Monday, March 29, 2010

Ushirika na maajaliwa ya ‘Fair Trade’ katika Tanzania

Tanzania ni nchi ya kwanza Kusini mwa Jangwa la Sahara kuingizwa katika mpango wa ‘FAIR TRADE’(biashara huru), ila makala haya itatumia neno 'fair trade' moja kwa moja. Mpango huu ambao ulianza mwaka 1988 kupitia kahawa, kwa sasa unahusisha pia chai na samani hasa zenye kurembwa kwa shanga.
Kagera Cooperative Union (KCU) ni chama cha kwanza kunufaika na ‘Fair Trade’, kwa kuanza kuuza kahawa yake katika masoko ya Ulaya na Amerika. Kimsingi mpango huu umejikita katika nadharia ya kuwapa nguvu wakulima masikini wadogo wa nchi changa kuweza kufikia masoko ya Ulaya, huku wakinufaika kwa kazi ya jasho lao, kwa kulipwa bei nzuri ambazo ni zaidi ya bei ya soko la dunia.
Baada ya manufaa ya mpango huu kwa sasa nchini Tanzania vyama vya ushirika kama Karagwe District Cooperative Union, Kilimanjaro Native Cooperative Union pia wapo katika kuuza kahawa. Pia wafanyakazi wa mashamba ya chai katika Kibena ana Luponde Iringa na Lushoto, Tanga wapo katika mpango huu. Pia kuna mau yanayouzwa na kampuni ya Kiliflora ya Arusha kwa kutumia nembo ya 'Fairtrade' yakiwa chini ya Max Havelaar nembo inayoratibu masoko ya Uholanzi, Ubelgiji na Ufaransa.
Ili kufanikisha mpango wa fair trade ushirika imara ni muhimu kwa uhakika wa soko na mgawo wa pato la mauzo. Ushirika ndiyo kiunganishi kati ya wanunuzi na wakulima. Na hili la kuundwa kwa ushirika imara ni moja kati ya masharti makubwa ya kuweza kusajiliwa kama mzalishaji wa kahawa chini ya mpango wa 'fair trade'. Kwa wamiliki wa mashamba makubwa ya chai moja ya masharti ni kuundwa kwa vyama vya wafanya kazi huru vikiundwa na wafanyakazi wakipata hali bora kama huduma za kiafya na elimu kwa ajili ya watoto wao kutokana na chumo la 'Fair Trade'.
Mpango wa Fair Trade unashika kasi katika Afrika, Uganda na Malawi zinauza sukari, Kenya na Afrika Kusini zikijikita katika chai.Ingawa Tanzania ni mmoja kati ya wakongwe katika nchi za kusini mwa Jangwa la Sahara lakini ushiriki wake unaonekana kupungua. Na hii si kama bei ya kahawa au chai inaonekana kutengemaa sokoni la hasha.
Kwa mujibu wa mtafiti Profesa Fautini Karani Bee katika chapisho Fair Trade- Fair Future anabaisha wazi kwamba mauzo ya chama cha KNCU ya kahawa katika mpango huu, ni milioni 105, 069, 272, kwa mwaka 2008 wakati mwaka 2004 yalikuwa 175, 320, 894. Pato hili ni ile pesa ya ziada ambayo walaji wa Ulaya na Marekani wako tayari kulipa, achiliambali bei ya zao husika kuwa ipo juu ya bei ya soko.Ni wazi kuwa ushiriki wetu unalegalega.
Fair Trade imaleta hali bora kwa wakulima wadogo wa Tanzania , kuna wanafunzi zaidi ya 250 wamepata udhamini wa kupata elimu ya sekondari kupitia mpango uliobuniwa na chama cha KNCU. Pia washirika hawa wameweza kununua hisa katika Kilimanjaro Cooperative Bank.
Upepo wa mafanikio pia unavuma kwa washirika waliochini ya KCU ambao wameweza kununua hisa za kiwanda cha kahawa cha Kagera. Haya na mambo mengine mengi ni mafanikio ya juu wakulima wameweza kujipatia kupitia mfapongo huu.
Changamoto za Fair Trade katika Tanzanai ni nyingi , miongoni mwa hizo ni ukosefu wa vyama vya ushirika imara. Vyama vya ushirika ndiyo nyenzo ya Fair Trade, hivyo kufanya juhudi zote za kuondoa walanguzi sokoni kutegemea vyama hivi.
Wakulima wa Tanzania wamedhalilika na kuoenewa sana na vyama vya Ushirika. Ushirika umekuwa ni mzigo mzito kwa wakulima wa Tanzania. Ingawa ni kweli kuwa hakuna kesho bila kuwa na ushirika na hasa kwa wakulima wadogo na masikini wa Tanzania. Inashangaza ni kwanini serikali imekuwa na kauli nyingi bila vitendo!
