Monday, June 14, 2010

RFID ni suluhu moja wapo kwa bidhaa feki kwa nchi zinazoendelea

Radio Frequency Indentification (RFID) si teknolojia mpya duniani, ila inaelezewa kuchipua sana katika miaka ya 2000. Teknolojia hii ilianza kutumika kwa mara ya kwanza wakati wa vita ya pili ya Dunia na waingereza katika rada za kijeshi kuweza kutambua ndege za maadui na washirika wake.
Tokea wakati huo RFID imekuwa ikitumika sana katika mambo ya kijeshi, ila miaka ya karibuni kuna mabadiliko makubwa hasa katika nyanja ya biashara kuanza kutumia technolojia hii katika kuongeza uongozi wa usambazaji bidhaa (supply chain management) na kupunguza hasara kampuni imekuwa zikipata.
Kampuni kubwa General Motor, imeanza kutumia tangu miaka ya 1984 kwa utambuzi wa bidhaa zenye thamani kubwa hasa injini za magari, pia Toyota kwa kiwanda chake kilichopo Afika Kusini. RFID ni nini?
RFID ni miali ambayo inasafiri katika mawimbi ya redio ikiweza kufanya utambuzi wa kitu bila hata kuweza kuangaliwa moja kwa moja na muhusika. Kwa sasa ulimwengu unatumia ‘bar code’ ili kuweza kutambua kama mzigo husika ni sahihi kwa kusoma namba na kutafsiri, lakini kwa RFDI unaweza kupata taarifa toka mbali bila hata kuona mzigo kama tulivyokwisha kusema.
Katika bidhaa husika badala ya kubandikwa ‘bar code’ RFID tag itabandikwa na msomaji akisaidiwa na mtambo ambao unafahamika kama RFID reader ataweza kung’amua nini kinaendelea kwa mzigo husika. Kuna aina tatu za RFID tag lakini tofauti kubwa ambayo wataalamu wa TEKNOHAMA wanaikubali ipo,ni ile inayotumia betri na isiyotumia betri.
Bidhaa ambazo hazina thamani kubwa hutumia ‘RFID tag’ zisizo na betri, ili kuweza kung’amua mpangilio wa bidhaa ndani ya ghala au hata bidhaa iliyo katika hatari ya kuharibika kwa uzembe wa mpokeaji. Kwa mfano maziwa yanaweza kusahaulika kuwekwa katika hali ya ubaridi RFID tag ina uwezo wa kupeleka taarifa kwa msomaji na kutambua kuwa kuna mabadiliko ya joto kwa bidhaa husika, hivyo kuharakisha uhifadhi sahihi wa bidhaa kama hizi zenye kuhitaji umakini wa hali ya juu.
Katika siku za karibuni ongezeko la bidhaa 'feki' limekuwa ni tatizo kwa nchi nyingi zilizoendelea na zinazoendelea Tanzania ikiwemo. Wakati wote huu Uchina imekuwa ikibeba lawama kuwa ndiyo mhusika na ni muendelezaji wa uuzaji wa bidhaa feki, kwa Afrika.
Hivi karibuni kuna sakata la kondomu feki, likiwa tu linafuatia baada ya sanya sanya ya taulo za usafi za kina mama, ‘always fake’ kukamatwa katika maduka mkoani Arusha. Hangaiko la bidhaa feki ni la uliwengu mzima, lakini jithihada za kupambana zinatofautiana toka nchi moja hadi nyingine.
Tanzania bidhaa zenye ubora mdogo zinatusumbua. Makala haya itajaribu kutupia jicho hali ya bidhaa feki na uwezekano wa teknolojia ya RFID katika kukabili changamoto hii.
Kamisheni ya Ushindani (FCC) inataja kuwa kiwi za milioni 20 na ‘tubelight’ za aina ya Phillips na Britimax zenye thamani ya dola 18000 zimeteketezwa mwaka 2007, kwa mujibu wa gazeti la Daily News la tarehe 1 Mei 2009.
Pia inakadiriwa kwa mwezi Machi pekee 2008, bidhaa zenye thamani ya dola za kimarekani 224,000, ziliteketezwa na FCC. Ni wazi kuwa FCC kwa uchanga wake inafanya kazi kadiri inavyoweza ili kudhibiti bidhaa ‘feki’.
Ni wazi kuwa vita hii inahitaji kuongezewa nguvu na sheria inayowapa walaji nafasi ya kuwa na chama imara chenye kuwalinda tena chenye nguvu ya kulinda masilahi ya walaji.Katika nchi nyingi vyama hivi vipo na vimekuwa mwiba na vimefanikiwa kulinda nchi zao kuwa majalala ya bidhaa ‘bomu’ si toka nje tu hata wazalishaji wa ndani.
Wataalamu wa TEKNOHAMA wanaelezea RFID kama teknolojia moja wapo yenye nguvu yakuweza kumpa mtu uwezo wa kutambua bidhaa tangu pale inapotengezwa kusafirishwa hadi kufika kwa mteja. Kimsingi inaongeza usalama na uwezo wa kufuatilia bidhaa wapi imetoka na imekumbana na hitilafu gani njiani.
Kwa sasa teknolojia hii ingawa iko katika majaribio makampuni mengi kama wauzaji wa bidhaa za reja reja (supermarkets) kama Wal-Mart, Tesco, ASDA , Zara na IKEA, lakini inaonekana kuvutia mno kampuni hizi kubwa, huku IKEA kampuni kubwa ya samani ikitaja kuweza kudhiti upotevu wa kontena zaidi ya arobaini kwa mwaka.Pia imeonekana ina manufaa kwa sekta ya afya katika kupambana na dawa feki na wagonjwa wasio meza dawa kwa wakati.
Marekani pekee inakadiriwa kupata hasara ya karibia dola bilioni 30 kwa mwaka katika dawa pekee kwa kuingizwa sokoni dawa feki na kughushiwa kwa nembo za kampuni husika (counterfeit). Taasisi ya chakula na dawa ya Marekani kwa kuzingatia hilo imepitisha azimio tangu mwaka 2007 kuhitaji wasambazaji wa dawa kutumia RFID ili kuongeza utambuzi wa dawa.
Wanazuoni Castro Linda na Fosso Wamba katika jarida la kisomi,Journal of Technology Management and Innovation, juzuu ya pili toleo la kwanza la mwaka 2007, wanabainisha wazi kuwa RFID ni teknolojia ya kipekee itakayo ongeza ufanishi na uwazi katika sekta ya afya kwani dawa zitaweza kuonekana tangu malighadi hadi kufika kwa mtumiaji wa mwisho.
Huu ni ushindi dhidi ya mapambano ya bidhaa bandia kwani kampuni nyingi kubwa sasa zinataka wasambazaji wake watumie RFID katika kufikisha bidhaa ili kukabili hali ya bidha feki.Hii ndiyo hali iliyoifanya serikali ya Marekani kuhitaji wasambazaji wa dawa na bidhaa za kitabibu kutumia teknolojia hii ili kuweza kuhakiki kwa uwazi.
Changamoto kubwa iliyopo katika kutumia teknolojia hii ni ukosefu wa wataalamu, bei ya RFID tag bado ni kubwa na nchi nyinyi bado hazijakubali matumimzi ya mawimbi ya redio kwa ajili ya usambazaji wa bidhaa. Na kubwa kuliko yote ni changamoto ya haki ya kuwa na siri (right of privacy), kwani kama RFID tag ikibandikwa katika kiatu ni wazi muuzaji ataweza kutambua wapi kiatu chake kipo, tangu akiuze kimepita, ingawa hili linategemea sana na aina ya RFID tag ambayo kwa hali ya kawaida hakuna kampuni itaweza kuweka tag ya namna hii kutokan na gharama yake.
Changamoto ya kukosa siri imefanya RFID kupingwa na watu wengi katika Marekani, hasa watetezi wa haki za binadamu wakidai kuwa teknolojia hii inaweza kufanya mtu kuweza kufuatiliwa na watu wa usalama na kumnyima uhuru wake.
Pia gharama ya tag ya RFID bado ni ghali, huku ikadiriwa kufikia senti 30 za Marekani kwa tag moja isiyo kuwa na betri, ambayo inakisiwa kupandisha gharama za uzalishaji kwa asilimia 26-60 ya zile za usafirishaji kwa masoko ya Ulaya na Marekani.
Pamoja naukweli kwamba RFID tag bei yake kuwa kubwa sokoni lakini kuna dalili kuwa bei yake imeanza kupungua na hasa baada ya kigingi cha haki miliki kupata suluhu na kampuni nyingi za Asia kuanza kuzalisha. Ila lililowazi ni kwamba Afya haiwekwi rehani ili kukabili dawa feki taratibu Tanzania inaweza kujongea katika matumizi ya teknolojia hii.

