, Poverty made in Japan, Unemployment made in Japan’ Si unyanyasaji wala aina fulani ya ubaguzi ni jitihada tu za kukumbushana kuwa yatupasa kupenda bidhaa za nyumbani.
Hivi karibuni kuna ujumbe wa e-mail wenye kuhimizana miongoni mwa watanzania kupenda bidhaa za nyumbani mtandao. Huu ni mwanzo mpya lakini hili kama tulivyokwisha kusema si jambo jipya, ila sasa linaonekana kushika moto miongoni mwa watanzania, hasa baada ya CTI kulivalia njuga.
Tanzania ikiwa miongoni mwa nchi zinazochipua kiuchumi tatizo kubwa inalokabiliana nalo wakati wote ni uzalishaji ‘supply side’ kwani mahitaji(demand) ni makubwa na mara nyingi chochote kinachoingia sokoni huwa kinapata wateja, na kutokana na hilo ndiyo maana bidhaa hizi za kutoka Asia zimefurika katika soko la ndani. Na nyingi ya bidhaa hizi hazina ubora, lakini tutafanyaje heri lawama kuliko fedheha, hapa ndipo inachukua nafasi.
Madhara ya kufurika kwa bidhaa hizi toka Asia, tumekwisha yaandika katika makala nyingi, leo hapa hayana nafasi ya kujadiliwa. Ila makala haya itajaribu kujadili mbinu za kukabiliana na madhara ya kupenda bidhaa za nje hasa kwa wenye viwanda Tanzania.Kwani hili ndilo suala kubwa tunalopambana nalo, wataalamu wa biashara wanaiita ‘Country of Origin effects (COO)’
Made in……mara nyingi ni moja kati ya vitu vinavyomfanya mlaji apunguze hofu kuhusu bidhaa anayotumia na hasa kuhusu ubora ikiwa kama hana taarifa sahihi kuhusu nchi iliyotengezeza bidhaa hiyo. Ingawa wataalamu wa tabia za mlaji (consumer behaviour) wanalumbana kuhusu uhalisia wa COO kuwa kama moja ya ‘extrinsic values’ mteja anayoweza kuitumia lakini matokeao yameonesha wazi kuwa hii ni moja kati ya maeneo mteja anaweza kutumia kufanya maamuzi ya kutumia bidhaa au la!
Fikiria mtumiaji wa chakula cha watoto cha viwandani atakavyofikiria mara mbili pale anapoona chakula kwa ajili ya watoto kimetengezwa Uchina. Hofu moja kwa moja itatawala na hasa akijaribu kuhusianisha na tatizo la melamine lililoikabili viwanda vya chakula cha watoto katika China. Hiyo hili linafanya mara moja mnunuzi aamue kuacha na kutafuta mbadala. Hiyo ndiyo changamoto inayoikabili sekta ya viwanda Tanzania kwa sasa kwani walaji wameshatendwa, sasa wakiona unyasi (Made in Tanzania) wanastuka.
Kupenda bidhaa za nyumbani ni ‘ethnocentrism’, yaani ni hali ya kuona chako ni bora kuliko cha mwingine anatafrisi Profesa Constance Falk katika jarida la kisomi, Agribusiness, toleo la pili, mwaka 1996.Hivyo hutia ndani imani kwa mlaji kuwa kutumia bidhaa za nje ni kudumaza uchumi wa ndani, na kusababisha kukosekana kwa ajira na nikukosa uzalendo (patriotism).
Hivyo basi ‘Ethnocentrism’ ni zaidi ya uzalendo, kwani hii ni hali ya kuweka maneno katika vitendo huku ukijigamba kuwa wewe ndiyo bora na kuringia nchi yako anaandika Profesa Falk (Tafsiri ni yangu). Ndiyo maana tafiti fulani inaonesha kuwa walaji katika Marekani zaidi ya asilimia 80 wanaona nyama bora na tamu ni ile inayozalishwa na wafugaji wa kimarekani. Wanajivunia cha kwao, na hili tumeliona katika medani za kimataifa katika mambo mengi, kuhusu ubora wa muamerika na Amerika yenyewe.
Lakini hali ni tofauti katika Asia, ambako kubeba begi la ‘GUCCI’ au ‘PRADA’ lililotegnezwa magharibi ni kuonesha kuwa we ni mtu wa thamani na mwenye kwenda na wakati, huku ukionesha kuwa uko na kipato kikubwa. Homa hiyo imeikumba Tanzania, ambako serikali iko tayari kutumia bilioni 3 kwa ajili ya samani toka Uchina, Malaya na Singapore huku wajasiriamali wa Changombe, Suma JKT kutaja wachache tu wakikosa soko la bidhaa zao!
Hali ndiyo hiyo hiyo kwa mtu mmoja mmoja ambapo kunywa juisi ya Del Monte toka Kenya au Ceres toka Afrika Kusini ni ufahari badala ya ile yaUnnat, Kingolwira Morogoro. Orodha inaweza kuwa ndefu kwani kuna vilio vingi vya wazalishaji wa ndani.
Wazalishaji wa ndani watambue kwamba serikali haiwezi kuzuia hili kwani tumelia vya kutosha, makala nyingi zimeandikwa za kutosha watu wamepata shahada zao kuhusu haya mambo na madhara yake na hata walio madarakani baadhi yao hizi ndiyo ‘titile’ za tafiti zao wakati wanasotea shahada zao!
Lakini leo hii katika vitendo ni vurugu tupu, hakuna anayesikia kilio cha wazalishaji. Serikali haiwezi kuacha hili kwa vile yenyewe inataka kodi tu, kwisha. Hivyo ni muhimu kwa wazalishahji kujipanga, na kutafuta mbinu za kibiashara kukabili hii hali, kwani tunaozungumza nao si wasikivu.Na kama wanatarekebisha itachukua muda.Hebu tutupie jicho kidogo mbinu ambazo tunaamini wenye viwanda wanapaswa kuzitumia kukabili ‘country of origin effects’.
Garantii inahitajika kwa bidhaa ambazo zinadumu kwa muda mrefu na zenye thamani kubwa. Kwa mfano, kufanya vizuri kwa magodoro ya Dodoma ni kutokana na kuwepo kwa garantii ya muda usiopungua mwaka kama likibonyea rudisha kwa ‘muuzaji’ naye atarudhisha kiwandani. Hii inafanya mlaji kuona kuwa kuna uhakika wa ubora kwani mzalishaji yupo tayari kupokea bidhaa zitakazorudiswa kwake (reverse logistic) ambayo kimsingi ni gharama kubwa.Hivyo niwazi kuwa kiwanda hakiko tayari kuona inaingia mtegoni, basi ubora ndiyo ngao yao.
Lakini wazalishaji wa nyumbani wengi hawana ‘garantii’ kwa bidhaa zao wala ‘motisha’ sasa anapokuja muuzaji toka nje naye anaweka ‘garantii’ kuonesha ubora wa bidhaa zake ni wazi kuwa ataliteka soko la Tanzania. Mfano mzuri wa ‘garantii’inavyovunja mwiko wa ‘Country of Origin’ ni Honda magari toka Korea yalipoingia Amerika kwani yalikosa wateja kwa dhana kuwa Korea si mtengezaji mzuri wa magari na hakuna anayeitambua kwa umakini katika eneo hilo. Pia kwa Czech magari yao ya Skoda na Hyundai katika soko la Uingereza.
Honda waliweka ‘garantii’ ya miaka kumi, hali iliyofanya wateja kuamini kuwa magari ya Honda si masihara katika ubora leo hii, Honda ni katika wauzaji wakubwa wa magari katika Marekani.
Kuimarisha mawasilinao, ya simu na wavuti. Kampuni nyingi za Tanzania zinatengeneza bidhaa na kuzileta sokoni huku wenyewe wakijificha wasijulikane wako wapi na wanafanya nini. Hili huchangia kwa kiasi kikubwa woga kwa mmlaji. Huu ni ulimwneug wa mawasilino ambako mlaji anafanya uchunguzi na kujiridhisha kabla hata kutumia bidhaa kunawaokwenda katika internet na kutafuta wahusika wa kampuni wanapatikan wapi na kwa namna gani lakini sisi hata ukienda katika website ni madudu tu.Hupati taarifa kamili.
Namba za simu zikitolewa zitaita hadi itakata hakuna anayepokea wala kujali. Sasa kama mteja anataka kutoa oda mpya unadhani atakuwa na imani na kampuni husika. Ukitembelea tovuti zao taarifa zipo kwa kificho sana zaidi ni picha na sanduku la posta,sasa mteja anajiuliza kama huyu ni mzalishaji makini kwa nini anaficha taarifa zake?
Mfano mzuri ni Tanzania Meat Pride kiwanda cha nyama cha Morogoro, wanaozalisha ‘soseji’ ukiwa muuzaji unahitaji soseji zao lakini hawana mawasialiano ya simu wala internet katika paketi zao, sasa sijui mteja akitaka kuongeza oda anawapata wapi. Ingawa wamefanikiwa katika kupunguza wasiwasi kwa walaji wa dini zingine kwa vile wanadai nyama yao imenchinjwa kwa imani ya dini ya Kiislamu (Islamic Doctrine) na BAKWATA wameweka muhuri wao katika kila duka lao na taarifa yao lakini hili pekee haliondoi hofu kama wewe ukiwa bado hutaki kuleta taarifa sahihi ya kuwa uko wapi , na unapatikana vip?
Taarifa kama faida na hasara zilizokaguliwa na wataalamu wa fedha si tu zinawafanya mupate mikopo, la hasha hata walaji wanavutiwa nazo. Kwani kampuni ambayo taarifa zake za kifedha zipo wazi mlaji anaamini kuwa kampuni inaimarika hivyo anaweza kutumia bidhaa husika. Hili ni hasa kwa watengezaji wa vitu vya urembo.
Watumiaji wa mafuta ya ngozi (lotion) na vipodozi vingine hawependi kubadili badili vipodozi kwa hofu ya kuchanganya ‘mambo’Hivyo taarifa hizi za kifedha zitawapa moyo kuwa munafanya vizuri hivyo kuamua kutumia bidhaa zenu kwani wanaimarika na muna nguvu ya kwenda mbele kwa muda mrefu. Hivi ni kwanini kampuni za simu zinatoa taarifa zao au benki unadhani ni kwa sababu ya sheri tu? La hasha walaji nao wanazisoma, ili kufanya maamuzi, kwani walaji wa leo si wale wa Tanzania ya jana, leo soko lina vizazivya 1980 (Generation Y) tena wengi ndiyo hao wapo daraja la kati. Hawa ni wepesi kuiga na wako tayari kujifunza, sasa usipokuja na mbinu za kisasa ni ngumu kuwashawishi.
Nembo za viwango vya ubora. Kulalamika tu hakutasaidia kitu lazima tupambane kisayansi. Njia moja wapo ni hii ya kupata nembo ya ubora kama vile TBS. Nembo hii inapunguza hofu kwa mlaji na kuanza kuamini kuwa bidhaa husika ina ubora inaotakikana. Kwa mfano kufanya vizuri kwa dawa ya meno ya White Dent ni pamoja na kupata hati ya ubora toka kwa Tanzania Dental Association (TDA), hivyo ingawa Aha ilikuwa chini kwa bei kuliko White dent lakini leo hii Aha haipo sokoni. Ni wazi kuwa TDA imeingozea White dent thamani na ubora miongoni mwa wateja .
Hivyo tunahimiza pia si kuamini katika nembo za kiserikali tu hata vyama vya kitaalamu vinapunguza hofu kwa wateja na hasa vyama hivi kwani vingi viko huru.Pia tunaona kuwa punguzo la bei si ushindi kwa kampuni sokoni.
Lingine ni hili la kujitangaza, wazalishaji wa ndani wengi hawajitangazi labda wanaamni katika msemo wa Kiswahili ‘chema chajiuza kibaya chajitangaza’. Ukweli ni kwamba katika sayansi ya bishara na hasa kwa upande wa mlaji(consumer behaviour), mlaji anahusianisha ubora na matangazo kwani kampuni isiyojiamini haiwezi kuweka fedha katika matangazo kwani inaogopa kupata hasara.
Hivyo ile kampuni inayojitangaza mara nyingi inakuwa inanafasi kubwa ya kupata ‘utiifu’ wa mlaji kwa dhana kwamba hii inaubora wa kutosha ndiyo maana imeingia gharama kujitangaza la sivyo isingeliwekeza katika matangazo. Matangazo ni gharama kurasa moja ya gazeti tena isiyo ya rangi ni zaidi ya laki tano katika Tanzania sasa kampuni isiyo na viwango inaogopa kuwekeza katika gharama kama hizi.
Ila mambo ni kinyume chake katika Tanzania leo hii ni kinyume chake kampuni nyingi zinadai zinazalisha bidhaa bora lakini hazijitangazi kwa nini? Jibu rahisi linaweza kuwa wanawasiwasi na bidhaa zao kuwa si bora. Angalia makutano ya barabara kubwa nyingi katika Tanzania kampuni za juisi za matunda toka Kenya na Afrika kusini ndiyo zimeweka mabango ya matangazo yao.Hivyo hili linawajengea imani wateja kuwa kama kampuni hizi zinagalikuwa zinazalisha bidhaa ‘feki’ wasingaliweka mabango na kukubali kuingia gharama, wamefanya hivi kwa vile wamejiamini. Hivyo wazalishaji wa Tanzania nanyi jitangazeni.
Mwisho ni hoja iliyotelewa na Profesa Han C Min mtaalamu wa Marketing, katika jarida la Marketing Reasearch toleo la 26, mwaka 1989, makala ‘Country image: Halo or summary construct? Profesa Han anahimiza wazalishaji kutolindana hasa kupitia umoja wao ili kulinda ubora wa bidhaa zao. Hili la kulindana ndiyo tatizo la wazalishaji wa nchi change Tanzania ikiwemo, kwani kama mutapata sifa kuwa munazalisha bidhaa bora na nzuri wanatokea watu wachache wakiharibu ni taswria ya nchi nzima. Ni taswira ya wazalishaji wote haina mjadala. Leo hii watu wanalalamika kupigwa ‘bambo’ mifuko ya simenti ya kilo hamsini haitimii, wazalishaji wako kimya, sasa ikija sementi toka nje munakimbilia kulalamika wakati kimsingi wenyewe ndiyo musioojali wala kusikiliza mteja anamashaka gani.
Watu wanaozalisha bidhaa feki za konyagi, unga wa mahindi, kufunga vipodozi visivyo na ubora wanaonekana na wanajulikana tena wakati mwingine wanatumia kampuni zilizosajiliwa lakini hakuna kukememeana na kuchukuliana hatua miongoni mwa wazalishaiji na taasisi zao.
Ni vyema kampeni hii ya kuwa mzalendo tumia bidhaa za nyumbani ikawagusa pia wazalishaji nao pia watafute mbinu za kisasa kupambana na hii hali makala haya imebainisha chache tu, lakini kimsingi mbinu za kukabili ‘country of origin effects’ zipo nyingi. Tukishirikiana tunaweza.

Sunday, April 18, 2010

Afrika ya weusi haiwezi kutumia ‘boom’?

