Monday, January 18, 2010

Ni muda muafaka kuongeza umri wa kustaafu

Majuma machache yaliyopita vyombo vya habari vya Tanzania. vilipambwa na sakata la serikali kumnyima ajira ya mkataba, mwanazuoni nguli wa siasa za kimataifa Profesa Mwesiga Baregu wa Chuo Kikuu cha Dar-Es-Salaam (UDSM).
Waziri mwenye dhamana, Mheshimiwa Hawa Abdulreihman Ghasia, aliweka wazi kuwa serikali kwa sasa haina nia ya kumpa mkataba mpya Profesa Baregu, baada ya kumpatia mara tatu tangu alipostaafu mwaka 1999, akiwa na miaka 55.
Tangu suala la kunyimwa mkataba kwa nguli huyu lilipoibuliwa katika vyombo vya habari, kuna makundi mawili makubwa yameibuka katika kuangalia, uhalali wa kama Profesa ameonewa au serikali ipo sahihi kusitisha kumpa mkataba.
Kuna waliojikita katika itikadi za kisiasa, ingawa waziri pia amegusia hilo kuwa ndiyo kiini cha kusitisha mkataba mpya kwa gwiji huyu. Lakini kuna madai kuwa wapo wana CCM mbona wamepata, wakienda mbali zaidi wakihusisha ukosoaji wake kwa serikali kuwa ndiyo kigingi cha yeye kutemwa UDSM.
Kichuguu cha pili kilikuwa na wale wanaoona kuwa maamuzi haya ni sahihi ingawa hawa hawakupata nafasi ya kuhojiwa sana na vyombo vya habari, huku wakiweka wazi kuwa sasa huu ni wakati wa damu changa kuchukua nafasi katika taasisi mbalimbali za serikali.

Makala haya haina nia ya kusema kati ya hivyo vichuguu viwili na hoja zao kipi kipo sahihi au yupi amekosea, la hasha ila itajaribu kupitia umuhimmu wa kuangalia nini tunajifunza kama 'nchi' kuhusu sakata hili, la Profesa Baregu.Serikali imekwisha hitimisha.

Somo tunalotaka kulijadili katika makala haya ni kuhusu umri wa kustaafu katika Tanzania.Na hasa kwa wanazuoni au wataalamu wengine ambao serikali hutumia gharama kubwa kuwasomesha.

Naweka wazi msimamo wangu kuwa umri wa kustaafu unapaswa kuongezwa na hasa katika kada za walimu wa vyuo vikuu. Kwa sasa kuna wanaostaafu katika 55 na wengine 60 kwa manufaa ya umma.

Ulimwengu wa leo watu wengi wananafasi kubwa yakuishi maisha marefu hii ni kutokana na mafanikio ya kisayansi ambayo yameweza kuboresha viwango vya ubora wa maisha kwa wale wanaozingatia na kufuatilia kwa ukaribu. Magonjwa ambayo yalikuwa tishio si tena tishio kwa binadamu.

Pia mafanikio ya kisayansi yanampa nafasi binadamu kuweza kufanya kazi kwa muda mrefu, wakati zamani miaka 55, ni umri uliokuwa kweli umechoka kweli kweli. Mfano Mzuri ni huyo Profesa, tangu astaafu amepewa mikataba mitatu na bado yu mwenye siha nzuri na anaonekana anaweza kumudu mikiki mikiki ya kazi yake.

Katika Tanzania, kustaafu katika miaka chini ya 65 ni pigo kwa nchi na hasa wahadhiri ambao wengi leo hii tulionao wako mbioni kustaafu, vyuo vingi vinakabiliwa na hatari ya kukosa hawa magwiji katika miaka mitano ijayo.

Inakadiriwa katika miaka mitano ijayo wengi ya wanataaluma waliobobea katika shahada za uzamivu watakuwa wamestaafu wakiwa na umri wa miaka 60. Kimsingi hii ni hasara kwa nchi.

Hasara kwa sababu, wengi ya wanazuoni tulionao wamapata PhD wakiwa na zaidi ya miaka 45 hadi 50. Sasa ukiangalia gharama za kumsomesha mwanafunzi wa PhD alafu anatumika chini ya miaka 10 anastaafu ni nchi ndiyo inapata hasara.

Hili suala la kuomba kuongeza muda wa kustaafu walau ufikie miaka 65 si jambo geni, na wala siyo hoja mpya katika Tanzania.Kati ya watu wanaopigia chapuo kuongezwa kwa umri wa kustaafu ni Balozi Juma Mwapachu, Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Sisi tumechelewa kusoma, na mifumo yetu mara nyingi inatubana kupata wanazuoni walio na umri chini ya miaka 30 wakiwa na PhD. labda katika miaka 10 ijayo tutakuwa na watanzania walio na PhD wakiwa chini ya 30 hii baada ya serikali ya awamu ya tatu kuhimiza kupeleka watoto shule mapema.

Na ujio wa shule binafsi umefungua mwanya kwa vijana wa kitanzania kwenda shule wakiwa na wastani wa miaka 4 hadi 6 kuanza darasa la kwanza huku wakirushwa baadhi ya madarasa, hasa la saba na wangine wakitumia elimu ya nje kama Kenya na Uganda kusonga mbele katika vyuo vikuu vya huko.

Ila kwa wale tuliosoma Tanzania ni wazi kuwa kupata PhD si chini ya miaka 45, na kupata Uprofesa kama ngazi ya juu ya kielimu katika kufundisha inaweza kuchukua zaidi ya miaka 10 kwa Tanzania.Ukijumlisha na uchelevu wa kwenda shule huko nyuma wengi wanakuwa maprofesa bado miaka michache kustaafu. Hawa ndiyo magwiji walioiva.

Sasa kwa nini wameiva sasa, ndiyo tunawapa taarifa ya kusataafu!Hapa pana ulakini.Katika nchi za magharibi kustaafu ni miaka 65, na wengi huku wamepata PhD wakiwa chini ya miaka 25. Hivyo anaitumikia nchi yake kwa zaidi ya 30.

Ni wazi kuwa atarudisha fedha ya walipa kodi kwa kazi atakayoifanyia nchi yake.
Hasara yake ni kwamba wakati tumetumia pesa nyingi kuwasomesha katika vyuo vya nchi za magharibi kwa gharama zisizopungua milioni 100 kwa mtu mmoja kwa PhD tunamtumia chini ya miaka 10,kwa vile tu sheria inasema astaafu chini ya miaka 65!

Pesa nyingine zinakuja kama mikopo, hivyo hata mkopo haujalipwa na mtu hajaitumikia jamii yake anaambimwa astaafu kwa manufaa ya umma.

