Sunday, February 21, 2010

Nembo za kijiografia ni chanzo cha mapato kilichosahaulika

Brand sina neno zuri la Kiswahili lakini katika makala haya tutatafsiri kama ‘nembo’.Kimsingi ni alama ya biashara inayojumuisha rangi, alama, na vifupisho vya herufi. Nembo ikilindwa kisheria inaitwa ‘trade mark’. Katika taaluma ya biashara inaaminika kuwa bidhaa zinatambulika zaidi kwa nembo.
Hili linatokana na ukweli kwamba mteja mara zote anapata faraja ya ‘kisaikolojia’ mara anapotumia bidhaa anayoitambua kuliko kutumia bidhaa asiyoijua na jina au asiyoikubali kwa nembo ingawa inaweza kufanya vizuri.
Mfano mzuri wa jinsi akili zetu zinavyoweza kutekwa na uhimara wa nembo hadi kila kitu ukajikuta unakitambua kwa jina hilo ni nembo ya ‘Shell’, hii ni miongoni mwa kampuni kubwa ya mafuta duniani inayomilikiwa kwa ushirikiano wa Wadachi na Waingereza, lakini hadi leo katika Tanzania kila anayeenda katika kituo cha mafuta anatamka anakwenda Shell ingawa ukweli wa mambo ni kuwa Shell haipo katika biashara ya mafuta Tanzania.
Hili linaonesha wazi kuwa mteja anaponunua bidhaa mara nyingi hanunui bidhaa ananunua nembo.Kibiashara nembo inafaida nyingi, ikiwemo urahisi wa utambuzi kwa mlaji na kuhimarisha marudio ya matumizi.
Ingawa kwa sasa ulimwengu unashuhudia kuibuka kwa nembo binafsi (own brand) kwa kampuni nyingi kubwa duniani, lakini bado mauzo ya nembo zilizobuniwa na kampuni husika kama vile Lee, Levis, bado yapo juu.Katika Tanzania mageuzi haya pia yapo ndiyo tuna dangirizi za KP,Tippo, na vyakula vinavyofungwa kwa majina ya Supermarkets kama Shoprite. Moja ya kampuni kubwa inayofanya vizuri kwa kutumia nembo yake na si za wazalishaji ni Mark Spencer wenye nguo zinazokwenda kwa jina la kampuni badala kuwa nguo kama Lee, Levi’s kama tulivyozoea.
Nembo ni msingi wa biashara na ndiyo maana kuna kampuni zinachaji gharama kubwa si kwa tofauti ya malighafi tu ni kwa vile nembo yao iko na thamani kubwa na yenye kuheshimika. Wataalamu wa mambo ya fedha na mitaji wanakadiria kuwa asilimia 70 ya mtaji wa kampuni iko katika nembo.
Kwa mfano kampuni ya Zain Tanzania mwaka 2007 ilitumia zaidi ya bilioni 5. 1 za kitanzania kwa ajili ya matangazo ya nembo yake tu, hii kwa mujibu wa gazeti la Advertising Age, la Desemba 8 mwaka 2008.Mfano huu unatuonesha wazi kuwa mara nyingi kampuni zinawekeza katika kutangaza nembo zao.
Makala haya itajaribu kujadili umuhimu wa Tanzania kama nchi kupigania haki yake kutoka kwa kampuni za kimataifa au za ndani zinazotumia majina ya vivutio vyetu vya asili nasi tupate sehemu la pato kutokana na mauzo.
Katika Tanzania leo hii kuna makampuni mengi yanayotumia Kilimajanro, Serengeti, Mikumi na kadhalika kama sehemu ya nembo zao kibiashara. Takwimu haziko wazi kama Tanzania inanufaika kutokana na kampuni hizi kutumia majina yetu ya kijiografia kama nembo zao za kibiashara nchi inapata chochote.
Ila mfano wa Ethiopia inaonesha wazi kuwa nchi nyingi za Afrika zinakosa pato kubwa kutokana na matumizi ya nembo zao za kijiografia kutumika nasi hatulipwi hata shilingi.