Mtafiti Pirotte (2006) katika tafiti ‘Fair-Trade coffee in Nicaragua and Tanzania: a comparison’ iliyochapwa katika jarida la kisomi la Development in Practice , chapisho la 16 namba 5 anabainisha wazi kuwa wakulima sasa katika Tanzania, wamefikia hatua ya kuona FAIR TRADE, ni sawa na wafanyabiashara wengine (walanguzi), lakini hili limechangiwa zaidi na mwenendo wa ushirika. Ni wazi kuwa aliyeumwa na nyoka akiona unyasi atastuka. Maoni hayo yanaonesha wakulima walivyo kata tamaa na Ushirika hivyo lolote lilillochini yake ni wazi kuwa ni ulaghai!
Ni wazi kuwa mwenendo wa ushirika hauridhishi na wenye kuhitaji kurekebishwa ili kufikia lengo la kuwanufaisha wakulima wa Tanzania.
Hivi karibuni Waziri Mkuu M.K. P Pinda na Waziri wa Kilimo J. Wasira kwa nyakati tofauti wakiwa ziarani Japan na Vietnam wamesikika wakiweka wazi juu ya umuhimu wa ushirika imara kwa masilahi ya wakulima wa Tanzania.
Hili la kilio cha kukosa ushirika imara si jambo jipya. Ni kilio cha muda mrefu, na wala kauli za viongozi wetu katika kuhimiza ushirika imara si mpya pia.
Kauli za viongozi ni sahihi lakini zinahitaji vitendo katika kuwajengea wakulima imani dhidi ya ushirika na hili la Fair Trade linaonesha wazi jinsi tunavyochezea shilingi chooni.
Hali ya mambo inaonesha wazi kuwa kukosekana kwa ushirika imara Tanzania iko hatarini kupoteza nafasi yake katika kufikia masoko ya Marekani na Ulaya kupitia mpango huu. Mtafiti Paul Attontile anabainisha wazi kuwa mapungufu ya watendaji na viongozi wa ushirika yamewafanya hata wanunuzi wa kahawa chini ya mpango huu kufikiria kama kuna namna nyingine ya kuwafikia wakulima wadogo wa Tanzania.
Wakati Tanzania inalega lega kutumia nafasi hii, lakini nchi nyingine wao wako wanapambana kuongeza ushiriki wao kwa kusajili bidhaa nyingine mpya zilizoingizwa chini ya mfumo huu, kama vile asali, ndizi, nguo za pamba na bidhaa za mikono.
Mauzo ya sasa duniani kote ni zadi paundi 1.6 bilioni ukijumalisha masoko ya Ulaya na Amerika. Ingawa biashara ya Fair Trade ni wastani wa asilimia 1 ya biashara ya ulimwengu, lakini lenye kutia moyo ni kukua kwa kasi kwa biashara ya mauzo ya huku Itialia ikukua kwa asilimia 404 na Uingereza asilimia 72.
Walaji pia wa masoko ya Ulaya wako tayari kununua bidhaa zenye kujari masilahi ya wakulima masikini wa Kizio cha Kusini kwa zaidi ya asilimia 70. Mwenendo huu wa walaji na soko unaonesha kufanikiwa kwa mpango huu katika kulifikia soko na ‘kukuna’ nyoyo za walaji za ‘Trade not Aid’
Tuimarishe ushirika, kwani majuto ni mjukuu na Fair Trade imeonesha wazi kuwa inamwisho mwema kwa wakulima wa Tanzania, basi tusichezee shilingi chooni, shime viongozi wetu maneno matupu hayavunji mfupa.

Changamoto ya mitaji toka nchi zinazoendelea

Ripoti ya mwenendo wa uwekezaji (World Investments Report) ya shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulika na Biashara na maendeleo (UNCTAD), ya mwaka 2009 inataja nchi zinazoendelea kuwa zimeweza kuhimili hali mbaya ya Uchumi wa Ulimwengu kwa kuweza kupata asilimi 27 ya mitaji toka nje (Foreign Direct Investments). Ingawa kiwango hiki ni cha chini ukilinganisha na mwaka 2007 lakini ni hali yenye kutia moyo.
Jumla ya dola za kimarekani bilioni 88 zimekezwa katika Afrika, kwa mwaka 2009 pekee, pamoja na mafanikio hayo bado miradi mingi toka nje ilishindwa kuendelezwa kutokana na heka heka ya kuyumba kwa uchumi wa Ulimwengu.