Wednesday, June 2, 2010

kigezo ni umri au utashi?

Uchaguzi mkuu wa rais na wabunge unakaribia katika Tanzania,kila kona kunatoka hoja na vioja. Kwa hakika kila mmoja anafaidi uhuru wake wa kuongea. Ndiyo demokrasia.
Katika maongezi hayo kuna kioja cha vijana wengi kujinadi kwa hoja ya umri na 'kuomba' wazeee wa wawapishe.
Hakika hiki ni kihoja, na wala si hoja kwani............................. fuatilia makala hii itakayotoka hivi karibuni.

wazalishaji wa ndani nao wajichunguze

Si kampeni mpya duniani na hasa kwa wale walio na nia ya kulinda ajira na uchumi wa nchi yao. Tanzania kupitia Confederation of Tanzania Industry inahimiza utumia wa bidhaa za nyumbani kwa sababu kadha wa kadha lakini lililokubwa ni kunusuru uchumi wa Tanzania. Katika Amerika kuna nembo kama ‘made in NY state’, ‘A taste of Iowa’ nakadhalika zote zikihimiza kupenda bidhaa za eneo lako.
Pia katika Amerika kuna wanaharakati wanavalia fulana za ‘Toyota made in Japan, Poverty made in Japan, Unemployment made in Japan’ Si unyanyasaji wala aina fulani ya ubaguzi ni jitihada tu za kukumbushana kuwa yatupasa kupenda bidhaa za nyumbani.
Hivi karibuni kuna ujumbe wa e-mail wenye kuhimizana miongoni mwa watanzania kupenda bidhaa za nyumbani mtandao. Huu ni mwanzo mpya lakini hili kama tulivyokwisha kusema si jambo jipya, ila sasa linaonekana kushika moto miongoni mwa watanzania, hasa baada ya CTI kulivalia njuga.
Tanzania ikiwa miongoni mwa nchi zinazochipua kiuchumi tatizo kubwa inalokabiliana nalo wakati wote ni uzalishaji ‘supply side’ kwani mahitaji(demand) ni makubwa na mara nyingi chochote kinachoingia sokoni huwa kinapata wateja, na kutokana na hilo ndiyo maana bidhaa hizi za kutoka Asia zimefurika katika soko la ndani. Na nyingi ya bidhaa hizi hazina ubora, lakini tutafanyaje heri lawama kuliko fedheha, hapa ndipo inachukua nafasi.
Madhara ya kufurika kwa bidhaa hizi toka Asia, tumekwisha yaandika katika makala nyingi, leo hapa hayana nafasi ya kujadiliwa. Ila makala haya itajaribu kujadili mbinu za kukabiliana na madhara ya kupenda bidhaa za nje hasa kwa wenye viwanda Tanzania.Kwani hili ndilo suala kubwa tunalopambana nalo, wataalamu wa biashara wanaiita ‘Country of Origin effects (COO)’
Made in……mara nyingi ni moja kati ya vitu vinavyomfanya mlaji apunguze hofu kuhusu bidhaa anayotumia na hasa kuhusu ubora ikiwa kama hana taarifa sahihi kuhusu nchi iliyotengezeza bidhaa hiyo. Ingawa wataalamu wa tabia za mlaji (consumer behaviour) wanalumbana kuhusu uhalisia wa COO kuwa kama moja ya ‘extrinsic values’ mteja anayoweza kuitumia lakini matokeao yameonesha wazi kuwa hii ni moja kati ya maeneo mteja anaweza kutumia kufanya maamuzi ya kutumia bidhaa au la!
Fikiria mtumiaji wa chakula cha watoto cha viwandani atakavyofikiria mara mbili pale anapoona chakula kwa ajili ya watoto kimetengezwa Uchina. Hofu moja kwa moja itatawala na hasa akijaribu kuhusianisha na tatizo la melamine lililoikabili viwanda vya chakula cha watoto katika China. Hiyo hili linafanya mara moja mnunuzi aamue kuacha na kutafuta mbadala. Hiyo ndiyo changamoto inayoikabili sekta ya viwanda Tanzania kwa sasa kwani walaji wameshatendwa, sasa wakiona unyasi (Made in Tanzania) wanastuka.
Kupenda bidhaa za nyumbani ni ‘ethnocentrism’, yaani ni hali ya kuona chako ni bora kuliko cha mwingine anatafrisi Profesa Constance Falk katika jarida la kisomi, Agribusiness, toleo la pili, mwaka 1996.Hivyo hutia ndani imani kwa mlaji kuwa kutumia bidhaa za nje ni kudumaza uchumi wa ndani, na kusababisha kukosekana kwa ajira na nikukosa uzalendo (patriotism).
Hivyo basi ‘Ethnocentrism’ ni zaidi ya uzalendo, kwani hii ni hali ya kuweka maneno katika vitendo huku ukijigamba kuwa wewe ndiyo bora na kuringia nchi yako anaandika Profesa Falk (Tafsiri ni yangu). Ndiyo maana tafiti fulani inaonesha kuwa walaji katika Marekani zaidi ya asilimia 80 wanaona nyama bora na tamu ni ile inayozalishwa na wafugaji wa kimarekani. Wanajivunia cha kwao, na hili tumeliona katika medani za kimataifa katika mambo mengi, kuhusu ubora wa muamerika na Amerika yenyewe.