‘Afrika haiwezi kutumia vyema kupanda kwa bei katika soko la ulimwengu (boom) wala kujihami na majanga yanayoathiri uchumi wake’ Hi ni sehemu ya taarifa ya ripoti ya Benki ya Maendeleo ya Afrika (ADB) kuhusu muenendo wa biashara na uchumi katika Afrika miaka 90.
Tumeona ni vyema kuanza na maneno hayo katika makala haya ili kujenga tafakari pana ya Afrika ya weusi na majaaliwa yake. ADB inaona hali hii na inaona jinsi bara hili linavyoshindwa kufanya vyema hata kama likawa na ziada kutoka mazao ya mashamba yake.
Afrika ya weusi haina ukame wala neema kila siku ni vilio, ni hali ya muda mrefu lakini lenye kuti uchungu ni kuona hali hii ikionekana kukomaa kama ni stahiki kwa bara hili. Isionekana kama tumekata tamaa la hasha ila tunajaribu kutafuta nji ya kutokea.
Mavuno yakiwa mazuri Afrika bado kuna watu watakufa njaa na wakulima watapata hasara kwa kukosa kuuza mazao kwa bei nzuri na hata kuharika. Hali hii inaonesha Afrika inahitaji zaidi ‘breki’ kuliko ‘kasi’ inayoenda nayo.
Ripoti moja ya UNDP inaelezea Tanzania kupoteza zaidi ya asimilia 60 ya matunda yake kuoza huku bado nchi ikiwa muagizaji mkubwa wa juisi za Maaza, toka Falme za Kiarabu, na Ceres (Hili ni jina la Mungu wa dini za kale za Kigiriki, Mungu wa uzao wa Ardhi) toka Afrika Kusini na Del Monte toka Kenya.
Bidhaa hizi zikifurika katika soko la ndani huku wakulima wa matunda katika mikoa ya Tanzaga, Iringa na Morogoro wakiingia katika lindi la umasikini. Hii ni hali ya kawaida hasa katika Afrika ya weusi.
Hivi karibuni kuna taarifa inaoashiria hayo ya ADB kuwa bado yanaendela katika Tanzania. Naibu Waziri wa Kilimo na Ushirika Dokta Mathayo amekaririwa na vyombo vya habari akisema kuwa wakulima wa nafaka wa Rukwa walio na kitisho cha kuharibikiwa zaidi ya tani 1.2 za mahindi kwa kukoka soko serikali iko mbioni kupata takwimu za ukweli. Taarifa hii ya kitisho cha kuharibika kwa nafasi Rukwa zilitolewa na Serikali ya Mkoa!
Hili likitokea kuna taarifa za kitafiti kuwa watanzania zaidi ya milioni 8 huwa wanashinda njaa kila siku. Hii ndiyo hali ya kutoweza kutumia ‘boom’ umevuna unashindwa kuuza, huku kuna wanaohitaji nao wakiwa hawajui watapata wapi!Sababu kubwa za hali hii imekwisha elezewa sana nalo ni miundo mbinu leo halina nafasi hapa.
Ni wazi kuwa mzunguko huu hauna mwisho mwema, na umasikini utaendelea kutuzunguka wakulima wa mahindi pia wale wanaoakadiriwa na kitisho cha njaa wataendelea kukiona cha moto huku kuna wenzao nafaka zinaoza. Hali ya mambo inaonesha kupanda kwa mfumuko wa bei, na hili katika tafsiri rahisi ni kuwa bei ya vyakula imepanda na hasa vyakula vikuu na hapa tunazungumzia mahindi, sasa iweje tena kuna watu wanakosa soko!Kuna dosari mahali.
Hivi karibuni Waziri Mkuu Mizengo Pinda ameruhusu wakulima wenye shehena za mpunga kuuza nje ya Tanzania. Hatua hii ni mwanzo mwema kuelekea kuwaunganisha wakulima wetu na masoko ya nchi jirani.
Ila wasiwasi wetu ni namna ya kuratibu zoezi hili. Isieleweke kuwa wakulima hawawezi kuuza katika soko la ndani na wala kwamba soko la ndani limeweza kupata inachohitaji isipokuwa ni wakwamba muenendo wa soko umeshindwa kuwaunganisha wakulima hawa.
Tatizo ni wakulima wetu kuunganishwa katika soko la ndani. Ni sisi tunaouza mchele huu nje punde tu tutaenda Thailand na Vietnam kuhitaji kununua mchele. Sasa kwanini tusiwaunganishe wakulima hawa na soko la ndani?Kwa nini tusinunue na kuhifadhi nafaka hii? Strategic Grain Reserve I wapi?
Hapa tena tunashindwa kutumia ‘boom’. Nilishatahadharisha katika makala iliyopita katika siku za nyuma kuwa bei ya mchele Duniani haionekani kupungua na hili linasababishwa na India na Philippines ambao ni walaji na wauzaji wakubwa wa mchele pia kwenda sokoni kuhaha kutaka kununua mchele. Unapomuona muuza mkubwa kaingia sokoini kununua ujue kuna jambo, India yupo sokoni.
Ingawa Philippines alipandisha dau la bei ya mchele lakini hakupata tani alizokuwa anahitaji.India yupo sokoni kwa vile anakabiliwa na hali mbaya ya hewa iliyokuwa kitisho kwa zaidi ya tani 650,000. Hivyo kuamua kupiga marufuku kuuza mchele nje ya nchi.
Tanzania si mmlaji wa mchele kama chakula kikuu ila tunaenda Asia kama kimbilio la njaa. Hali ya mambo ya bei ya mchele duniani inaonesha wazi kuwa hata ule mchele daraja la mwisho toka Vietnam uliovunjika kwa zadi ya asilimia 25 umepata soko katika Afrika nchi kama Mali, Senegal na Nigeria ambayo huagiza zaidi ya asilimia 60 ya mchele.
Hali hii inaonesha sisi hapa tunachezea ‘boom’ kwa kujifariji kuwa ni bora wauze katika masoko ya nchi jirani kwa hoja kuwa tumeshindwa kununua. Lakini hatari i yaja. Kwani bei ya nafaka na hasa mchele haitapungua zaidi ya dola 600, huku Thailand muuzaji mkubwa wa mchele duniani akisusa akingoje walau ipande.Ipande mpaka wapi hakuna anayejua, ni soko limeachiwa liamue.
Pia shirika la OECD, linabainisha wazi kuwa mchele hautashuka zaidi ya dola 600 kwa tani tena huu ni wa dajara la chini (25% broken) kwa vile Ulimwengu umeweka nguvu katika kutumia mahindi kutengeneza nishati ya mafuta (bio fuel) , hali ambayo inafanya mchele ugeuzwe kama chakula cha mifugo katika Uchina, Marekani na Ulaya!
Katika miaka ya karibuni China imebadili uuzaji wa mchele nje huku ulaji wa nyama ukipanda kwa zaidi ya alimia 40 hali inayoelezewa inatokana na kutumika kwa mchele kama chakula cha mifugo. Na Japani moja ya watoaji wa misaada ya mchele kwa Afrika iliyokatika hatari ya kuharibika na hasa kama wanasafisha maghala inatoza kodi wakulima wake wanaotumia ardhi kulima mpunga huku ikiwapa motisha wale wanaolima matunda na mboga mboga ‘tozo’ toka katika wakulima wa mpunga. Hali hii inafanya mchele kupungua duniani.
Pamoja na hayo Afrika ulaji wa mchele unaongezeka hali inayochangiwa na kukuwa kwa daraja la kati katika nchi nyingi za kusini mwa jangwa la Sahara, Tanzania ikiwemo.
Muenendo huu wa soko la nafaka duniani unaashiria kuwa sisi tunacheza na ‘boom’ tena katika nchi ambayo zaidi ya watu milioni 8 wanashinda njaa! Ni vyema tukaipa uwezo Strategic Grain Reserve wa kununua na kuhifadhi nafaka hizi kuliko kupigia chapuo uamauzi wa kuuza nje.
Na isitoshe utaratibu huu wa kuuza nje unapaswa kuratibiwa vyema kwani ni wazi kuwa soko la kimatiafa linasumbua na kama watu wetu hawakujipanga vyema tutaishia kuwa watengeza ajira kwa wenzetu. Kuna mashine za kukoboa nafaka, basi tusiuze nafaka ghafi ni bora tukawauzia mchele ulioongwezwa thamani.

Monday, March 29, 2010

Ushirika na maajaliwa ya ‘Fair Trade’ katika Tanzania

Tanzania ni nchi ya kwanza Kusini mwa Jangwa la Sahara kuingizwa katika mpango wa ‘FAIR TRADE’(biashara huru), ila makala haya itatumia neno 'fair trade' moja kwa moja. Mpango huu ambao ulianza mwaka 1988 kupitia kahawa, kwa sasa unahusisha pia chai na samani hasa zenye kurembwa kwa shanga.
Kagera Cooperative Union (KCU) ni chama cha kwanza kunufaika na ‘Fair Trade’, kwa kuanza kuuza kahawa yake katika masoko ya Ulaya na Amerika. Kimsingi mpango huu umejikita katika nadharia ya kuwapa nguvu wakulima masikini wadogo wa nchi changa kuweza kufikia masoko ya Ulaya, huku wakinufaika kwa kazi ya jasho lao, kwa kulipwa bei nzuri ambazo ni zaidi ya bei ya soko la dunia.
Baada ya manufaa ya mpango huu kwa sasa nchini Tanzania vyama vya ushirika kama Karagwe District Cooperative Union, Kilimanjaro Native Cooperative Union pia wapo katika kuuza kahawa. Pia wafanyakazi wa mashamba ya chai katika Kibena ana Luponde Iringa na Lushoto, Tanga wapo katika mpango huu. Pia kuna mau yanayouzwa na kampuni ya Kiliflora ya Arusha kwa kutumia nembo ya 'Fairtrade' yakiwa chini ya Max Havelaar nembo inayoratibu masoko ya Uholanzi, Ubelgiji na Ufaransa.
Ili kufanikisha mpango wa fair trade ushirika imara ni muhimu kwa uhakika wa soko na mgawo wa pato la mauzo. Ushirika ndiyo kiunganishi kati ya wanunuzi na wakulima. Na hili la kuundwa kwa ushirika imara ni moja kati ya masharti makubwa ya kuweza kusajiliwa kama mzalishaji wa kahawa chini ya mpango wa 'fair trade'. Kwa wamiliki wa mashamba makubwa ya chai moja ya masharti ni kuundwa kwa vyama vya wafanya kazi huru vikiundwa na wafanyakazi wakipata hali bora kama huduma za kiafya na elimu kwa ajili ya watoto wao kutokana na chumo la 'Fair Trade'.
Mpango wa Fair Trade unashika kasi katika Afrika, Uganda na Malawi zinauza sukari, Kenya na Afrika Kusini zikijikita katika chai.Ingawa Tanzania ni mmoja kati ya wakongwe katika nchi za kusini mwa Jangwa la Sahara lakini ushiriki wake unaonekana kupungua. Na hii si kama bei ya kahawa au chai inaonekana kutengemaa sokoni la hasha.
Kwa mujibu wa mtafiti Profesa Fautini Karani Bee katika chapisho Fair Trade- Fair Future anabaisha wazi kwamba mauzo ya chama cha KNCU ya kahawa katika mpango huu, ni milioni 105, 069, 272, kwa mwaka 2008 wakati mwaka 2004 yalikuwa 175, 320, 894. Pato hili ni ile pesa ya ziada ambayo walaji wa Ulaya na Marekani wako tayari kulipa, achiliambali bei ya zao husika kuwa ipo juu ya bei ya soko.Ni wazi kuwa ushiriki wetu unalegalega.
Fair Trade imaleta hali bora kwa wakulima wadogo wa Tanzania , kuna wanafunzi zaidi ya 250 wamepata udhamini wa kupata elimu ya sekondari kupitia mpango uliobuniwa na chama cha KNCU. Pia washirika hawa wameweza kununua hisa katika Kilimanjaro Cooperative Bank.
Upepo wa mafanikio pia unavuma kwa washirika waliochini ya KCU ambao wameweza kununua hisa za kiwanda cha kahawa cha Kagera. Haya na mambo mengine mengi ni mafanikio ya juu wakulima wameweza kujipatia kupitia mfapongo huu.
Changamoto za Fair Trade katika Tanzanai ni nyingi , miongoni mwa hizo ni ukosefu wa vyama vya ushirika imara. Vyama vya ushirika ndiyo nyenzo ya Fair Trade, hivyo kufanya juhudi zote za kuondoa walanguzi sokoni kutegemea vyama hivi.
Wakulima wa Tanzania wamedhalilika na kuoenewa sana na vyama vya Ushirika. Ushirika umekuwa ni mzigo mzito kwa wakulima wa Tanzania. Ingawa ni kweli kuwa hakuna kesho bila kuwa na ushirika na hasa kwa wakulima wadogo na masikini wa Tanzania. Inashangaza ni kwanini serikali imekuwa na kauli nyingi bila vitendo!
Mtafiti Pirotte (2006) katika tafiti ‘Fair-Trade coffee in Nicaragua and Tanzania: a comparison’ iliyochapwa katika jarida la kisomi la Development in Practice , chapisho la 16 namba 5 anabainisha wazi kuwa wakulima sasa katika Tanzania, wamefikia hatua ya kuona FAIR TRADE, ni sawa na wafanyabiashara wengine (walanguzi), lakini hili limechangiwa zaidi na mwenendo wa ushirika. Ni wazi kuwa aliyeumwa na nyoka akiona unyasi atastuka. Maoni hayo yanaonesha wakulima walivyo kata tamaa na Ushirika hivyo lolote lilillochini yake ni wazi kuwa ni ulaghai!
Ni wazi kuwa mwenendo wa ushirika hauridhishi na wenye kuhitaji kurekebishwa ili kufikia lengo la kuwanufaisha wakulima wa Tanzania.
Hivi karibuni Waziri Mkuu M.K. P Pinda na Waziri wa Kilimo J. Wasira kwa nyakati tofauti wakiwa ziarani Japan na Vietnam wamesikika wakiweka wazi juu ya umuhimu wa ushirika imara kwa masilahi ya wakulima wa Tanzania.
Hili la kilio cha kukosa ushirika imara si jambo jipya. Ni kilio cha muda mrefu, na wala kauli za viongozi wetu katika kuhimiza ushirika imara si mpya pia.
Kauli za viongozi ni sahihi lakini zinahitaji vitendo katika kuwajengea wakulima imani dhidi ya ushirika na hili la Fair Trade linaonesha wazi jinsi tunavyochezea shilingi chooni.
Hali ya mambo inaonesha wazi kuwa kukosekana kwa ushirika imara Tanzania iko hatarini kupoteza nafasi yake katika kufikia masoko ya Marekani na Ulaya kupitia mpango huu. Mtafiti Paul Attontile anabainisha wazi kuwa mapungufu ya watendaji na viongozi wa ushirika yamewafanya hata wanunuzi wa kahawa chini ya mpango huu kufikiria kama kuna namna nyingine ya kuwafikia wakulima wadogo wa Tanzania.
Wakati Tanzania inalega lega kutumia nafasi hii, lakini nchi nyingine wao wako wanapambana kuongeza ushiriki wao kwa kusajili bidhaa nyingine mpya zilizoingizwa chini ya mfumo huu, kama vile asali, ndizi, nguo za pamba na bidhaa za mikono.
Mauzo ya sasa duniani kote ni zadi paundi 1.6 bilioni ukijumalisha masoko ya Ulaya na Amerika. Ingawa biashara ya Fair Trade ni wastani wa asilimia 1 ya biashara ya ulimwengu, lakini lenye kutia moyo ni kukua kwa kasi kwa biashara ya mauzo ya huku Itialia ikukua kwa asilimia 404 na Uingereza asilimia 72.
Walaji pia wa masoko ya Ulaya wako tayari kununua bidhaa zenye kujari masilahi ya wakulima masikini wa Kizio cha Kusini kwa zaidi ya asilimia 70. Mwenendo huu wa walaji na soko unaonesha kufanikiwa kwa mpango huu katika kulifikia soko na ‘kukuna’ nyoyo za walaji za ‘Trade not Aid’
Tuimarishe ushirika, kwani majuto ni mjukuu na Fair Trade imeonesha wazi kuwa inamwisho mwema kwa wakulima wa Tanzania, basi tusichezee shilingi chooni, shime viongozi wetu maneno matupu hayavunji mfupa.