Ni sheria inapaswa kufuatwa. Lakini sheria hii kwa mmtazamo wangu nahisi ina matatizo na hasa kwa nchi yetu hii changa. Mbona Uingereza wanastaafu wakiwa na miaka 65.

Lengo kuu la sheria au taratibu za jamii yoyote ni kuwatumia jamii husika, sasa sheria hii inaonekana haina manufaa kwetu yatupasa kuijadili na kutafuta suluhu ya kudumu.

Rai yetu ni kwamba huu ni wakati muafaka wa kufikiria kuongeza kwa umri wa kustaafu iwe kwa hiyari au kwa manufaa ya umma umri uwe miaka 65.

Sunday, January 10, 2010

Bila walaji 'makini' ushiriki wetu u-mashakani

Gwiji wa Uchumi Profesa Michael Porter wa Chuo Kikuu cha Harvard katika nadharia yake maarufu kama 'Porter's Diamond Model' au 'faida ya ushindani'(Competitive Advantage) anabainisha wazi kuwa nchi ili ifanye vyema katika biashara ya kimataifa inahitaji kuwa na 'walaji makini'(Sophisticated Customers). Walaji wanaojua kuwa hii bidhaa haina ubora, na wapi waende ili wapate haki zao mara wanapokosa huduma bora toka kwa kampuni husika kwa 'uwongo' wa makusudi wa kibiashara.
Porter’s Diamond model inataja viashiria vikuu vinne vinavyo weza kufanya nchi iweze kushamiri katika biashara ya kimataifa, rasilimali (endowment factor),mahitaji ( demand condition), uhusiano wa kiviwanda (relating and supportive industries) na mbinu za kibiashara (firms strategy).
Makala haya itajadili umuhimu wa walaji makini kwa ustawi wa sekta ya kibiashara katika Tanzania na hasa viwanda. Tanzania inahaha kupanua wigo wake wa biashara ya nje, lakini wakati wote imekuwa haifanyi vyema.Kumekuwa na kauli mbiu za kila aina na taasisi kama CTI imekuja pia na kauli mbiu ya ‘kuwa mzalendo tumia bidhaa za nyumbani’
Kimsingi hakuna nchi iliyokuwa na kuimarika katika uchumi wake bila uchumi wa nchi husika kuimarika kwanza katika soko la ndani. Soko la ndani ni muhimu na mara zote limekuwa halina hadhari kubwa kama vile soko la kimataifa.
Tafiti fulani inabainisha kuwa kampuni nyingi zilizokwenda katika soko la kimataifa asilimia 50 zilianguka, kwa sababu mbalimbali. Pamoja na ukweli huo soko la kimataifa bado limebakia kuwa ni suluhu moja wapo ya kuimarika kwa uchumi si kwa nchi changa kama Tanzania tu bali hata nchi tajiri nazo zinahaha kuweza kujiimarisha katika masoko ya kimataifa mapya (Emerging markets) ya Asia na Afrika.
Sekta ya viwanda kwa sasa Tanzania ipo nyuma pamoja na mambo mengi inayoielemea sekta hii likiwemo uchakavu wa mitambo, miundo mbinu, ukosefu wa nishati(umeme wa mgao) lakini pia hili la kukosa walaji makini linasababisha kilio kwa viwanda vyetu.
Kwa mujibu wa Profesa Porter, soko la ndani linanafasi kubwa kwa kuchochea uhitaji wa bidhaa zenye ubora wa hali ya juu na hivyo kuipa changamoto kampuni katika kuinua na kuboresha bidhaa zake.
Ripoti ya Benki ya Tanazania(BoT) ya mwaka 2006/2007 inataja kuwa sekta ya viwanda imekuwa huku ikichangia pato la taifa kwa asilimia 9.2, ikiwa kuna mauzo ya nje kwa bidhaa za viwandani zenye thamani ya dola za kimarekani 226.8, huu ni mchupo wa dola milioni 34.6.
Mauzo yameimarika katika masoko ya Rwanda, Burundi na Kongo-Kinshasa kwa bidhaa za nguo kama vitenge na kangha, glasi, plasiti kukiwa na mafaniko toka kwa kiwanda cha Simba Plastiki inayouza katika nchi za SADC na pia viwanda vya chuma vinavyouza nondo.Uuzaji wa pombe kali kama konyagi na bia.
Ripoti hii haitaji kuhusu viwanda vya bidhaa za walaji kama sabuni na dawa za meno, lakini kuna taarifa za sabuni ya Foma Gold kufanya vizuri katika masoko ya Malawi na Zambia.
Pamoja na mafanikio haya tuliyojaribu kuyaorodhesha hapo juu, bado Tanzania inakaribiwa na mchango mdogo kutoka katika sekta ya viwanda vyake katika pato la taifa.
Mara zote kilio kimekekuwa kutoka miongoni mwa walaji na wazalishaji kuwa bidhaa za watanzania hazinunuliki sokoni.
Unaweza kujiuliza pamoja na kilio cha ubora mdogo wa bidhaa toka Uchina? Mbona bado tunagombania bidhaa hizo?Hii ni wazi kuwa walaji wa soko la Tanzania, siyo makini.
Ni walaji wanaoweza kununua kiatu cha plastiki kwa bei ya elfu 15000 toka Uchina na kuacha kiatu cha ngozi cha pale Moshi-Kilimanjaro.
Ni wazi kuwa mzalishaji wa kiatu naye atapunguza umakini hali ambayo itafanya kudorora kwa ubora wa bidhaa zake ili aweze kupambana na bidhaa feki za Uchina. Lakini kwa kufanya hivi ni wazi kuwa mbio hizi zinapunguza uwezo wetu katika kuyafikia masoko ya nje.
Ni walaji ambao hatuangalii ubora, ila tunajali uwingi na faida ya mlinganisho wa kifedha ya muda mfupi.
Mlaji makini anafahamu ubora wa bidhaa anayotaka kutumia kwa thamani ya fedha zake.Uhitaji wa bidhaa zenye ubora wa juu katika soko la ndani unavifanya viwanda husika kufikiri namna ya kuongeza jitihada katika tafiti zao(research and development)
Walaji wa Tanzania tunapokea kila kitu hatuko makini, hili linafanya viwanda vyetu vya ndani kubweteka na kusahau kuwa kuna siku za ushindani na hivyo ujio wa bidhaa toka nje zikipiga hodi.
Juhudi za kamisheni ya usawa wa biashara (FCC) za kuponda bidhaa mbovu zinazoingizwa nchini ni zenye kuungwa mkono kwani hizi bidhaa feki zinalemaza si tu walaji na wazalishaji pia.
Kabla ya Tanzania kuingia katika mfumo wa soko huria nadharia iliyokuwa imejengeka ni kuwa kwa vile ni serikali ndiyo mmiliki mkuu wa viwanda hivi hakuna namna ya kudhibiti, wala mteja hakuwa na nguvu ya kupinga bidhaa mbovu ikiwa imezalisha katika kiwanda cha umma.