Wakisaidiwa kisheria na Oxfam; Ethiopia ilichachamaa na kufungua madai ya haki miliki katika Ofisi za Haki Miliki nchini Marekani, ikiitaka Starbuck kampuni kubwa ya kimarekani kufikiria kuipa stahiki yake kwa kutumia nembo ya eneo moja katika Ethiopia kwa bidhaa zake za kahawa inayozalishwa na Starbuck.Kilio cha Ethiopia ilikuwa kudai pato linalotokana na chumo la 'premium price' linalovunwa na 'Starbuck' kutokana na kuuzwa kwa kahawa hiyo katika mikahawa mbalimbali inayomilikiwa na Starbuck katika Ulaya na Marekani.
Starbuck inatumia majina ya Sidamo, Harar na Yirgaeteffe maeneo katika Ethiopia kama nembo ya kahawa yake. Ikimbukwe kuwa Sidamo ni mahali ambako inaaminika ni moja kati ya sehemu ambazo mbegu ya kahawa ya kwanza ilioteshwa na binadamu, hivyo eneo hili inaonesha kuwa ni sehemu nzuri na ipo katika vichwa vya walaji makini wa kahawa na ni wazi kuwa wataithamini kahawa yenye jina hilo kwa heshima ya kihistoria.
Na ubora wa Sidamo kama eneo unatumika na Starbcuk katika matangazo yake kuinadi kahawa yake.Kahawa yenye nembo ya Sidamo ikiuzwa hadi dola 26 kwa kilo huku wakulima wa Ethiopia wakiambulia dola moja tu ya chumo.
Baada ya vuta ni kuvute iliyoanza tangu Mei 2005, Starbuck ilikubali kuipa Ethiopia dola milioni 88 kama pato linalotokana na kutumiwa kwa maeneo yake kama sehemu ya nembo ya biashara.Oxfam iliuita ushindi huu kama ‘fair trade’ ya aina yake kwani wakulima masikini wa Sidamo nao watapata chumo lingine toka kwa kutumika kwa nembo ya eneo lao.
Katika chapisho, Regional Branding Marketing, Matthew Muntberg, anataja sababu moja wapo ya kufanikiwa katika kuchagua jina zuri la nembo ya kijiografia ni kutafuta sehemu yenye heshima ya ‘kipekee’. Hivyo wanaotumia majina yetu ya kihistoria na urithi wa nchi yetu kama nembo zao kibiashara wanatambua hili kuwa ni vitu vyenye mvuto na kuheshimika.
Tanzania ina bidhaa ambazo zinatumia majina ya vivutio, kama vile mlima Kilimanjaro, Serengeti kwa mbuga ya wanyama yenye heshima kubwa Duniani. Bidhaa hizi ni kuanzia maji, bia na hoteli za kisasa zenye kutumia majina yetu ya kijiografia.
Aina ya nembo za maeneo (Regional /geographical Brand) si kitu kipya duniani, kuna Idaho Commission kakika Marekani yenye zaidi ya miaka 70, ikisimamia wazalishaji wanaotaka kutumia nembo hiyo ya eneo kwa kuzalisha viazi mbatata kulipa, huku ikijikusanyia zaidi ya dola milioni 12 kama kamisheni, ya kutumika kwa eneo lao kama nembo.
Kutoza watumiaji wa nembo za kijiografia ni chanzo kingine cha mapato kilicho sahaulika katika Tanzania. Na hili litatupunguzia kutoza kodi watu walio na hali duni hasa wakulima wa nchi hii kwa kodi ambazo ni za kidhalilishaji huku kuna vyanzo wenzetu wameviona na wanavitumia.
Basi wakati umefika wa Tanzania kama nchi nayo ipate gawio kutoka katika matumizi ya vivutio vyetu kibiashara na si kuacha watu wachache wakinufaika na huku watu wengi waliozunguka maeneo husika wakitaabika. Ethiopia imeonesha njia, tujifunze kutoka huko.Shime wataalamu wa sheria.