Changamoto ya mitaji toka nchi zinazoendelea

Ripoti ya mwenendo wa uwekezaji (World Investments Report) ya shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulika na Biashara na maendeleo (UNCTAD), ya mwaka 2009 inataja nchi zinazoendelea kuwa zimeweza kuhimili hali mbaya ya Uchumi wa Ulimwengu kwa kuweza kupata asilimi 27 ya mitaji toka nje (Foreign Direct Investments). Ingawa kiwango hiki ni cha chini ukilinganisha na mwaka 2007 lakini ni hali yenye kutia moyo.
Jumla ya dola za kimarekani bilioni 88 zimekezwa katika Afrika, kwa mwaka 2009 pekee, pamoja na mafanikio hayo bado miradi mingi toka nje ilishindwa kuendelezwa kutokana na heka heka ya kuyumba kwa uchumi wa Ulimwengu.
Eneo la Afrika Mashariki lilijizolea shilingi bilioni 4, ikiwa ni eneo lililopata mgao mdogo kwa muda wa mwaka wa pili mfululizo. Pamoja na hali hiyo mitaji toka nchi zinazoendelea imeendelea kumiminika Afrika, wawekezaji wakubwa kutoka nchi masikini ni Uchina, India na Afrika Kusini. Huku Uchina ikijikita katika usakaji wa rasilimali ya mafuta katika Angola, Sudan na Nigeria, bila kusahau miradi mikubwa ya ujenzi katika Kongo-Kinshasa na Afrika Magharibi, pia Afrika Kusini ikifanya vyema katika uwekezaji wa madini katika Tanzania kwa kufanikiwa kununua hisa za Ghana na ikisambaa katika ufunguzi wa maduka ya rejareja (supermarkets) toka Nchi za SADC had ECOWAS, bila kusahau ufunguzi wa mabenki.
Wawekezaji wakubwa wa mitaji katika Tanzania ni Afrika Kusini, Kenya, Uchina, India, Pakistani, Mauritius na Malaysia. Lakini tangu ujio wa wawekezaji hawa mara zote imekuwa kilio katika hali ya uchumi wa Tanzania. Toka wafanyakazi, wafanyabisahara na viongozi wetu wetu wa kitaifa.
Wakati fulani Raisi Kikwete akiwa ziarani nchini Japani aliwahi kunukuliwa na vyombo vya habari akiwaasa wajapani wasiwape kazi za kusimamia mitaji yao wahindi na wapakistani kwa vile ‘wanawapunja’ watanzania.Pia Waziri Mkuu M. Pinda aliwahi kunukuliwa na vyombo vya habari akiwaambia wahandisi wa kichina mkoani Arusha kuwa wanakosa vijana wahandisi wa kufanya nao kazi katika kampuni zao kwa vile wanawalipa mishahara midogo. Hivi ni vilio vya kila siku
Katika Tanzania, nchi zinazoendelea zimewekeza kwa wastani wa asilimia 47, hivyo wawekezaji hawa kutoka nchi hizi ni nguzo muhimu katika mageuzi ya uchumi wa Tanzania. Tukitumia takwimu za idadi ya mitaji, Kenya mara zote uhibuka kama muwekezaji namba moja lakini kwa thamani ya pesa Afrika Kusini ndiyo muwekezaji mkubwa katika Uchumi wa Tanzania.
Mitaji toka nchi zinazoendelea imejikita katika maeneo mawili masoko na kiu ya utafutaji wa malighafi kwa viwanda vyao vya nyumbani. Hii ni changamoto kubwa kwa siku zijazo za majaaliwa ya Tanzania na ukuaji wa uchumi na ustawi wa jamii yake.
Lengo kuu la kuhimiza mitaji toka nje na kufanya mabadiliko makubwa ya kiuchumi tangu miaka ya 1980 ilikuwa ni kupata ahueni ya kiuchumi na kimaendeleo kwa jamii yetu. Swali la msingi ni je hawa wawekezaji wa kizio cha kusini wana mwisho mwema katika lile lengo letu?
Makala haya itajaribu kukusanya vipande vipande kuelekea ukweli. Kwani tunaamini uwekezaji ni muhimu kwa ukuaji wa uchumi wa Tanzania ila yatupasa kuangalia na kujali masilahi yetu kama nchi na basi lengo kuu ni kujaribu kukumbushana hasa juu ya mwenendo wa uwekezaji wa siku za karibuni uliojitokeza na makampuni toka Kusini.
Na wala isieleweke kuwa tunataka kutia chumvi au tunapinga harakati za mageuzi ya uchumi la hasha, lengo ni lile lile kujenga Tanzania yenye neema na heshima kwa wananchi wake.
Tunapotupia jicho wawekezaji toka kusini haiimaanishi kuwa wawekezaji wa kasikazini ndiyo wazuri la hasha ila yatupasa kujadili hali ya mambo katika misingi ya makundi ili walau tujue wapi tunakwenda kwa kuzingatia kile tunakichokiona kulingana na matarajio yetu.
Kwa sasa Tanzania ipo katika hali ngumu ya kujaribu kufuta hali ya sura yake katika biashara ya kimataifa, baada ya RITES wakezaji katika sekta ya usafiri mkataba wake kusitishwa. RITES ni kampuni ya India, ni wawekezaji toka nchi zinazoendelea.
Huu si mktaba wa kwanza Tanzania kuufuta, kuna mkataba wa awali ambao nchi iliuingia na wawekezaji toka Uingereza Biwater na wakashindwa kufanya kazi nao ulifutwa , huku Biwater ikienda mahakamani na kushindwa na ikitakiwa kulipa paundi milioni 8 kwa serikali ya Tanzania.
Lakini lililowazi ni kwamba hatujifunzi somo, na kwa sasa kuna hali ya kuendelea kwa yale yale yaliyopita kwa Biwater ndiyo yametokea kwa RITES. Labda tuweke wazi kuwa hili la RITES lilionekana toka mapema kwani mwekezaji mwingine GAPCO aliyepewa hisa bila hata kuwa na mtaji alidumaza jitihada za kufufufua shirika hili, kwani uwepo wa GAPCO ulifanya IFC kusita kutoa pesa za mkopo dola milioni 44, kwa hoja kuwa huyo aliyepewa hisa, GAPCO, ni mdeni wa IFC hivyo kuna ulakini kama hatua hii itaenda sawa kama ikipewa tena dhamana ya deni la dola milioni 44!
Kutokana na GAPCO kukumbana na kigingi cha IFC, serikali ikaingia kuwa mbia na RITES bila maandalizi.Ni wazi kuwa hatua hii ilichangia kwa kiasi kikubwa kuyumba na kupungua imani miongoni mwa wafanyakazi kwa RITES. Katika mchakato huu kuna mwekezaji mwingine toka India aliyekuwa na wastani wa hisa mbili alijitoa! Bila shaka maji yalizidi unga waswahili wanasema naye aliweza kubashiri vyema.
Hili la RITES si la kwanza ila inaonekana hatujajifunza somo hasa inapokuja wawekezaji toka Kusini, kwani mwaka 2007, Brookside kampuni ya Kenya ilinunua kwa mbwembwe kiwanda cha kusindika maziwa cha Arusha na kuahidi kufanya uwekezaji wa dola milioni 100, katika sekta ya maziwa. Lakini kilichokuja kushuhudiwa ni Tanzania kugeuzwa kuwa shamba la malighafi na uzalishaji unafanyika Kenya.
Mwaka jana ndipo waziri mwenye dhamana ya Afrika Mashariki Dk.Deodorus Kamala alipoifukuzilia mbali Brookside. Ingawa sura ya Tanzania imechafuka lakini liliwazo kuwa hawa wawekezaji toka nchi zinazoendelea mara zote wamekuwa ni wajanja wajanja na wanafanikiwa kwa gia ya kuonekana kama watu wanaoweza kustahimili hali ngumu za miundo mbinu ya Afrika lakini mwisho wake ndiyo haya.
Wawekezaji toka kusini kila wanapowekeza kila wakati imekuwa ni vitendo vya malalamiko na manung’uniko nchini. Hivi karibuni kuna wawekezaji katika sekta ndogo ya ngozi wenye asili ya India na Pakistani kuwa hawapo tayari kuongeza thamani ya ngozi katika viwanda vya ndani na badala yake wanasafirisha ngozi ghafi kwao!
Hilo likiwa halitoshi Ripoti moja ya FAO inataja kuwa kuongezeka kwa vyakula toka nje ya Tanzania ni kwa sababau wawekezaji katika sekta ya utalii na hasa hoteli huagiza vyakula toka nje huku vikiweza kupatikana Tanzania.
Hivi karibuni Waziri Ngeleja amenukuriwa na vyombo vya habari kuwa wawekezaji katika migodi waache kununua nyama nje ya Tanzania badala yake wanunue nyama Tanzania ili tuongeze tija katika viwanda vyetu vya ndani na kuongeza ajira. Katika sekta ya nyama kuna SAAFA ya Rukwa na Tanzania Meat Pride Morogoro. Hatua ya muheshimiwa Ngeleja, ni rai njema sijui katika vitendo itakuwaje, ni suala la kusubiri na kuona, ila ni mwanzo mwema.
Kila kitu sasa tunaagiza toka nje huku ndani kuna wajasiriamali wadogo waliowekeza katika kilimo na usindikaji wakitaka kupata hizo kazi tunapewa hoja chakavu kuwa minofu yao haina viwango mara minofu ya kuku ina harufu ya dagaa!
Bila mabadiliko ya kisera katika kuhakikisha wawekezaji wanatumia bidhaa za ndani ni wazi kuwa tutabakia kuwa watazamaji. Kuna nchi zimeweka wazi kuwa mwekezaji anapaswa kufanya nini anapoingia nchini na asilimia ngapi ya malighafi anayotumia inapaswa kutoka soko la ndani.
Bidhaa wawekezaji wa ndani wanaikataa lakini inapenya na kufanya vyema katika masoko ya Ulaya, tena ikisifiwa kuwa na viwango bora. Kuna mifano mingi ya bidhaa za kilimo zinazofanya vyema Ulaya lakini nyumbani hazina nafasi!
Tusibwete katika ‘kulainisha’ mambo kwa kigezo cha kuvutia mitaji. Hili la kuwa na wachuuzi wa Kichina Kariakoo, Kenya majirani zetu tangu miaka 1960 wameweka wazi kuwa mwekezaji wa nje hapaswi kuingia katika sekta ya’ juakali’. Lakini Tanzania hapana.
Niliwahi kuhudhruia ‘carrier workshop’ ya moja ya benki katika Tanzania, wakati wa majadiliano kuhusu mishahara Mkurugenzi wa Benki alieleza wazi kuwa hataweza kulipa zaidi ya mshahara wa serikali. Kigezo alichotumia ni kuwa serikali inawalipa wenzenu TGSD, tena wenye shahada kama nyinyi!
Kumbe katika malipo ni sisi ndiyo tumejimaliza na hakuna mchawi ila ni serikali kuwa na viwango vidogo vya mishahara na wageni wakija wanaangalia ‘skeli’ za serikali nao wanatumia kigezo hicho hicho katika hali kama hii ni vigumu kuona mitaji kutoka nje ikiwaneemesha watanzania.

Friday, March 19, 2010

Bravo TRA

BRAVO TRA kwa kufuta kodi ya silimia 18 ya VAT kwa wauzaji wa mboga mboga nje ya nchi.Hakika huu ni mwendelezo wa mwanzo mpya tuliwahi kuandika juu ya hili, januari 4 mwaka huu.KUpitia gazeti la serikali Daily News la tarehe 18.03.2010, Kamishna wa kodi amefuta kodi ya VAT ya asilimia 18.
Kila la heri wakulima na wajasiriamli katika sekta ndogo ya mbogamboga na maua.