Lakini imani yetu dhidi ya soko huria kuweza kutuletea bidhaa zenye ubora, imedimimizwa na ujio wa bidhaa feki.
Ni wazi kuwa sasa hivi tatizo ni walaji wasiolindwa wala kupata elimu juu ya umuhimu wa kiuchumi na kiusalama na afya wa kutumia bidhaa zenye ubora.
Ni ngumu kupata wateja walio makini kwa kutegemea nguvu za kiuchumi(soko) tu, yatupasa kuunda chama cha walaji. Chama cha walaji kitadai haki za walaji toka kwa watoa huduma hadi wazalishaji wa bidhaa.
Kwa kudai bidhaa zenye ubora ni wazi pia wazalishaji wa ndani wataamka na kuzalisha bidhaa zenye ubora kwa soko la nje pia.

Ni China au ni Afrika ambayo haiwezi kusema 'hapana'?

Katika siku za karibuni ongezeko la bidhaa 'feki' limekuwa ni tatizo kwa nchi nyingi zinazoendelea na Tanzania ikiwemo. Wakati wote huu Uchina imekuwa ikibeba lawama kuwa ndiyo mhusika na ni muendelezaji wa uuzaji wa bidhaa feki, kwa Afrika.
Niliwahi kuhudhruia sherehe moja ya harusi, nikashuhudia mama mmoja akipatwa na kadhia ya kuvunjika kwa kisigino cha kiatu chake cha ‘mchuchumio’ (High heels). Nilipomdadisi aliniambia kuwa ndiyo kwanza anakivaa(ulikuwa palo wa sare ya sherehe). Lakini alijifariji kuwa, amenunua 15000 tu, kariakoo.
Hasara ni hasara, je wale wanaounguliwa nyumba kwa kutumia nyaya au vifaa vyenye viwango vidogo!Ingawa ni ngumu kupata takwimu sahihi, lakini lililowazi ni kwamba miongoni mwetu tupo tunaopata hasara kwa kutumia bidhaa zenye viwango duni kutoka Uchina.
Tanzania bidhaa zenye ubora mdogo zinatusumbua. Makala haya itajaribu kutupia jicho hali ya kibiashara kati ya Uchina na Afrika.Lakini iweje katika maduka ya nchi za magharibi bidhaa za kichina zimejaa, lakini hawalalamiki kuwa kuna 'ufeki' kwa kiwango kama cha Tanzania?
Biashara kati ya Afrika na Uchina imeimarika kuanzia miaka ya 1990, huku Uchina ikiwa inaongoza kwa kufanya biashara na Afrika kwa miongoni mwa nchi za Asia, ikiwa na asilimia 39 ya biashara yake na Afrika.
Kutoshiri katika siasa za ndani za nchi za Afrika kunaifanya Uchina iwe kimbilio la bara hili.Hii ni sera ya mambo ya nje ya Uchina. Hivyo dikteta ana nafasi sawa na mlinda haki za binadamu mbele ya Uchina, ili mradi tu wao wanapata wanachohitaji na masilahi yao yanalindwa.
Biashara kati ya Afrika na Uchina imejikita zaidi katika , ujenzi wa miundo na usakaji wa malighafi hiki ikinunua mafuta kutoka Angola na Nigeria na Sudan. Ujio wa Uchina katika Afrika unahusishwa zaidi na kiu yake ya kusaka mafuta na maliasili zingine, huku ikiwa mtumiaji wa pili wa nishati ya mafuta baada ya Marekani ni wazi kuwa ni mshiriki mkubwa wa Afrika inayokidariwa kuwa na hifahdi ya asilimi 9 ya hifadhi ya mafuta ya Ulimweungu, lakini lenye kuvutia zaidi ni kuwa bara hili bado linaendelea kuvumbua vyanzo vingi vya mafuta katika maeneo mengi ya bara hili.
Jitihada za ushiriki wa Uchina unaimarishwa zaidi na jitihada zake za kufuta madeni ya bilioni 10 za kimarekani kwa nchi za Afrika. Ni wazi kuwa China ni mshiriki mzuri na mwenye kuangaliwa vyema katika kila analolifanya kwa maendeleo ya bara hili.
Kwa mujibu wa vyombo mbalimbali vya habari vya Uchina, Tanzania ni nchi inayoongoza katika Afrika kwa kupata misaada kutoka Uchina. Ni China ndiyo inayotoa mabilioni ya misaada katika kupiga’ jeki’ bajeti yetu na vyombo vya habari vimeripoti ‘mvua’ ya mabilioni ya mikopo kwa Tanzania katika siku za karibuni.
Misaada ipo kaitka kila kona, elimu, afya, jeshi, miundo mbinu nakadhalika. Ushiriki wa Uchina katika maendeleo ya Tanzania ni wa muda mrefu tangu (enzi zaMwalimu) awamu ya kwanza.
Urari wa kibiashara kati ya nchi hizi mbili upo chanya kwa China, huku ikiuza bidhaa zenye thamani ya dola milioni 128 na Tanzania ikiuza bidhaa zenye thamani ya dola milioni 6.62 kwa ripoti za mwaka 2002.
Kwa sasa biashara miongoni mwa nchi hizi mbili imeingiwa na mdudu ‘bidhaa feki’ huku Uchina ikipewa lawama, kwa kila bidhaa inayokamatwa na kila lalamiko katika Tanzania.
Wadadisi wa biashara za Uchina, wanabainisha kuwa ni ngumu kwa Uchina kudhibiti uzalishaji wa bidhaa hizi kwani baadhi ya majemedari wa jeshi wanamiliki au wanahisa katika baadhi ya viwanda.
Lakini, Uchina si muuzaji wa Afrika tu, akiwa na urari wa biashara wa zaidi ya dola 102 bilioni , ni muuzaji mkubwa katika masoko ya Ulaya na Marekani pia.Ni wazi kuwa kieneo si ni sehemu ndogo sana ya chumo lake biashara ya nje.