Lakini hali ni tofauti katika Asia, ambako kubeba begi la ‘GUCCI’ au ‘PRADA’ lililotegnezwa magharibi ni kuonesha kuwa we ni mtu wa thamani na mwenye kwenda na wakati, huku ukionesha kuwa uko na kipato kikubwa. Homa hiyo imeikumba Tanzania, ambako serikali iko tayari kutumia bilioni 3 kwa ajili ya samani toka Uchina, Malaya na Singapore huku wajasiriamali wa Changombe, Suma JKT kutaja wachache tu wakikosa soko la bidhaa zao!
Hali ndiyo hiyo hiyo kwa mtu mmoja mmoja ambapo kunywa juisi ya Del Monte toka Kenya au Ceres toka Afrika Kusini ni ufahari badala ya ile yaUnnat, Kingolwira Morogoro. Orodha inaweza kuwa ndefu kwani kuna vilio vingi vya wazalishaji wa ndani.
Wazalishaji wa ndani watambue kwamba serikali haiwezi kuzuia hili kwani tumelia vya kutosha, makala nyingi zimeandikwa za kutosha watu wamepata shahada zao kuhusu haya mambo na madhara yake na hata walio madarakani baadhi yao hizi ndiyo ‘titile’ za tafiti zao wakati wanasotea shahada zao!
Lakini leo hii katika vitendo ni vurugu tupu, hakuna anayesikia kilio cha wazalishaji. Serikali haiwezi kuacha hili kwa vile yenyewe inataka kodi tu, kwisha. Hivyo ni muhimu kwa wazalishahji kujipanga, na kutafuta mbinu za kibiashara kukabili hii hali, kwani tunaozungumza nao si wasikivu.Na kama wanatarekebisha itachukua muda.Hebu tutupie jicho kidogo mbinu ambazo tunaamini wenye viwanda wanapaswa kuzitumia kukabili ‘country of origin effects’.
Garantii inahitajika kwa bidhaa ambazo zinadumu kwa muda mrefu na zenye thamani kubwa. Kwa mfano, kufanya vizuri kwa magodoro ya Dodoma ni kutokana na kuwepo kwa garantii ya muda usiopungua mwaka kama likibonyea rudisha kwa ‘muuzaji’ naye atarudhisha kiwandani. Hii inafanya mlaji kuona kuwa kuna uhakika wa ubora kwani mzalishaji yupo tayari kupokea bidhaa zitakazorudiswa kwake (reverse logistic) ambayo kimsingi ni gharama kubwa.Hivyo niwazi kuwa kiwanda hakiko tayari kuona inaingia mtegoni, basi ubora ndiyo ngao yao.
Lakini wazalishaji wa nyumbani wengi hawana ‘garantii’ kwa bidhaa zao wala ‘motisha’ sasa anapokuja muuzaji toka nje naye anaweka ‘garantii’ kuonesha ubora wa bidhaa zake ni wazi kuwa ataliteka soko la Tanzania. Mfano mzuri wa ‘garantii’inavyovunja mwiko wa ‘Country of Origin’ ni Honda magari toka Korea yalipoingia Amerika kwani yalikosa wateja kwa dhana kuwa Korea si mtengezaji mzuri wa magari na hakuna anayeitambua kwa umakini katika eneo hilo. Pia kwa Czech magari yao ya Skoda na Hyundai katika soko la Uingereza.
Honda waliweka ‘garantii’ ya miaka kumi, hali iliyofanya wateja kuamini kuwa magari ya Honda si masihara katika ubora leo hii, Honda ni katika wauzaji wakubwa wa magari katika Marekani.
Kuimarisha mawasilinao, ya simu na wavuti. Kampuni nyingi za Tanzania zinatengeneza bidhaa na kuzileta sokoni huku wenyewe wakijificha wasijulikane wako wapi na wanafanya nini. Hili huchangia kwa kiasi kikubwa woga kwa mmlaji. Huu ni ulimwneug wa mawasilino ambako mlaji anafanya uchunguzi na kujiridhisha kabla hata kutumia bidhaa kunawaokwenda katika internet na kutafuta wahusika wa kampuni wanapatikan wapi na kwa namna gani lakini sisi hata ukienda katika website ni madudu tu.Hupati taarifa kamili.
Namba za simu zikitolewa zitaita hadi itakata hakuna anayepokea wala kujali. Sasa kama mteja anataka kutoa oda mpya unadhani atakuwa na imani na kampuni husika. Ukitembelea tovuti zao taarifa zipo kwa kificho sana zaidi ni picha na sanduku la posta,sasa mteja anajiuliza kama huyu ni mzalishaji makini kwa nini anaficha taarifa zake?
Mfano mzuri ni Tanzania Meat Pride kiwanda cha nyama cha Morogoro, wanaozalisha ‘soseji’ ukiwa muuzaji unahitaji soseji zao lakini hawana mawasialiano ya simu wala internet katika paketi zao, sasa sijui mteja akitaka kuongeza oda anawapata wapi. Ingawa wamefanikiwa katika kupunguza wasiwasi kwa walaji wa dini zingine kwa vile wanadai nyama yao imenchinjwa kwa imani ya dini ya Kiislamu (Islamic Doctrine) na BAKWATA wameweka muhuri wao katika kila duka lao na taarifa yao lakini hili pekee haliondoi hofu kama wewe ukiwa bado hutaki kuleta taarifa sahihi ya kuwa uko wapi , na unapatikana vip?
Taarifa kama faida na hasara zilizokaguliwa na wataalamu wa fedha si tu zinawafanya mupate mikopo, la hasha hata walaji wanavutiwa nazo. Kwani kampuni ambayo taarifa zake za kifedha zipo wazi mlaji anaamini kuwa kampuni inaimarika hivyo anaweza kutumia bidhaa husika. Hili ni hasa kwa watengezaji wa vitu vya urembo.