Eneo la Afrika Mashariki lilijizolea shilingi bilioni 4, ikiwa ni eneo lililopata mgao mdogo kwa muda wa mwaka wa pili mfululizo. Pamoja na hali hiyo mitaji toka nchi zinazoendelea imeendelea kumiminika Afrika, wawekezaji wakubwa kutoka nchi masikini ni Uchina, India na Afrika Kusini. Huku Uchina ikijikita katika usakaji wa rasilimali ya mafuta katika Angola, Sudan na Nigeria, bila kusahau miradi mikubwa ya ujenzi katika Kongo-Kinshasa na Afrika Magharibi, pia Afrika Kusini ikifanya vyema katika uwekezaji wa madini katika Tanzania kwa kufanikiwa kununua hisa za Ghana na ikisambaa katika ufunguzi wa maduka ya rejareja (supermarkets) toka Nchi za SADC had ECOWAS, bila kusahau ufunguzi wa mabenki.
Wawekezaji wakubwa wa mitaji katika Tanzania ni Afrika Kusini, Kenya, Uchina, India, Pakistani, Mauritius na Malaysia. Lakini tangu ujio wa wawekezaji hawa mara zote imekuwa kilio katika hali ya uchumi wa Tanzania. Toka wafanyakazi, wafanyabisahara na viongozi wetu wetu wa kitaifa.
Wakati fulani Raisi Kikwete akiwa ziarani nchini Japani aliwahi kunukuliwa na vyombo vya habari akiwaasa wajapani wasiwape kazi za kusimamia mitaji yao wahindi na wapakistani kwa vile ‘wanawapunja’ watanzania.Pia Waziri Mkuu M. Pinda aliwahi kunukuliwa na vyombo vya habari akiwaambia wahandisi wa kichina mkoani Arusha kuwa wanakosa vijana wahandisi wa kufanya nao kazi katika kampuni zao kwa vile wanawalipa mishahara midogo. Hivi ni vilio vya kila siku
Katika Tanzania, nchi zinazoendelea zimewekeza kwa wastani wa asilimia 47, hivyo wawekezaji hawa kutoka nchi hizi ni nguzo muhimu katika mageuzi ya uchumi wa Tanzania. Tukitumia takwimu za idadi ya mitaji, Kenya mara zote uhibuka kama muwekezaji namba moja lakini kwa thamani ya pesa Afrika Kusini ndiyo muwekezaji mkubwa katika Uchumi wa Tanzania.
Mitaji toka nchi zinazoendelea imejikita katika maeneo mawili masoko na kiu ya utafutaji wa malighafi kwa viwanda vyao vya nyumbani. Hii ni changamoto kubwa kwa siku zijazo za majaaliwa ya Tanzania na ukuaji wa uchumi na ustawi wa jamii yake.
Lengo kuu la kuhimiza mitaji toka nje na kufanya mabadiliko makubwa ya kiuchumi tangu miaka ya 1980 ilikuwa ni kupata ahueni ya kiuchumi na kimaendeleo kwa jamii yetu. Swali la msingi ni je hawa wawekezaji wa kizio cha kusini wana mwisho mwema katika lile lengo letu?
Makala haya itajaribu kukusanya vipande vipande kuelekea ukweli. Kwani tunaamini uwekezaji ni muhimu kwa ukuaji wa uchumi wa Tanzania ila yatupasa kuangalia na kujali masilahi yetu kama nchi na basi lengo kuu ni kujaribu kukumbushana hasa juu ya mwenendo wa uwekezaji wa siku za karibuni uliojitokeza na makampuni toka Kusini.
Na wala isieleweke kuwa tunataka kutia chumvi au tunapinga harakati za mageuzi ya uchumi la hasha, lengo ni lile lile kujenga Tanzania yenye neema na heshima kwa wananchi wake.
Tunapotupia jicho wawekezaji toka kusini haiimaanishi kuwa wawekezaji wa kasikazini ndiyo wazuri la hasha ila yatupasa kujadili hali ya mambo katika misingi ya makundi ili walau tujue wapi tunakwenda kwa kuzingatia kile tunakichokiona kulingana na matarajio yetu.
Kwa sasa Tanzania ipo katika hali ngumu ya kujaribu kufuta hali ya sura yake katika biashara ya kimataifa, baada ya RITES wakezaji katika sekta ya usafiri mkataba wake kusitishwa. RITES ni kampuni ya India, ni wawekezaji toka nchi zinazoendelea.
Huu si mktaba wa kwanza Tanzania kuufuta, kuna mkataba wa awali ambao nchi iliuingia na wawekezaji toka Uingereza Biwater na wakashindwa kufanya kazi nao ulifutwa , huku Biwater ikienda mahakamani na kushindwa na ikitakiwa kulipa paundi milioni 8 kwa serikali ya Tanzania.