Tunachojiuliza ni kwa vipi bidhaa za kichina ziwepo kwa wingi na kutumiwa katika nchi kama Uingereza. Ufeki huku haupo kwa kiwango cha Tanzania?
Kamisheni ya Ushindani (FCC) inataja kuwa kiwi za milioni 20 na ‘tubelight’ za aina ya Phillips na Britimax zenye thamani ya dola 18000 zimeteketezwa mwaka 2007, kwa mujibu wa gazeti la Daily News la 1 May 2009.
Pia inakadiriwa kwa mwezi machi pekee 2008, bidhaa zenye thamani dola za kimarekani 224,000, ziliteketezwa na FCC. Ni wazi kuwa FCC kwa uchanga wake inafanya kazi kadiri inavyoweza ili kudhibiti bidhaa ‘feki’.
Vita hii inaonekana kwa sasa inasumbuliwa na ‘balkanization’ kila wizara na idara ya serikali ikipigana kutoka kivyake vyake. Kimsingi vita ya bidhaa feki ni ya jamii nzima, na bila chama cha walaji imara kinachoundwa na walaji wenyewe wafanya biashara wetu watandelea kujaza nchi yetu na bidhaa feki.
Vyombo vyenye mamalaka vimekuwa vingi hadi tuchanganyikiwa tuna TFDA, TBS, FCC.Walaji hatujui tukipata bidhaa ‘feki’ tuanzie wapi? Je tunaitambuaje bidhaa feki?Kuna muongozo wa viwango vya bidhaa, kuwa ubora wa bati unapaswa kuwa ni mchangayiko wa malighafi hizi kwa viwango anuai?Mlaji anayefahamu haya yote?Ni ngumu kwa baadhi ya mbinu kwa mlaji kuweza kutambua.
Ni wazi kuwa vita hii inahitaji kuongezewa nguvu na sheria inayowapa walaji nafasi ya kuwa na chama imara chenye kuwalinda tena chenye nguvu ya kulinda masilahi ya walaji.Katika nchi nyingi vyama hivi vipo na vimekuwa mwiba na vimefanikiwa kulinda nchi zao kuwa majalala ya bidhaa ‘bomu’ si toka nje tu hata wazalishaji wa ndani.
Vyama vya walaji(consumer Associations) vimekuwa vikiheshimiwa kuliko hata taasisi za serikali, kwa vile mara nyingi zimekuwa zikitoa taarifa bila kulinda masilahi ya kisiasa. Mfano mzuri ni imani ya waingereza juu ya FSA(Food Standard Agency) ni ndogo kwa vile ‘walibinya’ ukweli kuhusu homa ya kichaa cha ng’ombe (Bovine spongiform encephalopathy) kwa nia ya kulinda uchumi kwa gharama za walaji!
Ukiangalia mfano huu ni mingine sehemu zingine Duniani, utapata picha kwamba chama cha walaji kinahitajika zaidi kwa sasa Tanzania ili kulinda wateja katika siku za mfumo huu wa soko huria.Kwa sasa kuna chama cha kutetea wasafiria, hii ni hatua nzuri. Lakini yatupasa kukiimarisha chama hiki ili kiendelee kulinda manufaa ya walaji katika sekta ya usafairi.
Hii ni hatua moja tu kama nilivyosema, Tanzania ni kubwa na ushawishi wa wafanya biashara wetu katika kuleta na kufanikiwa kuingiza bidhaa feki unongeeka kila siku. Kwa mfano ukimwambia mteja kuwa ataweza kutambua bidhaa feki kwa tofauti ya jina(brand) hii inakosa nguvu sana kwani kwa sasa biashara ya Ulimwengu imejawa na wazuaji wa nembo zao(Own brand).
Hivyo tajiri anaweza kuagiza tani za vitasa toka Uchina akavipa jina la hardware yake. Ila hoja yetu ya ‘ufeki’ ipo katika malighafi zilizotumika kama zinakubarika katika soko la Tanzania.
Kwa kuangalia uwingi wa bidhaa za uchina katika nchi za magharibi na jinsi zinavyojipenyeza huko na kupapatikiwa na walaji kwa ‘upenyo’ wa bei ni wazi kuwa hatuna njia zaidi nasi pia kutumia bidhaa kutoka Uchina.
Ila kama nilivyokwisha kusema, hapa ni wauzaji wetu ndiyo walio kuwa na kasoro, ama hawana ufahamu na viwango vya nchi kwa bidhaa mbalimbali pale wanapoagiza. Suala la viwango vya ubora ni suala ‘tete’ na ni wazi kuwa viwango vya Tanzania, si sawa na Uingereza, ingawa kuna viwango vya bidhaa vya Ulimwengu, pia kuna nchi wanatumia viwango vyao bila hata kujali hivyo vya ulimwengu.
Hatuwatetei wajasiriamali ila yatupasa kupeleka elimu ya viwango kwa waaagizaji wa bidhaa toka nje, si kwa walaji tu. Inawezekana pia kati ya waagizaji ni wachahe wenye ufahamu juu ya viwango au kuona ‘muongozo’ wa viwango wa TBS, katika saketi inayotakiwa Tanzania iwe na ubora gani, kwa malighafi na uzito upi.
Pendekezo letu katika vita hii, mosi ni kuundwa kwa chama imara cha haki za walaji na pili kutungwa kwa sheria zenye kumpa mlaji haki za kiuchumi pale itakapogundulika kuwa bidhaa aliyotumia haikuwa na viwango husika,maana kwa sasa vinachomwa moto tu, vipi waliotumia wanapata malipo yoyote?Jibu ni kuwa hatupati
Pia tunapendekeza kutolewa kwa elimu ya viwango kwa waagizaji wa bidhaa toka nje ya nchi wafahamu kabla hatujawahukumu.
Ingawa Uchina ni mdau mkuu kwa maendeleo ya Tanzania kama nilivyokwisha kuonesha, yatupasa kuungana kama nchi kusema ‘HAPANA’ kwa bidhaa feki toka Uchina kwa masilahi ya nchi yetu. Tukiungana tunaweza.