Watumiaji wa mafuta ya ngozi (lotion) na vipodozi vingine hawependi kubadili badili vipodozi kwa hofu ya kuchanganya ‘mambo’Hivyo taarifa hizi za kifedha zitawapa moyo kuwa munafanya vizuri hivyo kuamua kutumia bidhaa zenu kwani wanaimarika na muna nguvu ya kwenda mbele kwa muda mrefu. Hivi ni kwanini kampuni za simu zinatoa taarifa zao au benki unadhani ni kwa sababu ya sheri tu? La hasha walaji nao wanazisoma, ili kufanya maamuzi, kwani walaji wa leo si wale wa Tanzania ya jana, leo soko lina vizazivya 1980 (Generation Y) tena wengi ndiyo hao wapo daraja la kati. Hawa ni wepesi kuiga na wako tayari kujifunza, sasa usipokuja na mbinu za kisasa ni ngumu kuwashawishi.
Nembo za viwango vya ubora. Kulalamika tu hakutasaidia kitu lazima tupambane kisayansi. Njia moja wapo ni hii ya kupata nembo ya ubora kama vile TBS. Nembo hii inapunguza hofu kwa mlaji na kuanza kuamini kuwa bidhaa husika ina ubora inaotakikana. Kwa mfano kufanya vizuri kwa dawa ya meno ya White Dent ni pamoja na kupata hati ya ubora toka kwa Tanzania Dental Association (TDA), hivyo ingawa Aha ilikuwa chini kwa bei kuliko White dent lakini leo hii Aha haipo sokoni. Ni wazi kuwa TDA imeingozea White dent thamani na ubora miongoni mwa wateja .
Hivyo tunahimiza pia si kuamini katika nembo za kiserikali tu hata vyama vya kitaalamu vinapunguza hofu kwa wateja na hasa vyama hivi kwani vingi viko huru.Pia tunaona kuwa punguzo la bei si ushindi kwa kampuni sokoni.
Lingine ni hili la kujitangaza, wazalishaji wa ndani wengi hawajitangazi labda wanaamni katika msemo wa Kiswahili ‘chema chajiuza kibaya chajitangaza’. Ukweli ni kwamba katika sayansi ya bishara na hasa kwa upande wa mlaji(consumer behaviour), mlaji anahusianisha ubora na matangazo kwani kampuni isiyojiamini haiwezi kuweka fedha katika matangazo kwani inaogopa kupata hasara.
Hivyo ile kampuni inayojitangaza mara nyingi inakuwa inanafasi kubwa ya kupata ‘utiifu’ wa mlaji kwa dhana kwamba hii inaubora wa kutosha ndiyo maana imeingia gharama kujitangaza la sivyo isingeliwekeza katika matangazo. Matangazo ni gharama kurasa moja ya gazeti tena isiyo ya rangi ni zaidi ya laki tano katika Tanzania sasa kampuni isiyo na viwango inaogopa kuwekeza katika gharama kama hizi.
Ila mambo ni kinyume chake katika Tanzania leo hii ni kinyume chake kampuni nyingi zinadai zinazalisha bidhaa bora lakini hazijitangazi kwa nini? Jibu rahisi linaweza kuwa wanawasiwasi na bidhaa zao kuwa si bora. Angalia makutano ya barabara kubwa nyingi katika Tanzania kampuni za juisi za matunda toka Kenya na Afrika kusini ndiyo zimeweka mabango ya matangazo yao.Hivyo hili linawajengea imani wateja kuwa kama kampuni hizi zinagalikuwa zinazalisha bidhaa ‘feki’ wasingaliweka mabango na kukubali kuingia gharama, wamefanya hivi kwa vile wamejiamini. Hivyo wazalishaji wa Tanzania nanyi jitangazeni.
Mwisho ni hoja iliyotelewa na Profesa Han C Min mtaalamu wa Marketing, katika jarida la Marketing Reasearch toleo la 26, mwaka 1989, makala ‘Country image: Halo or summary construct? Profesa Han anahimiza wazalishaji kutolindana hasa kupitia umoja wao ili kulinda ubora wa bidhaa zao. Hili la kulindana ndiyo tatizo la wazalishaji wa nchi change Tanzania ikiwemo, kwani kama mutapata sifa kuwa munazalisha bidhaa bora na nzuri wanatokea watu wachache wakiharibu ni taswria ya nchi nzima. Ni taswira ya wazalishaji wote haina mjadala. Leo hii watu wanalalamika kupigwa ‘bambo’ mifuko ya simenti ya kilo hamsini haitimii, wazalishaji wako kimya, sasa ikija sementi toka nje munakimbilia kulalamika wakati kimsingi wenyewe ndiyo musioojali wala kusikiliza mteja anamashaka gani.
Watu wanaozalisha bidhaa feki za konyagi, unga wa mahindi, kufunga vipodozi visivyo na ubora wanaonekana na wanajulikana tena wakati mwingine wanatumia kampuni zilizosajiliwa lakini hakuna kukememeana na kuchukuliana hatua miongoni mwa wazalishaiji na taasisi zao.
Ni vyema kampeni hii ya kuwa mzalendo tumia bidhaa za nyumbani ikawagusa pia wazalishaji nao pia watafute mbinu za kisasa kupambana na hii hali makala haya imebainisha chache tu, lakini kimsingi mbinu za kukabili ‘country of origin effects’ zipo nyingi. Tukishirikiana tunaweza.