Sunday, February 14, 2010

Elimu ya biashara na anguko la uchumi wa Ulimwengu

Anguko la Uchumi wa Ulimwengu limeleta madhara makubwa lakini lililowazi ni juu ya UBORA na UMAKINI kwa ujuzi unaotolewa katika shule za biashara DUNIANI.Katika Marekani swali lilikuwa juu ya majaaliwa ya elimu ya MBA (Masters of Business Administration). Katika Afrika Kusini kuna waliojiuliza kwa nini waafrika waende kusoma katika nchi ambazo zimeshindwa kuzalisha wasomi walioweza kulinda ‘msusuko’ huu.Yaani katika vyuo vya Marekani na Ulaya.
Pamoja na madai hayo bado MBA imekuwa ni elimu pendwa kwa sasa, hasa nchini Marekani kwani inakadiriwa watu wengi waliokosa kazi walirudi madarasani na wengi walirudi kusoma hizo elimu za biashara.Kampuni kubwa za kimarekani zilizoanguka zinaongozwa na wataalamu wa biashara kutoka vyuo bora kama vile Harvard, Stanford, MIT na kadhalika.
Makala haya haina nia ya kujaribu kusimulia nini kilichosababisha ‘msukosuko’ huu mkubwa wa kiuchumi duniani ulioanzia Marekani mwishoni mmwa 2007, ila tutajaribu kuangalia majaaliwa ya sekta ya Elimu ya Biashara katika Tanzania na nini tunaweza kujifunza.
Rais Barack Obama alipoingia madarakani aliendeleza mpango wa kunusuru taasisi za fedha na bima mpango ambao uliasisiwa na rais aliyemtangulia George Walker Bush Jr. Lakini mpango huu uligubikwa na utata wa matumizi yasiyorasmi ya malipo ya posho za maofisa wa ngazi za juu.
AIG (American Insurances Group), ilitumia dola milioni 165 kulipa posho ya maofisa wake. Hali hii ilifanya White House kuingilia kati na kuweka wazi kuwa haipo tayari kuona ‘bailout’ ikitumika kujilipa posho na malipo mengine manono ya maofisa wakuu wa benki na hasa katika kipindi hiki cha kupambana na anguko la Uchumi wa Ulimwengu.
Hili linaashiria kutokuwepo kwa umakini wa hali ya juu ambao unalalamikiwa na watu wengi duniani miongoni mwa watendaji wa sekta za fedha.Na hasa lililowazi ni hili la kukosekana kwa maadili, watu wachache wajilipe wakale ‘starehe’ ufukweni au kidogo kilichopo kitumike kwa ajili ya kulinda masilahi ya wengi!
Katika Marekani kuna walioenda mbali zaidi kwa kuikebehi elimu ya MBA kama ‘Masters of Disaster’. Ni wazi kuwa anguko la uchumi wa ulimwengu ni changamoto kwa elimu ya MBA na hasa shule za biashara duniani.
Kwa mwaka nchini Marekani pekee wahitimu wanaokadiriwa kufikia 100,000 uhitimu katika ’specialization’ mbalimbali za elimu ya MBA, huku asilimia 40 wakiajiriwa katika sekta ya fedha. Na sekta hii inasadikiwa ndiyo ‘chokochoko’ ya mdororo wa Uchumi ulikoanzia, pale maofisa walipokuwa wakikimbizana kutoa mikopo ili kupata ‘bonuses’ bila kujali uwezo wa mlipaji. Mikopo iliwafikia, NINJA (No Investment, No Job, No Asset) Hapo ndipo mtafutano ulipoanza, huku wakiwa na lundo kubwa la kadi wakitumia kwa mtindo wa ‘credit card’, hili lilipelekea ‘mkusanyiko’ mwingine wa madeni usiolipika kutoka sekta nyingine.