Monday, January 4, 2010

Sekta changa ya 'mboga mboga' na kitanzi cha VAT

Hivi karibuni Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) imenukuliwa na Gazeti la Serikali Daily News la tarehe 26 Desemba 2009 kuwa limepitisha ‘tozo’ mpya ya kodi ya ongezeko la thamani ,VAT, kwa wauzaji wa masoko ya nje hata kama muuzaji ana pato lililochini ya milioni 40.
Mabadiliko haya yanatekelezwa kwa utetezi wa masilahi ya kulinda nchi hii ni kwa mujibu wa TRA. Safari hii VAT itatozwa hata kwa wale wajasiriamali wadogo, lakini tatizo si VAT, ila ni marejesho kuwa ‘yanabagua’. Kimsingi mlipaji wa VAT ni mlaji, kwani muuzaji hurejeshewa malipo yake, lakini hawa wadogo waliochini ya milioni 40 hawana cha ‘kurejeshewa’.
Tatizo hili la kukosa kuwarudishia ‘wajasiliamali’ ndiyo kiini cha makala haya. Tutajaribu kuangalia manufaa ya dhana hii kwa Taifa na pia tutatoa mchango wetu kuhusu hili.Ingawa tunaaamini hiki inawezekana ikawa ni kilio cha samaki machozi huenda na maji anaimba gwiji wa muziki wa dansi, Dr. Ramadhani Mtoro Ongala.Lakini tunaamini sauti yetu itasikika.
Kati ya sekta zilizoathirika na marekebisho haya ya kisheria ya VAT, ambayo kimsingi kamishina wa kodi ananguvu kisheria kuamaua nani alipe VAT ingawa sheria yenyewe ya inasema ni yule mwenye zaidi ya milioni 40.Sheria ya VAT kifungu sura ya 148 kifungu 19 kifungu kidogo 4, kinampa uwezo Kamishina wa Kodi kuamua nani alipe ingawa utakuwa upo chini ya milioni 40.
Ni vyema ikaeleweka wazi kuwa hatuna nia ya kujenga wala kutetea jamii ya watu wasio penda kulipa kodi, ila tunashaka na maamuzi haya kama kweli ya nia kuona nchi hii inang’ona ‘nanga’ kiuchumi.
Jitihada za kupambana na anguko la uchumi duniani imeona serikali nyingi zinahamasisha kuuza katika masoko ya nje, na zinatoa motisha ya punguzo la kodi kama si kufuta kabisa. Itakumbukwa pia katika siku za mwanzo za msukosuko huu kauli iliyokuwa inapigiwa chapuo na Marekani ni kuhakikisha nchi hazifungi mipaka yake ya kibiashara kwa kutumia njia kale (traditional barriers kama vile kodi za aina yoyote)
Ni kweli kuwa Tanzania inahaha ikitafuta kujinasua kutokana na msukosuko wa kiuchumi wa dunia kwa kutafuta kuongeza pato lake. Lakini kwa njia hii ya kutoza wauzaji wa nje na hasa wauzaji wa sekta changa ya mboga mboga ambayo imejawa na wazalisahjo wadogo wengi hauna mwisho mwema.
Sekta hii changa ya mboga mboga (horticulture) lakini katika makala haya tutajumlisha pia na floriculture, pale tutakoposema mboga mboga inakadiriwa tani kati ya 15 hadi 40 husafirishwa kwa wiki, kuelekea masoko ya ng’ambo kwa kutumia usafiri wa anga.
Hii ni bidhaa inayohitaji kufika sokoni haraka kutokana na tishio la kuharibika haraka (fast moving consumer goods). Kupitia chama chawazalishaji wa mboga mboga (TAHA) Tanzania ilijinyakulia tuzo ya shaba katika maonesho ya Amsterdam kwa mara ya kwanza wakati tukiwa washiriki kwa mara ya kwanza mwaka 2007.
Ikiwa inaleta chumo la dola milioni 50 kwa mwaka, na kuajiri watu wanaokadiriwa kufikia 10000, huku zaidi ya kampuni 20 zikiaminika kushiriki katika sekta hii. Ni wazi kuwa inahitaji kuangaliwa vizuri. Tanzania inakila sababu ya kuilinda sekta hii inayochipua kwa kuipa motisha lakini yanayotokea nchini ni kinyume chake.
Uzalishaji mkubwa wa mboga mboga upo Arusha, Kilimanjaro, lakini mikoa mingine kama Morogoro, Mbeya, Rukwa ,Tanga na Iringa nayo inafanya vyema na inakila hali ya kijiografia kuiwezesha kufanya vyema.
Mwenendo wa soko la ulimwengu wa mbogamboga katika nchi za Ulaya ni wenye kutia matumaini kwa siku za baadaye wa sekta hii nchini. Hii inatokana na ukweli kwamba katika Ulaya kuna mwamko wa kiafya kupinga ulaji wa nyama nyekundu kuanzia miaka ya kati ya sabini hali iliyopelekea kukubalika kwa nyama nyeupe kama kuku na nguruwe miongoni mwa watu wazee.
Uoga wa ulaji nyama ulishamiri zaidi baada ya kuibuka kwa ugonjwa kichaa za ng’ombe, BSE( Bovine spongiform encephalopathy) katika Uingereza miaka ya 1996.
Mwenendo wa soko umeimarika baada pia kuongezeka kwa hali ya kulinda wanyama, na ongezeko la walaji majani katika nchi hizi kwa imani za kisayansi. Kwa mfano tangu ongezeko la vitisho hivi soko la walaji wa nyama wa Uingereza umepungua ukiwa ni kilo 14.4 tu kwa mwaka.