Sunday, April 18, 2010

Afrika ya weusi haiwezi kutumia ‘boom’?

‘Afrika haiwezi kutumia vyema kupanda kwa bei katika soko la ulimwengu (boom) wala kujihami na majanga yanayoathiri uchumi wake’ Hi ni sehemu ya taarifa ya ripoti ya Benki ya Maendeleo ya Afrika (ADB) kuhusu muenendo wa biashara na uchumi katika Afrika miaka 90.
Tumeona ni vyema kuanza na maneno hayo katika makala haya ili kujenga tafakari pana ya Afrika ya weusi na majaaliwa yake. ADB inaona hali hii na inaona jinsi bara hili linavyoshindwa kufanya vyema hata kama likawa na ziada kutoka mazao ya mashamba yake.
Afrika ya weusi haina ukame wala neema kila siku ni vilio, ni hali ya muda mrefu lakini lenye kuti uchungu ni kuona hali hii ikionekana kukomaa kama ni stahiki kwa bara hili. Isionekana kama tumekata tamaa la hasha ila tunajaribu kutafuta nji ya kutokea.
Mavuno yakiwa mazuri Afrika bado kuna watu watakufa njaa na wakulima watapata hasara kwa kukosa kuuza mazao kwa bei nzuri na hata kuharika. Hali hii inaonesha Afrika inahitaji zaidi ‘breki’ kuliko ‘kasi’ inayoenda nayo.
Ripoti moja ya UNDP inaelezea Tanzania kupoteza zaidi ya asimilia 60 ya matunda yake kuoza huku bado nchi ikiwa muagizaji mkubwa wa juisi za Maaza, toka Falme za Kiarabu, na Ceres (Hili ni jina la Mungu wa dini za kale za Kigiriki, Mungu wa uzao wa Ardhi) toka Afrika Kusini na Del Monte toka Kenya.
Bidhaa hizi zikifurika katika soko la ndani huku wakulima wa matunda katika mikoa ya Tanzaga, Iringa na Morogoro wakiingia katika lindi la umasikini. Hii ni hali ya kawaida hasa katika Afrika ya weusi.
Hivi karibuni kuna taarifa inaoashiria hayo ya ADB kuwa bado yanaendela katika Tanzania. Naibu Waziri wa Kilimo na Ushirika Dokta Mathayo amekaririwa na vyombo vya habari akisema kuwa wakulima wa nafaka wa Rukwa walio na kitisho cha kuharibikiwa zaidi ya tani 1.2 za mahindi kwa kukoka soko serikali iko mbioni kupata takwimu za ukweli. Taarifa hii ya kitisho cha kuharibika kwa nafasi Rukwa zilitolewa na Serikali ya Mkoa!
Hili likitokea kuna taarifa za kitafiti kuwa watanzania zaidi ya milioni 8 huwa wanashinda njaa kila siku. Hii ndiyo hali ya kutoweza kutumia ‘boom’ umevuna unashindwa kuuza, huku kuna wanaohitaji nao wakiwa hawajui watapata wapi!Sababu kubwa za hali hii imekwisha elezewa sana nalo ni miundo mbinu leo halina nafasi hapa.
Ni wazi kuwa mzunguko huu hauna mwisho mwema, na umasikini utaendelea kutuzunguka wakulima wa mahindi pia wale wanaoakadiriwa na kitisho cha njaa wataendelea kukiona cha moto huku kuna wenzao nafaka zinaoza. Hali ya mambo inaonesha kupanda kwa mfumuko wa bei, na hili katika tafsiri rahisi ni kuwa bei ya vyakula imepanda na hasa vyakula vikuu na hapa tunazungumzia mahindi, sasa iweje tena kuna watu wanakosa soko!Kuna dosari mahali.
Hivi karibuni Waziri Mkuu Mizengo Pinda ameruhusu wakulima wenye shehena za mpunga kuuza nje ya Tanzania. Hatua hii ni mwanzo mwema kuelekea kuwaunganisha wakulima wetu na masoko ya nchi jirani.
Ila wasiwasi wetu ni namna ya kuratibu zoezi hili. Isieleweke kuwa wakulima hawawezi kuuza katika soko la ndani na wala kwamba soko la ndani limeweza kupata inachohitaji isipokuwa ni wakwamba muenendo wa soko umeshindwa kuwaunganisha wakulima hawa.
Tatizo ni wakulima wetu kuunganishwa katika soko la ndani. Ni sisi tunaouza mchele huu nje punde tu tutaenda Thailand na Vietnam kuhitaji kununua mchele. Sasa kwanini tusiwaunganishe wakulima hawa na soko la ndani?Kwa nini tusinunue na kuhifadhi nafaka hii? Strategic Grain Reserve I wapi?
Hapa tena tunashindwa kutumia ‘boom’. Nilishatahadharisha katika makala iliyopita katika siku za nyuma kuwa bei ya mchele Duniani haionekani kupungua na hili linasababishwa na India na Philippines ambao ni walaji na wauzaji wakubwa wa mchele pia kwenda sokoni kuhaha kutaka kununua mchele. Unapomuona muuza mkubwa kaingia sokoini kununua ujue kuna jambo, India yupo sokoni.
Ingawa Philippines alipandisha dau la bei ya mchele lakini hakupata tani alizokuwa anahitaji.India yupo sokoni kwa vile anakabiliwa na hali mbaya ya hewa iliyokuwa kitisho kwa zaidi ya tani 650,000. Hivyo kuamua kupiga marufuku kuuza mchele nje ya nchi.
Tanzania si mmlaji wa mchele kama chakula kikuu ila tunaenda Asia kama kimbilio la njaa. Hali ya mambo ya bei ya mchele duniani inaonesha wazi kuwa hata ule mchele daraja la mwisho toka Vietnam uliovunjika kwa zadi ya asilimia 25 umepata soko katika Afrika nchi kama Mali, Senegal na Nigeria ambayo huagiza zaidi ya asilimia 60 ya mchele.
Hali hii inaonesha sisi hapa tunachezea ‘boom’ kwa kujifariji kuwa ni bora wauze katika masoko ya nchi jirani kwa hoja kuwa tumeshindwa kununua. Lakini hatari i yaja. Kwani bei ya nafaka na hasa mchele haitapungua zaidi ya dola 600, huku Thailand muuzaji mkubwa wa mchele duniani akisusa akingoje walau ipande.Ipande mpaka wapi hakuna anayejua, ni soko limeachiwa liamue.
Pia shirika la OECD, linabainisha wazi kuwa mchele hautashuka zaidi ya dola 600 kwa tani tena huu ni wa dajara la chini (25% broken) kwa vile Ulimwengu umeweka nguvu katika kutumia mahindi kutengeneza nishati ya mafuta (bio fuel) , hali ambayo inafanya mchele ugeuzwe kama chakula cha mifugo katika Uchina, Marekani na Ulaya!
Katika miaka ya karibuni China imebadili uuzaji wa mchele nje huku ulaji wa nyama ukipanda kwa zaidi ya alimia 40 hali inayoelezewa inatokana na kutumika kwa mchele kama chakula cha mifugo. Na Japani moja ya watoaji wa misaada ya mchele kwa Afrika iliyokatika hatari ya kuharibika na hasa kama wanasafisha maghala inatoza kodi wakulima wake wanaotumia ardhi kulima mpunga huku ikiwapa motisha wale wanaolima matunda na mboga mboga ‘tozo’ toka katika wakulima wa mpunga. Hali hii inafanya mchele kupungua duniani.
Pamoja na hayo Afrika ulaji wa mchele unaongezeka hali inayochangiwa na kukuwa kwa daraja la kati katika nchi nyingi za kusini mwa jangwa la Sahara, Tanzania ikiwemo.
Muenendo huu wa soko la nafaka duniani unaashiria kuwa sisi tunacheza na ‘boom’ tena katika nchi ambayo zaidi ya watu milioni 8 wanashinda njaa! Ni vyema tukaipa uwezo Strategic Grain Reserve wa kununua na kuhifadhi nafaka hizi kuliko kupigia chapuo uamauzi wa kuuza nje.
Na isitoshe utaratibu huu wa kuuza nje unapaswa kuratibiwa vyema kwani ni wazi kuwa soko la kimatiafa linasumbua na kama watu wetu hawakujipanga vyema tutaishia kuwa watengeza ajira kwa wenzetu. Kuna mashine za kukoboa nafaka, basi tusiuze nafaka ghafi ni bora tukawauzia mchele ulioongwezwa thamani.