Lakini lililowazi ni kwamba hatujifunzi somo, na kwa sasa kuna hali ya kuendelea kwa yale yale yaliyopita kwa Biwater ndiyo yametokea kwa RITES. Labda tuweke wazi kuwa hili la RITES lilionekana toka mapema kwani mwekezaji mwingine GAPCO aliyepewa hisa bila hata kuwa na mtaji alidumaza jitihada za kufufufua shirika hili, kwani uwepo wa GAPCO ulifanya IFC kusita kutoa pesa za mkopo dola milioni 44, kwa hoja kuwa huyo aliyepewa hisa, GAPCO, ni mdeni wa IFC hivyo kuna ulakini kama hatua hii itaenda sawa kama ikipewa tena dhamana ya deni la dola milioni 44!
Kutokana na GAPCO kukumbana na kigingi cha IFC, serikali ikaingia kuwa mbia na RITES bila maandalizi.Ni wazi kuwa hatua hii ilichangia kwa kiasi kikubwa kuyumba na kupungua imani miongoni mwa wafanyakazi kwa RITES. Katika mchakato huu kuna mwekezaji mwingine toka India aliyekuwa na wastani wa hisa mbili alijitoa! Bila shaka maji yalizidi unga waswahili wanasema naye aliweza kubashiri vyema.
Hili la RITES si la kwanza ila inaonekana hatujajifunza somo hasa inapokuja wawekezaji toka Kusini, kwani mwaka 2007, Brookside kampuni ya Kenya ilinunua kwa mbwembwe kiwanda cha kusindika maziwa cha Arusha na kuahidi kufanya uwekezaji wa dola milioni 100, katika sekta ya maziwa. Lakini kilichokuja kushuhudiwa ni Tanzania kugeuzwa kuwa shamba la malighafi na uzalishaji unafanyika Kenya.
Mwaka jana ndipo waziri mwenye dhamana ya Afrika Mashariki Dk.Deodorus Kamala alipoifukuzilia mbali Brookside. Ingawa sura ya Tanzania imechafuka lakini liliwazo kuwa hawa wawekezaji toka nchi zinazoendelea mara zote wamekuwa ni wajanja wajanja na wanafanikiwa kwa gia ya kuonekana kama watu wanaoweza kustahimili hali ngumu za miundo mbinu ya Afrika lakini mwisho wake ndiyo haya.
Wawekezaji toka kusini kila wanapowekeza kila wakati imekuwa ni vitendo vya malalamiko na manung’uniko nchini. Hivi karibuni kuna wawekezaji katika sekta ndogo ya ngozi wenye asili ya India na Pakistani kuwa hawapo tayari kuongeza thamani ya ngozi katika viwanda vya ndani na badala yake wanasafirisha ngozi ghafi kwao!
Hilo likiwa halitoshi Ripoti moja ya FAO inataja kuwa kuongezeka kwa vyakula toka nje ya Tanzania ni kwa sababau wawekezaji katika sekta ya utalii na hasa hoteli huagiza vyakula toka nje huku vikiweza kupatikana Tanzania.
Hivi karibuni Waziri Ngeleja amenukuriwa na vyombo vya habari kuwa wawekezaji katika migodi waache kununua nyama nje ya Tanzania badala yake wanunue nyama Tanzania ili tuongeze tija katika viwanda vyetu vya ndani na kuongeza ajira. Katika sekta ya nyama kuna SAAFA ya Rukwa na Tanzania Meat Pride Morogoro. Hatua ya muheshimiwa Ngeleja, ni rai njema sijui katika vitendo itakuwaje, ni suala la kusubiri na kuona, ila ni mwanzo mwema.
Kila kitu sasa tunaagiza toka nje huku ndani kuna wajasiriamali wadogo waliowekeza katika kilimo na usindikaji wakitaka kupata hizo kazi tunapewa hoja chakavu kuwa minofu yao haina viwango mara minofu ya kuku ina harufu ya dagaa!
Bila mabadiliko ya kisera katika kuhakikisha wawekezaji wanatumia bidhaa za ndani ni wazi kuwa tutabakia kuwa watazamaji. Kuna nchi zimeweka wazi kuwa mwekezaji anapaswa kufanya nini anapoingia nchini na asilimia ngapi ya malighafi anayotumia inapaswa kutoka soko la ndani.
Bidhaa wawekezaji wa ndani wanaikataa lakini inapenya na kufanya vyema katika masoko ya Ulaya, tena ikisifiwa kuwa na viwango bora. Kuna mifano mingi ya bidhaa za kilimo zinazofanya vyema Ulaya lakini nyumbani hazina nafasi!
Tusibwete katika ‘kulainisha’ mambo kwa kigezo cha kuvutia mitaji. Hili la kuwa na wachuuzi wa Kichina Kariakoo, Kenya majirani zetu tangu miaka 1960 wameweka wazi kuwa mwekezaji wa nje hapaswi kuingia katika sekta ya’ juakali’. Lakini Tanzania hapana.