Ni wazi kuwa Tanzania inazewa kunufaika na hakuna shaka kuwa sekta hii changa inahitaji kupigiwa ‘chapuo’ kuhakikisha kuwa tunakataa kuwa wauzaji wa wanunuzi wasio makini kama vile Kenya ambao hununua vitunguu na matunda toka kwetu kisha kuuza Ulaya kwa faida kubwa.
Hili la tozo ya VAT ya asilimia 18, ambapo hawa wadogo hawarejeshewi imevunja nguvu za wajasiriamali wanaohaha usiku na mchana kuona wanaunganishwa na soko la nje, na ni wazi kuwa si njia sahihi. Kwani Tanzania sasa hivi haihitaji kutoza kodi kubwa na hasa wauzaji wa nje ili kuongeza pato inahitaji kuhahakikisha wajasiriamali hawa wanauza katika soko la nje na wanapata suluhu katika mashaka yao.
Iweje wakubwa walio na pato kubwa la milioni zaidi ya 40 warudishiwe lakini wadogo wasirudishiwe? Hii si sawa. VAT analipa mlaji lakini safari hii wamekandamizwa wazalishaji tena wa sekta changa, kwa kigingi cha kulinda masilahi ya Taifa.Taifa gani linalolindwa wakati utekezaji wa sheria hii ni wazi kuwagawa watanzania, na hasa hawa wakulima wadogo wa mboga mboga!
Tanzania inavyanzo vingi vya kodi na tangu tumeamua kuchauga mabadiliko ya kiuchumi miaka ya 1980 ya soko huria, nia ilikuwa kuona utawala wa kodi unakuwa huru na wa haki.
Lakini safari hii tunaona kodi inakuwa kandamizi tena wakati wa hangaiko la Uchumi. Sekta hii ya mboga mboga nayo pia imepata msuko msuko, huku la soko la Uingereza likiwa limepungua kwa asilimia 20 kwa bidhaa toka Tanzania.Ni wazi kuwa sekta hii inahitaji kulindwa hasa ukizangatia kuwa ni wakulima wadogo ndiyo wanaoshiriki katika kuzalisha bidhaa hizi katika maeneo mengi nchini.
Kukosa pato kwa TRA kusihusishwe na kubinya walipa kodi waliojitoa na kukubali kulipa kodi kwa maendeleo ya Taifa. Na hili ndilo tatizo la Tanzania, mara zote nchi inakuwa iko mbele kuhakikisha inawakamua wale walipa kodi na si kuziba mianya ya uvujaji wa kodi.
Hivi karibuni gazeti la serikali Daily News la tarehe 20 Desmeba 2009, lilikuwa na taarifa kuwa wauzaji wa magogo na mbao nje ya nchi walikuwa wanataka kupunguzwa kwa kodi. Ombi ambalo serikali kupitia Waziri wa Viwanda na Biashara, Dr. Mary Nagu amekubali kulipokea na kuliona, huku Naibu wa Waziri wa Maliasili akilipigia ‘chapuo’ kuwa nchi inahitaji kupunguza tozo ya mbao na mazao mengine ya misitu ili kuongeza pato la taifa na hasa mauzo ya nje. Kwa sasa tozo ni 200,000/= kwa meta za ujazo.
Cha ajabu hapa tunapigia chapuo uvunaji wa maliasili ambayo ikivunwa ni hatari kuliko ikiachwa. Na wala hakuna anayeomba punguzo katika ‘mboga mboga’. Makala haya inaweka wazi kuwa Tanzania haiitaji kupunguza kodi kwa ajili ya mavuno ya misitu kama magogo na mbao, isipokuwa inahitaji kuweka ‘udhibiti’ ili kupambana na upotevu unaokisiwa kufikia dola milioni 58 za kimarekani kutokana na udanganyifu na utoroshaji wa mavuno ya misitu katika Asia na hasa Uchina.
Pia kuna eneo jingine nalo ni la uuzaji wa pombe kali(spirit) ambako TRA inaweza kuziba mianya ya upotevu na si kuwabinya wajasiriamali. Inakadiriwa zaidi ya bilioni 2 za kitanzania zinapotea kutokana na wakwepaji wa kodi wanaouza pombe kali. Na hivi karibuni kuna hawa wakurugenzi zaidi ya saba ambao TRA inawatafuta kwa kukwepa kodi ya uuzaji wa pombe kali.
Hatujitaji kupandisha kodi Tanzania ili tuweze kuendesha serkali yetu, changamoto ni katika kukusanya kodi kwa ufasaha na kwa uwazi.
Sekta ya mboga mboga inahitaji kung’oa nanga, ni vizuri ikiachwa ikue na ni vema kuiongezea motisha na si kuizima kila inapochipua. Chonde TRA angalieni mara mbili uamuzi wenu wa kutoza VAT ya asilimia 18 kwa mizigo inayosafirishwa kwa ndege nje ya nchi na wajasiriamali katika sekta ya mboga mboga.
Kwa sasa kuna madai kuwa wajasiriamali wameanza kutumia Kenya kusafirisha mizigo yao, ingawa hatuna takwimu za wazi, lakini kuna vitu tunapoteza. Njia ya Kenya haina mwisho mwema kwani mwaka 2007/2008 hasara ya bilioni moja ya kitanzania ilipatikana kutokana na kukatishwa kwa ruti kufuatia mapigano ya wenyewe kufuatia sintofahamu ya matokeo ya Uchaguzi.
Tunahitaji kufikira mara mbili katika kipindi hiki cha ‘msukosuko’ wa uchumi tunahitaji kupandisha kodi au kupunguza na hasa bidhaa tunazouza katika soko la nje. Jibu sahihi ni kwamba hatuhitaji kupandisha kodi kwa bidhaa za kilimo.
Yatupasa kuilinda sekta hii changa, kwa maendeleo ya watanzania na hasa waishio vijijini, ambao wanajishughulisha na uzalishaji wa mboga mboga. Na si kuwapigania wavuna magogo na wauza mbao.