Monday, March 29, 2010

Ushirika na maajaliwa ya ‘Fair Trade’ katika Tanzania

Tanzania ni nchi ya kwanza Kusini mwa Jangwa la Sahara kuingizwa katika mpango wa ‘FAIR TRADE’(biashara huru), ila makala haya itatumia neno 'fair trade' moja kwa moja. Mpango huu ambao ulianza mwaka 1988 kupitia kahawa, kwa sasa unahusisha pia chai na samani hasa zenye kurembwa kwa shanga.
Kagera Cooperative Union (KCU) ni chama cha kwanza kunufaika na ‘Fair Trade’, kwa kuanza kuuza kahawa yake katika masoko ya Ulaya na Amerika. Kimsingi mpango huu umejikita katika nadharia ya kuwapa nguvu wakulima masikini wadogo wa nchi changa kuweza kufikia masoko ya Ulaya, huku wakinufaika kwa kazi ya jasho lao, kwa kulipwa bei nzuri ambazo ni zaidi ya bei ya soko la dunia.
Baada ya manufaa ya mpango huu kwa sasa nchini Tanzania vyama vya ushirika kama Karagwe District Cooperative Union, Kilimanjaro Native Cooperative Union pia wapo katika kuuza kahawa. Pia wafanyakazi wa mashamba ya chai katika Kibena ana Luponde Iringa na Lushoto, Tanga wapo katika mpango huu. Pia kuna mau yanayouzwa na kampuni ya Kiliflora ya Arusha kwa kutumia nembo ya 'Fairtrade' yakiwa chini ya Max Havelaar nembo inayoratibu masoko ya Uholanzi, Ubelgiji na Ufaransa.
Ili kufanikisha mpango wa fair trade ushirika imara ni muhimu kwa uhakika wa soko na mgawo wa pato la mauzo. Ushirika ndiyo kiunganishi kati ya wanunuzi na wakulima. Na hili la kuundwa kwa ushirika imara ni moja kati ya masharti makubwa ya kuweza kusajiliwa kama mzalishaji wa kahawa chini ya mpango wa 'fair trade'. Kwa wamiliki wa mashamba makubwa ya chai moja ya masharti ni kuundwa kwa vyama vya wafanya kazi huru vikiundwa na wafanyakazi wakipata hali bora kama huduma za kiafya na elimu kwa ajili ya watoto wao kutokana na chumo la 'Fair Trade'.
Mpango wa Fair Trade unashika kasi katika Afrika, Uganda na Malawi zinauza sukari, Kenya na Afrika Kusini zikijikita katika chai.Ingawa Tanzania ni mmoja kati ya wakongwe katika nchi za kusini mwa Jangwa la Sahara lakini ushiriki wake unaonekana kupungua. Na hii si kama bei ya kahawa au chai inaonekana kutengemaa sokoni la hasha.
Kwa mujibu wa mtafiti Profesa Fautini Karani Bee katika chapisho Fair Trade- Fair Future anabaisha wazi kwamba mauzo ya chama cha KNCU ya kahawa katika mpango huu, ni milioni 105, 069, 272, kwa mwaka 2008 wakati mwaka 2004 yalikuwa 175, 320, 894. Pato hili ni ile pesa ya ziada ambayo walaji wa Ulaya na Marekani wako tayari kulipa, achiliambali bei ya zao husika kuwa ipo juu ya bei ya soko.Ni wazi kuwa ushiriki wetu unalegalega.
Fair Trade imaleta hali bora kwa wakulima wadogo wa Tanzania , kuna wanafunzi zaidi ya 250 wamepata udhamini wa kupata elimu ya sekondari kupitia mpango uliobuniwa na chama cha KNCU. Pia washirika hawa wameweza kununua hisa katika Kilimanjaro Cooperative Bank.
Upepo wa mafanikio pia unavuma kwa washirika waliochini ya KCU ambao wameweza kununua hisa za kiwanda cha kahawa cha Kagera. Haya na mambo mengine mengi ni mafanikio ya juu wakulima wameweza kujipatia kupitia mfapongo huu.
Changamoto za Fair Trade katika Tanzanai ni nyingi , miongoni mwa hizo ni ukosefu wa vyama vya ushirika imara. Vyama vya ushirika ndiyo nyenzo ya Fair Trade, hivyo kufanya juhudi zote za kuondoa walanguzi sokoni kutegemea vyama hivi.
Wakulima wa Tanzania wamedhalilika na kuoenewa sana na vyama vya Ushirika. Ushirika umekuwa ni mzigo mzito kwa wakulima wa Tanzania. Ingawa ni kweli kuwa hakuna kesho bila kuwa na ushirika na hasa kwa wakulima wadogo na masikini wa Tanzania. Inashangaza ni kwanini serikali imekuwa na kauli nyingi bila vitendo!
Mtafiti Pirotte (2006) katika tafiti ‘Fair-Trade coffee in Nicaragua and Tanzania: a comparison’ iliyochapwa katika jarida la kisomi la Development in Practice , chapisho la 16 namba 5 anabainisha wazi kuwa wakulima sasa katika Tanzania, wamefikia hatua ya kuona FAIR TRADE, ni sawa na wafanyabiashara wengine (walanguzi), lakini hili limechangiwa zaidi na mwenendo wa ushirika. Ni wazi kuwa aliyeumwa na nyoka akiona unyasi atastuka. Maoni hayo yanaonesha wakulima walivyo kata tamaa na Ushirika hivyo lolote lilillochini yake ni wazi kuwa ni ulaghai!
Ni wazi kuwa mwenendo wa ushirika hauridhishi na wenye kuhitaji kurekebishwa ili kufikia lengo la kuwanufaisha wakulima wa Tanzania.
Hivi karibuni Waziri Mkuu M.K. P Pinda na Waziri wa Kilimo J. Wasira kwa nyakati tofauti wakiwa ziarani Japan na Vietnam wamesikika wakiweka wazi juu ya umuhimu wa ushirika imara kwa masilahi ya wakulima wa Tanzania.
Hili la kilio cha kukosa ushirika imara si jambo jipya. Ni kilio cha muda mrefu, na wala kauli za viongozi wetu katika kuhimiza ushirika imara si mpya pia.
Kauli za viongozi ni sahihi lakini zinahitaji vitendo katika kuwajengea wakulima imani dhidi ya ushirika na hili la Fair Trade linaonesha wazi jinsi tunavyochezea shilingi chooni.
Hali ya mambo inaonesha wazi kuwa kukosekana kwa ushirika imara Tanzania iko hatarini kupoteza nafasi yake katika kufikia masoko ya Marekani na Ulaya kupitia mpango huu. Mtafiti Paul Attontile anabainisha wazi kuwa mapungufu ya watendaji na viongozi wa ushirika yamewafanya hata wanunuzi wa kahawa chini ya mpango huu kufikiria kama kuna namna nyingine ya kuwafikia wakulima wadogo wa Tanzania.
Wakati Tanzania inalega lega kutumia nafasi hii, lakini nchi nyingine wao wako wanapambana kuongeza ushiriki wao kwa kusajili bidhaa nyingine mpya zilizoingizwa chini ya mfumo huu, kama vile asali, ndizi, nguo za pamba na bidhaa za mikono.
Mauzo ya sasa duniani kote ni zadi paundi 1.6 bilioni ukijumalisha masoko ya Ulaya na Amerika. Ingawa biashara ya Fair Trade ni wastani wa asilimia 1 ya biashara ya ulimwengu, lakini lenye kutia moyo ni kukua kwa kasi kwa biashara ya mauzo ya huku Itialia ikukua kwa asilimia 404 na Uingereza asilimia 72.
Walaji pia wa masoko ya Ulaya wako tayari kununua bidhaa zenye kujari masilahi ya wakulima masikini wa Kizio cha Kusini kwa zaidi ya asilimia 70. Mwenendo huu wa walaji na soko unaonesha kufanikiwa kwa mpango huu katika kulifikia soko na ‘kukuna’ nyoyo za walaji za ‘Trade not Aid’
Tuimarishe ushirika, kwani majuto ni mjukuu na Fair Trade imeonesha wazi kuwa inamwisho mwema kwa wakulima wa Tanzania, basi tusichezee shilingi chooni, shime viongozi wetu maneno matupu hayavunji mfupa.