Monday, March 15, 2010

‘Food miles’ changamoto kwa biashara ya chakula toka Afrika

Mabadiliko ya tabia nchi na hali ya hewa Duniani yanaendelea kufanya wanasayansi kufikiria njia za kupambana na madhara yake kwa kila namna. Inakadiriwa watu 800,000 wamepoteza maisha na jumla ya dola za kimarekani trilioni 1 kama hasara jamii ya ulimwengu huu imeipata kutokana na mabadiliko hayo ya hali ya hewa ya ulimwengu.
Katika nchi za Ulaya na Marekani nadharia inayochipua kwa kasi na kuungwa mkono na wakulima wengi ni ‘food miles’ huku wakipiga chapuo ‘local is good’. Nadharia ya food miles iliyochomoza kwanza Uingereza sasa inaonekana kupendwa pia na wakulima na taasisi zinazotoa mikopo katika Marekani.
Food miles ni nini?(nitalitumia neno hili kama lilivyo kwani sina neno zuri la Kiswahili),hii ni nadharia rahisi inayozingatia umbali kwa kupima madhara ya uharibifu wa mazingira yatokanayo na uzalishaji wa chakula toka shambani hadi mezani kwa mlaji. Hivyo walaji wanashauriwa kususia vyakula vilivyo safiri umbali mrefu kwa lengo la kulinda mazingira, yanayochafuliwa na hewa ya ukaa(KABONIDAYOKSAIDI), na badala yake watumie vyakula vilivyozalishwa nchini kwao ambavyo mfumo wake wa uzalishaji na usambazaji ni wenye umbali mfupi!
Nadharia hii iliibuliwa miaka ya 1990 na Profesa Tim Lang ambaye kwa sasa ni mhadhiri katika City University London. Tangu wakati huo kama tulivyo sema hapo awali wakulima wa Kiingereza na Marekani kupitia vyama vyao wamekuwa wakihimiza utumiaji wa bidhaa zandani (Local is good) kwa hoja ya kulinda na kupunguza uharibifu wa mazingira.
Uingereza moja kati ya masoko mazuri ya bidhaa za kilimo katika Jumuiya ya Ulaya, inakadiriwa kutumia paundi milioni 105 kwa ajili ya ununuzi wa mboga mboga na milioni 89 kwa matunda kutoka Afrika ya Kusini mwa Jangwa la Sahara.
Ni wazi kuwa kushika kasi kwa nadharia hii katika biashara ya chakula kunahatarisha hali ya jamii ya wakulima wadogo masikini wa kizio cha kusini na hasa Afrika. Ingawa mpaka sasa wanasayansi wanasema kuwa mchango wa Afrika katika kuchangia uharibu wa hali ya hewa ni mdogo. Afrika inakisiwa kuchangia asilimia 0.5 ya gesi ya ukaa na bidhaa zinatoka eneo husika hulimwa kwa njia za kijadi (jembe la mkono, plau, mbole ya samadi, bila hata kutumia dawa za kuulia wadudu)
Kimsingi huu ni mwendelezo wa kuonesha wazi kuwa soko la Ulaya lilivyo kigeugeu na wala siyo la kuaminika. Lakini pamoja na hayo yote bado Afrika imekuwa ikiweka nguvu kuzalisha bidhaa kwa ajili ya soko hili. Hili tumelizungumza katika makala nyingi katika siku za nyuma.
Watetezi wa bara la Afrika nao hawakukaa kimya.Mashirika ya kimataifa kama Oxfarm GB na kampuni za wauzaji wakubwa wa bidhaa za kilimo toka Afrika kama Sainsbury wamejitokeza hadharani kupinga wimbi hili la ‘food miles’ lenye nia ya kuitoa Afrika katika biashara ya Ulimwengu kwa kigingi cha mabadiliko ya tabia nchi. Mkurugenzi Mkuu wa Sainsbury aliita hatua hii kama ‘protectionism’ ya aina yake na kampuni yake haiko tayari kukubali hii nadharia kwa ukweli kwamba kununua Afrika ni njia ambayo inapelekea ukombozi wa kiuchumi na kijamii kwa wakulima wengi wadogo wa bara hili.
Bado wataalamu wa kilimo wa Afrika na wanasayansi wanaendelea kupinga nadharia hii kwa hoja kuwa bara hili halizalishi kiwango kikubwa cha hewa ya ukaa wakati wa shughuli za kilimo na wala njia zinazotumia kusafirisha chakula toka Afrika bado hazichangii kwa kiasi kikubwa kuzalisha hewa ya ukaa. Kilimo cha Afrika bado cha jembe la mkono na kisichotumia mbolea, hivyo mazao yale yauzwayo nje ya bara hili kama kahawa, sukari, kakao, pamba, korosho, tumbaku, maua, mbogamboga chai huchangia kwa kiasi kidogo katika kuharibu ‘ozone layer’
Nchi nyingi za Afrika, kigingi hiki ni pigo kwani bado kilimo ni chanzo kikubwa cha ajira, pato la taifa, kwa mfano kwa Tanzania zaidi ya asilimia 50 ya pato la fedha za kigeni linategemea mauzo ya kilimo, Malawi ni zaidi ya asilimia 80, na Kenya ni zaidi ya asimilia 65.
Hivyo juhudi hizi hasi za kuona Afrika haifikii masoko ya Ulaya kwa kigingi cha ‘food miles’ na kampeni za kupambana na uharibu wa mazingira ni pigo kwa Afrika. Taasisi moja ya Kingereza inayojihusisha na maendeleo ya kilimo maeneo ya vijijini ilibainisha wazi kuwa msukumo mkubwa upo katika kulinda wakulima wa Kiingereza, kwani ni wazi kuwa kila kitu sasa kinaonekana kuwa kinatoka nje ya Uingereza.
Kilimo cha nyumbani (Local is good) kinapingwa pia kwa hoja kuwa hali ya hewa ya nchi hizi wakati wa wa baridi hutumia nishati kwa kiasi kikubwa (green house) na hivyo lile la kupambana na mabadiliko ya hali hewa halina nguvu.
Ni wazi kuwa suala la mazingira halina tajiri wala masikini, kila mmoja ana jukumu la kupambana na uharibifu wa mazingira, ila lililowazi kuwa Afrika safari hii inakabwa na juhudi hizi. Afrika ambayo inakabiriwa na mapigo makubwa ya mabadiliko ya tabia nchi ikiwa na tishio la kugeuka jangwa, ukosefu wa mvua, ongezeko la joto na mufuriko, inapaswa kujitahidi kupambana na haya yote.
Ila wataalamu wa mazingirwa wanabainisha kuwa, mifumo ya maisha ya wakazi wa kizio cha kaskazini ndiyo chanzo kikubwa cha mabadiliko ya hali ya tabia nchi. Katika Ulaya nyama inasadikiwa huchangia kwa kiasi kikubwa, kwani unenepeshaji wa mifugo kwa kutumia nafaka badala ya majani au nyasi. Wataalamu wanashauri kubadilisha milo toka nyama kwenda majani na mboga mboga.
Pia mtindo wa uendeshaji wa magari yenye injini kubwa (sports cars) yanayokula mafuta kwa kiasi kikubwa huchangia kwa kiasi kikubwa . Utupaji wa chakula, ambayo mabaki haya hutumia kuziba makorongo huzalisha kwa kiasi kikubwa hewa ya methane ambayo huchangia kwa kiasi kikubwa kuharibu anga la dunia. Japani hutupa tani milioni 20 kwa mwaka, hivyo rai ipo kwa watu wa kizio hiki kujitahidi kutotupa chakula.
Kigingi hiki kinatufanya kuangalia soko la ndani kwa masilahi ya Afrika. Biashara ya ndani ya bara la Afrika ni asilimia 4 tu, huku nguvu nyingi zikiwekwa katika kufikia soko la Ulaya. Ingawa ni kweli kuwa mahitaji ya fedha za kigeni ni makubwa kwa ajili ya kuagiza mahitaji mengine muhumi kama dawa, bidhaa za viwanda na mitambo. Lakini biashara ya ndani ingeweza kupanuwa uwigo wa wakulima wa bara la Afrika kuliko kukaa na kugombania kufikia katika soko la Ulaya pekee.
Soko la ndani katika nchi nyingi za kiafrika bado kufunguka huku kila nchi ikiwa iko tayari kuweka kigingi kwa nchi ya kiafrika lakini ipo tayari kufungua milango kwa nchi za magharibi. Hili la food miles ni changamoto nyingine kwa Afrika, tuna jukumu ya kuhakikisha linapata suluhu ya kudumu kwani ni nadharia inayosambaa kama moto katika nyasi za savana.Juhudi za kampeni ya kuhamasisha kupenda bidhaa za nyumbani ambayo Tanzania inafanya kupitia CTI ni suala la kuhimizwa kwa nguvu zote, na juhudi hizi zinapaswa kupelekwa katika shule na vyuo. Huu ni mwanzo mwema, kwani sasa food miles inashika kasi katika Ulaya na Marekani, kwa hoja ya mazingira. Basi yatupasa kupenda bidhaa za nyumbani.

Monday, March 1, 2010

Wakulima wadogo masikini watakombolewa na ‘fair trade’?

Ni mashamsham ya maazimisho ya wiki mbili ya kuhamasisha ‘fair trade’ katika nchi za Ulaya na Marekani kwa zaidi ya siku kumi na nne, toka Februari 22 hadi Machi 3. Miongoni mwa nchi zilizo katika mpango wa Fairtrade ni Uingereza, Ujerumani, Marekani, Japan,Ufaransa, Italia, Uholanzi, kuzitaja kwa uchahe tu. Kimsingi nchi hizi ndiyo masoko ya bidhaa za kilimo na za ubunifu wa mikono zinazotengenezwa katika nchi za Dunia ya tatu zikiingia sokoni kwa nembo ya fair trade.
Fair trade ni nadharia iliyojikita katika ‘utu’ huku ikiwa na msukumo wa kidini na maadili ili kuona wale watu waliomasikini kabisa duniani kutoka nchi masikini wanapata nafasi ya kufaidi jasho linalo tokana na kazi yao.Lengo kuu ni kuhakikisha bidhaa za watu wa kizio cha kusini zinafika katika masoko ya Ulaya na Amerika na wateja wakinunua bidhaa hizo ni wazi kuwa sehemu ya pato hurudi moja kwa moja katika nchi husika kusaidia maendeleo ya watu wa eneo hilo.
Nadharia hii inaweka katika vitendo, kile tunachokiita ‘trade not aid’. Lakini kwa sababu mfumo wa ulimwengu hauko wazi na bei za mazao mara zote zinaporomoka basi wakulima wa kizio cha kusini watapata nafuu, kwa kutoza bei ya juu kwa walaji wa kizio cha kaskazini na ile ziada iliyokuwa zaidi ya soko inakwenda kwa watu walio masikini.
Msukumo wa fair trade katika nchi za magharibi unaanzia katika makanisa, huku zaidi ya makanisa 6000 yakiwa yamejiunga katika mpango huu. Awali nimesema kuwa mpango huu umejikita katika maadili ya kiroho zaidi, na nyumba za ibada na taasisi za kidini na mashirika yao ndiyo yanayoongoza mpango huu wa ukombozi kwa watu wa kizio cha kusini.
Nguzo kuu ya maadili ya fairtrade yapo katika biblia, methali 13:23’Shamba la masikini hutoa mazao mengi , lakini bila haki hunyakuliwa’. Maneno hayo yamepamba baadhi ya makanisa katika Uingereza yanayojinadi kutumia bidhaa zenye nembo ya fair trade. Kupitia taasisi za kidini na mashirika yake wanaamini walaji wa nchi tajiri inabidi wanunue vitu kwa bei ya juu ili ziada irudi katika nchi asili ambako zao limelimwa ili kusaidia wakulima masikini.
Katika kutekeleza mpango huu njia moja wapo kuwa na chama cha ushirika na wakulima ujiunga pamoja kwa hiyari.Wakulima ni wale walio wadogo chini ya hekari 3 huku wakiwa wanaendesha shughuli zao za kilimo. Ingawa sasa kuna mjadala mkali wa kuangalia nini mantiki ya kutaka wakulima wadogo wapate haki ya kuuza kupitia mpango huu.
Inakadiriwa zaidi ya wakulima 500,000 na vyama vya ushirika 300 vipo katika mpango huu katika kizio cha kusini. Mauzo yanakadiriwa kufikia Euro bilioni 2.4 kwa mwaka jana.
Gazeti la The Independent la tarehe 25 Februari 2008 lilipoti mauzo ya bidhaa za fair trade kufikia paundi milioni 500 kwa Uingereza pekee. Huku idadi kubwa ya kampuni kubwa kama Mark Spencer, Waitrose,ASDA , Morrison na Tesco zikijiunga na kuahidi kuweka bidhaa za fairtrade katika maduka yao.
Fairtrade ni biashara inayovutia sana makampuni makubwa kwa sasa na kifimbo kinaonekana kupokonywa kutoka kwa taasisi za kihiyari kama Oxfarm, Traidcradt, Cafod sasa imekuwa ni biashara pendwa. Huu ni ushahidi wa wazi kuwa watu wengi wameitikia wito wa kununua kwa bei ya juu ili kwenda kusaidia watu masikini wa kizio cha kusini.
Tanzania inatajwa kama nchi ya kwanza kunufaika na mpango huu wa fairtrade, kwa kahawa kutoka Kagera mwaka 1988 kupitia chama cha Ushirika, Kagera Cooperative Union. Mpango huu pia unatumiwa na Kilimanjaro Native Cooperatives (KNCU) kwa kahawa yao kuuzwa Ulaya kupittia mpango huu.
Pia wamiliki wa mashamba ya chai wa Kibena, Iringa Tanzania ni miongozi mwa wafanyakazi wanaonufaika kwa bidhaa zao kufanikiwa kujipenyeza katika masoko ya Ulaya. Pia kuna bidhaa za mikono, zilizopo katika masoko ya Ulaya na Amerika kutoka Tanzania.
Mwenendo wa biashara unaonesha wazi kuzinufaisha nchi za dunia ya tatu. Tanzania kupitia KCU imeweza kuuza asilimia 7 ya kahawa yake yote inayozalisha. Kwa Mujibu ya mtandao wa taasisi ya Fair trade, inabainisha wazi kuwa wakulima wa Kagera wameweza kununua hisa za kiwanda cha Tanica kinachozalisha kahawa kwa asilimia 51.
Kahawa ya Arabica kutoka Afrika imewekwa katika bei ya dola 2.80 kwa Kilo,huku sent 11 dola za kimarekani kama bei ya juu (premium price) kwa kilo ikiwa fedha hii inapaswa kutumika kwa ajili ya maendeleo ya wakulima husika.
Bently W.R na wenzake katika Jarida la kisomi, Sustainable Development toleo 13, 2005 makala waliyoiita ‘What Tanzania’s farmers can teach the world’ wanabainisha kuwa kuna nyongeza ya kipato kwa wakulima wadogo wa kahawa wale walio katika mpango wa Fairtrade kulinganisha ni mifumo mingine .
Mafanikio mengine ni pale KNCU ilipoweza kuwalipia ada wanafunzi wanaokadiriwa kufikia 278, hawa ni wanafunzi wa shule za sekondari za serikali ambao wazazi wao wamefariki kwa ugonjwa wa Ukimwi au wanaoishi katika mazingira magumu.
Profesa Faustin K. Bee katika tafiti ‘Fair trade Fair futures: KNCU scholarship programme for children made vulnerable by AIDS’, 2009 anabaninsha wazi kuwa kipato cha kahawa kinachotokana na fairtrade kimekuwa si cha kuaminika kwa KNCU.Mwaka 2004 ilipatikana milioni 175 mwaka 2008 milioni 105. Majaaliwa ya mipango mizuri yote inawekwa majaribuni!
Haya ni mafanikio makubwa kufikiwa kwa wakulima wadogo waliojiunga chini ya chama cha ushirika. Lakini swali letu linabaki kuwa fairtrade ni mkombozi wa wakulima masikini toka mfumo mbovu wa biashara ya ulimwengu?Lililowazi ni kuwa fairtrade inaendeshwa nje ya nguvu za soko za ‘demand and supply’, kwani mlaji analipa zaidi ya bei ya soko na ziada inakwenda kwa wakulima wa nchi masikini.
Lililowazi kwamba wakulima wa Tanzania bado wanakumbukumbu ya maumivu ya walafi wachahce waliokula mali za ushirika bila kuchukuliwa hatua na safari hii fair trade inahimiza ushirika. Je Fair trade kupitia ushirika tutafikia lengo katika Tanzania, au yale yale?
Walaji wa Ulaya na Amerika hawatakuwa tayari kuona maadili ya utu yanavunjwa huku wao wakilipa bei ya juu kuliko bei ya soko na walafi wakihujumu chumo la fair trade. Ni wazi kuwa watasusa. Jukumu la kusukuma mbele malengo ya fair trade ni wazi kuwa Tanzania kama nchi ina nafasi kubwa ya kushiriki kuhakikisha wakulima wadogo wanalindwa na makucha ya walafi wanaojificha katika ushirika. Shime wenye mamlaka.