Pia kurunzi lilimulika ule utamaduni maarufu wa kuandaa mameneja, unaotambulika kama ‘Harvard Culture’. Msusuko huu wa uchumi unafanya kutimia kwa ubashiri wa Profesa Henry Mintzberg, mwanazuoni wa Masomo ya Uongozi, katika Chuo Kikuu cha McGill, Canada.
Profesa Mintzberg alipinga ‘utamaduni wa Harvard’ wa kumuandaa menejea darasani na aliweka wazi msimamo wake kuwa meneja siyo MBA, na kimsingi meneja bora anapaswa kunolewa huku akiwa anajifunza toka kwa waliomtangulia na situ kukabidhiwa wadhifa kwa msingi wa cheti.
Pamoja na yote hayo Ulimwengu umeendelea kushuhudia shule za Biashara na hasa elimu ya MBA ikipata wanafunzi wengi kuliko nafasi za udahili kama nilivyokwisha sema hapo awali. Ni wazi kuwa MBA inapendwa, na sokoni bado ipo juu.
Msususko huu wa kiuchumi umeshuhudia wasomi wa Harvard wakija na nadharia ya kuweka kiapo (oath) kwa wasomi wa MBA kuapa kukubali kulinda maadili ya biashara. Tunachojifunza hapa ni kwamba Ulimwengu wote sasa umetambua kuwa hangaiko hili la Uchumi limetokana na kukosekana kwa maadili miongoni mwa wafanyakazi wa taasisi za fedha. Hili likafanya wawe wasiri ingawa taasisi zao zilikuwa zinaanguka.Ndiyo hayo ya Ponzi Scheme!
Tanzania si kisiwa, nayo elimu ya MBA inashamiri kila kukicha vyuo vikuu vingi kwa sasa vinatoa elimu ya MBA.Huku,Mzumbe University mwaka jana ikiwa na wahitimu wanaokadiriwa kufikia 400 wakihitimu katika ‘Campus’ ya Elimu ya Biashara ya Dar-es-Salaam, pekee. Huu ni mwanzo mwema.
Lakini tunapaswa kujiuliza kama tunachokifanya darasani kuwaandaa viongozi wa biashara katika misingi ya kulinda ‘masilahi ya taifa’ au bado tunawafundisha wanafunzi ‘michakato’ ya biashara. Wanazuoni Leonidou na Kaleka wanaweka wazi kuwa elimu ya biashara kwa kiasi kikukwa imeweka msukumo katika, mbinu(strategy) mifumo na michakato badala ya ‘kufinyanga’ watu (1998)
Tanzania ya leo imekumbwa na rushwa katika sekta ya biashara huku ushindi wa rushwa kwa kupata ‘tenda’ ndiyo yamekuwa mambo ya kawaida.Sasa tunarudishiwa zaidi ya bilioni 30 za kitanzania kutokana na kashfa ya rada, Mheshimiwa Membe anaita chenji yetu!
Lakini hii ni changamoto kwa shule ya biashara, yatupasa kuandaa wasomi watakao ona kuwa kujihusisha na rushwa na kutojali masilahi ya watu wengi si jambo jema. Hapa ndipo suala la elimu ya maadili ya biashara linapoibuka.
Katika makala ya kisomi, ‘Challenges faced by business schools within newly founded catholic universities: the case of Tanzania, Mtawa (Sister) Dokta Helen A Bandiho, pia ni Mkuuwa wa Kitivo cha Biashara cha SAUT,Mwanza; anataja kuwa jukumu la shule za biashara ni kujenga jamii yenye viongozi wa biashara waliotayari kulinda masilahi ya taifa kwa kupigania masilahi ya wengi.
Akionya juu ya rushwa, ‘usiri’, matumizi mabaya ya mali ya umma,upendeleo katika zabuni havina mwisho mwema kwa shule za biashara.Hii ndiyo changamoto kubwa kwa shule za biashara kwa sasa katika Tanzania na ulimwengu kwa ujumla. Katika Tanzania ya leo huwezi kufanikiwa bila kuwa ‘network’ isiyorasmi katika biashara!