Niliwahi kuhudhruia ‘carrier workshop’ ya moja ya benki katika Tanzania, wakati wa majadiliano kuhusu mishahara Mkurugenzi wa Benki alieleza wazi kuwa hataweza kulipa zaidi ya mshahara wa serikali. Kigezo alichotumia ni kuwa serikali inawalipa wenzenu TGSD, tena wenye shahada kama nyinyi!
Kumbe katika malipo ni sisi ndiyo tumejimaliza na hakuna mchawi ila ni serikali kuwa na viwango vidogo vya mishahara na wageni wakija wanaangalia ‘skeli’ za serikali nao wanatumia kigezo hicho hicho katika hali kama hii ni vigumu kuona mitaji kutoka nje ikiwaneemesha watanzania.

Friday, March 19, 2010

Bravo TRA

BRAVO TRA kwa kufuta kodi ya silimia 18 ya VAT kwa wauzaji wa mboga mboga nje ya nchi.Hakika huu ni mwendelezo wa mwanzo mpya tuliwahi kuandika juu ya hili, januari 4 mwaka huu.KUpitia gazeti la serikali Daily News la tarehe 18.03.2010, Kamishna wa kodi amefuta kodi ya VAT ya asilimia 18.
Kila la heri wakulima na wajasiriamli katika sekta ndogo ya mbogamboga na maua.

Monday, March 15, 2010

‘Food miles’ changamoto kwa biashara ya chakula toka Afrika

Mabadiliko ya tabia nchi na hali ya hewa Duniani yanaendelea kufanya wanasayansi kufikiria njia za kupambana na madhara yake kwa kila namna. Inakadiriwa watu 800,000 wamepoteza maisha na jumla ya dola za kimarekani trilioni 1 kama hasara jamii ya ulimwengu huu imeipata kutokana na mabadiliko hayo ya hali ya hewa ya ulimwengu.
Katika nchi za Ulaya na Marekani nadharia inayochipua kwa kasi na kuungwa mkono na wakulima wengi ni ‘food miles’ huku wakipiga chapuo ‘local is good’. Nadharia ya food miles iliyochomoza kwanza Uingereza sasa inaonekana kupendwa pia na wakulima na taasisi zinazotoa mikopo katika Marekani.
Food miles ni nini?(nitalitumia neno hili kama lilivyo kwani sina neno zuri la Kiswahili),hii ni nadharia rahisi inayozingatia umbali kwa kupima madhara ya uharibifu wa mazingira yatokanayo na uzalishaji wa chakula toka shambani hadi mezani kwa mlaji. Hivyo walaji wanashauriwa kususia vyakula vilivyo safiri umbali mrefu kwa lengo la kulinda mazingira, yanayochafuliwa na hewa ya ukaa(KABONIDAYOKSAIDI), na badala yake watumie vyakula vilivyozalishwa nchini kwao ambavyo mfumo wake wa uzalishaji na usambazaji ni wenye umbali mfupi!
Nadharia hii iliibuliwa miaka ya 1990 na Profesa Tim Lang ambaye kwa sasa ni mhadhiri katika City University London. Tangu wakati huo kama tulivyo sema hapo awali wakulima wa Kiingereza na Marekani kupitia vyama vyao wamekuwa wakihimiza utumiaji wa bidhaa zandani (Local is good) kwa hoja ya kulinda na kupunguza uharibifu wa mazingira.
Uingereza moja kati ya masoko mazuri ya bidhaa za kilimo katika Jumuiya ya Ulaya, inakadiriwa kutumia paundi milioni 105 kwa ajili ya ununuzi wa mboga mboga na milioni 89 kwa matunda kutoka Afrika ya Kusini mwa Jangwa la Sahara.
Ni wazi kuwa kushika kasi kwa nadharia hii katika biashara ya chakula kunahatarisha hali ya jamii ya wakulima wadogo masikini wa kizio cha kusini na hasa Afrika. Ingawa mpaka sasa wanasayansi wanasema kuwa mchango wa Afrika katika kuchangia uharibu wa hali ya hewa ni mdogo. Afrika inakisiwa kuchangia asilimia 0.5 ya gesi ya ukaa na bidhaa zinatoka eneo husika hulimwa kwa njia za kijadi (jembe la mkono, plau, mbole ya samadi, bila hata kutumia dawa za kuulia wadudu)
Kimsingi huu ni mwendelezo wa kuonesha wazi kuwa soko la Ulaya lilivyo kigeugeu na wala siyo la kuaminika. Lakini pamoja na hayo yote bado Afrika imekuwa ikiweka nguvu kuzalisha bidhaa kwa ajili ya soko hili. Hili tumelizungumza katika makala nyingi katika siku za nyuma.