Tanzania na hatari ya majengo ya kifahari

Yapata miongo minne tangu Profesa Rene Durmont, kuandika kitabu chake 'AFRIKA INAKWENDA KOMBO' au kwa kiingereza 'FALSE START IN AFRIKA'.
Kitabu kilihusu Afrika ya 'WEUSI' yaani Kusini mwa Jangwa la Sahara na hasa, Afrika Magharibi.
Na kwa uchache kwa maombi ya Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, aliandika kuhusu Tanganyika iliyokuwa katika siku za mwanzo wa UHURU wake.
Mambo mengi yaliyoandikwa na mchumi huyu toka Ufaransa, mpaka leo yapo na yanaisumbua Afrika. Kwa hakika ni muendelezo wa matukio ambayo ukiyasikia unajiuliza, zamani tulikuwa tunadai matatizo yetu yalikuwa yanatokana na kutawaliwa(UKOLONI). Lakini mbona yale yale tu hata baada ya UHURU?
Jambo moja linalonifanya nikumbuke kitabu hiki na Tanzania ya leo ni, juu ya 'pupa' ya kuhitaji majengo ya 'kifahari' yanayomilikiwa na serikali.
Hili aliliona mapema na akalindika na kuionya Afrika , Tanzania ikiwemo, kuwa yapasa kuchagua njia moja ya maendeleo. Ni 'ufahari' wa majengo ambayo haujawahi kumpatia binadamu shibe isipokuwa fedheha, au kujibana huku mukitekeleza mambo muhumimu kwa taifa.
Leo hii Tanzania, inasononeka na ujenzi wa nyumba mbili za BoT zilizogharimu bilioni 2.5Nyumba hizi ni za gavana na naibu wake.
Hii ni baada ya kutujengea minara pacha iliyotugharimu pesa nyingi na kufanya kesi kuwepo mahakamani hadi leo.
Wataalamu wa maendeleo wa Ulaya na wanahistoria mara zote husema kuwa matatizo ya Afrika hayakuletwa na wakoloni tu, bali hata uongozi katika nchi zenyewe. Ilichukua muda kukubali ukweli huu kwa upande wa Waafrika.
Lakini kwa hali hii, ni wazi kuwa sasa vijana na damu mpya ya Tanzania inaona na kushuhudia kuwa taabu zetu ni 'mazao' ya viongozi weusi.
Kuna hoja za utetezi kuwa huu ujenzi ulishapitishwa na bodi miaka ya nyuma, hivyo Gavana wa sasa hana kosa. Sawa lakini, hiki kipindi alichojenga nyumba ni kipindi 'hatari'Uchumi duniani unayumba na tunasikia jinsi pato la taifa lilivyoathirika yeye alishindwa nini kuzuia kwa dhana hiyo kuu ya kiuchumi?Tena ni mchumi?
Niliwahi kuandika siku za nyuma katika gazeti la Majira Jumapili siku za mwanzo za ujio wa Profesa Beno Ndullu, kuwa yakupasa kuzingatia kuwa hutatoka kwa aibu BOT.
Leo, yanaendelea kutokea ni ushahidi kuwa labda utabiri utatimia.
Taasisi hii nyeti ya fedha katika nchi hii imekuwa ni mfululizo wa fedheha kila baada ya fedhea.
Katika magazeti ya Tanzania kila siku tunaoana picha za wanafunzi wakikosa madawati, wakikosa vyoo, wanafunzi wakisoma chini ya miti na majengo mabovu ya madarasa. Sasa hili la ujenzi wa nyumba za watu wawili kugharimu bilioni 2.5 katika nchi masikini kama Tanzania, chanzo chake nini?
Hatumaaninshi kuwa fedha hizi zingemaliza 'mashaka' yetu kwa siku moja yote, la hasha. Isipokuwa tunaona kuwa kama nchi tumekosa muelekeo, na kufahamu nini tunahitaji katika kujenga jamii yenye umoja na upendo.
Tanzania inahitaji nyumba ya bilini moja na ushei kwa familia moja?Ukiamka unaenda kazini unapita mitaani unakutana na watu wako wakiwa na mashaka sura zimekunjamana unajisikiaje?
Mipango katika nchi imekwama kwa hoja ya 'fungu' halitoshi! Tena mipango endelevu. Lakini inapokuja fungu la nyumba ya familia moja kugharimu bilioni fungu linatosha.
Serikali ya Tanzania inahitaji kubadilika, katika kupanga na kutekeleza miradi yenye tija kwa wananchi.
Mwalimu Nyerere alisema kupanga ni kuchagua, nasi lazima tuchague maendeleo chanya na si hasi.
Lazima tutumie kidogo tulicho nacho kwa maendeleo ya nchi na watu wake si vitu.Kimsingi maendelao ya vitu iachiwe sekta binafsi ndiyo ihangaike kujenga majumba ya kifahari, serikali kujenga nyumba ya bilioni moja na ushei hakuvumiliki.