Sunday, February 21, 2010

Nembo za kijiografia ni chanzo cha mapato kilichosahaulika

Brand sina neno zuri la Kiswahili lakini katika makala haya tutatafsiri kama ‘nembo’.Kimsingi ni alama ya biashara inayojumuisha rangi, alama, na vifupisho vya herufi. Nembo ikilindwa kisheria inaitwa ‘trade mark’. Katika taaluma ya biashara inaaminika kuwa bidhaa zinatambulika zaidi kwa nembo.
Hili linatokana na ukweli kwamba mteja mara zote anapata faraja ya ‘kisaikolojia’ mara anapotumia bidhaa anayoitambua kuliko kutumia bidhaa asiyoijua na jina au asiyoikubali kwa nembo ingawa inaweza kufanya vizuri.
Mfano mzuri wa jinsi akili zetu zinavyoweza kutekwa na uhimara wa nembo hadi kila kitu ukajikuta unakitambua kwa jina hilo ni nembo ya ‘Shell’, hii ni miongoni mwa kampuni kubwa ya mafuta duniani inayomilikiwa kwa ushirikiano wa Wadachi na Waingereza, lakini hadi leo katika Tanzania kila anayeenda katika kituo cha mafuta anatamka anakwenda Shell ingawa ukweli wa mambo ni kuwa Shell haipo katika biashara ya mafuta Tanzania.
Hili linaonesha wazi kuwa mteja anaponunua bidhaa mara nyingi hanunui bidhaa ananunua nembo.Kibiashara nembo inafaida nyingi, ikiwemo urahisi wa utambuzi kwa mlaji na kuhimarisha marudio ya matumizi.
Ingawa kwa sasa ulimwengu unashuhudia kuibuka kwa nembo binafsi (own brand) kwa kampuni nyingi kubwa duniani, lakini bado mauzo ya nembo zilizobuniwa na kampuni husika kama vile Lee, Levis, bado yapo juu.Katika Tanzania mageuzi haya pia yapo ndiyo tuna dangirizi za KP,Tippo, na vyakula vinavyofungwa kwa majina ya Supermarkets kama Shoprite. Moja ya kampuni kubwa inayofanya vizuri kwa kutumia nembo yake na si za wazalishaji ni Mark Spencer wenye nguo zinazokwenda kwa jina la kampuni badala kuwa nguo kama Lee, Levi’s kama tulivyozoea.
Nembo ni msingi wa biashara na ndiyo maana kuna kampuni zinachaji gharama kubwa si kwa tofauti ya malighafi tu ni kwa vile nembo yao iko na thamani kubwa na yenye kuheshimika. Wataalamu wa mambo ya fedha na mitaji wanakadiria kuwa asilimia 70 ya mtaji wa kampuni iko katika nembo.
Kwa mfano kampuni ya Zain Tanzania mwaka 2007 ilitumia zaidi ya bilioni 5. 1 za kitanzania kwa ajili ya matangazo ya nembo yake tu, hii kwa mujibu wa gazeti la Advertising Age, la Desemba 8 mwaka 2008.Mfano huu unatuonesha wazi kuwa mara nyingi kampuni zinawekeza katika kutangaza nembo zao.
Makala haya itajaribu kujadili umuhimu wa Tanzania kama nchi kupigania haki yake kutoka kwa kampuni za kimataifa au za ndani zinazotumia majina ya vivutio vyetu vya asili nasi tupate sehemu la pato kutokana na mauzo.
Katika Tanzania leo hii kuna makampuni mengi yanayotumia Kilimajanro, Serengeti, Mikumi na kadhalika kama sehemu ya nembo zao kibiashara. Takwimu haziko wazi kama Tanzania inanufaika kutokana na kampuni hizi kutumia majina yetu ya kijiografia kama nembo zao za kibiashara nchi inapata chochote.
Ila mfano wa Ethiopia inaonesha wazi kuwa nchi nyingi za Afrika zinakosa pato kubwa kutokana na matumizi ya nembo zao za kijiografia kutumika nasi hatulipwi hata shilingi.
Wakisaidiwa kisheria na Oxfam; Ethiopia ilichachamaa na kufungua madai ya haki miliki katika Ofisi za Haki Miliki nchini Marekani, ikiitaka Starbuck kampuni kubwa ya kimarekani kufikiria kuipa stahiki yake kwa kutumia nembo ya eneo moja katika Ethiopia kwa bidhaa zake za kahawa inayozalishwa na Starbuck.Kilio cha Ethiopia ilikuwa kudai pato linalotokana na chumo la 'premium price' linalovunwa na 'Starbuck' kutokana na kuuzwa kwa kahawa hiyo katika mikahawa mbalimbali inayomilikiwa na Starbuck katika Ulaya na Marekani.
Starbuck inatumia majina ya Sidamo, Harar na Yirgaeteffe maeneo katika Ethiopia kama nembo ya kahawa yake. Ikimbukwe kuwa Sidamo ni mahali ambako inaaminika ni moja kati ya sehemu ambazo mbegu ya kahawa ya kwanza ilioteshwa na binadamu, hivyo eneo hili inaonesha kuwa ni sehemu nzuri na ipo katika vichwa vya walaji makini wa kahawa na ni wazi kuwa wataithamini kahawa yenye jina hilo kwa heshima ya kihistoria.
Na ubora wa Sidamo kama eneo unatumika na Starbcuk katika matangazo yake kuinadi kahawa yake.Kahawa yenye nembo ya Sidamo ikiuzwa hadi dola 26 kwa kilo huku wakulima wa Ethiopia wakiambulia dola moja tu ya chumo.
Baada ya vuta ni kuvute iliyoanza tangu Mei 2005, Starbuck ilikubali kuipa Ethiopia dola milioni 88 kama pato linalotokana na kutumiwa kwa maeneo yake kama sehemu ya nembo ya biashara.Oxfam iliuita ushindi huu kama ‘fair trade’ ya aina yake kwani wakulima masikini wa Sidamo nao watapata chumo lingine toka kwa kutumika kwa nembo ya eneo lao.
Katika chapisho, Regional Branding Marketing, Matthew Muntberg, anataja sababu moja wapo ya kufanikiwa katika kuchagua jina zuri la nembo ya kijiografia ni kutafuta sehemu yenye heshima ya ‘kipekee’. Hivyo wanaotumia majina yetu ya kihistoria na urithi wa nchi yetu kama nembo zao kibiashara wanatambua hili kuwa ni vitu vyenye mvuto na kuheshimika.
Tanzania ina bidhaa ambazo zinatumia majina ya vivutio, kama vile mlima Kilimanjaro, Serengeti kwa mbuga ya wanyama yenye heshima kubwa Duniani. Bidhaa hizi ni kuanzia maji, bia na hoteli za kisasa zenye kutumia majina yetu ya kijiografia.
Aina ya nembo za maeneo (Regional /geographical Brand) si kitu kipya duniani, kuna Idaho Commission kakika Marekani yenye zaidi ya miaka 70, ikisimamia wazalishaji wanaotaka kutumia nembo hiyo ya eneo kwa kuzalisha viazi mbatata kulipa, huku ikijikusanyia zaidi ya dola milioni 12 kama kamisheni, ya kutumika kwa eneo lao kama nembo.
Kutoza watumiaji wa nembo za kijiografia ni chanzo kingine cha mapato kilicho sahaulika katika Tanzania. Na hili litatupunguzia kutoza kodi watu walio na hali duni hasa wakulima wa nchi hii kwa kodi ambazo ni za kidhalilishaji huku kuna vyanzo wenzetu wameviona na wanavitumia.
Basi wakati umefika wa Tanzania kama nchi nayo ipate gawio kutoka katika matumizi ya vivutio vyetu kibiashara na si kuacha watu wachache wakinufaika na huku watu wengi waliozunguka maeneo husika wakitaabika. Ethiopia imeonesha njia, tujifunze kutoka huko.Shime wataalamu wa sheria.

Sunday, February 14, 2010

Elimu ya biashara na anguko la uchumi wa Ulimwengu

Anguko la Uchumi wa Ulimwengu limeleta madhara makubwa lakini lililowazi ni juu ya UBORA na UMAKINI kwa ujuzi unaotolewa katika shule za biashara DUNIANI.Katika Marekani swali lilikuwa juu ya majaaliwa ya elimu ya MBA (Masters of Business Administration). Katika Afrika Kusini kuna waliojiuliza kwa nini waafrika waende kusoma katika nchi ambazo zimeshindwa kuzalisha wasomi walioweza kulinda ‘msusuko’ huu.Yaani katika vyuo vya Marekani na Ulaya.
Pamoja na madai hayo bado MBA imekuwa ni elimu pendwa kwa sasa, hasa nchini Marekani kwani inakadiriwa watu wengi waliokosa kazi walirudi madarasani na wengi walirudi kusoma hizo elimu za biashara.Kampuni kubwa za kimarekani zilizoanguka zinaongozwa na wataalamu wa biashara kutoka vyuo bora kama vile Harvard, Stanford, MIT na kadhalika.
Makala haya haina nia ya kujaribu kusimulia nini kilichosababisha ‘msukosuko’ huu mkubwa wa kiuchumi duniani ulioanzia Marekani mwishoni mmwa 2007, ila tutajaribu kuangalia majaaliwa ya sekta ya Elimu ya Biashara katika Tanzania na nini tunaweza kujifunza.
Rais Barack Obama alipoingia madarakani aliendeleza mpango wa kunusuru taasisi za fedha na bima mpango ambao uliasisiwa na rais aliyemtangulia George Walker Bush Jr. Lakini mpango huu uligubikwa na utata wa matumizi yasiyorasmi ya malipo ya posho za maofisa wa ngazi za juu.
AIG (American Insurances Group), ilitumia dola milioni 165 kulipa posho ya maofisa wake. Hali hii ilifanya White House kuingilia kati na kuweka wazi kuwa haipo tayari kuona ‘bailout’ ikitumika kujilipa posho na malipo mengine manono ya maofisa wakuu wa benki na hasa katika kipindi hiki cha kupambana na anguko la Uchumi wa Ulimwengu.
Hili linaashiria kutokuwepo kwa umakini wa hali ya juu ambao unalalamikiwa na watu wengi duniani miongoni mwa watendaji wa sekta za fedha.Na hasa lililowazi ni hili la kukosekana kwa maadili, watu wachache wajilipe wakale ‘starehe’ ufukweni au kidogo kilichopo kitumike kwa ajili ya kulinda masilahi ya wengi!
Katika Marekani kuna walioenda mbali zaidi kwa kuikebehi elimu ya MBA kama ‘Masters of Disaster’. Ni wazi kuwa anguko la uchumi wa ulimwengu ni changamoto kwa elimu ya MBA na hasa shule za biashara duniani.
Kwa mwaka nchini Marekani pekee wahitimu wanaokadiriwa kufikia 100,000 uhitimu katika ’specialization’ mbalimbali za elimu ya MBA, huku asilimia 40 wakiajiriwa katika sekta ya fedha. Na sekta hii inasadikiwa ndiyo ‘chokochoko’ ya mdororo wa Uchumi ulikoanzia, pale maofisa walipokuwa wakikimbizana kutoa mikopo ili kupata ‘bonuses’ bila kujali uwezo wa mlipaji. Mikopo iliwafikia, NINJA (No Investment, No Job, No Asset) Hapo ndipo mtafutano ulipoanza, huku wakiwa na lundo kubwa la kadi wakitumia kwa mtindo wa ‘credit card’, hili lilipelekea ‘mkusanyiko’ mwingine wa madeni usiolipika kutoka sekta nyingine.
Pia kurunzi lilimulika ule utamaduni maarufu wa kuandaa mameneja, unaotambulika kama ‘Harvard Culture’. Msusuko huu wa uchumi unafanya kutimia kwa ubashiri wa Profesa Henry Mintzberg, mwanazuoni wa Masomo ya Uongozi, katika Chuo Kikuu cha McGill, Canada.
Profesa Mintzberg alipinga ‘utamaduni wa Harvard’ wa kumuandaa menejea darasani na aliweka wazi msimamo wake kuwa meneja siyo MBA, na kimsingi meneja bora anapaswa kunolewa huku akiwa anajifunza toka kwa waliomtangulia na situ kukabidhiwa wadhifa kwa msingi wa cheti.
Pamoja na yote hayo Ulimwengu umeendelea kushuhudia shule za Biashara na hasa elimu ya MBA ikipata wanafunzi wengi kuliko nafasi za udahili kama nilivyokwisha sema hapo awali. Ni wazi kuwa MBA inapendwa, na sokoni bado ipo juu.
Msususko huu wa kiuchumi umeshuhudia wasomi wa Harvard wakija na nadharia ya kuweka kiapo (oath) kwa wasomi wa MBA kuapa kukubali kulinda maadili ya biashara. Tunachojifunza hapa ni kwamba Ulimwengu wote sasa umetambua kuwa hangaiko hili la Uchumi limetokana na kukosekana kwa maadili miongoni mwa wafanyakazi wa taasisi za fedha. Hili likafanya wawe wasiri ingawa taasisi zao zilikuwa zinaanguka.Ndiyo hayo ya Ponzi Scheme!
Tanzania si kisiwa, nayo elimu ya MBA inashamiri kila kukicha vyuo vikuu vingi kwa sasa vinatoa elimu ya MBA.Huku,Mzumbe University mwaka jana ikiwa na wahitimu wanaokadiriwa kufikia 400 wakihitimu katika ‘Campus’ ya Elimu ya Biashara ya Dar-es-Salaam, pekee. Huu ni mwanzo mwema.
Lakini tunapaswa kujiuliza kama tunachokifanya darasani kuwaandaa viongozi wa biashara katika misingi ya kulinda ‘masilahi ya taifa’ au bado tunawafundisha wanafunzi ‘michakato’ ya biashara. Wanazuoni Leonidou na Kaleka wanaweka wazi kuwa elimu ya biashara kwa kiasi kikukwa imeweka msukumo katika, mbinu(strategy) mifumo na michakato badala ya ‘kufinyanga’ watu (1998)
Tanzania ya leo imekumbwa na rushwa katika sekta ya biashara huku ushindi wa rushwa kwa kupata ‘tenda’ ndiyo yamekuwa mambo ya kawaida.Sasa tunarudishiwa zaidi ya bilioni 30 za kitanzania kutokana na kashfa ya rada, Mheshimiwa Membe anaita chenji yetu!
Lakini hii ni changamoto kwa shule ya biashara, yatupasa kuandaa wasomi watakao ona kuwa kujihusisha na rushwa na kutojali masilahi ya watu wengi si jambo jema. Hapa ndipo suala la elimu ya maadili ya biashara linapoibuka.
Katika makala ya kisomi, ‘Challenges faced by business schools within newly founded catholic universities: the case of Tanzania, Mtawa (Sister) Dokta Helen A Bandiho, pia ni Mkuuwa wa Kitivo cha Biashara cha SAUT,Mwanza; anataja kuwa jukumu la shule za biashara ni kujenga jamii yenye viongozi wa biashara waliotayari kulinda masilahi ya taifa kwa kupigania masilahi ya wengi.
Akionya juu ya rushwa, ‘usiri’, matumizi mabaya ya mali ya umma,upendeleo katika zabuni havina mwisho mwema kwa shule za biashara.Hii ndiyo changamoto kubwa kwa shule za biashara kwa sasa katika Tanzania na ulimwengu kwa ujumla. Katika Tanzania ya leo huwezi kufanikiwa bila kuwa ‘network’ isiyorasmi katika biashara!
Network ya aina hii haina mwisho mwema kwani wasio na sifa ndiyo wanapata kazi na tenda, huku walio na sifa wakikata tamaa.Mara zote huwa ni majuto ambayo makala haya ikiyaorodhesha yatajaa kurasa. Mbaya zaidi wale waliotayari kuongeza bei ‘quote’ ndiyo wanaonekana kuwa wajanja, huku nchi ikiteketea. Hela zinazojenga vyumba vya madara kumi shule binafsi shule ya serikali ni vyumba viwili tu na haviishi! Hii ni hatari.
Tunahitaji kuhimarisha shule za biashara kwa kufundisha maadili ya biashara kwa kuwaandaa wanafunzi kupambana na rushwa, huku wakiwa tayari kuchukua madaraka ya kutoa maamuzi. Ingawa itaweza kutolewa hoja kuwa maadili ni suala la mtu binafsi na alivyofunzwa akiwa na familia yake.Hii ni sawa.
Lakini bado shule ya biashara ina nafasi kubwa katika kubadilisha kwa ‘kufinyanga’ wasomi wenye maadili na waliotayari kutetea masilahi ya taifa katika kila nafasi ya uongozi watakayokabidhiwa.
Kwa sasa katika Tanzania vyuo vingi vinavyotoa elimu ya biashara havina elimu ya maadili (business ethics) isipokuwa ni IFM tu waliokuwa na kozi hiyo tena kwa Shahada ya MB-International Business wanayoitoa kwa pamoja na Taasisi ya Biashara za Nje ya India.
Katika vyuo vingi kuna waliobuni Business Ethic and Law kama kozi, lakini lazima ifahamike kuwa ‘business ethics’ siyo sheria, ila ni elimu ya kumpa mwanafunzi uwezo wa kung’amua mema na mabaya, ingawa sheria inaweza ikawa inakupa nguvu.
Kwa mfano hakuna sheria itakayo kubana ukiwa unataka kufungua bar au kioski cha kitimoto karibu na msikiti. Lakini kimaadili hili si sawa. Ndivyo hivyo tunaona mifano mingi ambayo kama watoa maamuzi katika sekta ya biashara wangeweza kupata msasa kuhusu elimu ya maadili wasingaliweza kufikia maamuzi wanayoyapinga leo.
Msusuko wa Ulimwengu umefanya Harvard kufikiria kuweka kiapo kwa wasomi,wa biashara, basi yatupasa nasi kufikiria kufundisha maadili ya biashara, kwani mashaka yetu ya ubadhirifu wa mali ya umma, rushwa, upendeleo na mengine ya hovyo yanachangiwa na kukosa maadili.
MUNGU IBARIKI TANZANIA,
MUNGU IBARIKI AFRIKA.