Network ya aina hii haina mwisho mwema kwani wasio na sifa ndiyo wanapata kazi na tenda, huku walio na sifa wakikata tamaa.Mara zote huwa ni majuto ambayo makala haya ikiyaorodhesha yatajaa kurasa. Mbaya zaidi wale waliotayari kuongeza bei ‘quote’ ndiyo wanaonekana kuwa wajanja, huku nchi ikiteketea. Hela zinazojenga vyumba vya madara kumi shule binafsi shule ya serikali ni vyumba viwili tu na haviishi! Hii ni hatari.
Tunahitaji kuhimarisha shule za biashara kwa kufundisha maadili ya biashara kwa kuwaandaa wanafunzi kupambana na rushwa, huku wakiwa tayari kuchukua madaraka ya kutoa maamuzi. Ingawa itaweza kutolewa hoja kuwa maadili ni suala la mtu binafsi na alivyofunzwa akiwa na familia yake.Hii ni sawa.
Lakini bado shule ya biashara ina nafasi kubwa katika kubadilisha kwa ‘kufinyanga’ wasomi wenye maadili na waliotayari kutetea masilahi ya taifa katika kila nafasi ya uongozi watakayokabidhiwa.
Kwa sasa katika Tanzania vyuo vingi vinavyotoa elimu ya biashara havina elimu ya maadili (business ethics) isipokuwa ni IFM tu waliokuwa na kozi hiyo tena kwa Shahada ya MB-International Business wanayoitoa kwa pamoja na Taasisi ya Biashara za Nje ya India.
Katika vyuo vingi kuna waliobuni Business Ethic and Law kama kozi, lakini lazima ifahamike kuwa ‘business ethics’ siyo sheria, ila ni elimu ya kumpa mwanafunzi uwezo wa kung’amua mema na mabaya, ingawa sheria inaweza ikawa inakupa nguvu.
Kwa mfano hakuna sheria itakayo kubana ukiwa unataka kufungua bar au kioski cha kitimoto karibu na msikiti. Lakini kimaadili hili si sawa. Ndivyo hivyo tunaona mifano mingi ambayo kama watoa maamuzi katika sekta ya biashara wangeweza kupata msasa kuhusu elimu ya maadili wasingaliweza kufikia maamuzi wanayoyapinga leo.
Msusuko wa Ulimwengu umefanya Harvard kufikiria kuweka kiapo kwa wasomi,wa biashara, basi yatupasa nasi kufikiria kufundisha maadili ya biashara, kwani mashaka yetu ya ubadhirifu wa mali ya umma, rushwa, upendeleo na mengine ya hovyo yanachangiwa na kukosa maadili.
MUNGU IBARIKI TANZANIA,
MUNGU IBARIKI AFRIKA.

Sunday, February 7, 2010

Tunachojifunza kutokana kupanda kwa bei ya mchele duniani

Mchele unaozalishwa kwa asilimia 90 katika bara la Asia, ni asilimia saba tu huingia katika biashara ya Ulimwengu. Ulimwengu bado unakumbuka hofu ya kitisho cha chakula ilivyopandisha bidhaa hii, huku ikifanya baadhi ya nchi kama Philippines kukosa shehena aliyoihitaji pamoja na dau kubwa la dola 680 kwa tani wauzaji na ‘waroho’ wa pesa walikataa kuiuzia tani 500,000 alizohitaji.
Tangu Januari 2008 biashara ya Ulimwengu ya chakula imekumbwa na msusuko wa kupanda kwa bei, huku mchele ambao ni chakula cha watu wengi walio masikini katika Asia ukipanda maradufu.Hali iliyofanya kuleta hofu zaidi miongoini mwa wa jamii ya kimataifa.
Kwa sasa bei ya mchele inaonekana kushuka kwa mujibu wa takwimu za FAO. Lakini Idara ya chakula ya Marekani inaonya kuwa hali bado ni ‘tete’ hasa kwa mchele na bei yake kutengemaa katika siku za karibuni.