Changamoto ya mitaji toka nchi zinazoendelea

Ripoti ya mwenendo wa uwekezaji (World Investments Report) ya shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulika na Biashara na maendeleo (UNCTAD), ya mwaka 2009 inataja nchi zinazoendelea kuwa zimeweza kuhimili hali mbaya ya Uchumi wa Ulimwengu kwa kuweza kupata asilimi 27 ya mitaji toka nje (Foreign Direct Investments). Ingawa kiwango hiki ni cha chini ukilinganisha na mwaka 2007 lakini ni hali yenye kutia moyo.
Jumla ya dola za kimarekani bilioni 88 zimekezwa katika Afrika, kwa mwaka 2009 pekee, pamoja na mafanikio hayo bado miradi mingi toka nje ilishindwa kuendelezwa kutokana na heka heka ya kuyumba kwa uchumi wa Ulimwengu.
Eneo la Afrika Mashariki lilijizolea shilingi bilioni 4, ikiwa ni eneo lililopata mgao mdogo kwa muda wa mwaka wa pili mfululizo. Pamoja na hali hiyo mitaji toka nchi zinazoendelea imeendelea kumiminika Afrika, wawekezaji wakubwa kutoka nchi masikini ni Uchina, India na Afrika Kusini. Huku Uchina ikijikita katika usakaji wa rasilimali ya mafuta katika Angola, Sudan na Nigeria, bila kusahau miradi mikubwa ya ujenzi katika Kongo-Kinshasa na Afrika Magharibi, pia Afrika Kusini ikifanya vyema katika uwekezaji wa madini katika Tanzania kwa kufanikiwa kununua hisa za Ghana na ikisambaa katika ufunguzi wa maduka ya rejareja (supermarkets) toka Nchi za SADC had ECOWAS, bila kusahau ufunguzi wa mabenki.
Wawekezaji wakubwa wa mitaji katika Tanzania ni Afrika Kusini, Kenya, Uchina, India, Pakistani, Mauritius na Malaysia. Lakini tangu ujio wa wawekezaji hawa mara zote imekuwa kilio katika hali ya uchumi wa Tanzania. Toka wafanyakazi, wafanyabisahara na viongozi wetu wetu wa kitaifa.
Wakati fulani Raisi Kikwete akiwa ziarani nchini Japani aliwahi kunukuliwa na vyombo vya habari akiwaasa wajapani wasiwape kazi za kusimamia mitaji yao wahindi na wapakistani kwa vile ‘wanawapunja’ watanzania.Pia Waziri Mkuu M. Pinda aliwahi kunukuliwa na vyombo vya habari akiwaambia wahandisi wa kichina mkoani Arusha kuwa wanakosa vijana wahandisi wa kufanya nao kazi katika kampuni zao kwa vile wanawalipa mishahara midogo. Hivi ni vilio vya kila siku
Katika Tanzania, nchi zinazoendelea zimewekeza kwa wastani wa asilimia 47, hivyo wawekezaji hawa kutoka nchi hizi ni nguzo muhimu katika mageuzi ya uchumi wa Tanzania. Tukitumia takwimu za idadi ya mitaji, Kenya mara zote uhibuka kama muwekezaji namba moja lakini kwa thamani ya pesa Afrika Kusini ndiyo muwekezaji mkubwa katika Uchumi wa Tanzania.
Mitaji toka nchi zinazoendelea imejikita katika maeneo mawili masoko na kiu ya utafutaji wa malighafi kwa viwanda vyao vya nyumbani. Hii ni changamoto kubwa kwa siku zijazo za majaaliwa ya Tanzania na ukuaji wa uchumi na ustawi wa jamii yake.
Lengo kuu la kuhimiza mitaji toka nje na kufanya mabadiliko makubwa ya kiuchumi tangu miaka ya 1980 ilikuwa ni kupata ahueni ya kiuchumi na kimaendeleo kwa jamii yetu. Swali la msingi ni je hawa wawekezaji wa kizio cha kusini wana mwisho mwema katika lile lengo letu?
Makala haya itajaribu kukusanya vipande vipande kuelekea ukweli. Kwani tunaamini uwekezaji ni muhimu kwa ukuaji wa uchumi wa Tanzania ila yatupasa kuangalia na kujali masilahi yetu kama nchi na basi lengo kuu ni kujaribu kukumbushana hasa juu ya mwenendo wa uwekezaji wa siku za karibuni uliojitokeza na makampuni toka Kusini.
Na wala isieleweke kuwa tunataka kutia chumvi au tunapinga harakati za mageuzi ya uchumi la hasha, lengo ni lile lile kujenga Tanzania yenye neema na heshima kwa wananchi wake.
Tunapotupia jicho wawekezaji toka kusini haiimaanishi kuwa wawekezaji wa kasikazini ndiyo wazuri la hasha ila yatupasa kujadili hali ya mambo katika misingi ya makundi ili walau tujue wapi tunakwenda kwa kuzingatia kile tunakichokiona kulingana na matarajio yetu.
Kwa sasa Tanzania ipo katika hali ngumu ya kujaribu kufuta hali ya sura yake katika biashara ya kimataifa, baada ya RITES wakezaji katika sekta ya usafiri mkataba wake kusitishwa. RITES ni kampuni ya India, ni wawekezaji toka nchi zinazoendelea.
Huu si mktaba wa kwanza Tanzania kuufuta, kuna mkataba wa awali ambao nchi iliuingia na wawekezaji toka Uingereza Biwater na wakashindwa kufanya kazi nao ulifutwa , huku Biwater ikienda mahakamani na kushindwa na ikitakiwa kulipa paundi milioni 8 kwa serikali ya Tanzania.