Sunday, February 7, 2010

Tunachojifunza kutokana kupanda kwa bei ya mchele duniani

Mchele unaozalishwa kwa asilimia 90 katika bara la Asia, ni asilimia saba tu huingia katika biashara ya Ulimwengu. Ulimwengu bado unakumbuka hofu ya kitisho cha chakula ilivyopandisha bidhaa hii, huku ikifanya baadhi ya nchi kama Philippines kukosa shehena aliyoihitaji pamoja na dau kubwa la dola 680 kwa tani wauzaji na ‘waroho’ wa pesa walikataa kuiuzia tani 500,000 alizohitaji.
Tangu Januari 2008 biashara ya Ulimwengu ya chakula imekumbwa na msusuko wa kupanda kwa bei, huku mchele ambao ni chakula cha watu wengi walio masikini katika Asia ukipanda maradufu.Hali iliyofanya kuleta hofu zaidi miongoini mwa wa jamii ya kimataifa.
Kwa sasa bei ya mchele inaonekana kushuka kwa mujibu wa takwimu za FAO. Lakini Idara ya chakula ya Marekani inaonya kuwa hali bado ni ‘tete’ hasa kwa mchele na bei yake kutengemaa katika siku za karibuni.
Tanzania si muagizaji mkubwa wa mchele katika Afrika, lakini umuhimu wa zao la mchele kutoka Asia hakuna asiyeujua katika nchi hii. Mchele umekuwa siyo chakula kikuu hivyo kufanya mara zote iwe ni kimbilio letu wakati wa njaa.Mchele kutoka Thailand na Vietnam huwa ndiyo chakula mkombozi wetu wakati wa njaa.Kuna aina maarufu kama kitumbo na V.I.P ni aina ya Indica, wenye thamani ndogo katika soko la dunia.
Bei ya mchele ya ulimwengu inaonakana kuwa tata, kwa vile kuna madai kuwa India imeanza kupita kupita kwa nchi wazalishaji huku ikitangaza kuhitaji shehena ya mchele. Hii ni dalili ya wazi kuwa kitisho hiki cha India kuna jambo laja.
Ripoti ya FAO, Food Outlook, 2009, inabainisha wazi kuwa, India ipo sokoni ikiwa inavizia maeneo ya kununua mchele. Nia ikiwa kuongeza shehena yake ya mchele kwa tani milioni 9 zaidi. Ingawa haikuwa na uhakika juu ya madai ya kupipita kwa India katika kutafuta wauzaji wa mchele.Biashara ya Ulimwengu ya mchele inakadiriwa kupanda kwa tani 800,000 zaidi ya mwaka jana.
Wadadisi wa biashara ya mchele duniani wanabashiri wazi kuwa mahitaji ya ulaji ya mchele yanakadiriwa kupungua katika Asia.Lakini wanaonya kuwa kupungua kwa ulaji kwa jamii za Uchina, Thailand, India, Korea na Japan haimaanishi kuwa mchele utapungua bei kwa vile umekosa walaji.
Ila kitakachotokea ni kwamba uzalishaji wa mchele utapungua, kutokana na ukweli kuwa mashamba mengi yananyakuliwa kwa ajili ya ujenzi wa makazi kutokana na ukuaji wa miji mingi katika Asia.
Ukuaji wa miji unakadiriwa pia kuchochea ujenzi wa viwanda na barabara hali ambayo shirika la Utafiti wa mchele (IRI) lenye makazi yake Phillipines; linaelezea kuwa itapunguza ardhi kwa kilimo cha mpunga.
Pia kuna taarifa kuwa kuimarika kwa kipato cha familia kutapunguza walaji wa mchele, hali inayokadiriwa kuchangiwa mno na mafanikio ya uzazi wa mpango katika nchi nyingi za Asia ya Kusini na hasa Uchina.
Ukuaji huu wa chumo la familia unapelekea familia nyingi kubadili iana ya chakula, basi hili linajionesha wazi na kurufurika kwa maduka ya makubwa ‘supermarkets’ kutoka magharibi katika nchi hizi. Maduka kama Tesco, Asda, Mark Spencer Spencer na WalMart, wauzaji wa ‘fast food’ McDonalds, Kentucky Fried Chicken, StarBuck na kadhalika. Jamii ya Asia ya leo si walaji mchele tena, bali hupenda kula zaidi vyakula vya 'magharibi’
Mabadiliko ya chakula yanapeleka mbinyo tena katika ardhi iliyokuwa inatumika kulima mchele, sasa hutumika kulima mboga mboga , matunda, kukidhi mahitaji na mabadiliko ya jamii za Asia.
Mwenendo huu wa matumizi ya mchele katika Asia yanatufanya tujiulize juu ya siku za baadaye kwa Afrika ambayo hutumia Asia kama kapu lake la chakula wakati wa njaa?
Katika Afrika waagizaji wakubwa wa mchele ni Nigeria ambayo huagiza asilimia 6 na Senegal asilimia 4 ya mchele unaoingia katika soko la Ulimwengu, huku maeneo mengi yakiwa si walaji wakubwa wa mchele hadi ukame au kitisho cha njaa ndipo hukimbilia katika masoko ya Asia.
Tanzania ni miongoni mwa nchi ambazo si walaji wakubwa wa mchele, chakula kikuu ni mahindi. Pamoja na hayo lakini lililowazi ni kwamba mchele kutoka Asia ni mkombozi wa njaa katika Tanzania.
Indica, ni aina ya mchele ambao ni wenye kiwango cha chini cha ubora ukiwa umevunjika kwa asimilia 25, mara nyingi ulikuwa umeonekana kukosa soko lakini hali ya mambo hadi mwanzoni mwa Januari mwaka huu, ilionesha kuwa mchele huu utapata wateja, hii ni baada ya Philippines kuinngia sokoni akiwa ananunua aina hii ya mchele.
Lakini lililowazi ni kwamba hali ya bei ya biashara ya mchele inatarajiwa kupanda Ulimwenguni. Asia ikiwa mlimaji mkubwa wa mpunga, ndiyo pia kuna walaji wakubwa, lakini nchi nyingi za eneo hilo zimeweka vikwazo kwa biashara ya mchele kwa kuweka kodi ya mauzo ya nje na hata kuzuia kwa hofu ya kutokea upungufu wa chakula na kuathiri raia wengi walio maskini.
Tunachoweza kujifunza kwa mwenendo wa biashara ya mchele, Afrika inahitaji kuongeza nguvu katika kilimo cha chakula. Tangu azimio la Maputo kupitishwa kwa nchi za Afrika kuweka bajeti ya asilimia kumi katika kilimo ni nchi chache zimeweza kufikia lengo hili.
Hali ya mambo katika Asia, ambako mchele unalimwa inaonekana kubadilika mno, hasa kutokana na ukweli kuwa ‘style’ ya ulaji imebadilika na kufanya jamii nyingi za huko kupenda kula vyakula vya magharibi,hiki ni kitisho kwa Afrika.
Ingawa mabadiliko haya kasi yake kitakwimu hazipo wazi, lakini ongezo la maduka makubwa ya magharibi na kuongezeka uzito kunakosabishwa na ulaji wa ‘junk food’ ni dalili kuwa sasa Asia inaondoka katika kula mchele kama chakula kikuu.
Afrika haina budi kujipanga, katika kuhakikisha inalisha jamii ya watu wake, kwani kwa sasa hali ya uhakika wa chakula na biashara ya chakula duniani imebadilika mno.
Tuchague moja, kulima mau na viepepeo au kulima mazao ya chakula. Jibu tunalo waafrika wenyewe. Profesa Steve Carter na Dr Kiefer Lee, wanaonya juu ya hatari ya kufikiria zaidi soko la nje na kujitahidi kukidhi mahitaji ya soko hilo, katika kitabu Global Marketing Management wanaandika ‘biashara hii itakuwa haina maana kama chumo lake na zaidi litakwenda tena katika kuagiza kitu ambacho nchi inahitaji zaidi’
Ni wazi kuwa Afrika inahitaji zaidi chakula kuliko chumo hilo la vipepeo au maua, ambayo hata soko la ndani hakuna anayevitumia. Kenya sasa inahaha kuhamasisha matumizi ya maua kwa soko la ndani; kwani asilimia 96, hutegemea soko la nje. Ni wazi kuwa ‘ndoto’ hizi haziwezi kutimia, kwani maua si hitaji la wakenya.
Vinyo hivyo kwa nchi nyingine za Afrika ya joto tumejikuta tunaingia katika mtego kama huu, wa kuhangaika kufikia matarajio ya soko la Ulaya wakati, faida ya huko kimsingi baada ya muda inarudi tena na ziada inahitajika katika kununua chakula.
Hatumaanishi kuwa hii biashara ni mbaya, lakini yatupasa kulinganisha na kutambua mahitaji yetu je yametimizwa? Basi tuweke nguvu katika kilimo cha mazao ya chakula na tuache ‘ushabiki’, kwani hakuna mgeni atakaye kuja Afrika kuja kulima mpunga.

Monday, January 18, 2010

Ni muda muafaka kuongeza umri wa kustaafu

Majuma machache yaliyopita vyombo vya habari vya Tanzania. vilipambwa na sakata la serikali kumnyima ajira ya mkataba, mwanazuoni nguli wa siasa za kimataifa Profesa Mwesiga Baregu wa Chuo Kikuu cha Dar-Es-Salaam (UDSM).
Waziri mwenye dhamana, Mheshimiwa Hawa Abdulreihman Ghasia, aliweka wazi kuwa serikali kwa sasa haina nia ya kumpa mkataba mpya Profesa Baregu, baada ya kumpatia mara tatu tangu alipostaafu mwaka 1999, akiwa na miaka 55.
Tangu suala la kunyimwa mkataba kwa nguli huyu lilipoibuliwa katika vyombo vya habari, kuna makundi mawili makubwa yameibuka katika kuangalia, uhalali wa kama Profesa ameonewa au serikali ipo sahihi kusitisha kumpa mkataba.
Kuna waliojikita katika itikadi za kisiasa, ingawa waziri pia amegusia hilo kuwa ndiyo kiini cha kusitisha mkataba mpya kwa gwiji huyu. Lakini kuna madai kuwa wapo wana CCM mbona wamepata, wakienda mbali zaidi wakihusisha ukosoaji wake kwa serikali kuwa ndiyo kigingi cha yeye kutemwa UDSM.
Kichuguu cha pili kilikuwa na wale wanaoona kuwa maamuzi haya ni sahihi ingawa hawa hawakupata nafasi ya kuhojiwa sana na vyombo vya habari, huku wakiweka wazi kuwa sasa huu ni wakati wa damu changa kuchukua nafasi katika taasisi mbalimbali za serikali.

Makala haya haina nia ya kusema kati ya hivyo vichuguu viwili na hoja zao kipi kipo sahihi au yupi amekosea, la hasha ila itajaribu kupitia umuhimmu wa kuangalia nini tunajifunza kama 'nchi' kuhusu sakata hili, la Profesa Baregu.Serikali imekwisha hitimisha.

Somo tunalotaka kulijadili katika makala haya ni kuhusu umri wa kustaafu katika Tanzania.Na hasa kwa wanazuoni au wataalamu wengine ambao serikali hutumia gharama kubwa kuwasomesha.

Naweka wazi msimamo wangu kuwa umri wa kustaafu unapaswa kuongezwa na hasa katika kada za walimu wa vyuo vikuu. Kwa sasa kuna wanaostaafu katika 55 na wengine 60 kwa manufaa ya umma.

Ulimwengu wa leo watu wengi wananafasi kubwa yakuishi maisha marefu hii ni kutokana na mafanikio ya kisayansi ambayo yameweza kuboresha viwango vya ubora wa maisha kwa wale wanaozingatia na kufuatilia kwa ukaribu. Magonjwa ambayo yalikuwa tishio si tena tishio kwa binadamu.

Pia mafanikio ya kisayansi yanampa nafasi binadamu kuweza kufanya kazi kwa muda mrefu, wakati zamani miaka 55, ni umri uliokuwa kweli umechoka kweli kweli. Mfano Mzuri ni huyo Profesa, tangu astaafu amepewa mikataba mitatu na bado yu mwenye siha nzuri na anaonekana anaweza kumudu mikiki mikiki ya kazi yake.

Katika Tanzania, kustaafu katika miaka chini ya 65 ni pigo kwa nchi na hasa wahadhiri ambao wengi leo hii tulionao wako mbioni kustaafu, vyuo vingi vinakabiliwa na hatari ya kukosa hawa magwiji katika miaka mitano ijayo.

Inakadiriwa katika miaka mitano ijayo wengi ya wanataaluma waliobobea katika shahada za uzamivu watakuwa wamestaafu wakiwa na umri wa miaka 60. Kimsingi hii ni hasara kwa nchi.

Hasara kwa sababu, wengi ya wanazuoni tulionao wamapata PhD wakiwa na zaidi ya miaka 45 hadi 50. Sasa ukiangalia gharama za kumsomesha mwanafunzi wa PhD alafu anatumika chini ya miaka 10 anastaafu ni nchi ndiyo inapata hasara.

Hili suala la kuomba kuongeza muda wa kustaafu walau ufikie miaka 65 si jambo geni, na wala siyo hoja mpya katika Tanzania.Kati ya watu wanaopigia chapuo kuongezwa kwa umri wa kustaafu ni Balozi Juma Mwapachu, Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Sisi tumechelewa kusoma, na mifumo yetu mara nyingi inatubana kupata wanazuoni walio na umri chini ya miaka 30 wakiwa na PhD. labda katika miaka 10 ijayo tutakuwa na watanzania walio na PhD wakiwa chini ya 30 hii baada ya serikali ya awamu ya tatu kuhimiza kupeleka watoto shule mapema.

Na ujio wa shule binafsi umefungua mwanya kwa vijana wa kitanzania kwenda shule wakiwa na wastani wa miaka 4 hadi 6 kuanza darasa la kwanza huku wakirushwa baadhi ya madarasa, hasa la saba na wangine wakitumia elimu ya nje kama Kenya na Uganda kusonga mbele katika vyuo vikuu vya huko.

Ila kwa wale tuliosoma Tanzania ni wazi kuwa kupata PhD si chini ya miaka 45, na kupata Uprofesa kama ngazi ya juu ya kielimu katika kufundisha inaweza kuchukua zaidi ya miaka 10 kwa Tanzania.Ukijumlisha na uchelevu wa kwenda shule huko nyuma wengi wanakuwa maprofesa bado miaka michache kustaafu. Hawa ndiyo magwiji walioiva.