Tanzania si muagizaji mkubwa wa mchele katika Afrika, lakini umuhimu wa zao la mchele kutoka Asia hakuna asiyeujua katika nchi hii. Mchele umekuwa siyo chakula kikuu hivyo kufanya mara zote iwe ni kimbilio letu wakati wa njaa.Mchele kutoka Thailand na Vietnam huwa ndiyo chakula mkombozi wetu wakati wa njaa.Kuna aina maarufu kama kitumbo na V.I.P ni aina ya Indica, wenye thamani ndogo katika soko la dunia.
Bei ya mchele ya ulimwengu inaonakana kuwa tata, kwa vile kuna madai kuwa India imeanza kupita kupita kwa nchi wazalishaji huku ikitangaza kuhitaji shehena ya mchele. Hii ni dalili ya wazi kuwa kitisho hiki cha India kuna jambo laja.
Ripoti ya FAO, Food Outlook, 2009, inabainisha wazi kuwa, India ipo sokoni ikiwa inavizia maeneo ya kununua mchele. Nia ikiwa kuongeza shehena yake ya mchele kwa tani milioni 9 zaidi. Ingawa haikuwa na uhakika juu ya madai ya kupipita kwa India katika kutafuta wauzaji wa mchele.Biashara ya Ulimwengu ya mchele inakadiriwa kupanda kwa tani 800,000 zaidi ya mwaka jana.
Wadadisi wa biashara ya mchele duniani wanabashiri wazi kuwa mahitaji ya ulaji ya mchele yanakadiriwa kupungua katika Asia.Lakini wanaonya kuwa kupungua kwa ulaji kwa jamii za Uchina, Thailand, India, Korea na Japan haimaanishi kuwa mchele utapungua bei kwa vile umekosa walaji.
Ila kitakachotokea ni kwamba uzalishaji wa mchele utapungua, kutokana na ukweli kuwa mashamba mengi yananyakuliwa kwa ajili ya ujenzi wa makazi kutokana na ukuaji wa miji mingi katika Asia.
Ukuaji wa miji unakadiriwa pia kuchochea ujenzi wa viwanda na barabara hali ambayo shirika la Utafiti wa mchele (IRI) lenye makazi yake Phillipines; linaelezea kuwa itapunguza ardhi kwa kilimo cha mpunga.
Pia kuna taarifa kuwa kuimarika kwa kipato cha familia kutapunguza walaji wa mchele, hali inayokadiriwa kuchangiwa mno na mafanikio ya uzazi wa mpango katika nchi nyingi za Asia ya Kusini na hasa Uchina.
Ukuaji huu wa chumo la familia unapelekea familia nyingi kubadili iana ya chakula, basi hili linajionesha wazi na kurufurika kwa maduka ya makubwa ‘supermarkets’ kutoka magharibi katika nchi hizi. Maduka kama Tesco, Asda, Mark Spencer Spencer na WalMart, wauzaji wa ‘fast food’ McDonalds, Kentucky Fried Chicken, StarBuck na kadhalika. Jamii ya Asia ya leo si walaji mchele tena, bali hupenda kula zaidi vyakula vya 'magharibi’
Mabadiliko ya chakula yanapeleka mbinyo tena katika ardhi iliyokuwa inatumika kulima mchele, sasa hutumika kulima mboga mboga , matunda, kukidhi mahitaji na mabadiliko ya jamii za Asia.
Mwenendo huu wa matumizi ya mchele katika Asia yanatufanya tujiulize juu ya siku za baadaye kwa Afrika ambayo hutumia Asia kama kapu lake la chakula wakati wa njaa?
Katika Afrika waagizaji wakubwa wa mchele ni Nigeria ambayo huagiza asilimia 6 na Senegal asilimia 4 ya mchele unaoingia katika soko la Ulimwengu, huku maeneo mengi yakiwa si walaji wakubwa wa mchele hadi ukame au kitisho cha njaa ndipo hukimbilia katika masoko ya Asia.