Sunday, January 3, 2010

Tuwalinde watoto na matangazo ya 'Junk' food

Tafiti fulani iliyofanyika katika mkoa wa Morogoro kuhusu afya na ulaji, ilibaini watu wazima wenye umri kati ya 45-51 wanakabiliwa na hatari ya unene kwa asilimia 45.5. Hali ni mbaya kwa watoto, hasa kwa vile wanakula kula hovyo juisi na ubuyu kwa nyakati tofauti wakiwa nje ya mikono ya wazazi.
Unene ni hatari inayoinyemelea Tanzania, na ndiyo maana ongezeko la magonjwa ya ‘shinikizo’ la damu, kisukari imemekuwa ni hali ya kawaida. Kisukari sasa kinasumbua watoto wadogo. Haya ni magonjwa yatokanayo na ‘ulaji wa vyakula hatari' pia.Kliniki za kisukari zinachipua kila mahali, hali ambayo haikuwa kawaida katika muongo mmoja na nusu hivi.
Obesity( Unene usio na tija) ingawa ni vigumu kutambua chanzo chake kama vile ni sababu za kibailojia au mabadilko ya kimazingira. Lililowazi ni kwamba mifumo ya maisha ya siku za leo huchangia sana.
Tafsiri rahisi ni ya ‘unene’ ni kuwa tumekula zaidi ya mahitaji halisi ya miili yetu katika chakula husika katika kufanya kazi. Wadadisi wa mambo wanadai katika India kuna zaidi ya asilimia 10 ya watoto wanaohitaji kushona nguo kwa vitambaa vya watu sita wa umri wao!
Hili kwa sasa ni hangaiko la Ulimwengu, na hasa katika nchi zilizoendelea kila nchi inajitahidi kupambana vilivyo ili kulinda jamii ya watu wake. Inakadiriwa hadi kufikia 2015 kama hali itaendelea kama ilivyo Uingereza itahitaji paundi bilioni 50 kutibu magojwa yatokanayo na unene unaosababishwa na ulaji.
Katika Tanzania tabala la kati ‘linachapua’ kila siku, tabaka hili likiwa na hali ya kipato cha wastani na kuweza kujikimu ndiyo wateja wakubwa wa maduka ya haya ya chakula.Ni vijana hawana muda wa kupika, chakula chao ni ‘fast foods’ na juisi za makopo!
‘Fast Food’ and ‘Take Away’ zinaongezeka katika miji mbalimbali, na lililowazi ni kuwa uangalizi wake haupo wa kutosha.Wanapika nini? Wanapikaje? Hakuna anayejua.
Migahawa haina tatizo, tatizo linakuja namna ya uendeshaji wa migahawa katika nchi zinazoendelea mara zote ni kilio mara baada ya muda mfupi. Kwa mfano waendeshaji wa migawa iliyojaa Sinza wanahitaji elimu ya lishe na afya itolewe, ili wajasiriamali hawa wajue madhara ya chumvi, mafuta na sukari. Hii ni kwa faida ya Tanzania na kama nilivyosema wateja wakubwa ni vijana wenye kipato cha wastani (tabaka la kati).Hili la elimu linawezekana na ni mbinu endelevu.
Mila zetu zinachangia kuhusu matatizo ya ongezeko la tatizo hili la kiafya na hakuna anayejua gharama nchi inayoingia kwa mwaka katika kutibu magonjwa yanayotokana na unene.
Hatari inayotukabili ni jinsi watoto wetu walivyokuwa ‘windo’ jepesi kwa kampuni hizi za vyakula. Kuanzia vyakula vya sukari kama juice, biskuti, ‘chipsi kuku’, siagi,pipi na chumvi nyingi kama Pringles!
Hii ni hatari, katika Ulaya na hasa Uingereza matangazo yote ya vyakula hayawausishi watoto ni marufuku. Niliwahi kukumbana na kisa cha mtoto wa miaka mitatu ‘anayejipendelea’ blue band pekee kwa kulamba. Mukisahau kopo limekwisha kwa utamu wa chumvi!
Nchi nyingi zipo katika vita hii,nguvu zimeelekezwa katika kuwalinda watoto, dhidi ya ‘ulaghai’ wa matangazo ya redio na televisheni na mabango ya barabarani.
Ulaya wameenda mbali zadi hata uwekajiwa bidhaa katika ‘shelf’ unaratibiwa, haipaswi kuweka vyakula vyenye chumvi na sukari nyingi karibu na uwezo wa watoto kuona! Hii yote ni katika kulinda taifa la kesho ili lifanye maamuzi sahihi ya uchaguzi wa chakula.
Katika Uingereza sheria inakataza kurusha matangazo ya vyakula ambavyo ni ‘junk’ food kati ya saa 12 hadi 4 asubuhi. Vyakula hivi mara nyingi ni vyenye sukari na chumvi nyingi yenye ‘kurembwa’ na mafuta.
Kampuni za vyakula zinatumia matangazo ya redio na televisheni kuhamasisha ulaji wa siagi tena kwa kauli mbiu za watoto. Unilever wanainadi Blue Band kwa tangazo la’ HAKUNA B, Bila, B’ likisindikizwa na sauti za watoto. Huku wakifadhili vipindi kama LEO TENA cha CLOUDS FM kirushwacho kati ya saa 3 hadi sita.
Kimsingi kampuni za kimataifa( Multinational Companies) zinajukumu la kutulinda lakini kampuni hizi zimesaini mikataba ya kudumisha na kujali haki za wateja nyumbani kwao na zinajitahidi ‘kupumbuza’ watu wa magharibi kuwa ni wanajali afya za walaji katika Dunia ya tatu.
Society Marketing inayoshika kasi katika Ulaya haimaanishi kampuni hizi zitatufanyia kwa staha lazima tutambue kuwa hakuna mtafutaji atakayejali jamii kama hakuna sheria za kudhibiti mwenendo wa wa wafanyabiashara hawa
Ukweli wa mambo wanapofika huko ‘hawachezi’ fair. Wanaongeza sukari na chumvi kuliko viwango na matangazo ya hamasa yanatumika kama kawaida. Mfano mzuri ni jinsi kampuni za kimataifa zinavyolishambulia soko laThailand.
Kampuni kubwa za chakula na wauzaji wa chakula kwa pamoja mara zote wamekuwa wakaidi hata kupinga tafiti za kitaalamu. Bado tunakumbuka jinsi walivyokuwa wakipinga kupunguzwa kwa chumvi kwa madai kuwa tafiti zilizofanyika zinaonesha tu ‘uhusiano’ kati ya chumvi na magonjwa ya shinikizo la damu .Na si kwamba ni kisababishi.
Madai yao yalikuwa ya kibiashara zaidi na wanajua kuwa wakipunguza utamu wa chumvi katika Pringle au nyama ni wazi kuwa ulaji utapungua.
Unene unapofikiriwa kuwa ndiyo utajiri wa familia mara nyingi ni hatari na kampuni hizi hazifanyi makosa. Katika Thailand, mtoto mnene ‘Baby Elephant’ ilikuwa ndiyo ‘hulka’ ya familia.
Nazo kampuni kama Nestle, Kellogg’s, Tesco,ASDA,Coca Cola, KFC zilipopiga hodi kwa mgongo wa FDI hazikufanya makosa waliijaza nchi na vyakula hatari kwa afya.Leo hii takwimu ni za kutisha katika nchi ambayo watu wake walikuwa walaji wa vyakula vya baharini na mboga mboga.
Kwa mfano katika Uingereza 5g tano ya sukari ndiyo itakuwa kipimo cha sukari kwa vyakula.Wakienda masoko ya kimataifa wanaweka zaidi ya hapo hadi kufikia 20g ripoti zinaonesha kuwa Thailand ya leo ni wahanga.
Tanzania haijakwepa uchu wa wawindaji hawa wa uchumi wa kimataifa, kuna matangazo na supermarkets zinaanzishwa pia kampuni tanzu zinazosambaza vyakula hivi zikiwa na matawi katika mikoa.Kampuni za juisi, chewing gum, pipi biskuti nakadhalika.
Ukosefu wa sheria za kudhibiti kampuni hizi ndiyo chanzo cha hatari hii. Wanaruhusiwa kufanya matangazo ambayo ni hatari.
Vifungashio vya pipi kwa sasa vina picha za wachezaji bora duniani, wapiganaji wa mieleka mashuhuri na mabondia.
Jojo (Chewing Gum) zimefungwa na picha za Christina Ronaldo, Didier Drogba, Nicholas Anelka, Samuel E’Too na Evander Holyfield.
‘Mbinu’ hizi hawarushusiwi kutumia ulaya.
Ni marufuku kutumia ‘model’ kwa ajili ya kuhamasisha vyakula hatari na hasa ukitambua kuwa kuna watu wanaweza kufanya maamuzi kwa vile tu wameona picha ya Drogba.
Hawa ni watoto, lakini vyakula kama chocolate, na biskuti zinafungwa katika mtindo huu.
Hili ni bomu, tunashindwa kutibu malaria, itakuwaje kisukari cha umri wa utotoni?
Hali itakuwa mbaya zaidi kwa nchi ambayo viwanja vya mazoezi tumeuza tumekubali kuasi mipango miji kwa, hongo ya kula siku mbili tatu.
Watoto hawa hawana muda wa mazoezi shuleni wala nyumbani, na familia hazimudu kuwapeleka ‘gym’
Tunaloliweza ni hili la kudhibiti matangazo ya yanayochochea watoto kula vyakula hatari. Na hasa kwa kutumia picha za watu mashuhuri.
Kipindi cha watoto kinadhaminiwa na kampuni ya kutengeza ‘junk’ food tena mbaya zaidi gramu za sukari ni zaidi ya 20!
Hii ni vita ya nchi moja moja ulimwengu unatutizama, na kwa vile sisi ni watu wakusubiri misaada hata katika jambo dogo la kutumia maarifa tu yakuzaliwa nayo tumezubaa.Adui wa afya za watoto wa Tanzania ni kwashiorkor. Mpaka leo unatushinda, sasa tukizalisha tatizo jingine itakuwaje?
Yatupasa kubadilika, tuuanze mwaka 2010 kwa kuwalinda watoto wetu na matangazo ya vyakula hatari pia.Tubuni sheria zinazobana matumizi ya picha za watu maarufu kwa ajili ya matangazo ya vyakula hatari, pipi, juisi, biskuti na kadhalika.