Lakini lililowazi ni kwamba hatujifunzi somo, na kwa sasa kuna hali ya kuendelea kwa yale yale yaliyopita kwa Biwater ndiyo yametokea kwa RITES. Labda tuweke wazi kuwa hili la RITES lilionekana toka mapema kwani mwekezaji mwingine GAPCO aliyepewa hisa bila hata kuwa na mtaji alidumaza jitihada za kufufufua shirika hili, kwani uwepo wa GAPCO ulifanya IFC kusita kutoa pesa za mkopo dola milioni 44, kwa hoja kuwa huyo aliyepewa hisa, GAPCO, ni mdeni wa IFC hivyo kuna ulakini kama hatua hii itaenda sawa kama ikipewa tena dhamana ya deni la dola milioni 44!
Kutokana na GAPCO kukumbana na kigingi cha IFC, serikali ikaingia kuwa mbia na RITES bila maandalizi.Ni wazi kuwa hatua hii ilichangia kwa kiasi kikubwa kuyumba na kupungua imani miongoni mwa wafanyakazi kwa RITES. Katika mchakato huu kuna mwekezaji mwingine toka India aliyekuwa na wastani wa hisa mbili alijitoa! Bila shaka maji yalizidi unga waswahili wanasema naye aliweza kubashiri vyema.
Hili la RITES si la kwanza ila inaonekana hatujajifunza somo hasa inapokuja wawekezaji toka Kusini, kwani mwaka 2007, Brookside kampuni ya Kenya ilinunua kwa mbwembwe kiwanda cha kusindika maziwa cha Arusha na kuahidi kufanya uwekezaji wa dola milioni 100, katika sekta ya maziwa. Lakini kilichokuja kushuhudiwa ni Tanzania kugeuzwa kuwa shamba la malighafi na uzalishaji unafanyika Kenya.
Mwaka jana ndipo waziri mwenye dhamana ya Afrika Mashariki Dk.Deodorus Kamala alipoifukuzilia mbali Brookside. Ingawa sura ya Tanzania imechafuka lakini liliwazo kuwa hawa wawekezaji toka nchi zinazoendelea mara zote wamekuwa ni wajanja wajanja na wanafanikiwa kwa gia ya kuonekana kama watu wanaoweza kustahimili hali ngumu za miundo mbinu ya Afrika lakini mwisho wake ndiyo haya.
Wawekezaji toka kusini kila wanapowekeza kila wakati imekuwa ni vitendo vya malalamiko na manung’uniko nchini. Hivi karibuni kuna wawekezaji katika sekta ndogo ya ngozi wenye asili ya India na Pakistani kuwa hawapo tayari kuongeza thamani ya ngozi katika viwanda vya ndani na badala yake wanasafirisha ngozi ghafi kwao!
Hilo likiwa halitoshi Ripoti moja ya FAO inataja kuwa kuongezeka kwa vyakula toka nje ya Tanzania ni kwa sababau wawekezaji katika sekta ya utalii na hasa hoteli huagiza vyakula toka nje huku vikiweza kupatikana Tanzania.
Hivi karibuni Waziri Ngeleja amenukuriwa na vyombo vya habari kuwa wawekezaji katika migodi waache kununua nyama nje ya Tanzania badala yake wanunue nyama Tanzania ili tuongeze tija katika viwanda vyetu vya ndani na kuongeza ajira. Katika sekta ya nyama kuna SAAFA ya Rukwa na Tanzania Meat Pride Morogoro. Hatua ya muheshimiwa Ngeleja, ni rai njema sijui katika vitendo itakuwaje, ni suala la kusubiri na kuona, ila ni mwanzo mwema.
Kila kitu sasa tunaagiza toka nje huku ndani kuna wajasiriamali wadogo waliowekeza katika kilimo na usindikaji wakitaka kupata hizo kazi tunapewa hoja chakavu kuwa minofu yao haina viwango mara minofu ya kuku ina harufu ya dagaa!
Bila mabadiliko ya kisera katika kuhakikisha wawekezaji wanatumia bidhaa za ndani ni wazi kuwa tutabakia kuwa watazamaji. Kuna nchi zimeweka wazi kuwa mwekezaji anapaswa kufanya nini anapoingia nchini na asilimia ngapi ya malighafi anayotumia inapaswa kutoka soko la ndani.
Bidhaa wawekezaji wa ndani wanaikataa lakini inapenya na kufanya vyema katika masoko ya Ulaya, tena ikisifiwa kuwa na viwango bora. Kuna mifano mingi ya bidhaa za kilimo zinazofanya vyema Ulaya lakini nyumbani hazina nafasi!
Tusibwete katika ‘kulainisha’ mambo kwa kigezo cha kuvutia mitaji. Hili la kuwa na wachuuzi wa Kichina Kariakoo, Kenya majirani zetu tangu miaka 1960 wameweka wazi kuwa mwekezaji wa nje hapaswi kuingia katika sekta ya’ juakali’. Lakini Tanzania hapana.
Niliwahi kuhudhruia ‘carrier workshop’ ya moja ya benki katika Tanzania, wakati wa majadiliano kuhusu mishahara Mkurugenzi wa Benki alieleza wazi kuwa hataweza kulipa zaidi ya mshahara wa serikali. Kigezo alichotumia ni kuwa serikali inawalipa wenzenu TGSD, tena wenye shahada kama nyinyi!
Kumbe katika malipo ni sisi ndiyo tumejimaliza na hakuna mchawi ila ni serikali kuwa na viwango vidogo vya mishahara na wageni wakija wanaangalia ‘skeli’ za serikali nao wanatumia kigezo hicho hicho katika hali kama hii ni vigumu kuona mitaji kutoka nje ikiwaneemesha watanzania.

Friday, March 19, 2010

Bravo TRA

BRAVO TRA kwa kufuta kodi ya silimia 18 ya VAT kwa wauzaji wa mboga mboga nje ya nchi.Hakika huu ni mwendelezo wa mwanzo mpya tuliwahi kuandika juu ya hili, januari 4 mwaka huu.KUpitia gazeti la serikali Daily News la tarehe 18.03.2010, Kamishna wa kodi amefuta kodi ya VAT ya asilimia 18.
Kila la heri wakulima na wajasiriamli katika sekta ndogo ya mbogamboga na maua.