Watetezi wa bara la Afrika nao hawakukaa kimya.Mashirika ya kimataifa kama Oxfarm GB na kampuni za wauzaji wakubwa wa bidhaa za kilimo toka Afrika kama Sainsbury wamejitokeza hadharani kupinga wimbi hili la ‘food miles’ lenye nia ya kuitoa Afrika katika biashara ya Ulimwengu kwa kigingi cha mabadiliko ya tabia nchi. Mkurugenzi Mkuu wa Sainsbury aliita hatua hii kama ‘protectionism’ ya aina yake na kampuni yake haiko tayari kukubali hii nadharia kwa ukweli kwamba kununua Afrika ni njia ambayo inapelekea ukombozi wa kiuchumi na kijamii kwa wakulima wengi wadogo wa bara hili.
Bado wataalamu wa kilimo wa Afrika na wanasayansi wanaendelea kupinga nadharia hii kwa hoja kuwa bara hili halizalishi kiwango kikubwa cha hewa ya ukaa wakati wa shughuli za kilimo na wala njia zinazotumia kusafirisha chakula toka Afrika bado hazichangii kwa kiasi kikubwa kuzalisha hewa ya ukaa. Kilimo cha Afrika bado cha jembe la mkono na kisichotumia mbolea, hivyo mazao yale yauzwayo nje ya bara hili kama kahawa, sukari, kakao, pamba, korosho, tumbaku, maua, mbogamboga chai huchangia kwa kiasi kidogo katika kuharibu ‘ozone layer’
Nchi nyingi za Afrika, kigingi hiki ni pigo kwani bado kilimo ni chanzo kikubwa cha ajira, pato la taifa, kwa mfano kwa Tanzania zaidi ya asilimia 50 ya pato la fedha za kigeni linategemea mauzo ya kilimo, Malawi ni zaidi ya asilimia 80, na Kenya ni zaidi ya asimilia 65.
Hivyo juhudi hizi hasi za kuona Afrika haifikii masoko ya Ulaya kwa kigingi cha ‘food miles’ na kampeni za kupambana na uharibu wa mazingira ni pigo kwa Afrika. Taasisi moja ya Kingereza inayojihusisha na maendeleo ya kilimo maeneo ya vijijini ilibainisha wazi kuwa msukumo mkubwa upo katika kulinda wakulima wa Kiingereza, kwani ni wazi kuwa kila kitu sasa kinaonekana kuwa kinatoka nje ya Uingereza.
Kilimo cha nyumbani (Local is good) kinapingwa pia kwa hoja kuwa hali ya hewa ya nchi hizi wakati wa wa baridi hutumia nishati kwa kiasi kikubwa (green house) na hivyo lile la kupambana na mabadiliko ya hali hewa halina nguvu.
Ni wazi kuwa suala la mazingira halina tajiri wala masikini, kila mmoja ana jukumu la kupambana na uharibifu wa mazingira, ila lililowazi kuwa Afrika safari hii inakabwa na juhudi hizi. Afrika ambayo inakabiriwa na mapigo makubwa ya mabadiliko ya tabia nchi ikiwa na tishio la kugeuka jangwa, ukosefu wa mvua, ongezeko la joto na mufuriko, inapaswa kujitahidi kupambana na haya yote.
Ila wataalamu wa mazingirwa wanabainisha kuwa, mifumo ya maisha ya wakazi wa kizio cha kaskazini ndiyo chanzo kikubwa cha mabadiliko ya hali ya tabia nchi. Katika Ulaya nyama inasadikiwa huchangia kwa kiasi kikubwa, kwani unenepeshaji wa mifugo kwa kutumia nafaka badala ya majani au nyasi. Wataalamu wanashauri kubadilisha milo toka nyama kwenda majani na mboga mboga.
Pia mtindo wa uendeshaji wa magari yenye injini kubwa (sports cars) yanayokula mafuta kwa kiasi kikubwa huchangia kwa kiasi kikubwa . Utupaji wa chakula, ambayo mabaki haya hutumia kuziba makorongo huzalisha kwa kiasi kikubwa hewa ya methane ambayo huchangia kwa kiasi kikubwa kuharibu anga la dunia. Japani hutupa tani milioni 20 kwa mwaka, hivyo rai ipo kwa watu wa kizio hiki kujitahidi kutotupa chakula.
Kigingi hiki kinatufanya kuangalia soko la ndani kwa masilahi ya Afrika. Biashara ya ndani ya bara la Afrika ni asilimia 4 tu, huku nguvu nyingi zikiwekwa katika kufikia soko la Ulaya. Ingawa ni kweli kuwa mahitaji ya fedha za kigeni ni makubwa kwa ajili ya kuagiza mahitaji mengine muhumi kama dawa, bidhaa za viwanda na mitambo. Lakini biashara ya ndani ingeweza kupanuwa uwigo wa wakulima wa bara la Afrika kuliko kukaa na kugombania kufikia katika soko la Ulaya pekee.