Sasa kwa nini wameiva sasa, ndiyo tunawapa taarifa ya kusataafu!Hapa pana ulakini.Katika nchi za magharibi kustaafu ni miaka 65, na wengi huku wamepata PhD wakiwa chini ya miaka 25. Hivyo anaitumikia nchi yake kwa zaidi ya 30.

Ni wazi kuwa atarudisha fedha ya walipa kodi kwa kazi atakayoifanyia nchi yake.
Hasara yake ni kwamba wakati tumetumia pesa nyingi kuwasomesha katika vyuo vya nchi za magharibi kwa gharama zisizopungua milioni 100 kwa mtu mmoja kwa PhD tunamtumia chini ya miaka 10,kwa vile tu sheria inasema astaafu chini ya miaka 65!

Pesa nyingine zinakuja kama mikopo, hivyo hata mkopo haujalipwa na mtu hajaitumikia jamii yake anaambimwa astaafu kwa manufaa ya umma.

Ni sheria inapaswa kufuatwa. Lakini sheria hii kwa mmtazamo wangu nahisi ina matatizo na hasa kwa nchi yetu hii changa. Mbona Uingereza wanastaafu wakiwa na miaka 65.

Lengo kuu la sheria au taratibu za jamii yoyote ni kuwatumia jamii husika, sasa sheria hii inaonekana haina manufaa kwetu yatupasa kuijadili na kutafuta suluhu ya kudumu.

Rai yetu ni kwamba huu ni wakati muafaka wa kufikiria kuongeza kwa umri wa kustaafu iwe kwa hiyari au kwa manufaa ya umma umri uwe miaka 65.

Sunday, January 10, 2010

Bila walaji 'makini' ushiriki wetu u-mashakani

Gwiji wa Uchumi Profesa Michael Porter wa Chuo Kikuu cha Harvard katika nadharia yake maarufu kama 'Porter's Diamond Model' au 'faida ya ushindani'(Competitive Advantage) anabainisha wazi kuwa nchi ili ifanye vyema katika biashara ya kimataifa inahitaji kuwa na 'walaji makini'(Sophisticated Customers). Walaji wanaojua kuwa hii bidhaa haina ubora, na wapi waende ili wapate haki zao mara wanapokosa huduma bora toka kwa kampuni husika kwa 'uwongo' wa makusudi wa kibiashara.
Porter’s Diamond model inataja viashiria vikuu vinne vinavyo weza kufanya nchi iweze kushamiri katika biashara ya kimataifa, rasilimali (endowment factor),mahitaji ( demand condition), uhusiano wa kiviwanda (relating and supportive industries) na mbinu za kibiashara (firms strategy).
Makala haya itajadili umuhimu wa walaji makini kwa ustawi wa sekta ya kibiashara katika Tanzania na hasa viwanda. Tanzania inahaha kupanua wigo wake wa biashara ya nje, lakini wakati wote imekuwa haifanyi vyema.Kumekuwa na kauli mbiu za kila aina na taasisi kama CTI imekuja pia na kauli mbiu ya ‘kuwa mzalendo tumia bidhaa za nyumbani’
Kimsingi hakuna nchi iliyokuwa na kuimarika katika uchumi wake bila uchumi wa nchi husika kuimarika kwanza katika soko la ndani. Soko la ndani ni muhimu na mara zote limekuwa halina hadhari kubwa kama vile soko la kimataifa.
Tafiti fulani inabainisha kuwa kampuni nyingi zilizokwenda katika soko la kimataifa asilimia 50 zilianguka, kwa sababu mbalimbali. Pamoja na ukweli huo soko la kimataifa bado limebakia kuwa ni suluhu moja wapo ya kuimarika kwa uchumi si kwa nchi changa kama Tanzania tu bali hata nchi tajiri nazo zinahaha kuweza kujiimarisha katika masoko ya kimataifa mapya (Emerging markets) ya Asia na Afrika.
Sekta ya viwanda kwa sasa Tanzania ipo nyuma pamoja na mambo mengi inayoielemea sekta hii likiwemo uchakavu wa mitambo, miundo mbinu, ukosefu wa nishati(umeme wa mgao) lakini pia hili la kukosa walaji makini linasababisha kilio kwa viwanda vyetu.
Kwa mujibu wa Profesa Porter, soko la ndani linanafasi kubwa kwa kuchochea uhitaji wa bidhaa zenye ubora wa hali ya juu na hivyo kuipa changamoto kampuni katika kuinua na kuboresha bidhaa zake.
Ripoti ya Benki ya Tanazania(BoT) ya mwaka 2006/2007 inataja kuwa sekta ya viwanda imekuwa huku ikichangia pato la taifa kwa asilimia 9.2, ikiwa kuna mauzo ya nje kwa bidhaa za viwandani zenye thamani ya dola za kimarekani 226.8, huu ni mchupo wa dola milioni 34.6.
Mauzo yameimarika katika masoko ya Rwanda, Burundi na Kongo-Kinshasa kwa bidhaa za nguo kama vitenge na kangha, glasi, plasiti kukiwa na mafaniko toka kwa kiwanda cha Simba Plastiki inayouza katika nchi za SADC na pia viwanda vya chuma vinavyouza nondo.Uuzaji wa pombe kali kama konyagi na bia.
Ripoti hii haitaji kuhusu viwanda vya bidhaa za walaji kama sabuni na dawa za meno, lakini kuna taarifa za sabuni ya Foma Gold kufanya vizuri katika masoko ya Malawi na Zambia.
Pamoja na mafanikio haya tuliyojaribu kuyaorodhesha hapo juu, bado Tanzania inakaribiwa na mchango mdogo kutoka katika sekta ya viwanda vyake katika pato la taifa.
Mara zote kilio kimekekuwa kutoka miongoni mwa walaji na wazalishaji kuwa bidhaa za watanzania hazinunuliki sokoni.
Unaweza kujiuliza pamoja na kilio cha ubora mdogo wa bidhaa toka Uchina? Mbona bado tunagombania bidhaa hizo?Hii ni wazi kuwa walaji wa soko la Tanzania, siyo makini.
Ni walaji wanaoweza kununua kiatu cha plastiki kwa bei ya elfu 15000 toka Uchina na kuacha kiatu cha ngozi cha pale Moshi-Kilimanjaro.
Ni wazi kuwa mzalishaji wa kiatu naye atapunguza umakini hali ambayo itafanya kudorora kwa ubora wa bidhaa zake ili aweze kupambana na bidhaa feki za Uchina. Lakini kwa kufanya hivi ni wazi kuwa mbio hizi zinapunguza uwezo wetu katika kuyafikia masoko ya nje.
Ni walaji ambao hatuangalii ubora, ila tunajali uwingi na faida ya mlinganisho wa kifedha ya muda mfupi.
Mlaji makini anafahamu ubora wa bidhaa anayotaka kutumia kwa thamani ya fedha zake.Uhitaji wa bidhaa zenye ubora wa juu katika soko la ndani unavifanya viwanda husika kufikiri namna ya kuongeza jitihada katika tafiti zao(research and development)
Walaji wa Tanzania tunapokea kila kitu hatuko makini, hili linafanya viwanda vyetu vya ndani kubweteka na kusahau kuwa kuna siku za ushindani na hivyo ujio wa bidhaa toka nje zikipiga hodi.
Juhudi za kamisheni ya usawa wa biashara (FCC) za kuponda bidhaa mbovu zinazoingizwa nchini ni zenye kuungwa mkono kwani hizi bidhaa feki zinalemaza si tu walaji na wazalishaji pia.
Kabla ya Tanzania kuingia katika mfumo wa soko huria nadharia iliyokuwa imejengeka ni kuwa kwa vile ni serikali ndiyo mmiliki mkuu wa viwanda hivi hakuna namna ya kudhibiti, wala mteja hakuwa na nguvu ya kupinga bidhaa mbovu ikiwa imezalisha katika kiwanda cha umma.

Lakini imani yetu dhidi ya soko huria kuweza kutuletea bidhaa zenye ubora, imedimimizwa na ujio wa bidhaa feki.
Ni wazi kuwa sasa hivi tatizo ni walaji wasiolindwa wala kupata elimu juu ya umuhimu wa kiuchumi na kiusalama na afya wa kutumia bidhaa zenye ubora.
Ni ngumu kupata wateja walio makini kwa kutegemea nguvu za kiuchumi(soko) tu, yatupasa kuunda chama cha walaji. Chama cha walaji kitadai haki za walaji toka kwa watoa huduma hadi wazalishaji wa bidhaa.
Kwa kudai bidhaa zenye ubora ni wazi pia wazalishaji wa ndani wataamka na kuzalisha bidhaa zenye ubora kwa soko la nje pia.

Ni China au ni Afrika ambayo haiwezi kusema 'hapana'?

Katika siku za karibuni ongezeko la bidhaa 'feki' limekuwa ni tatizo kwa nchi nyingi zinazoendelea na Tanzania ikiwemo. Wakati wote huu Uchina imekuwa ikibeba lawama kuwa ndiyo mhusika na ni muendelezaji wa uuzaji wa bidhaa feki, kwa Afrika.
Niliwahi kuhudhruia sherehe moja ya harusi, nikashuhudia mama mmoja akipatwa na kadhia ya kuvunjika kwa kisigino cha kiatu chake cha ‘mchuchumio’ (High heels). Nilipomdadisi aliniambia kuwa ndiyo kwanza anakivaa(ulikuwa palo wa sare ya sherehe). Lakini alijifariji kuwa, amenunua 15000 tu, kariakoo.
Hasara ni hasara, je wale wanaounguliwa nyumba kwa kutumia nyaya au vifaa vyenye viwango vidogo!Ingawa ni ngumu kupata takwimu sahihi, lakini lililowazi ni kwamba miongoni mwetu tupo tunaopata hasara kwa kutumia bidhaa zenye viwango duni kutoka Uchina.
Tanzania bidhaa zenye ubora mdogo zinatusumbua. Makala haya itajaribu kutupia jicho hali ya kibiashara kati ya Uchina na Afrika.Lakini iweje katika maduka ya nchi za magharibi bidhaa za kichina zimejaa, lakini hawalalamiki kuwa kuna 'ufeki' kwa kiwango kama cha Tanzania?
Biashara kati ya Afrika na Uchina imeimarika kuanzia miaka ya 1990, huku Uchina ikiwa inaongoza kwa kufanya biashara na Afrika kwa miongoni mwa nchi za Asia, ikiwa na asilimia 39 ya biashara yake na Afrika.
Kutoshiri katika siasa za ndani za nchi za Afrika kunaifanya Uchina iwe kimbilio la bara hili.Hii ni sera ya mambo ya nje ya Uchina. Hivyo dikteta ana nafasi sawa na mlinda haki za binadamu mbele ya Uchina, ili mradi tu wao wanapata wanachohitaji na masilahi yao yanalindwa.
Biashara kati ya Afrika na Uchina imejikita zaidi katika , ujenzi wa miundo na usakaji wa malighafi hiki ikinunua mafuta kutoka Angola na Nigeria na Sudan. Ujio wa Uchina katika Afrika unahusishwa zaidi na kiu yake ya kusaka mafuta na maliasili zingine, huku ikiwa mtumiaji wa pili wa nishati ya mafuta baada ya Marekani ni wazi kuwa ni mshiriki mkubwa wa Afrika inayokidariwa kuwa na hifahdi ya asilimi 9 ya hifadhi ya mafuta ya Ulimweungu, lakini lenye kuvutia zaidi ni kuwa bara hili bado linaendelea kuvumbua vyanzo vingi vya mafuta katika maeneo mengi ya bara hili.
Jitihada za ushiriki wa Uchina unaimarishwa zaidi na jitihada zake za kufuta madeni ya bilioni 10 za kimarekani kwa nchi za Afrika. Ni wazi kuwa China ni mshiriki mzuri na mwenye kuangaliwa vyema katika kila analolifanya kwa maendeleo ya bara hili.
Kwa mujibu wa vyombo mbalimbali vya habari vya Uchina, Tanzania ni nchi inayoongoza katika Afrika kwa kupata misaada kutoka Uchina. Ni China ndiyo inayotoa mabilioni ya misaada katika kupiga’ jeki’ bajeti yetu na vyombo vya habari vimeripoti ‘mvua’ ya mabilioni ya mikopo kwa Tanzania katika siku za karibuni.
Misaada ipo kaitka kila kona, elimu, afya, jeshi, miundo mbinu nakadhalika. Ushiriki wa Uchina katika maendeleo ya Tanzania ni wa muda mrefu tangu (enzi zaMwalimu) awamu ya kwanza.
Urari wa kibiashara kati ya nchi hizi mbili upo chanya kwa China, huku ikiuza bidhaa zenye thamani ya dola milioni 128 na Tanzania ikiuza bidhaa zenye thamani ya dola milioni 6.62 kwa ripoti za mwaka 2002.
Kwa sasa biashara miongoni mwa nchi hizi mbili imeingiwa na mdudu ‘bidhaa feki’ huku Uchina ikipewa lawama, kwa kila bidhaa inayokamatwa na kila lalamiko katika Tanzania.
Wadadisi wa biashara za Uchina, wanabainisha kuwa ni ngumu kwa Uchina kudhibiti uzalishaji wa bidhaa hizi kwani baadhi ya majemedari wa jeshi wanamiliki au wanahisa katika baadhi ya viwanda.
Lakini, Uchina si muuzaji wa Afrika tu, akiwa na urari wa biashara wa zaidi ya dola 102 bilioni , ni muuzaji mkubwa katika masoko ya Ulaya na Marekani pia.Ni wazi kuwa kieneo si ni sehemu ndogo sana ya chumo lake biashara ya nje.
Tunachojiuliza ni kwa vipi bidhaa za kichina ziwepo kwa wingi na kutumiwa katika nchi kama Uingereza. Ufeki huku haupo kwa kiwango cha Tanzania?
Kamisheni ya Ushindani (FCC) inataja kuwa kiwi za milioni 20 na ‘tubelight’ za aina ya Phillips na Britimax zenye thamani ya dola 18000 zimeteketezwa mwaka 2007, kwa mujibu wa gazeti la Daily News la 1 May 2009.
Pia inakadiriwa kwa mwezi machi pekee 2008, bidhaa zenye thamani dola za kimarekani 224,000, ziliteketezwa na FCC. Ni wazi kuwa FCC kwa uchanga wake inafanya kazi kadiri inavyoweza ili kudhibiti bidhaa ‘feki’.
Vita hii inaonekana kwa sasa inasumbuliwa na ‘balkanization’ kila wizara na idara ya serikali ikipigana kutoka kivyake vyake. Kimsingi vita ya bidhaa feki ni ya jamii nzima, na bila chama cha walaji imara kinachoundwa na walaji wenyewe wafanya biashara wetu watandelea kujaza nchi yetu na bidhaa feki.
Vyombo vyenye mamalaka vimekuwa vingi hadi tuchanganyikiwa tuna TFDA, TBS, FCC.Walaji hatujui tukipata bidhaa ‘feki’ tuanzie wapi? Je tunaitambuaje bidhaa feki?Kuna muongozo wa viwango vya bidhaa, kuwa ubora wa bati unapaswa kuwa ni mchangayiko wa malighafi hizi kwa viwango anuai?Mlaji anayefahamu haya yote?Ni ngumu kwa baadhi ya mbinu kwa mlaji kuweza kutambua.
Ni wazi kuwa vita hii inahitaji kuongezewa nguvu na sheria inayowapa walaji nafasi ya kuwa na chama imara chenye kuwalinda tena chenye nguvu ya kulinda masilahi ya walaji.Katika nchi nyingi vyama hivi vipo na vimekuwa mwiba na vimefanikiwa kulinda nchi zao kuwa majalala ya bidhaa ‘bomu’ si toka nje tu hata wazalishaji wa ndani.
Vyama vya walaji(consumer Associations) vimekuwa vikiheshimiwa kuliko hata taasisi za serikali, kwa vile mara nyingi zimekuwa zikitoa taarifa bila kulinda masilahi ya kisiasa. Mfano mzuri ni imani ya waingereza juu ya FSA(Food Standard Agency) ni ndogo kwa vile ‘walibinya’ ukweli kuhusu homa ya kichaa cha ng’ombe (Bovine spongiform encephalopathy) kwa nia ya kulinda uchumi kwa gharama za walaji!
Ukiangalia mfano huu ni mingine sehemu zingine Duniani, utapata picha kwamba chama cha walaji kinahitajika zaidi kwa sasa Tanzania ili kulinda wateja katika siku za mfumo huu wa soko huria.Kwa sasa kuna chama cha kutetea wasafiria, hii ni hatua nzuri. Lakini yatupasa kukiimarisha chama hiki ili kiendelee kulinda manufaa ya walaji katika sekta ya usafairi.
Hii ni hatua moja tu kama nilivyosema, Tanzania ni kubwa na ushawishi wa wafanya biashara wetu katika kuleta na kufanikiwa kuingiza bidhaa feki unongeeka kila siku. Kwa mfano ukimwambia mteja kuwa ataweza kutambua bidhaa feki kwa tofauti ya jina(brand) hii inakosa nguvu sana kwani kwa sasa biashara ya Ulimwengu imejawa na wazuaji wa nembo zao(Own brand).
Hivyo tajiri anaweza kuagiza tani za vitasa toka Uchina akavipa jina la hardware yake. Ila hoja yetu ya ‘ufeki’ ipo katika malighafi zilizotumika kama zinakubarika katika soko la Tanzania.
Kwa kuangalia uwingi wa bidhaa za uchina katika nchi za magharibi na jinsi zinavyojipenyeza huko na kupapatikiwa na walaji kwa ‘upenyo’ wa bei ni wazi kuwa hatuna njia zaidi nasi pia kutumia bidhaa kutoka Uchina.
Ila kama nilivyokwisha kusema, hapa ni wauzaji wetu ndiyo walio kuwa na kasoro, ama hawana ufahamu na viwango vya nchi kwa bidhaa mbalimbali pale wanapoagiza. Suala la viwango vya ubora ni suala ‘tete’ na ni wazi kuwa viwango vya Tanzania, si sawa na Uingereza, ingawa kuna viwango vya bidhaa vya Ulimwengu, pia kuna nchi wanatumia viwango vyao bila hata kujali hivyo vya ulimwengu.
Hatuwatetei wajasiriamali ila yatupasa kupeleka elimu ya viwango kwa waaagizaji wa bidhaa toka nje, si kwa walaji tu. Inawezekana pia kati ya waagizaji ni wachahe wenye ufahamu juu ya viwango au kuona ‘muongozo’ wa viwango wa TBS, katika saketi inayotakiwa Tanzania iwe na ubora gani, kwa malighafi na uzito upi.
Pendekezo letu katika vita hii, mosi ni kuundwa kwa chama imara cha haki za walaji na pili kutungwa kwa sheria zenye kumpa mlaji haki za kiuchumi pale itakapogundulika kuwa bidhaa aliyotumia haikuwa na viwango husika,maana kwa sasa vinachomwa moto tu, vipi waliotumia wanapata malipo yoyote?Jibu ni kuwa hatupati
Pia tunapendekeza kutolewa kwa elimu ya viwango kwa waagizaji wa bidhaa toka nje ya nchi wafahamu kabla hatujawahukumu.
Ingawa Uchina ni mdau mkuu kwa maendeleo ya Tanzania kama nilivyokwisha kuonesha, yatupasa kuungana kama nchi kusema ‘HAPANA’ kwa bidhaa feki toka Uchina kwa masilahi ya nchi yetu. Tukiungana tunaweza.