Tanzania ni miongoni mwa nchi ambazo si walaji wakubwa wa mchele, chakula kikuu ni mahindi. Pamoja na hayo lakini lililowazi ni kwamba mchele kutoka Asia ni mkombozi wa njaa katika Tanzania.
Indica, ni aina ya mchele ambao ni wenye kiwango cha chini cha ubora ukiwa umevunjika kwa asimilia 25, mara nyingi ulikuwa umeonekana kukosa soko lakini hali ya mambo hadi mwanzoni mwa Januari mwaka huu, ilionesha kuwa mchele huu utapata wateja, hii ni baada ya Philippines kuinngia sokoni akiwa ananunua aina hii ya mchele.
Lakini lililowazi ni kwamba hali ya bei ya biashara ya mchele inatarajiwa kupanda Ulimwenguni. Asia ikiwa mlimaji mkubwa wa mpunga, ndiyo pia kuna walaji wakubwa, lakini nchi nyingi za eneo hilo zimeweka vikwazo kwa biashara ya mchele kwa kuweka kodi ya mauzo ya nje na hata kuzuia kwa hofu ya kutokea upungufu wa chakula na kuathiri raia wengi walio maskini.
Tunachoweza kujifunza kwa mwenendo wa biashara ya mchele, Afrika inahitaji kuongeza nguvu katika kilimo cha chakula. Tangu azimio la Maputo kupitishwa kwa nchi za Afrika kuweka bajeti ya asilimia kumi katika kilimo ni nchi chache zimeweza kufikia lengo hili.
Hali ya mambo katika Asia, ambako mchele unalimwa inaonekana kubadilika mno, hasa kutokana na ukweli kuwa ‘style’ ya ulaji imebadilika na kufanya jamii nyingi za huko kupenda kula vyakula vya magharibi,hiki ni kitisho kwa Afrika.
Ingawa mabadiliko haya kasi yake kitakwimu hazipo wazi, lakini ongezo la maduka makubwa ya magharibi na kuongezeka uzito kunakosabishwa na ulaji wa ‘junk food’ ni dalili kuwa sasa Asia inaondoka katika kula mchele kama chakula kikuu.
Afrika haina budi kujipanga, katika kuhakikisha inalisha jamii ya watu wake, kwani kwa sasa hali ya uhakika wa chakula na biashara ya chakula duniani imebadilika mno.
Tuchague moja, kulima mau na viepepeo au kulima mazao ya chakula. Jibu tunalo waafrika wenyewe. Profesa Steve Carter na Dr Kiefer Lee, wanaonya juu ya hatari ya kufikiria zaidi soko la nje na kujitahidi kukidhi mahitaji ya soko hilo, katika kitabu Global Marketing Management wanaandika ‘biashara hii itakuwa haina maana kama chumo lake na zaidi litakwenda tena katika kuagiza kitu ambacho nchi inahitaji zaidi’
Ni wazi kuwa Afrika inahitaji zaidi chakula kuliko chumo hilo la vipepeo au maua, ambayo hata soko la ndani hakuna anayevitumia. Kenya sasa inahaha kuhamasisha matumizi ya maua kwa soko la ndani; kwani asilimia 96, hutegemea soko la nje. Ni wazi kuwa ‘ndoto’ hizi haziwezi kutimia, kwani maua si hitaji la wakenya.
Vinyo hivyo kwa nchi nyingine za Afrika ya joto tumejikuta tunaingia katika mtego kama huu, wa kuhangaika kufikia matarajio ya soko la Ulaya wakati, faida ya huko kimsingi baada ya muda inarudi tena na ziada inahitajika katika kununua chakula.
Hatumaanishi kuwa hii biashara ni mbaya, lakini yatupasa kulinganisha na kutambua mahitaji yetu je yametimizwa? Basi tuweke nguvu katika kilimo cha mazao ya chakula na tuache ‘ushabiki’, kwani hakuna mgeni atakaye kuja Afrika kuja kulima mpunga.