Soko la ndani katika nchi nyingi za kiafrika bado kufunguka huku kila nchi ikiwa iko tayari kuweka kigingi kwa nchi ya kiafrika lakini ipo tayari kufungua milango kwa nchi za magharibi. Hili la food miles ni changamoto nyingine kwa Afrika, tuna jukumu ya kuhakikisha linapata suluhu ya kudumu kwani ni nadharia inayosambaa kama moto katika nyasi za savana.Juhudi za kampeni ya kuhamasisha kupenda bidhaa za nyumbani ambayo Tanzania inafanya kupitia CTI ni suala la kuhimizwa kwa nguvu zote, na juhudi hizi zinapaswa kupelekwa katika shule na vyuo. Huu ni mwanzo mwema, kwani sasa food miles inashika kasi katika Ulaya na Marekani, kwa hoja ya mazingira. Basi yatupasa kupenda bidhaa za nyumbani.

Monday, March 1, 2010

Wakulima wadogo masikini watakombolewa na ‘fair trade’?

Ni mashamsham ya maazimisho ya wiki mbili ya kuhamasisha ‘fair trade’ katika nchi za Ulaya na Marekani kwa zaidi ya siku kumi na nne, toka Februari 22 hadi Machi 3. Miongoni mwa nchi zilizo katika mpango wa Fairtrade ni Uingereza, Ujerumani, Marekani, Japan,Ufaransa, Italia, Uholanzi, kuzitaja kwa uchahe tu. Kimsingi nchi hizi ndiyo masoko ya bidhaa za kilimo na za ubunifu wa mikono zinazotengenezwa katika nchi za Dunia ya tatu zikiingia sokoni kwa nembo ya fair trade.
Fair trade ni nadharia iliyojikita katika ‘utu’ huku ikiwa na msukumo wa kidini na maadili ili kuona wale watu waliomasikini kabisa duniani kutoka nchi masikini wanapata nafasi ya kufaidi jasho linalo tokana na kazi yao.Lengo kuu ni kuhakikisha bidhaa za watu wa kizio cha kusini zinafika katika masoko ya Ulaya na Amerika na wateja wakinunua bidhaa hizo ni wazi kuwa sehemu ya pato hurudi moja kwa moja katika nchi husika kusaidia maendeleo ya watu wa eneo hilo.
Nadharia hii inaweka katika vitendo, kile tunachokiita ‘trade not aid’. Lakini kwa sababu mfumo wa ulimwengu hauko wazi na bei za mazao mara zote zinaporomoka basi wakulima wa kizio cha kusini watapata nafuu, kwa kutoza bei ya juu kwa walaji wa kizio cha kaskazini na ile ziada iliyokuwa zaidi ya soko inakwenda kwa watu walio masikini.
Msukumo wa fair trade katika nchi za magharibi unaanzia katika makanisa, huku zaidi ya makanisa 6000 yakiwa yamejiunga katika mpango huu. Awali nimesema kuwa mpango huu umejikita katika maadili ya kiroho zaidi, na nyumba za ibada na taasisi za kidini na mashirika yao ndiyo yanayoongoza mpango huu wa ukombozi kwa watu wa kizio cha kusini.
Nguzo kuu ya maadili ya fairtrade yapo katika biblia, methali 13:23’Shamba la masikini hutoa mazao mengi , lakini bila haki hunyakuliwa’. Maneno hayo yamepamba baadhi ya makanisa katika Uingereza yanayojinadi kutumia bidhaa zenye nembo ya fair trade. Kupitia taasisi za kidini na mashirika yake wanaamini walaji wa nchi tajiri inabidi wanunue vitu kwa bei ya juu ili ziada irudi katika nchi asili ambako zao limelimwa ili kusaidia wakulima masikini.
Katika kutekeleza mpango huu njia moja wapo kuwa na chama cha ushirika na wakulima ujiunga pamoja kwa hiyari.Wakulima ni wale walio wadogo chini ya hekari 3 huku wakiwa wanaendesha shughuli zao za kilimo. Ingawa sasa kuna mjadala mkali wa kuangalia nini mantiki ya kutaka wakulima wadogo wapate haki ya kuuza kupitia mpango huu.
Inakadiriwa zaidi ya wakulima 500,000 na vyama vya ushirika 300 vipo katika mpango huu katika kizio cha kusini. Mauzo yanakadiriwa kufikia Euro bilioni 2.4 kwa mwaka jana.