Monday, January 4, 2010

Sekta changa ya 'mboga mboga' na kitanzi cha VAT

Hivi karibuni Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) imenukuliwa na Gazeti la Serikali Daily News la tarehe 26 Desemba 2009 kuwa limepitisha ‘tozo’ mpya ya kodi ya ongezeko la thamani ,VAT, kwa wauzaji wa masoko ya nje hata kama muuzaji ana pato lililochini ya milioni 40.
Mabadiliko haya yanatekelezwa kwa utetezi wa masilahi ya kulinda nchi hii ni kwa mujibu wa TRA. Safari hii VAT itatozwa hata kwa wale wajasiriamali wadogo, lakini tatizo si VAT, ila ni marejesho kuwa ‘yanabagua’. Kimsingi mlipaji wa VAT ni mlaji, kwani muuzaji hurejeshewa malipo yake, lakini hawa wadogo waliochini ya milioni 40 hawana cha ‘kurejeshewa’.
Tatizo hili la kukosa kuwarudishia ‘wajasiliamali’ ndiyo kiini cha makala haya. Tutajaribu kuangalia manufaa ya dhana hii kwa Taifa na pia tutatoa mchango wetu kuhusu hili.Ingawa tunaaamini hiki inawezekana ikawa ni kilio cha samaki machozi huenda na maji anaimba gwiji wa muziki wa dansi, Dr. Ramadhani Mtoro Ongala.Lakini tunaamini sauti yetu itasikika.
Kati ya sekta zilizoathirika na marekebisho haya ya kisheria ya VAT, ambayo kimsingi kamishina wa kodi ananguvu kisheria kuamaua nani alipe VAT ingawa sheria yenyewe ya inasema ni yule mwenye zaidi ya milioni 40.Sheria ya VAT kifungu sura ya 148 kifungu 19 kifungu kidogo 4, kinampa uwezo Kamishina wa Kodi kuamua nani alipe ingawa utakuwa upo chini ya milioni 40.
Ni vyema ikaeleweka wazi kuwa hatuna nia ya kujenga wala kutetea jamii ya watu wasio penda kulipa kodi, ila tunashaka na maamuzi haya kama kweli ya nia kuona nchi hii inang’ona ‘nanga’ kiuchumi.
Jitihada za kupambana na anguko la uchumi duniani imeona serikali nyingi zinahamasisha kuuza katika masoko ya nje, na zinatoa motisha ya punguzo la kodi kama si kufuta kabisa. Itakumbukwa pia katika siku za mwanzo za msukosuko huu kauli iliyokuwa inapigiwa chapuo na Marekani ni kuhakikisha nchi hazifungi mipaka yake ya kibiashara kwa kutumia njia kale (traditional barriers kama vile kodi za aina yoyote)
Ni kweli kuwa Tanzania inahaha ikitafuta kujinasua kutokana na msukosuko wa kiuchumi wa dunia kwa kutafuta kuongeza pato lake. Lakini kwa njia hii ya kutoza wauzaji wa nje na hasa wauzaji wa sekta changa ya mboga mboga ambayo imejawa na wazalisahjo wadogo wengi hauna mwisho mwema.
Sekta hii changa ya mboga mboga (horticulture) lakini katika makala haya tutajumlisha pia na floriculture, pale tutakoposema mboga mboga inakadiriwa tani kati ya 15 hadi 40 husafirishwa kwa wiki, kuelekea masoko ya ng’ambo kwa kutumia usafiri wa anga.
Hii ni bidhaa inayohitaji kufika sokoni haraka kutokana na tishio la kuharibika haraka (fast moving consumer goods). Kupitia chama chawazalishaji wa mboga mboga (TAHA) Tanzania ilijinyakulia tuzo ya shaba katika maonesho ya Amsterdam kwa mara ya kwanza wakati tukiwa washiriki kwa mara ya kwanza mwaka 2007.
Ikiwa inaleta chumo la dola milioni 50 kwa mwaka, na kuajiri watu wanaokadiriwa kufikia 10000, huku zaidi ya kampuni 20 zikiaminika kushiriki katika sekta hii. Ni wazi kuwa inahitaji kuangaliwa vizuri. Tanzania inakila sababu ya kuilinda sekta hii inayochipua kwa kuipa motisha lakini yanayotokea nchini ni kinyume chake.
Uzalishaji mkubwa wa mboga mboga upo Arusha, Kilimanjaro, lakini mikoa mingine kama Morogoro, Mbeya, Rukwa ,Tanga na Iringa nayo inafanya vyema na inakila hali ya kijiografia kuiwezesha kufanya vyema.
Mwenendo wa soko la ulimwengu wa mbogamboga katika nchi za Ulaya ni wenye kutia matumaini kwa siku za baadaye wa sekta hii nchini. Hii inatokana na ukweli kwamba katika Ulaya kuna mwamko wa kiafya kupinga ulaji wa nyama nyekundu kuanzia miaka ya kati ya sabini hali iliyopelekea kukubalika kwa nyama nyeupe kama kuku na nguruwe miongoni mwa watu wazee.
Uoga wa ulaji nyama ulishamiri zaidi baada ya kuibuka kwa ugonjwa kichaa za ng’ombe, BSE( Bovine spongiform encephalopathy) katika Uingereza miaka ya 1996.
Mwenendo wa soko umeimarika baada pia kuongezeka kwa hali ya kulinda wanyama, na ongezeko la walaji majani katika nchi hizi kwa imani za kisayansi. Kwa mfano tangu ongezeko la vitisho hivi soko la walaji wa nyama wa Uingereza umepungua ukiwa ni kilo 14.4 tu kwa mwaka.
Ni wazi kuwa Tanzania inazewa kunufaika na hakuna shaka kuwa sekta hii changa inahitaji kupigiwa ‘chapuo’ kuhakikisha kuwa tunakataa kuwa wauzaji wa wanunuzi wasio makini kama vile Kenya ambao hununua vitunguu na matunda toka kwetu kisha kuuza Ulaya kwa faida kubwa.
Hili la tozo ya VAT ya asilimia 18, ambapo hawa wadogo hawarejeshewi imevunja nguvu za wajasiriamali wanaohaha usiku na mchana kuona wanaunganishwa na soko la nje, na ni wazi kuwa si njia sahihi. Kwani Tanzania sasa hivi haihitaji kutoza kodi kubwa na hasa wauzaji wa nje ili kuongeza pato inahitaji kuhahakikisha wajasiriamali hawa wanauza katika soko la nje na wanapata suluhu katika mashaka yao.
Iweje wakubwa walio na pato kubwa la milioni zaidi ya 40 warudishiwe lakini wadogo wasirudishiwe? Hii si sawa. VAT analipa mlaji lakini safari hii wamekandamizwa wazalishaji tena wa sekta changa, kwa kigingi cha kulinda masilahi ya Taifa.Taifa gani linalolindwa wakati utekezaji wa sheria hii ni wazi kuwagawa watanzania, na hasa hawa wakulima wadogo wa mboga mboga!
Tanzania inavyanzo vingi vya kodi na tangu tumeamua kuchauga mabadiliko ya kiuchumi miaka ya 1980 ya soko huria, nia ilikuwa kuona utawala wa kodi unakuwa huru na wa haki.
Lakini safari hii tunaona kodi inakuwa kandamizi tena wakati wa hangaiko la Uchumi. Sekta hii ya mboga mboga nayo pia imepata msuko msuko, huku la soko la Uingereza likiwa limepungua kwa asilimia 20 kwa bidhaa toka Tanzania.Ni wazi kuwa sekta hii inahitaji kulindwa hasa ukizangatia kuwa ni wakulima wadogo ndiyo wanaoshiriki katika kuzalisha bidhaa hizi katika maeneo mengi nchini.
Kukosa pato kwa TRA kusihusishwe na kubinya walipa kodi waliojitoa na kukubali kulipa kodi kwa maendeleo ya Taifa. Na hili ndilo tatizo la Tanzania, mara zote nchi inakuwa iko mbele kuhakikisha inawakamua wale walipa kodi na si kuziba mianya ya uvujaji wa kodi.
Hivi karibuni gazeti la serikali Daily News la tarehe 20 Desmeba 2009, lilikuwa na taarifa kuwa wauzaji wa magogo na mbao nje ya nchi walikuwa wanataka kupunguzwa kwa kodi. Ombi ambalo serikali kupitia Waziri wa Viwanda na Biashara, Dr. Mary Nagu amekubali kulipokea na kuliona, huku Naibu wa Waziri wa Maliasili akilipigia ‘chapuo’ kuwa nchi inahitaji kupunguza tozo ya mbao na mazao mengine ya misitu ili kuongeza pato la taifa na hasa mauzo ya nje. Kwa sasa tozo ni 200,000/= kwa meta za ujazo.
Cha ajabu hapa tunapigia chapuo uvunaji wa maliasili ambayo ikivunwa ni hatari kuliko ikiachwa. Na wala hakuna anayeomba punguzo katika ‘mboga mboga’. Makala haya inaweka wazi kuwa Tanzania haiitaji kupunguza kodi kwa ajili ya mavuno ya misitu kama magogo na mbao, isipokuwa inahitaji kuweka ‘udhibiti’ ili kupambana na upotevu unaokisiwa kufikia dola milioni 58 za kimarekani kutokana na udanganyifu na utoroshaji wa mavuno ya misitu katika Asia na hasa Uchina.
Pia kuna eneo jingine nalo ni la uuzaji wa pombe kali(spirit) ambako TRA inaweza kuziba mianya ya upotevu na si kuwabinya wajasiriamali. Inakadiriwa zaidi ya bilioni 2 za kitanzania zinapotea kutokana na wakwepaji wa kodi wanaouza pombe kali. Na hivi karibuni kuna hawa wakurugenzi zaidi ya saba ambao TRA inawatafuta kwa kukwepa kodi ya uuzaji wa pombe kali.
Hatujitaji kupandisha kodi Tanzania ili tuweze kuendesha serkali yetu, changamoto ni katika kukusanya kodi kwa ufasaha na kwa uwazi.
Sekta ya mboga mboga inahitaji kung’oa nanga, ni vizuri ikiachwa ikue na ni vema kuiongezea motisha na si kuizima kila inapochipua. Chonde TRA angalieni mara mbili uamuzi wenu wa kutoza VAT ya asilimia 18 kwa mizigo inayosafirishwa kwa ndege nje ya nchi na wajasiriamali katika sekta ya mboga mboga.
Kwa sasa kuna madai kuwa wajasiriamali wameanza kutumia Kenya kusafirisha mizigo yao, ingawa hatuna takwimu za wazi, lakini kuna vitu tunapoteza. Njia ya Kenya haina mwisho mwema kwani mwaka 2007/2008 hasara ya bilioni moja ya kitanzania ilipatikana kutokana na kukatishwa kwa ruti kufuatia mapigano ya wenyewe kufuatia sintofahamu ya matokeo ya Uchaguzi.
Tunahitaji kufikira mara mbili katika kipindi hiki cha ‘msukosuko’ wa uchumi tunahitaji kupandisha kodi au kupunguza na hasa bidhaa tunazouza katika soko la nje. Jibu sahihi ni kwamba hatuhitaji kupandisha kodi kwa bidhaa za kilimo.
Yatupasa kuilinda sekta hii changa, kwa maendeleo ya watanzania na hasa waishio vijijini, ambao wanajishughulisha na uzalishaji wa mboga mboga. Na si kuwapigania wavuna magogo na wauza mbao.