Gazeti la The Independent la tarehe 25 Februari 2008 lilipoti mauzo ya bidhaa za fair trade kufikia paundi milioni 500 kwa Uingereza pekee. Huku idadi kubwa ya kampuni kubwa kama Mark Spencer, Waitrose,ASDA , Morrison na Tesco zikijiunga na kuahidi kuweka bidhaa za fairtrade katika maduka yao.
Fairtrade ni biashara inayovutia sana makampuni makubwa kwa sasa na kifimbo kinaonekana kupokonywa kutoka kwa taasisi za kihiyari kama Oxfarm, Traidcradt, Cafod sasa imekuwa ni biashara pendwa. Huu ni ushahidi wa wazi kuwa watu wengi wameitikia wito wa kununua kwa bei ya juu ili kwenda kusaidia watu masikini wa kizio cha kusini.
Tanzania inatajwa kama nchi ya kwanza kunufaika na mpango huu wa fairtrade, kwa kahawa kutoka Kagera mwaka 1988 kupitia chama cha Ushirika, Kagera Cooperative Union. Mpango huu pia unatumiwa na Kilimanjaro Native Cooperatives (KNCU) kwa kahawa yao kuuzwa Ulaya kupittia mpango huu.
Pia wamiliki wa mashamba ya chai wa Kibena, Iringa Tanzania ni miongozi mwa wafanyakazi wanaonufaika kwa bidhaa zao kufanikiwa kujipenyeza katika masoko ya Ulaya. Pia kuna bidhaa za mikono, zilizopo katika masoko ya Ulaya na Amerika kutoka Tanzania.
Mwenendo wa biashara unaonesha wazi kuzinufaisha nchi za dunia ya tatu. Tanzania kupitia KCU imeweza kuuza asilimia 7 ya kahawa yake yote inayozalisha. Kwa Mujibu ya mtandao wa taasisi ya Fair trade, inabainisha wazi kuwa wakulima wa Kagera wameweza kununua hisa za kiwanda cha Tanica kinachozalisha kahawa kwa asilimia 51.
Kahawa ya Arabica kutoka Afrika imewekwa katika bei ya dola 2.80 kwa Kilo,huku sent 11 dola za kimarekani kama bei ya juu (premium price) kwa kilo ikiwa fedha hii inapaswa kutumika kwa ajili ya maendeleo ya wakulima husika.
Bently W.R na wenzake katika Jarida la kisomi, Sustainable Development toleo 13, 2005 makala waliyoiita ‘What Tanzania’s farmers can teach the world’ wanabainisha kuwa kuna nyongeza ya kipato kwa wakulima wadogo wa kahawa wale walio katika mpango wa Fairtrade kulinganisha ni mifumo mingine .
Mafanikio mengine ni pale KNCU ilipoweza kuwalipia ada wanafunzi wanaokadiriwa kufikia 278, hawa ni wanafunzi wa shule za sekondari za serikali ambao wazazi wao wamefariki kwa ugonjwa wa Ukimwi au wanaoishi katika mazingira magumu.
Profesa Faustin K. Bee katika tafiti ‘Fair trade Fair futures: KNCU scholarship programme for children made vulnerable by AIDS’, 2009 anabaninsha wazi kuwa kipato cha kahawa kinachotokana na fairtrade kimekuwa si cha kuaminika kwa KNCU.Mwaka 2004 ilipatikana milioni 175 mwaka 2008 milioni 105. Majaaliwa ya mipango mizuri yote inawekwa majaribuni!
Haya ni mafanikio makubwa kufikiwa kwa wakulima wadogo waliojiunga chini ya chama cha ushirika. Lakini swali letu linabaki kuwa fairtrade ni mkombozi wa wakulima masikini toka mfumo mbovu wa biashara ya ulimwengu?Lililowazi ni kuwa fairtrade inaendeshwa nje ya nguvu za soko za ‘demand and supply’, kwani mlaji analipa zaidi ya bei ya soko na ziada inakwenda kwa wakulima wa nchi masikini.
Lililowazi kwamba wakulima wa Tanzania bado wanakumbukumbu ya maumivu ya walafi wachahce waliokula mali za ushirika bila kuchukuliwa hatua na safari hii fair trade inahimiza ushirika. Je Fair trade kupitia ushirika tutafikia lengo katika Tanzania, au yale yale?
Walaji wa Ulaya na Amerika hawatakuwa tayari kuona maadili ya utu yanavunjwa huku wao wakilipa bei ya juu kuliko bei ya soko na walafi wakihujumu chumo la fair trade. Ni wazi kuwa watasusa. Jukumu la kusukuma mbele malengo ya fair trade ni wazi kuwa Tanzania kama nchi ina nafasi kubwa ya kushiriki kuhakikisha wakulima wadogo wanalindwa na makucha ya walafi wanaojificha katika ushirika. Shime wenye mamlaka.